Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w25 Machi kur. 20-25
  • Endelea Kutembea kwa Imani

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Endelea Kutembea kwa Imani
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2025
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • TUNAPOTAFUTA KAZI
  • TUNAPOTAFUTA MWENZI WA NDOA
  • TUNAPOPOKEA MWONGOZO WA KITHEOKRASI
  • Maamuzi Yanayoonyesha Unamtegemea Yehova
    Daftari la Mkutano wa Huduma na Maisha Yetu ya Kikristo—2023
  • Uwe Mwenye Kiasi Inapohusu Mambo Usiyoyajua
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2025
  • Jinsi ya Kushinda Shaka
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2024
  • Fanya Maamuzi Yanayomfurahisha Yehova
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2025
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2025
w25 Machi kur. 20-25

MAKALA YA 12

WIMBO 119 Lazima Tuwe na Imani

Endelea Kutembea kwa Imani

“Tunatembea kwa imani, si kwa kuona.”—2 KOR. 5:7.

JAMBO KUU

Jinsi ya kuendelea kutembea kwa imani tunapofanya maamuzi muhimu.

1. Kwa nini mtume Paulo angeweza kuwa na hisia za kuridhika alipokumbuka maisha yake?

PINDI moja, mtume Paulo alijua kwamba baada ya muda mfupi angeuawa, lakini alikuwa na kila sababu ya kuwa na hisia za kuridhika alipokumbuka maisha yake. Alisema hivi: “Nimekimbia mbio mpaka mwisho, nimeishika imani.” (2 Tim. 4:​6-8) Paulo alikuwa amefanya maamuzi ya hekima kuhusu huduma yake ya Kikristo, na alikuwa na uhakika kwamba Yehova alipendezwa naye. Sisi pia tungependa kufanya maamuzi mazuri na kukubaliwa na Mungu. Tunawezaje kufanya hivyo?

2. Kutembea kwa imani kunamaanisha nini?

2 Paulo alisema hivi kujihusu na kuhusu Wakristo wengine waaminifu: “Tunatembea kwa imani, si kwa kuona.” (2 Kor. 5:7) Paulo alimaanisha nini? Katika Biblia, mara nyingine neno ‘kutembea’ humaanisha njia ya maisha ambayo mtu anachagua. Mtu anapotembea kwa kuona tu, anafanya maamuzi yanayotegemea tu mambo anayoweza kuona, kusikia, na kuhisi. Kwa upande mwingine, mtu anapotembea kwa imani, anafanya maamuzi yanayotegemea uhakika wake katika Yehova Mungu. Matendo yake yanaonyesha ana uhakika kwamba Mungu atamthawabisha, na atanufaika kwa kufuata ushauri unaopatikana katika Neno Lake.—Zab. 119:66; Ebr. 11:6.

3. Tunapata manufaa gani kwa kutembea kwa imani? (2 Wakorintho 4:18)

3 Kwa kweli, sisi sote hufanya maamuzi yanayotegemea mambo tunayoona, kusikia, na kuhisi. Hata hivyo, huenda tukakabili matatizo ikiwa tutafanya maamuzi muhimu kwa kutegemea tu mambo tunayoona au kusikia. Kwa nini? Nyakati nyingine, mambo tunayoona au kusikia huenda yakatupotosha. Na hata ikiwa hayatatupotosha, tukitembea tu kwa kuona, huenda tukapuuza mapenzi ya Mungu au ushauri wake. (Mhu. 11:9; Mt. 24:​37-39) Hata hivyo, tunapotembea kwa imani, tutafanya maamuzi ‘yanayokubalika kwa Bwana.’ (Efe. 5:10) Kufuata ushauri wa Mungu kutatupatia amani ya moyoni na furaha ya kweli. (Zab. 16:​8, 9; Isa. 48:​17, 18) Na tukiendelea kutembea kwa imani, tutakuwa na tumaini la kuishi milele.—Soma 2 Wakorintho 4:18.

4. Mtu anaweza kutambuaje ikiwa anatembea kwa imani au kwa kuona?

4 Tunaweza kutambuaje ikiwa tunatembea kwa imani au kwa kuona? Maswali yafuatayo yanaweza kutusaidia: Ni mambo gani yanayoongoza maamuzi yetu? Je, tunaongozwa tu na mambo tunayoweza kuona? Au je, tunaongozwa na ushauri unaotoka kwa Yehova? Acheni tuchunguze jinsi tunavyoweza kuendelea kutembea kwa imani katika mambo haya muhimu: tunapotafuta kazi, tunapotafuta mwenzi wa ndoa, na tunapopokea mwongozo wa kitheokrasi. Katika kila hali, tutazungumzia mambo tunayopaswa kufikiria ili kufanya maamuzi yanayofaa.

TUNAPOTAFUTA KAZI

5. Tunapaswa kufikiria mambo gani tunapotafuta kazi?

5 Sisi sote tungependa kuwa na uwezo wa kushughulikia mahitaji yetu na ya familia yetu. (Mhu. 7:12; 1 Tim. 5:8) Baadhi ya kazi zina mshahara mkubwa. Huenda zikamsaidia mfanyakazi kutimiza mahitaji yake ya kila siku na kuweka akiba ya pesa kwa ajili ya wakati ujao. Lakini huenda kazi nyingine zina mshahara mdogo unaomwezesha mfanyakazi kutimiza mahitaji muhimu tu ya familia yake. Tunapochagua aina ya kazi tutakayofanya, inaeleweka kwamba tutafikiria pia kuhusu mshahara tutakaopata. Hata hivyo, mtu atakuwa anatembea kwa kuona, ikiwa uamuzi wake unategemea jambo hilo tu.

6. Tunawezaje kutembea kwa imani tunapotafuta kazi? (Waebrania 13:5)

6 Ikiwa tunatembea kwa imani, tutafikiria pia jinsi kazi tutakayofanya itakavyoathiri urafiki wetu na Yehova. Tunaweza kujiuliza hivi: ‘Je, kazi hiyo itahusisha mambo ambayo Yehova anachukia?’ (Met. 6:​16-19) ‘Je, nitakosa mikutano na sitakuwa na muda wa kutosha kwa ajili ya kuhubiri na kujifunza Biblia, na nitakuwa mbali na familia yangu kwa muda mrefu?’ (Flp. 1:10) Ikiwa umejibu ndiyo katika maswali hayo, litakuwa jambo la hekima kukataa kazi hiyo hata ikiwa ni vigumu kupata kazi. Kwa kuwa tunatembea kwa imani, tunafanya maamuzi yanayoonyesha tuna uhakika kwamba kwa njia fulani Yehova atatimiza mahitaji yetu.—Mt. 6:33; soma Waebrania 13:5.

7-8. Ndugu mmoja katika bara la Amerika Kusini alitembeaje kwa imani? (Tazama pia picha.)

7 Ona jinsi Javier,a ndugu kutoka Amerika Kusini, alivyotambua umuhimu wa kutembea kwa imani. Anasema hivi: “Nilituma maombi ya kupata kazi nzuri ambayo mshahara wake ni mara mbili ya mshahara ninaopata sasa na ambayo ningefurahia sana kuifanya.” Hata hivyo, Javier alitamani sana kufanya upainia. Anaongezea hivi: “Niliitwa kwa ajili ya mahojiano ya kazi na meneja wa kitaifa. Kabla ya mahojiano hayo, nilisali kwa Yehova ili anisaidie, nikiwa na uhakika kwamba Yehova anajua kilicho bora kwa ajili yangu. Nilitaka kuongezewa majukumu na kulipwa pesa nyingi zaidi, lakini sikutaka kukubali kazi hiyo ikiwa ingenizuia kufikia malengo yangu ya kiroho.”

8 Javier anaeleza hivi: “Wakati wa mahojiano ya kazi, meneja aliniambia kwamba mara kwa mara ningelazimika kufanya kazi muda wa ziada. Kwa fadhili, nilimweleza kwamba nisingeweza kukubali kazi hiyo kwa sababu ingeathiri huduma yangu.” Ndiyo, Javier alikataa kazi hiyo. Baada ya majuma mawili, alianza upainia. Na baadaye mwaka huo, akapata kazi ya muda. Anasema hivi: “Yehova alisikia sala zangu na akaniwezesha kupata kazi iliyoniruhusu kufanya upainia. Ninafurahi sana kupata kazi ambayo inaniruhusu kutumia wakati mwingi kumtumikia Yehova na ndugu zangu.”

Ndugu akiwa ameshika kofia ngumu na amevalia nguo za kazi anapelekwa na msimamizi wake wa kazi kwenye ofisi isiyo na mtu. Msimamizi huyo wa kazi anataka kumpandisha cheo.

Ikiwa utapandishwa cheo kazini, je, uamuzi wako utaonyesha una uhakika kwamba Yehova anajua kilicho bora kwa ajili yako? (Tazama fungu la 7-8)


9. Unajifunza nini kutokana na kisa cha Trésor?

9 Namna gani ikiwa tunatambua kwamba kazi tunayofanya inatuzuia kutembea kwa imani? Fikiria kisa cha Ndugu Trésor, kutoka Kongo. Anasema hivi: “Niliipenda sana kazi mpya niliyokuwa nimeipata. Mshahara wangu ulikuwa mara tatu ya ule niliokuwa nikipata katika kazi yangu ya awali, na niliheshimiwa sana.” Hata hivyo, Trésor alikosa mikutano kwa ukawaida kwa sababu ya kufanya kazi muda wa ziada. Pia, alishinikizwa kuficha mazoea yasiyo ya unyoofu yaliyoendelea kazini. Trésor alitaka kuacha kazi hiyo, lakini alikuwa na wasiwasi kwamba hangepata kazi nyingine. Ni nini kilichomsaidia? Anasema hivi: “Habakuki 3:​17-19 ilinisaidia kuelewa kwamba hata kama ningepoteza kazi hiyo, Yehova angenitunza kwa njia fulani. Hivyo, nikaacha kazi.” Anamalizia kwa kusema hivi: “Waajiri wengi wanafikiri kwamba mtu akipata kazi yenye mshahara mzuri, atakuwa tayari kudhabihu jambo lolote, kutia ndani familia na utendaji wa kiroho. Ninafurahi kwamba nililinda uhusiano wangu pamoja na Yehova na familia yangu. Mwaka mmoja baadaye, Yehova alinisaidia kupata kazi inayotegemeka ambayo inanisaidia kutimiza mahitaji yangu na kuwa na muda mwingi zaidi kwa ajili ya utendaji wa Kikristo. Tunapomtanguliza Yehova maishani, huenda tukakabili changamoto za kiuchumi kwa muda fulani, lakini Yehova atatutunza.” Naam, ikiwa tutategemea ushauri wa Yehova na ahadi zake, tutaendelea kutembea kwa imani na atatubariki.

TUNAPOTAFUTA MWENZI WA NDOA

10. Ni nini kinachoweza kutufanya tutembee kwa kuona tunapotafuta mwenzi wa ndoa?

10 Ndoa ni zawadi kutoka kwa Yehova, na ni jambo la kawaida kutaka kufunga ndoa. Dada anapotafakari kuhusu mwenzi wa ndoa atakayemfaa, huenda akafikiria utu wa ndugu huyo, mwonekano, sifa yake, hali yake ya kiuchumi, majukumu yake ya kifamilia, pamoja na jinsi anavyomfanya ahisi.b Mambo hayo ni muhimu. Hata hivyo, ikiwa atakazia fikira mambo hayo tu, atakuwa anatembea kwa kuona.

11. Tunawezaje kutembea kwa imani tunapotafuta mwenzi wa ndoa? (1 Wakorintho 7:39)

11 Yehova anajivunia sana anapowaona dada na ndugu zetu wakifuata ushauri wake kuhusu kutafuta mwenzi wa ndoa! Kwa mfano, wanazingatia shauri la kusubiri mpaka watakapopita “upeo wa ujana” ndipo waanze kufikiria kufunga ndoa. (1 Kor. 7:36) Wanapotafuta mwenzi wa ndoa anayefaa, wanahakikisha kwamba anatimiza hasa sifa ambazo Yehova anasema zinamfanya mtu awe mume au mke anayefaa. (Met. 31:​10-13, 26-28; Efe. 5:33; 1 Tim. 5:8) Ikiwa mtu ambaye si Shahidi anapendezwa nao kimahaba, wanatii shauri la kuoa au kuolewa “katika Bwana tu,” linalopatikana kwenye 1 Wakorintho 7:39. (Soma.) Wanaendelea kutembea kwa imani, wakiwa na uhakika kwamba Yehova anaweza kuwatunza kihisia kuliko mtu mwingine yeyote.—Zab. 55:22.

12. Unajifunza nini kutokana na mfano wa Rosa?

12 Fikiria kisa cha Rosa, painia nchini Kolombia. Kazi yake ilimfanya aonane mara kwa mara na mwanamume mmoja ambaye hakuwa Shahidi, na aliyeanza kuvutiwa naye. Rosa pia alivutiwa naye. Anasema hivi: “Alionekana kuwa mwanamume mzuri sana. Aliwasaidia watu katika eneo aliloishi na alikuwa na mazoea mazuri. Nilipendezwa na jinsi alivyonitendea. Alikuwa na sifa ambazo nilitamani mume nitakayempata awe nazo, hata hivyo hakuwa Shahidi.” Anaongezea hivi: “Ilikuwa vigumu sana kumkataa kwa sababu hisia zangu zilihusika. Wakati huo, nilihisi upweke na nilitamani kufunga ndoa, lakini sikuwa nimepata mtu katika kweli.” Hata hivyo, Rosa hakukazia tu fikira mambo ambayo anaweza kuona. Alitafakari kuhusu jinsi ambavyo uamuzi huo ungeathiri urafiki wake na Yehova. Hivyo, akasitisha mawasiliano yote na mwanamume huyo na kuwa na mengi ya kufanya katika utendaji wa kitheokrasi. Muda mfupi baadaye, Rosa alialikwa kuhudhuria Shule ya Waeneza-Injili wa Ufalme, na sasa anatumikia akiwa painia wa pekee. Rosa anasema hivi: “Yehova amenifanya niwe mwenye furaha sana.” Ingawa huenda isiwe rahisi kutembea kwa imani katika mambo yanayohusisha hisia, sikuzote jitihada hizo si za bure.

TUNAPOPOKEA MWONGOZO WA KITHEOKRASI

13. Ni nini kinachoweza kutufanya tutembee kwa kuona tunapopokea mwongozo wa kitheokrasi?

13 Mara nyingi tunapokea mwongozo wa kitheokrasi—kutoka kwa wazee wa kutaniko, mwangalizi wa mzunguko, ofisi ya tawi, au Baraza Linaloongoza—unaotusaidia kumwabudu Yehova. Lakini namna gani ikiwa pindi fulani hatuelewi kwa nini mwongozo fulani umetolewa? Huenda tukaona tu jinsi ambavyo mwongozo huo utafanya hali zetu ziwe ngumu zaidi. Huenda hata tukaanza kukazia fikira udhaifu wa ndugu ambao wametoa mwongozo huo.

14. Ni nini kitakachotusaidia kutembea kwa imani tunapopokea mwongozo wa kitheokrasi? (Waebrania 13:17)

14 Tunapotembea kwa imani, tunatumaini kwamba Yehova anaongoza mambo na anaelewa hali zetu. Matokeo ni kwamba tunakuwa wepesi kutii, na tunafanya hivyo tukiwa na mtazamo unaofaa. (Soma Waebrania 13:17.) Tunatambua kwamba utii wetu unachangia umoja katika kutaniko letu. (Efe. 4:​2, 3) Tuna uhakika kwamba ingawa ndugu wanaoongoza mambo si wakamilifu, Yehova atatubariki tunapotii. (1 Sam. 15:22) Kwa wakati unaofaa, atarekebisha jambo lolote ambalo kwa kweli linahitaji kurekebishwa.—Mika 7:7.

15-16. Ni nini kilichomsaidia ndugu mmoja kutembea kwa imani ingawa alikuwa na shaka kuhusu mwongozo aliopewa? (Tazama pia picha.)

15 Fikiria kisa kinachoonyesha manufaa ya kutembea kwa imani. Ingawa nchini Peru Kihispania huzungumzwa na watu wengi, wenye nyumba wengi huzungumza lugha za kienyeji. Mojawapo ya lugha hizo ni Kikwechua. Kwa miaka mingi, ndugu na dada wanaozungumza Kikwechua waliwatafuta watu wanaozungumza lugha hiyo katika eneo lao. Hata hivyo, ili kutii sheria za serikali, marekebisho yalifanywa ya jinsi ya kuwapata watu. (Rom. 13:1) Matokeo ni kwamba baadhi ya wahubiri walijiuliza ikiwa mwongozo huo ungefanya iwe vigumu kuhubiri katika eneo hilo. Kwa kuwa akina ndugu walitii miongozo hiyo, Yehova alibariki jitihada zao za kuwapata watu wengi wanaozungumza Kikwechua.

16 Kevin, mzee katika kutaniko la Kikwechua, alikuwa miongoni mwa wale waliokuwa na wasiwasi. Anaeleza hivi: “Niliwaza, ‘Sasa tutawapataje watu wanaozungumza Kikwechua?’” Kevin alifanya nini? Anasema hivi: “Nilitafakari kuhusu Methali 3:5. Na nilimfikiria Musa. Alipaswa kuwaongoza Waisraeli kutoka Misri na kuelekea kwenye njia ambayo ilionekana hawangeweza kuponyoka, na hivyo ingekuwa rahisi kukamatwa na Wamisri waliokuwa wakiwafuatia. Hata hivyo, alitii, na Yehova alibariki utii wake kwa njia ya pekee.” (Kut. 14:​1, 2, 9-11, 21, 22) Kevin alikuwa tayari kubadili njia yake ya kuhubiri. Matokeo yalikuwaje? Anasema hivi: “Nilishangazwa na jinsi ambavyo Yehova alitubariki. Awali, tungetembea kwa muda mrefu katika huduma na mara nyingine tungempata mtu mmoja au wawili wanaoongea Kikwechua. Sasa tunakazia fikira maeneo ambayo yana watu wengi wanaozungumza Kikwechua. Matokeo ni kwamba tunazungumza na watu wengi zaidi, tunawarudia watu wengi, na tunawafundisha watu wengi Biblia. Watu wengi zaidi wanahudhuria mikutano.” Naam, tunapotembea kwa imani, sikuzote Yehova anatuthawabisha.

Mwanamume anayezungumza Kikwechua akizungumza na wenzi wa ndoa Mashahidi ambao wako katika huduma. Anawaonyesha nyumba ya mtu fulani.

Akina ndugu walitambua kwamba watu wengi waliokutana nao waliweza kuwaonyesha maeneo ambayo wangeweza kupata watu waliozungumza Kikwechua (Tazama fungu la 15-16)


17. Umejifunza nini katika makala hii?

17 Tumechunguza jinsi ya kuendelea kutembea kwa imani katika hali tatu. Hata hivyo, tunapaswa kuendelea kutembea kwa imani katika nyanja zote za maisha yetu, kama vile burudani au tafrija, na tunapofanya maamuzi kuhusu elimu au malezi ya watoto wetu. Tunapofanya uamuzi wowote, tunapaswa kuongozwa, si tu na mambo tunayoona, bali pia tunapaswa kuzingatia uhusiano wetu na Yehova, ushauri wake, na ahadi yake kwamba atatutunza. Ikiwa tutafanya hivyo, “tutatembea katika jina la Yehova Mungu wetu milele na milele.”—Mika 4:5.

TUNAWEZAJE KUTEMBEA KWA IMANI . . .

  • tunapotafuta kazi?

  • tunapotafuta mwenzi wa ndoa?

  • tunapopokea mwongozo wa Kitheokrasi?

WIMBO 156 Kwa Imani

a Baadhi ya majina yamebadilishwa.

b Ingawa fungu hili linazungumzia dada anayetafuta mume, ushauri huohuo unaweza kutumiwa na ndugu anayetafuta mke.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki