Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w24 Agosti kur. 26-31
  • Wazee Wanawezaje Kuwasaidia Wale Wanaoondolewa Kutanikoni?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Wazee Wanawezaje Kuwasaidia Wale Wanaoondolewa Kutanikoni?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2024
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • “MWONDOENI MTU MWOVU”
  • JINSI WAZEE WANAVYOWASAIDIA WALE AMBAO WAMEONDOLEWA KUTANIKONI
  • KUTANIKO LINAWEZA KUFANYA NINI?
  • IGA HURUMA NA REHEMA ZA YEHOVA
  • Jinsi ya Kuwaonyesha Watenda Dhambi Upendo na Rehema
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2024
  • Jinsi Kutaniko Linavyoweza Kuiga Maoni ya Yehova Kuhusu Watenda Dhambi
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2024
  • Je, Mashahidi wa Yehova Huwaepuka Watu Ambao Zamani Walishirikiana na Dini Yao?
    Maswali Yanayoulizwa Mara Nyingi Kuhusu Mashahidi wa Yehova
  • Toba Inayorudisha Mtu Kwa Mungu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1981
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2024
w24 Agosti kur. 26-31

MAKALA YA 35

WIMBO 123 Kutii Utaratibu wa Kitheokrasi kwa Ushikamanifu

Wazee Wanawezaje Kuwasaidia Wale Wanaoondolewa Kutanikoni?

“Kutakuwa na shangwe nyingi mbinguni kwa sababu ya mtenda dhambi mmoja anayetubu kuliko kwa waadilifu 99 ambao hawahitaji kutubu.”—LUKA 15:7.

JAMBO KUU

Sababu zinazofanya baadhi ya watu waondolewe kutanikoni na jinsi wazee wanavyoweza kuwasaidia watu hao kutubu na kupata tena kibali cha Yehova.

1-2. (a) Yehova ana maoni gani kuhusu watenda dhambi wasiotubu? (b) Yehova anataka watenda dhambi wafanye nini?

YEHOVA si Mungu anayeendekeza uovu; anachukia dhambi. (Zab. 5:​4-6) Anataka tuheshimu viwango vyake vya uadilifu, ambavyo vinapatikana katika Neno lake. Bila shaka, Yehova hatarajii ukamilifu kutoka kwa watu ambao si wakamilifu. (Zab. 130:​3, 4) Wakati uleule, hawavumilii ‘watu ambao hawamwogopi Mungu, wanaotumia fadhili zake zisizostahiliwa kuwa kisingizio cha mwenendo mpotovu.’ (Yuda 4) Kwa sababu hiyo, Biblia inazungumzia “kuangamizwa kwa watu wasiomwogopa Mungu” katika vita vya Mungu vya Har–​Magedoni.—2 Pet. 3:7; Ufu. 16:16.

2 Hata hivyo, Yehova hataki mtu yeyote aangamizwe. Kama tulivyozungumzia katika makala zilizotangulia za mfululizo huu, Biblia inaeleza waziwazi kwamba Yehova “hutaka wote wafikie toba.” (2 Pet. 3:9) Wazee Wakristo humwiga Yehova wanapojitahidi kwa subira kuwasaidia watenda dhambi wabadili njia zao na kupata tena kibali cha Yehova. Hata hivyo, si watenda dhambi wote wanaoitikia kwa njia nzuri. (Isa. 6:9) Baadhi yao wanaendelea kufanya mambo mabaya licha ya jitihada za wazee za kuwaongoza kwenye toba. Wazee wanapaswa kufanya nini katika hali hizo?

“MWONDOENI MTU MWOVU”

3. (a) Biblia inasema watenda dhambi wasiotubu wanapaswa kutendewaje? (b) Kwa nini tunaweza kusema kwamba kwa njia fulani, mtenda dhambi amechagua mwenyewe kuondolewa kutanikoni?

3 Mtenda dhambi asipotubu, ni lazima wazee wafuate mwongozo huu unaopatikana kwenye 1 Wakorintho 5:13: “Mwondoeni mtu mwovu miongoni mwenu.” Kwa njia fulani, mtenda dhambi amechagua matokeo hayo; anavuna kile ambacho yeye mwenyewe amepanda. (Gal. 6:7) Kwa nini tunaweza kusema hivyo? Kwa sababu alikataa kuitikia kwa njia nzuri wazee walipojaribu tena na tena kumwongoza kwenye toba. (2 Fal. 17:​12-15) Matendo yake yanaonyesha kwamba amechagua kutotii viwango vya Yehova.—Kum. 30:​19, 20.

4. Kwa nini tangazo linatolewa mtenda dhambi asiyetubu anapoondolewa kutanikoni?

4 Mtenda dhambi asiyetubu anapoondolewa kutanikoni, tangazo linatolewa ili kulijulisha kutaniko kwamba sasa mtu huyo si mmoja wa Mashahidi wa Yehova tena.a Kusudi la tangazo hilo si kumwaibisha mtenda dhambi. Badala yake, linatolewa ili kutaniko liweze kufuata himizo la Kimaandiko la ‘kuacha kushirikiana’ na mtu huyo, na ‘hata kutokula chakula pamoja’ naye. (1 Kor. 5:​9-11) Mwongozo huo unatolewa kwa sababu nzuri. Mtume Paulo aliandika hivi: “Chachu kidogo huchachisha donge lote.” (1 Kor. 5:6) Watenda dhambi wasiotubu wanaweza kudhoofisha azimio la wale wanaojitahidi kuishi kulingana na viwango vya Yehova vya uadilifu.—Met. 13:20; 1 Kor. 15:33.

5. Tunapaswa kuwa na maoni gani kuhusu mtu aliyeondolewa kutanikoni, na kwa nini?

5 Tunapaswa kuwa na maoni gani kuhusu mwabudu mwenzetu aliyeondolewa kutanikoni? Ingawa hatushirikiani naye, tunapaswa kumwona kama kondoo aliyepotea, na si mtu asiyeweza kubadilika. Kondoo aliyepotea anaweza kurudi zizini. Kumbuka kwamba kondoo huyo aliyepotea alijiweka wakfu kwa Yehova. Kwa kusikitisha, sasa haishi kulingana na wakfu wake na jambo hilo ni hatari sana. (Eze. 18:31) Hata hivyo, maadamu wakati bado upo na Yehova yuko tayari kuonyesha rehema yake, kuna tumaini kwamba mtu huyo atarudi kutanikoni. Wazee wanawezaje kumsaidia mtenda dhambi ambaye ameondolewa kutanikoni?

JINSI WAZEE WANAVYOWASAIDIA WALE AMBAO WAMEONDOLEWA KUTANIKONI

6. Wazee watachukua hatua gani ili kumsaidia yule ambaye ameondolewa kutanikoni?

6 Je, mtu huyo aliyeondolewa kutanikoni ameachwa—ametelekezwa kabisa ajitafutie mwenyewe njia ya kumrudia Yehova? La, hasha! Halmashauri ya wazee inapomjulisha mtenda dhambi kwamba ataondolewa kutanikoni, inamfafanulia hatua ambazo anaweza kuchukua ili arudishwe kutanikoni. Lakini wazee hao watafanya mengi hata zaidi. Katika visa vingi, watamwambia aliyetenda dhambi kwamba wangependa kukutana naye tena baada ya miezi michache ili kuona ikiwa amebadili mtazamo wake. Ikiwa mtenda dhambi huyo yuko tayari kukutana nao tena, wazee watamhimiza kwa upendo katika kikao hicho atubu na kumrudia Yehova. Hata ikiwa kwa wakati huo mtazamo wake bado haujabadilika, wazee watafanya jitihada za kukutana naye pindi fulani wakati ujao.

7. Wazee wanaigaje huruma ya Yehova wanaposhughulika na mtu ambaye ameondolewa kutanikoni? (Yeremia 3:12)

7 Wazee wanajitahidi kuiga huruma ya Yehova wanaposhughulika na mtu aliyeondolewa kutanikoni. Kwa mfano, Yehova hakusubiri watu wake waliopotoka katika taifa la Israeli wachukue hatua ya kwanza. Badala yake, Yehova alichukua hatua ya kwanza kwa kuwatuma manabii hata kabla watu wake hawajaonyesha dalili zozote za kutubu. Kama tulivyoona kwenye makala ya pili ya mfululizo huu, Yehova alionyesha huruma yake kwa kumwambia nabii Hosea amsamehe mke wake, ingawa bado alikuwa akifanya dhambi. (Hos. 3:1; Mal. 3:7) Kwa kumwiga Yehova, tamaa ya moyoni ya wazee Wakristo ni kwamba wangependa mtenda dhambi arudi, na hawafanyi iwe vigumu kwake kurudi.—Soma Yeremia 3:12.

8. Mfano wa Yesu wa mwana mpotevu unatusaidiaje kuelewa vizuri zaidi huruma na rehema za Yehova? (Luka 15:7)

8 Kumbuka mfano wa Yesu wa mwana mpotevu tuliozungumzia katika makala ya pili kwenye mfululizo huu. Alipomwona akirudi nyumbani, baba yake ‘alikimbia, akamkumbatia na kumbusu kwa wororo.’ (Luka 15:20) Ona kwamba baba huyo hakusubiri hadi mwana wake aanze kuomba msamaha. Badala yake, alichukua hatua ya kwanza kama ambavyo baba yeyote mwenye upendo angefanya. Wazee hujitahidi kuonyesha mtazamo kama huo kuelekea wale ambao wamepotea. Wanataka kondoo hao waliopotea warudi nyumbani. (Luka 15:​22-24, 32) Kunakuwa na shangwe mbinguni na pia duniani mtenda dhambi anaporudi!—Soma Luka 15:7.

9. Yehova anawahimizaje kwa upendo watenda dhambi?

9 Kulingana na mambo ambayo tumejifunza kufikia sasa, ni wazi kwamba Yehova haruhusu mtenda dhambi asiyetubu abaki kutanikoni. Hata hivyo, bado anaendelea kuwasaidia watenda dhambi. Anataka wamrudie. Hisia za Yehova kuelekea watenda dhambi zinafunuliwa kwenye andiko la Hosea 14:​4, linalosema hivi: “Nitauponya ukosefu wao wa uaminifu. Nitawapenda kwa hiari yangu mwenyewe, kwa sababu hasira yangu imegeuka na kuwaacha.” Hicho ni kichocheo kikubwa sana kwa wazee kumsaidia mtenda dhambi wanapoona dalili zozote za toba. Pia, ni kichocheo kikubwa sana kwa wale ambao wamemwacha Yehova warudi haraka bila kukawia.

10-11. Wazee watajitahidi jinsi gani kuwasaidia wale walioondolewa kutanikoni zamani?

10 Namna gani kuhusu watu ambao zamani waliondolewa kutanikoni, labda miaka mingi iliyopita? Huenda kwa sasa watu hao hawaendelei kufanya dhambi iliyosababisha waondolewe kutanikoni. Katika baadhi ya visa, huenda hata hawakumbuki kwa nini waliondolewa kutanikoni. Vyovyote vile, wazee watajitahidi kuwatafuta na kuwatembelea watu hao. Katika ziara hizo, wazee wa kutaniko hata watasali pamoja nao na kuwahimiza kwa upendo warudi kutanikoni. Bila shaka, ikiwa mtu amekuwa mbali na kutaniko kwa miaka mingi, ni wazi kwamba atakuwa dhaifu sana kiroho. Hivyo, ikiwa atasema anataka kurudi kutanikoni, huenda wazee wakapanga mtu fulani ajifunze naye Biblia ingawa bado hajarudishwa kutanikoni. Katika kila kisa, wazee ndio watakaochagua mtu atakayeongoza funzo hilo la Biblia.

11 Kwa kuiga huruma ya Yehova, wazee wanataka kuwafikia na kuwasaidia watu wengi kadiri iwezekanavyo wajue kwamba mlango uko wazi kwa ajili ya kurudi kutanikoni. Mtenda dhambi anapoonyesha toba na kuacha mwenendo wake mbaya, anaweza kurudishwa kutanikoni bila kukawia.—2 Kor. 2:​6-8.

12. (a) Ni katika hali gani wazee wanapaswa kuwa makini sana? (b) Kwa nini hatupaswi kuhisi kwamba haiwezekani kwa aina fulani ya watenda dhambi kupata rehema za Yehova? (Tazama pia maelezo ya chini.)

12 Katika hali fulani, wazee wanapaswa kuwa makini sana kabla ya kumrudisha mtu kutanikoni. Kwa mfano, ikiwa mtu ana hatia ya kumtenda mtoto vibaya au ya uasi-imani au alipanga njama ya kumwacha mwenzi wake wa ndoa, wazee wangependa kuhakikisha ikiwa anaonyesha toba ya kweli. (Mal. 2:14; 2 Tim. 3:6) Ni lazima walilinde kundi. Wakati huohuo, tunahitaji kutambua kwamba Yehova atamkubali tena mtenda dhambi yeyote anayeonyesha toba ya kweli na kuacha matendo yake mabaya. Ingawa wazee wanahitaji kuwa na tahadhari inayofaa wanaposhughulika na wale ambao wamewatendea wengine kwa hila, hawapaswi kufikia hatua ya kusema kwamba aina fulani ya watenda dhambi hawatapata kamwe rehema za Yehova.b—1 Pet. 2:10.

KUTANIKO LINAWEZA KUFANYA NINI?

13. Kuna tofauti gani kati ya jinsi tunavyoshughulika na mtu aliyekaripiwa na wazee na jinsi tunavyoshughulika na mtu aliyeondolewa kutanikoni?

13 Kama tulivyozungumzia kwenye makala iliyopita, nyakati nyingine tangazo linatolewa kwamba mtu amekaripiwa. Katika kisa hicho, tunaweza kuendelea kushirikiana naye tukijua kwamba ametubu na ameacha njia yake mbaya. (1 Tim. 5:20) Bado yeye ni sehemu ya kutaniko na anahitaji kitia moyo kinachotokana na kushirikiana na waabudu wenzake. (Ebr. 10:​24, 25) Hata hivyo, hali ni tofauti kabisa na mtu ambaye ameondolewa kutanikoni. ‘Tunaacha kushirikiana’ na mtu huyo, ‘hata hatuli chakula pamoja na mtu wa namna hiyo.’—1 Kor. 5:11.

14. Wakristo wanawezaje kutumia dhamiri zao zilizozoezwa na Biblia wanaposhughulika na wale walioondolewa kutanikoni? (Tazama pia picha.)

14 Je, mwongozo ambao tumezungumzia unamaanisha kwamba tunapaswa kumpuuza kabisa mtu aliyeondolewa kutanikoni? Hapana. Ni wazi kwamba hatutashirikiana na mtu huyo. Lakini Wakristo wanaweza kutumia dhamiri zao zilizozoezwa na Biblia wanapoamua ikiwa watamwalika mtu aliyeondolewa kutanikoni—huenda mtu wao wa ukoo au mtu ambaye awali alikuwa rafiki yao wa karibu—ahudhurie mkutano wa kutaniko. Namna gani ikiwa atahudhuria mkutano? Zamani, hatungemsalimu mtu huyo. Katika kisa hiki pia, kila Mkristo anahitaji kutumia dhamiri yake iliyozoezwa na Biblia inapohusu jambo hili. Huenda baadhi ya watu wakajihisi huru kumsalimu mtu huyo au kumkaribisha kwenye mkutano. Hata hivyo, hatutakuwa na mazungumzo marefu na mtu huyo au kushirikiana naye katika mambo mengine.

Mkusanyo wa picha: 1. Dada anampigia simu mwanamke ambaye aliondolewa kutanikoni na kumwalika kwenye mkutano wa kutaniko. 2. Yule dada na mume wake wakimsalimu kwa uchangamfu mwanamke huyo kwenye mkutano.

Wakristo wanaweza kutumia dhamiri zao zilizozoezwa na Biblia wanapoamua ikiwa watamwalika mtu aliyeondolewa kutanikoni ahudhurie mkutano au kumkaribisha kwenye mkutano kwa kumsalimu kifupi (Tazama fungu la 14)


15. Ni aina gani ya watenda dhambi wanaozungumziwa kwenye 2 Yohana 9-11? (Tazama pia sanduku “Je, Yohana na Paulo Walikuwa Wakizungumzia Aina Ileile ya Dhambi?”)

15 Huenda baadhi ya watu wakauliza, ‘Je, Biblia haisemi kwamba Mkristo anayemsalimu mtu huyo anashiriki matendo yake maovu?’ (Soma 2 Yohana 9-11.) Muktadha wa andiko hilo unaonyesha kwamba mwongozo huo unarejelea waasi-imani na watu wanaowachochea wengine kutenda mambo mabaya. (Ufu. 2:20) Hivyo, ikiwa mtu anaendeleza mafundisho ya waasi-imani au anawachochea wengine kutenda mambo mabaya, wazee hawatapanga kumtembelea. Bila shaka, tunatumaini kwamba atarudiwa na fahamu. Hata hivyo, mpaka wakati huo ufike, hatutamsalimu mtu huyo, wala kumkaribisha kwenye mikutano.

Je, Yohana na Paulo Walikuwa Wakizungumzia Aina Ileile ya Dhambi?

Katika barua yake ya pili iliyoongozwa na roho, mtume Yohana aliandika hivi: “Mtu yeyote akija kwenu naye haleti fundisho hili, msimpokee nyumbani mwenu wala kumsalimu. Kwa maana mtu anayemsalimu anashiriki matendo yake maovu.”—2 Yoh. 10, 11.

Aliposema kwamba Wakristo hawapaswi hata ‘kumsalimu,’ je, Yohana alikuwa akitoa mwongozo zaidi ya ule ambao mtume Paulo alitoa kwenye 1 Wakorintho 5:11 unaosema, “mwache kushirikiana” na watu ambao wameondolewa kutanikoni? Je, Yohana na Paulo walikuwa wakizungumzia aina ileile ya dhambi? Inaonekana haikuwa hivyo.

Fikiria tofauti kati ya hali zilizotajwa na kila mtume. Katika barua yake, Paulo aliandika kuhusu mwanamume aliyefanya dhambi ya uasherati. Miaka 43 hivi baadaye, Yohana aliandika kuhusu waasi-imani, ambao waliendeleza mafundisho ya uwongo na kuchochea mwenendo usiofaa. Kwa mfano, baadhi ya watu walikuwa wakifundisha kwamba Yesu hakuwa Kristo.—1 Yoh. 2:22; 4:​2, 3.

Yohana alipoandika barua zake, uasi-imani ulikuwa umeenea sana. Ingawa alijua kwamba hangeweza kuukomesha kabisa, alitimiza wajibu wake akiwa mtume kwa kutenda kama “yule anayeuzuia” uasi-imani, kwa kuuzuia kwa muda mrefu kadiri alivyoweza.—2 The. 2:7.

Hivyo, Yohana aliwaonya waabudu wenzake waepuke kupotoshwa na wadanganyifu na walimu wa uwongo. Aliwaagiza Wakristo wasiwapokee kamwe watu wa aina hiyo nyumbani kwao au hata kuwasalimu. Kumsalimu mtu anayeendeleza mafundisho ya uwongo kungempa nafasi ya kuanza kuzungumzia mafundisho yake yaliyopotoka. Jambo kama hilo linaweza kutokea ikiwa mtu ataandika maoni yake kwenye tovuti ya mwasi-imani au mtandao wa kijamii. Mtu yeyote ambaye angemkaribisha mwasi-imani kwa kumsalimu, angekuwa ‘akishiriki matendo yake maovu.’

Kwa upande mwingine, Paulo aliandika kuhusu mwanamume aliyehitaji kuondolewa kutanikoni kwa sababu ya kufanya uasherati, kama inavyoonyeshwa kwenye 1 Wakorintho sura ya 5. Lakini inaonekana kwamba mwanamume huyo hakuwa mwasi-imani; wala hakuwa akiwafundisha wengine wavunje viwango vya Mungu. (Linganisha Ufunuo 2:20.) Ingawa Paulo aliwaagiza wale walio kutanikoni waache kushirikiana naye—hata wasile pamoja naye—hakusema kwamba hawakupaswa kamwe kumsalimu kifupi.

IGA HURUMA NA REHEMA ZA YEHOVA

16-17. (a) Yehova anataka watenda dhambi wafanye nini? (Ezekieli 18:32) (b) Wazee wanawezaje kuonyesha kwamba wao ni wafanyakazi wenzi wa Yehova wanapojitahidi kuwasaidia watenda dhambi?

16 Tumejifunza nini katika mfululizo huu wenye sehemu tano? Yehova hataki mtu yeyote aangamizwe! (Soma Ezekieli 18:32.) Anataka watenda dhambi wapatanishwe naye. (2 Kor. 5:20) Ndiyo sababu katika historia yote, Yehova amewahimiza tena na tena watu wake waliopotoka, pamoja na mtu mmoja-mmoja, watubu na kumrudia. Wazee wa kutaniko wana pendeleo la kuwa wafanyakazi wenzi wa Yehova wanapojitahidi kumwongoza mtenda dhambi kwenye toba.—Rom. 2:4; 1 Kor. 3:9.

17 Wazia shangwe inayokuwa mbinguni mtenda dhambi anapotubu! Baba yetu wa mbinguni, Yehova, anakuwa na shangwe kila mara anapojionea kondoo wake aliyepotea akirudi kutanikoni. Upendo wetu kwa Yehova unaendelea kuimarika tunapotafakari huruma, rehema, na fadhili zake zisizostahiliwa.—Luka 1:78.

UNGEJIBUJE?

  • Kwa nini baadhi ya watu wanahitaji kuondolewa kutanikoni?

  • Wazee wanawezaje kuiga huruma ya Yehova?

  • Ndugu na dada kutanikoni wanawezaje kutumia dhamiri zao zilizozoezwa na Biblia wanaposhughulika na mtu aliyeondolewa kutanikoni?

WIMBO 111 Sababu za Kuwa na Shangwe

a Hatutawarejelea tena watu hao kuwa waliotengwa na ushirika. Kulingana na maneno ya Paulo kwenye 1 Wakorintho 5:​13, sasa tutawarejelea kuwa wameondolewa kutanikoni.

b Kulingana na Biblia, dhambi isiyoweza kusamehewa si aina hususa ya dhambi, bali ni dhambi inayofanywa na mtu mwenye mtazamo wa ukaidi ambaye sikuzote anampinga Mungu. Ni Yehova na Yesu tu ndio wanaoweza kuhukumu kwamba mtu amefanya dhambi isiyoweza kusamehewa.—Marko 3:29; Ebr. 10:​26, 27.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki