Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w25 Machi kur. 8-13
  • Mwige Yehova na Yesu Katika Njia Yako ya Kufikiri

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Mwige Yehova na Yesu Katika Njia Yako ya Kufikiri
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2025
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • IGA NJIA YA YEHOVA YA KUFIKIRI
  • UWE MNYENYEKEVU
  • IWENI NA “UTIMAMU WA AKILI”
  • Alijifunza Kusamehe Kutoka kwa Bwana Wake
    Igeni Imani Yao
  • Mtume Petro—Kwa Sababu Gani Anapendwa Sana na Wengi?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1978
  • Maamuzi Yanayoonyesha Unamtegemea Yehova
    Daftari la Mkutano wa Huduma na Maisha Yetu ya Kikristo—2023
  • Alikuwa Mshikamanifu Licha ya Majaribu
    Igeni Imani Yao
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2025
w25 Machi kur. 8-13

MAKALA YA 10

WIMBO 31 Tembea Pamoja na Mungu!

Mwige Yehova na Yesu Katika Njia Yako ya Kufikiri

“Kwa kuwa Kristo aliteseka katika mwili, ninyi pia jiimarisheni kwa mwelekeo uleule wa akili.”—1 PET. 4:1.

JAMBO KUU

Jinsi mtume Petro alivyojifunza kutokana na njia ya Yesu ya kufikiri na jinsi sisi pia tunavyoweza kufanya hivyo.

1-2. Kumpenda Yehova kunahusisha nini, na Yesu alionyeshaje kwamba anampenda Yehova?

“LAZIMA umpende Yehova Mungu wako kwa moyo wako wote kwa nafsi yako yote kwa nguvu zako zote na kwa akili yako yote.” (Luka 10:27) Yesu alionyesha wazi kwamba hiyo ni amri muhimu zaidi katika Sheria ya Musa. Ona kwamba upendo wetu kwa Yehova unahusisha moyo wetu, yaani, tamaa na hisia zetu. Pia, unahusisha nguvu zetu na kujitoa kwetu kwa nafsi yote. Hata hivyo, kumpenda Yehova kunahusisha pia akili yetu, hilo linatia ndani pia njia yetu ya kufikiri. Kwa kweli, hatuwezi kamwe kuelewa kikamili njia ya Yehova ya kufikiri. Lakini kwa kujifunza “akili ya Kristo,” tunaweza kuelewa vizuri zaidi njia ya Mungu ya kufikiri kwa sababu Yesu anaiga kikamilifu njia ya Baba yake ya kufikiri.—1 Kor. 2:16 na habari za utafiti “we do have the mind of Christ,” nwsty.

2 Yesu alimpenda Yehova kwa akili yake yote. Alijua mapenzi ya Mungu kumwelekea na aliazimia kutenda kulingana na mapenzi hayo, ingawa alijua kwamba kufanya hivyo kungemaanisha kuteseka kwa ajili ya yaliyo sawa. Kwa kuwa Yesu alikazia fikira kutimiza mapenzi ya Baba yake, hakuruhusu chochote kimkengeushe kutimiza lengo hilo.

3. Mtume Petro alijifunza nini kutoka kwa Yesu, na Petro aliwatia moyo Wakristo wenzake wafanye nini? (1 Petro 4:1)

3 Petro na mitume wenzake walikuwa na pendeleo la kuwa pamoja na Yesu na kujifunza moja kwa moja njia yake ya kufikiri. Petro alipoandika barua yake ya kwanza iliyoongozwa na roho, aliwatia moyo Wakristo wajiimarishe kwa mwelekeo uleule wa akili ya Kristo.a (Soma 1 Petro 4:1.) Petro alitumia msemo uliotumika jeshini alipoandika: “Jiimarisheni.” Hivyo, ikiwa Wakristo wataiga mwelekeo wa akili ya Yesu, au njia yake ya kufikiri, watakuwa na silaha yenye nguvu katika vita vyao dhidi ya mielekeo ya dhambi na dhidi ya ulimwengu unaotawaliwa na Shetani.—2 Kor. 10:​3-5; Efe. 6:12.

4. Makala hii inawezaje kutusaidia kufuata ushauri wa Petro?

4 Acheni tuchunguze njia ya Yesu ya kufikiri na tuone jinsi tunavyoweza kumwiga. Tutajifunza jinsi tunavyoweza (1) kuiga njia ya Yehova ya kufikiri, ambayo itatusaidia kufikiri kwa upatano, (2) kuwa wanyenyekevu, na (3) kuwa na utimamu wa akili kwa kumtegemea Yehova katika sala.

IGA NJIA YA YEHOVA YA KUFIKIRI

5. Pindi moja Petro alishindwaje kuiga njia ya Yehova ya kufikiri?

5 Fikiria pindi moja ambayo Petro alishindwa kuiga njia ya Yehova ya kufikiri. Yesu aliwaambia mitume wake kwamba lazima aende Yerusalemu, akamatwe na viongozi wa dini, ateswe, na kuuawa. (Mt. 16:21) Huenda haikuwa rahisi kwa Petro kukubali kwamba Yehova angeruhusu Yesu—tumaini la Israeli na Masihi aliyeahidiwa—auawe. (Mt. 16:16) Hivyo, Petro akampeleka Yesu kando na kumwambia: “Bwana jihurumie; hutapatwa kamwe na mambo hayo.” (Mt. 16:22) Kwa kuwa Petro hakuiga njia ya Yehova ya kufikiri kuhusiana na jambo hilo, maoni yake hayakupatana na maoni ya Yesu.

6. Yesu alionyeshaje kwamba njia yake ya kufikiri ilipatana na ya Yehova?

6 Njia ya Yesu ya kufikiri ilipatana kikamili na njia ya kufikiri ya Baba yake wa mbinguni. Yesu alimwambia hivi Petro: “Nenda nyuma yangu, Shetani! Wewe ni kikwazo kwangu, kwa sababu hufikirii mawazo ya Mungu, bali ya wanadamu.” (Mt. 16:23) Huenda Petro alikuwa na nia nzuri, lakini Yesu alikataa ushauri wa Petro. Tunajifunza nini? Hayakuwa mapenzi ya Yehova kwamba Yesu aishi maisha ya kujihurumia. Katika pindi hiyo, Petro alijifunza somo muhimu sana kuhusu kupatanisha njia yake ya kufikiri na njia ya Mungu ya kufikiri.

7. Baadaye Petro alionyeshaje kwamba alipatanisha njia yake ya kufikiri na njia ya Yehova ya kufikiri? (Tazama picha.)

7 Hatimaye, Petro alionyesha kwamba alitaka kupatanisha njia yake ya kufikiri na ile ya Yehova. Wakati ulikuwa umefika kwa Watu wa Mataifa kuwa sehemu ya watu wa Mungu. Petro alipewa mgawo wa kumhubiria Kornelio aliyekuwa Mtu wa Mataifa, ambaye angekuwa miongoni mwa watu wa kwanza katika kikundi hiki kipya cha waabudu. Wayahudi waliepuka kushirikiana na Watu wa Mataifa, hivyo haishangazi kwamba Petro alihitaji msaada ili ajitayarishe kutimiza mgawo wake. Petro alipotambua mapenzi ya Mungu kuhusiana na jambo hilo, alibadili mtazamo wake. Matokeo ni kwamba Kornelio alipomwita, alienda “bila kupinga.” (Mdo. 10:​28, 29) Petro akamhubiria Kornelio na watu wa nyumba yake, nao wakabatizwa.—Mdo. 10:​21-23, 34, 35, 44-48.

Petro na wenzake wakiongozwa na Kornelio kwenye chumba cha juu katika nyumba yake.

Petro akiingia katika nyumba ya Kornelio (Tazama fungu la 7)


8. Tunawezaje kuonyesha kwamba njia yetu ya kufikiri inapatana na njia ya Yehova ya kufikiri? (1 Petro 3:8)

8 Miaka mingi baadaye, Petro aliwatia moyo Wakristo wenzake ‘wafikiri kwa upatano.’ (Soma 1 Petro 3:8.) Tukiwa watu wa Yehova, tunaweza kufikiri kwa upatano kwa kuiga njia ya Yehova ya kufikiri inayoonyeshwa katika Neno lake. Kwa mfano, Yesu aliwasihi wafuasi wake watangulize Ufalme maishani mwao. (Mt. 6:33) Akiwa na hilo akilini, mhubiri katika kutaniko lenu anaweza kuamua kuanza aina fulani ya utumishi wa wakati wote. Badala ya kumwambia ajihurumie, tunapaswa kumtia moyo na kumuunga mkono.

UWE MNYENYEKEVU

9-10. Yesu alionyeshaje unyenyekevu wa kipekee?

9 Usiku kabla ya kifo chake, Yesu alimfundisha Petro na mitume wengine somo muhimu kuhusu unyenyekevu. Mapema, Yesu alimtuma Petro na Yohana kufanya matayarisho kwa ajili ya mlo wa mwisho ambao Yesu angekula pamoja nao akiwa mwanadamu. Huenda maandalizi hayo yalitia ndani kuhakikisha kwamba kulikuwa na beseni na taulo ili wageni waweze kuoshwa miguu yao kabla ya mlo. Lakini nani angefanya kazi hiyo ya hali ya chini?

10 Bila kusita, Yesu alionyesha unyenyekevu wa kipekee. Ni lazima mitume wake walishangaa sana, walipomwona Yesu akifanya kazi ambayo kwa kawaida ingefanywa na mtumishi. Yesu aliyaweka kando mavazi yake ya nje, akajifunga taulo kiunoni, akatia maji kwenye beseni, na kuanza kuosha miguu yao. (Yoh. 13:​4, 5) Huenda ilichukua muda mrefu kwa Yesu kuosha miguu ya mitume wote 12—kutia ndani ya Yuda, ambaye angemsaliti. Hata hivyo, kwa unyenyekevu Yesu alitimiza kazi hiyo. Kisha Yesu akasema hivi kwa subira: “Je, mnaelewa jambo ambalo nimewafanyia? Ninyi huniita, ‘Mwalimu,’ na, ‘Bwana,’ nanyi hamjakosea, kwa maana ndivyo nilivyo. Kwa hiyo, ingawa mimi ni Bwana na Mwalimu, niliiosha miguu yenu, basi ninyi pia mnapaswa kuoshana miguu.”—Yoh. 13:​12-14.

Unyenyekevu wa kweli unahusisha . . . mawazo yetu ya ndani kabisa

11. Petro alionyeshaje kwamba alijifunza kuwa mnyenyekevu? (1 Petro 5:5 na maelezo ya chini) (Tazama pia picha.)

11 Petro alijifunza sifa ya unyenyekevu kutoka kwa Yesu. Baada ya Yesu kurudi mbinguni, Petro alimponya mwanamume aliyekuwa kilema tangu kuzaliwa kwake. (Mdo. 1:​8, 9; 3:​2, 6-8) Umati mkubwa wa watu uliona muujiza huo na kumzunguka Petro. (Mdo. 3:11) Je, Petro angefurahia kupokea utukufu pindi hiyo, ukizingatia kwamba alilelewa katika jamii ambayo ilikazia fikira sana vyeo na umashuhuri? Hapana, kwa unyenyekevu Petro hakuelekeza sifa kwake, bali kwa Yehova na Yesu ambao wanastahili. Alisema hivi: “Kupitia jina [la Yesu], na kwa imani yetu katika jina lake, mtu huyu mnayemwona na kumfahamu amefanywa awe mwenye nguvu.” (Mdo. 3:​12-16) Maneno ambayo Petro alitumia katika barua yake kwa Wakristo kuhusu umuhimu wa kusitawisha unyenyekevu, huenda yakatukumbusha wakati ambapo Yesu alijifunga taulo kiunoni na kuosha miguu ya mitume.—Soma 1 Petro 5:5 na maelezo ya chini.

Petro na Yohana wakiwa wamesimama ndani ya hekalu. Petro ananyoosha mkono wake kuelekea mbinguni huku mwanamume ambaye alikuwa kilema tangu kuzaliwa kwake amesimama kando yao akiwa ameponywa.

Baada ya Petro kufanya muujiza, kwa unyenyekevu alielekeza sifa kwa Yehova na Yesu. Sisi pia tunaweza kuonyesha unyenyekevu kwa kutenda mema, bila kutarajia kutambuliwa au kuthawabishwa (Tazama fungu la 11-12)


12. Kama Petro, tunawezaje kuendelea kusitawisha sifa ya unyenyekevu?

12 Tunaweza kuiga mfano wa Petro kwa kusitawisha unyenyekevu. Kumbuka kwamba unyenyekevu wa kweli unahusisha mengi zaidi ya mambo tunayosema. Neno alilotumia Petro, linalotafsiriwa unyenyekevu, linahusisha mawazo yetu ya ndani kabisa, yaani, “unyenyekevu wa akili.” Tunafanya mambo kwa ajili ya wengine kwa sababu tunampenda Yehova na tunawapenda watu, na si kwa sababu tunapenda kusifiwa. Tutaonyesha kwamba sisi ni wanyenyekevu, ikiwa kwa furaha tunamtumikia Yehova na ndugu zetu kadiri tuwezavyo, iwe wengine wanaona jitihada zetu au la.—Mt. 6:​1-4.

IWENI NA “UTIMAMU WA AKILI”

13. Fafanua maana ya kuwa na “utimamu wa akili.”

13 Kuwa na “utimamu wa akili” kunahusisha nini? (1 Pet. 4:7) Mkristo aliye na utimamu wa akili anajitahidi kadiri awezavyo kufanya maamuzi mazuri yanayopatana na njia ya Yehova ya kufikiri. Mkristo huyo anajua kwamba hakuna jambo muhimu zaidi maishani kuliko uhusiano wake na Yehova. Ana maoni yaliyosawazika kujihusu, akijua kwamba hajui kila kitu. Na anaonyesha kwamba anamtegemea Yehova kwa kusali kwake mara nyingi kwa unyenyekevu.b

14. Pindi moja Petro alishindwaje kumtegemea Yehova?

14 Usiku wa mwisho kabla ya kifo chake, Yesu aliwaonya wanafunzi wake hivi: “Ninyi nyote mtakwazika kuhusiana nami usiku wa leo.” Petro alijibu hivi kwa uhakika: “Hata wengine wote wakikwazika kuhusiana nawe, mimi sitakwazika kamwe!” Usiku huo, Yesu aliwahimiza hivi baadhi ya wanafunzi wake: “Endeleeni kukesha na kusali bila kuacha.” (Mt. 26:​31, 33, 41) Ikiwa Petro angefuata ushauri huo mapema, huenda angekuwa na ujasiri wa kujitambulisha kwamba alikuwa mfuasi wa Yesu. Badala yake, Petro alimkana Bwana wake, na alijutia sana jambo hilo.—Mt. 26:​69-75.

15. Yesu alionyeshaje utimamu wa akili usiku wake wa mwisho akiwa mwanadamu?

15 Yesu alimtegemea kikamili Yehova. Ingawa Yesu alikuwa mkamilifu, alisali tena na tena. Hilo lilimpa ujasiri wa kutenda kulingana na mapenzi ya Yehova kumwelekea. (Mt. 26:​39, 42, 44; Yoh. 18:​4, 5) Bila shaka, Petro hakusahau kamwe kwamba Yesu alisali mara nyingi katika usiku wake wa mwisho.

16. Petro alionyeshaje kwamba alikuwa amesitawisha utimamu wa akili? (1 Petro 4:7)

16 Mwishowe, Petro alijifunza kumtegemea Yehova zaidi katika sala. Yesu aliyefufuliwa alimhakikishia Petro na mitume wengine kwamba wangepokea roho takatifu ili waweze kutimiza mgawo wao wa kuhubiri. Hata hivyo, Yesu aliwaambia wasubiri Yerusalemu hadi hilo litakapotokea. (Luka 24:49; Mdo. 1:​4, 5) Petro alifanya nini alipokuwa akisubiri? Petro na Wakristo wenzake “walidumu katika sala.” (Mdo. 1:​13, 14) Baadaye, katika barua yake ya kwanza, Petro aliwatia moyo Wakristo wenzake wawe na utimamu wa akili na wamtegemee Yehova katika sala. (Soma 1 Petro 4:7.) Petro alijifunza kumtegemea Yehova na akawa nguzo katika kutaniko.—Gal. 2:9.

17. Licha ya vipawa vyovyote ambavyo huenda tunavyo, tunapaswa kuendelea kufanya nini? (Tazama pia picha.)

17 Ili kuwa na utimamu wa akili, tunapaswa kusali kwa Yehova mara nyingi. Tunatambua kwamba tunapaswa kuendelea kusali kwa Yehova licha ya vipawa vyovyote ambavyo huenda tunavyo. Hivyo, tunapohitaji kufanya maamuzi muhimu maishani, tunasali kwa Yehova ili atupatie mwongozo, tukiwa na uhakika kwamba anajua kilicho bora.

Petro alijifunza kumtegemea Yehova katika sala. Sisi pia tunaweza kuwa na utimamu wa akili kwa kuomba msaada wa Yehova katika sala, hasa tunapohitaji kufanya maamuzi muhimu maishani (Tazama fungu la 17)c


18. Tunawezaje kupatanisha hata zaidi njia yetu ya kufikiri na njia ya Yehova ya kufikiri?

18 Tunashukuru sana kwamba Yehova ametuumba kwa njia ambayo tunaweza kuiga sifa zake. (Mwa. 1:26) Bila shaka, hatuwezi kumwiga Yehova kikamilifu. (Isa. 55:9) Hata hivyo, kama Petro, tunaweza kupatanisha hata zaidi njia yetu ya kufikiri na ile ya Yehova. Acheni tufanye hivyo kwa kuendelea kuiga njia ya Mungu ya kufikiri, kuwa wanyenyekevu, na kuwa na utimamu wa akili.

TUNAWEZAJE . . .

  • kuiga njia ya Yehova ya kufikiri?

  • kuwa wanyenyekevu?

  • kuwa na “utimamu wa akili”?

WIMBO 30 Baba Yangu, Mungu Wangu, Rafiki Yangu

a ‘Mwelekeo wa akili,’ unaotajwa katika 1 Petro 4:​1, unaweza pia kumaanisha “mtazamo, njia ya kufikiri.”

b Kwa habari zaidi kuhusu kinachomaanishwa na utimamu wa akili, tazama makala katika mfululizo wa “Mistari ya Biblia Yafafanuliwa” yenye kichwa “2 Timotheo 1:7—‘Mungu Hakutupa Roho ya Woga,’” chini ya sehemu, “Utimamu wa akili,” kwenye JW Library® au katika jw.org.

c MAELEZO YA PICHA: Dada akitoa sala kimyakimya kabla ya mahojiano ya kazi.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki