MAKALA YA 16
WIMBO 87 Njooni! Mburudishwe
Kusitawisha Urafiki wa Karibu na Waabudu Wenzetu Ni Jambo Jema Kwetu!
“Tazama! Jinsi ilivyo vema na jinsi inavyopendeza ndugu kukaa pamoja kwa umoja!”—ZAB. 133:1.
JAMBO KUU
Mapendekezo ya jinsi ya kuwa na urafiki wa karibu zaidi na waabudu wenzetu na baraka tunazopata kutokana na urafiki huo.
1-2. Ni jambo gani lililo muhimu kwa Yehova, na anataka tufanye nini?
JINSI tunavyowatendea wanadamu wenzetu ni jambo muhimu sana kwa Yehova. Yesu alifundisha kwamba ni lazima tumpende jirani yetu kama tunavyojipenda mwenyewe. (Mt. 22:37-39) Hilo linatia ndani kuwaonyesha fadhili hata wale ambao si waabudu wenzetu. Tunapofanya hivyo, tunamwiga Yehova, ambaye “huwaangazia jua lake waovu na wema, na hunyesha mvua juu ya waadilifu na wasio waadilifu.”—Mt. 5:45.
2 Ingawa Yehova anawapenda wanadamu wote, anawapenda hasa wale wanaotenda yaliyo sawa. (Yoh. 14:21) Anataka tumwige. Anatuhimiza ‘tuwapende sana’ ndugu na dada zetu na tuwaonyeshe “upendo mwororo.” (1 Pet. 4:8; Rom. 12:10) Upendo huo unafanana na ule tunaohisi kumwelekea mtu wa ukoo tunayempenda au rafiki mpendwa.
3. Tunapaswa kukumbuka nini kuhusu upendo?
3 Upendo ni kama mmea unaohitaji kutunzwa ili ukue. Mtume Paulo aliwashauri hivi Wakristo: “Upendo wenu wa kindugu na uendelee.” (Ebr. 13:1) Yehova anataka tuendelee kusitawisha upendo wetu kwa wengine. Katika makala hii, tutazungumzia kwa nini tunapaswa kusitawisha urafiki wa karibu zaidi na waabudu wenzetu na jinsi tunavyoweza kuendelea kufanya hivyo.
KWA NINI TUNAPASWA KUSITAWISHA URAFIKI WA KARIBU ZAIDI NA WAABUDU WENZETU?
4. Kulingana na Zaburi 133:1, tunawezaje kuendelea kuthamini undugu wetu wenye umoja? (Tazama pia picha.)
4 Soma Zaburi 133:1. Tunakubaliana na mtunga zaburi aliyeandika kwamba urafiki wa kweli na wale wanaompenda Yehova ni jambo ‘jema’ na ‘linalopendeza.’ Kama tu ambavyo mtu anaweza kutokazia fikira uzuri wa mti mkubwa anaouona kila siku, tunaweza kuchukulia kivivi hivi uzuri wa umoja wetu wa Kikristo. Tunaonana na ndugu na dada zetu mara nyingi, huenda mara kadhaa katika juma. Tunawezaje kuendelea kuwathamini? Upendo wetu kwa ndugu na dada zetu utakua ikiwa tutatumia wakati kufikiria jinsi kila mmoja wao alivyo mwenye thamani kutanikoni na kwetu pia.
Kamwe tusichukulie kivivi hivi uzuri wa umoja wetu wa Kikristo (Tazama fungu la 4)
5. Undugu wetu wenye upendo unaweza kuwa na matokeo gani kwa wengine?
5 Baadhi ya watu ambao wamehudhuria mkutano kwa mara ya kwanza, wameguswa moyo sana na upendo tunaoonyesha miongoni mwetu. Kwa msingi huo pekee, huenda wakafikia mkataa kwamba wameipata kweli. Yesu alisema hivi: “Kwa jambo hili wote watajua kwamba ninyi ni wanafunzi wangu—mkiwa na upendo miongoni mwenu.” (Yoh. 13:35) Fikiria mfano wa Chaithra, mwanafunzi wa chuo kikuu aliyekuwa anajifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova. Alikubali mwaliko wa kuhudhuria kusanyiko la eneo. Baada ya kuhudhuria siku ya kwanza, alimwambia hivi mwalimu wake wa Biblia: “Sijawahi kukumbatiwa na wazazi wangu. Lakini katika kusanyiko lenu, nimekumbatiwa mara 52 ndani ya siku moja! Nimehisi upendo wa Yehova kupitia familia hii ya kiroho. Ninataka kuwa sehemu ya familia hii.” Chaithra alifanya maendeleo na kubatizwa mwaka wa 2024. Naam, wapya wanapoona matendo yetu mema, kutia ndani upendo tulio nao miongoni mwetu, mara nyingi wanachochewa kumtumikia Yehova.—Mt. 5:16.
6. Kusitawisha urafiki wa karibu zaidi pamoja na ndugu na dada zetu kunawezaje kutulinda?
6 Kusitawisha urafiki wa karibu zaidi pamoja na ndugu na dada zetu kunaweza kutulinda. Paulo aliwahimiza Wakristo wenzake hivi: “Endeleeni kutiana moyo kila siku . . . ili yeyote kati yenu asifanywe kuwa mgumu kwa nguvu za udanganyifu za dhambi.” (Ebr. 3:13) Ikiwa tutavunjika moyo sana hivi kwamba miguu yetu ianze kukengeuka kutoka katika njia ya uadilifu, Yehova anaweza kumchochea mwabudu mwenzetu aliyetambua jambo hilo atupatie msaada tunaohitaji. (Zab. 73:2, 17, 23) Kwa kweli, msaada wa aina hiyo ni jambo jema kwetu.
7. Kuna uhusiano gani kati ya upendo na umoja? (Wakolosai 3:13, 14)
7 Sisi ni sehemu ya kikundi cha watu wanaojitahidi sana kuonyesha upendo, hivyo tunafurahia baraka nyingi. (1 Yoh. 4:11) Kwa mfano, upendo unatuchochea ‘kuendelea kuvumiliana,’ jambo ambalo linachangia umoja wetu wa Kikristo. (Soma Wakolosai 3:13, 14; Efe. 4:2-6) Hivyo, katika mikutano yetu, tunafurahia mazingira yenye kustarehesha ambayo hayapatikani katika kikundi kingine chochote duniani.
ONYESHANENI HESHIMA
8. Yehova anatusaidiaje tuwe na umoja miongoni mwetu?
8 Umoja wa ulimwenguni pote tunaofurahia ni muujiza. Yehova anafanya umoja huo uwezekane licha ya kwamba sisi si wakamilifu. (1 Kor. 12:25) Biblia inasema kwamba ‘tunafundishwa na Mungu kupendana.’ (1 The. 4:9) Kwa maneno mengine, Yehova anatueleza kihususa katika Maandiko mambo tunayohitaji kufanya ili tuwe na urafiki wa karibu zaidi na waabudu wenzetu. Tunaweza ‘kufundishwa na Mungu’ kwa kuchunguza kwa makini mafundisho yake na kuyatumia maishani. (Ebr. 4:12; Yak. 1:25) Na hilo ndilo jambo ambalo Mashahidi wa Yehova wanajitahidi kufanya.
9. Tunajifunza nini katika Waroma 12:9-13 kuhusu kuonyeshana heshima?
9 Neno la Mungu linatufundishaje kusitawisha urafiki wa karibu zaidi na waabudu wenzetu? Fikiria kile ambacho Paulo alisema kuhusu jambo hilo, kama inavyoonyeshwa kwenye Waroma 12:9-13. (Soma.) Ona kwamba alisema, “katika kuonyeshana heshima, iweni wa kwanza.” Hilo linamaanisha nini? Linamaanisha kwamba tunapaswa kuchukua hatua ya kwanza kuwaonyesha wengine “upendo mwororo” kwa kuwasamehe, kuwa wakaribishaji wageni, kuwa wakarimu, na kadhalika. (Efe. 4:32) Huhitaji kusubiri hadi ndugu au dada yako achukue hatua ya kwanza ili kusitawisha urafiki wa karibu zaidi pamoja nawe. Unaweza ‘kuwa wa kwanza’ kufanya hivyo. Yesu alisema hivi: “Kuna furaha zaidi katika kutoa kuliko ilivyo katika kupokea.”—Mdo. 20:35.
10. Tunawezaje kuwa wenye bidii “katika kuonyeshana heshima”? (Tazama pia picha.)
10 Kwa kupendeza, mara tu baada ya kutuambia tuwe wa kwanza katika kuonyeshana heshima, Paulo anatuhimiza ‘tuwe wenye bidii, tusiwe wavivu.’ Mtu mwenye sifa hiyo anapopewa kazi, anaifanya kwa bidii. Methali 3:27, 28 inatuhimiza hivi: “Usiwanyime mema wale unaopaswa kuwatendea mema ikiwa una uwezo wa kuwasaidia.” Hivyo, tunapoona mtu mwenye uhitaji, tunajitahidi kadiri tuwezavyo kumsaidia. Hatuahirishi mambo; wala kufikiri kwamba mtu mwingine atashughulikia hali hiyo.—1 Yoh. 3:17, 18.
Tunapaswa kuchukua hatua ya kwanza kuwasaidia ndugu na dada zetu wenye uhitaji (Tazama fungu la 10)
11. Ni jambo gani linaloweza kutusaidia kusitawisha urafiki wa karibu zaidi na waabudu wenzetu?
11 Njia nyingine tunayoweza kuwaonyesha wengine heshima ni kwa kuwasamehe mara tu wanapotukosea. Waefeso 4:26 inasema: “Jua lisitue mkiwa bado mmekasirika.” Kwa nini? Mstari wa 27 unasema kwamba kufanya hivyo ‘kutampa Ibilisi nafasi.’ Katika Neno lake, Yehova anatuambia tena na tena tusameheane. Wakolosai 3:13 inatuhimiza ‘tuendelee kusameheana kwa hiari.’ Kuwasamehe wengine makosa yao, ni mojawapo ya njia bora zaidi za kusitawisha urafiki wa karibu zaidi na waabudu wenzetu. Tunapofanya hivyo, “[tunadumisha] roho ya umoja katika kifungo cha muungano cha amani.” (Efe. 4:3) Kwa ufupi, kuwasamehe wengine kunaweza kuchangia moja kwa moja amani na umoja wetu.
12. Yehova anatusaidiaje kuwa wenye kusamehe?
12 Ni kweli kwamba huenda ikawa vigumu kwetu kuwasamehe wale waliotuumiza. Lakini tunaweza kufanikiwa kwa msaada wa roho ya Mungu. Baada ya kutuhimiza tuwe na “upendo mwororo kwa mtu na mwenzake” na ‘tuwe wenye bidii,’ Biblia inatuambia hivi: “Wakeni roho.” Mtu ‘anayewaka roho’ ana bidii na shauku inayotokana na roho takatifu. (Rom. 12:11) Hivyo, roho ya Mungu inaweza kutusaidia kuonyesha upendo mwororo na kusameheana kwa hiari. Kwa sababu hiyo, tunamsihi Yehova kwa bidii ili atusaidie.—Luka 11:13.
“KUSIWE NA MIGAWANYIKO KATI YENU”
13. Ni mambo gani yanayoweza kusababisha migawanyiko kati yetu?
13 Kutaniko limefanyizwa na “watu wa namna zote” kutoka katika malezi mbalimbali. (1 Tim. 2:3, 4) Tusipokuwa waangalifu, hilo linaweza kusababisha migawanyiko inapohusu mambo ya kibinafsi kama vile, mavazi na mapambo, matibabu, au burudani. (Rom. 14:4; 1 Kor. 1:10) Kwa sababu tumefundishwa na Mungu kupendana, ni lazima tuwe waangalifu ili tusisisitize kwamba mapendezi yetu ya kibinafsi ni mazuri zaidi kuliko ya wengine.—Flp. 2:3.
14. Tunapaswa kujitahidi kufanya nini, na kwa nini?
14 Pia, tunaweza kuzuia migawanyiko katika kutaniko kwa kujitahidi kuwa wenye kuburudisha na kuwajenga wengine nyakati zote. (1 The. 5:11) Katika siku za karibuni, wahubiri wengi ambao waliacha kutenda au walioondolewa kutanikoni, wamerudi. Tunawakaribisha kwa uchangamfu! (2 Kor. 2:8) Ona kile alichosema dada mmoja aliyeanza kuhudhuria mikutano tena baada ya kuacha kutenda kwa miaka kumi. Alisema hivi: “Kila mtu alitabasamu na kunishika mkono aliponisalimu.” (Mdo. 3:19) Matendo hayo ya fadhili yalimchocheaje? Anasema hivi: “Yalinifanya nihisi kwamba mkono wa Yehova ulikuwa ukiniongoza ili niwe na furaha tena.” Tukijitahidi kuwa wenye kuwajenga wengine, Kristo anaweza kututumia kuwaburudisha ‘wanaotaabika na kulemewa na mizigo.’—Mt. 11:28, 29.
15. Taja njia nyingine tunayoweza kuchangia umoja. (Tazama pia picha.)
15 Njia nyingine tunayoweza kuchangia umoja ni kupitia mambo tunayosema. Ayubu 12:11 inasema hivi: “Je, sikio halipimi maneno kama ulimi unavyoonja chakula?” Kama tu ambavyo mpishi mzuri sikuzote ataonja chakula ili kuhakikisha kwamba kina ladha nzuri kabla ya kuwapa wengine, sisi pia tunapaswa kufikiria kwa makini mambo tutakayosema kabla ya kuyasema. (Zab. 141:3) Sikuzote tunapaswa kuwa na lengo la kuhakikisha kwamba mambo tunayotaka kusema ni yenye kujenga, kuburudisha, na ‘yatawanufaisha wale wanaoyasikia.’—Efe. 4:29.
Fikiria mambo utakayosema kabla ya kuyasema (Tazama fungu la 15)
16. Ni nani hasa wanaopaswa kuwa makini ili kutumia usemi wenye kutia moyo?
16 Waume na wazazi wanapaswa hasa kuwa makini ili kuzungumza kwa njia yenye kujenga. (Kol. 3:19, 21; Tito 2:4) Wazee wa kutaniko pia wanapaswa kuwa chanzo cha faraja na burudisho wakiwa wachungaji wa kundi la Yehova. (Isa. 32:1, 2; Gal. 6:1) Methali moja katika Biblia inatukumbusha hivi: “Neno linalosemwa wakati unaofaa—ni jema sana!”—Met. 15:23.
MPENDANE “KWA TENDO NA KWELI”
17. Tunawezaje kuhakikisha kwamba upendo wetu kwa ndugu na dada zetu unatoka moyoni?
17 Mtume Yohana anatutia moyo “kupendana, si kwa neno au kwa ulimi, bali kwa tendo na kweli.” (1 Yoh. 3:18) Tunataka kuwapenda ndugu na dada zetu kutoka moyoni. Tunawezaje kufanya hivyo? Kadiri tunavyotumia wakati mwingi zaidi na ndugu na dada zetu, ndivyo tutakavyozidi kusitawisha urafiki wa karibu zaidi nao, na ndivyo upendo wetu kuwaelekea utakavyoimarika zaidi. Hivyo, tafuta fursa za kutumia wakati pamoja na wengine, katika mikutano na huduma. Tenga wakati ili uwatembelee wengine. Tunapofanya hivyo, tunaonyesha kwamba ‘tunafundishwa na Mungu kupendana.’ (1 The. 4:9) Na tutaendelea kujionea “jinsi ilivyo vema na jinsi inavyopendeza ndugu kukaa pamoja kwa umoja!”—Zab. 133:1.
WIMBO 90 Tianeni Moyo