MAKALA YA 15
WIMBO 30 Baba Yangu, Mungu Wangu, Rafiki Yangu
“Kumkaribia Mungu Ni Jambo Jema” Kwetu!
“Kwa upande wangu, kumkaribia Mungu ni jambo jema kwangu.”—ZAB. 73:28.
JAMBO KUU
Jinsi tunavyoweza kumkaribia zaidi Yehova na manufaa tutakayopata kwa kufanya hivyo.
1-2. (a) Tunahitaji kufanya jitihada gani ili kusitawisha urafiki wa karibu pamoja na mtu? (b) Tutachunguza nini katika makala hii?
JE, UNA rafiki wa karibu? Ulisitawishaje urafiki wako pamoja naye? Inaelekea ulitumia wakati pamoja naye, ukajua changamoto anazokabili, na ulijua mambo anayopenda na asiyopenda. Ukatambua kwamba ana sifa nzuri sana ambazo ungependa kuiga. Mambo hayo yakakufanya umpende rafiki yako.
2 Kusitawisha urafiki wa karibu pamoja na mtu kunahitaji wakati na jitihada. Ndivyo ilivyo pia na kusitawisha urafiki wa karibu pamoja na Yehova Mungu. Katika makala hii, tutachunguza jinsi tunavyoweza kumkaribia zaidi Mungu wetu na manufaa tunayopata tunapofanya hivyo. Kwanza, tuchunguze kwa nini ni vema kumkaribia Yehova, Rafiki yetu wa karibu zaidi.
3. Kwa nini tunapaswa kutafakari kuhusu manufaa ya kumkaribia Yehova? Toa mfano.
3 Hapana shaka unakubali kwamba kumkaribia Yehova ni jambo jema. Lakini kutafakari kihususa kuhusu jinsi ilivyo vema kufanya hivyo, kunaweza kutuchochea kuendelea kumkaribia zaidi. (Zab. 63:6-8) Kwa mfano, tunajua kwamba kula chakula chenye lishe, kufanya mazoezi, kupumzika vya kutosha, na kunywa maji ya kutosha ni mambo yanayotufaa. Lakini watu wengi hawazingatii mambo hayo, na hawatunzi afya zao. Hata hivyo, kadiri tunavyotafakari jinsi mazoea hayo yanavyotunufaisha kiafya, ndivyo tutakavyokuwa tayari zaidi kudumisha mazoea hayo. Vivyo hivyo, huenda tunajua kwamba kumkaribia Yehova ni jambo jema, lakini tukitafakari kuhusu manufaa ya kufanya hivyo tunaweza kuchochewa kuendelea kumkaribia zaidi Rafiki yetu.—Zab. 119:27-30.
4. Kulingana na Zaburi 73:28, mtunga zaburi alisema nini?
4 Soma Zaburi 73:28. Mwandikaji wa Zaburi ya 73 alikuwa Mlawi aliyewekwa rasmi kutumikia akiwa mwanamuziki katika hekalu la Yehova. Inaelekea kwamba alikuwa mwabudu mwaminifu wa Yehova kwa miaka mingi. Hata hivyo, bado aliona umuhimu wa kujikumbusha na kuwakumbusha wengine kwamba “kumkaribia Mungu” lilikuwa jambo jema kwake na kwao pia. Tunanufaikaje kwa kumkaribia Mungu?
“KUMKARIBIA MUNGU” HUTUPATIA FURAHA
5. (a) Kwa nini kumkaribia zaidi Yehova hutupatia furaha? (b) Kwa kutegemea Methali 2:6-16, toa mifano hususa inayoonyesha jinsi hekima ya Yehova inavyoweza kukunufaisha na kukulinda kibinafsi.
5 Kadiri tunavyomkaribia zaidi Yehova, ndivyo tutakavyokuwa na furaha zaidi. (Zab. 65:4) Kuna sababu nyingi kwa nini hilo ni kweli. Sababu moja ni kwamba tunanufaika kutokana na hekima inayotumika ambayo inapatikana katika Biblia, Neno lake. Hekima hiyo inatulinda dhidi ya mambo yanayoweza kutudhuru na dhidi ya kufanya makosa mazito. (Soma Methali 2:6-16.) Kwa kufaa, Biblia inasema hivi: “Mwenye furaha ni mtu anayepata hekima na mtu anayepata utambuzi.”—Met. 3:13.
6. Ni nini kilichosababisha mtunga zaburi apoteze shangwe yake?
6 Bila shaka, hata marafiki wa Yehova huwa na huzuni pindi fulani. Mwandikaji wa Zaburi ya 73 alipoteza shangwe yake alipoanza kuwa na maoni yasiyofaa. Alikasirika na kuwa na wivu kwa sababu, kulingana na maoni yake, watu wabaya ambao hawakumjali Mungu au viwango Vyake walikuwa na maisha mazuri. Alifikiri kimakosa kwamba watu wakatili na wenye kiburi sikuzote walikuwa na utajiri mwingi zaidi, afya nzuri zaidi, na hawakuteseka. (Zab. 73:3-7, 12) Mtunga zaburi huyo alihangaishwa sana na jambo hilo hivi kwamba pindi moja alijiuliza ikiwa jitihada zake za kumtumikia Yehova zilikuwa za bure. Akiwa na huzuni alisema hivi: “Kwa hakika nimeusafisha moyo wangu bure na kunawa mikono yangu katika ukosefu wa hatia.”—Zab. 73:13.
7. Tunawezaje kukabiliana na pindi za huzuni zinazoweza kufanya tupoteze furaha yetu? (Tazama picha.)
7 Mtunga zaburi hakuruhusu huzuni hiyo imzuie kutenda, alichukua hatua. ‘Aliingia mahali patakatifu pa Mungu penye utukufu,’ ambapo Yehova alirekebisha njia yake ya kufikiri. (Zab. 73:17-19) Tunapokuwa na huzuni, Yehova, Rafiki yetu wa karibu anajua hilo. Ikiwa tutasali kwake ili atupatie mwongozo na kukubali msaada anaotoa kupitia Neno lake na kutaniko, tutapata nguvu za kuvumilia huzuni yetu. Hata tunapohisi kwamba mahangaiko yetu yanatulemea, Yehova atatufariji na kututegemeza.—Zab. 94:19.a
Mlawi aliyeandika Zaburi ya 73, akiwa amesimama “mahali patakatifu pa Mungu penye utukufu” (Tazama fungu la 7)
“KUMKARIBIA MUNGU” HUTUPATIA KUSUDI NA TUMAINI
8. Ni katika njia gani nyingine muhimu kumkaribia Mungu ni jambo jema kwetu?
8 Kumkaribia Mungu ni jambo jema kwetu katika njia mbili nyingine muhimu. Kwanza, kunatupatia maisha yenye kusudi. Pili, kunatupatia tumaini hakika la wakati ujao. (Yer. 29:11) Acheni tuchunguze manufaa hayo kwa undani zaidi.
9. Kumkaribia Yehova kunatupatiaje furaha maishani?
9 Kumkaribia Yehova hutupatia kusudi maishani. Watu wengi leo wanaokataa kwamba kuna Mungu wanafikiri kwamba maisha hayana kusudi na hatimaye wanadamu hawatakuwepo tena. Hata hivyo, kutokana na mambo tuliyojifunza katika Neno la Mungu, tumesadiki kwamba Mungu “yuko na kwamba yeye huwa mthawabishaji wa wale wanaomtafuta kwa bidii.” (Ebr. 11:6) Hata sasa, tunaishi maisha yenye furaha zaidi kwa sababu tunafanya kile ambacho tuliumbwa kufanya, yaani, kumtumikia Baba yetu wa mbinguni, Yehova.—Kum. 10:12, 13.
10. Zaburi 37:29 inafunua nini kuhusu wakati ujao wa wale wanaomtumaini Yehova?
10 Watu wengi leo hawana tumaini la kweli. Wao hufanya tu kazi, hulea watoto wao, na kuweka akiba kwa ajili ya wakati watakapostaafu. Hawajui kile ambacho Mungu ameahidi kuhusu wakati ujao. Kwa upande mwingine, watumishi wa Yehova wanamtumaini yeye. (Zab. 25:3-5; 1 Tim. 6:17) Tunamtumaini Mungu ambaye tumemkaribia, na tuna uhakika na alichotuahidi. Wakati wetu ujao unatia ndani tumaini la kumwabudu milele katika Paradiso.—Soma Zaburi 37:29.
11. Kumkaribia Mungu kutakuwa na matokeo gani kwetu, naye Mungu atahisije?
11 Kumkaribia Mungu ni jambo jema kwetu katika njia nyingine nyingi. Kwa mfano, Yehova anaahidi kuwasamehe watenda dhambi wanaotubu na wanaomkaribia. (Isa. 1:18) Matokeo ni kwamba hatuhitaji kulemewa na dhamiri yenye hatia kwa sababu ya dhambi tulizofanya wakati uliopita. (Zab. 32:1-5) Na tuna fursa ya kufanya moyo wa Yehova ushangilie. (Met. 23:15) Bila shaka unaweza kufikiria baraka nyingine ambazo zinatokana na kuwa na urafiki wa karibu na Mungu. Hata hivyo, unawezaje kuendelea kumkaribia Mungu?
JINSI YA KUENDELEA “KUMKARIBIA MUNGU”
12. Umefanya mambo gani ili kumkaribia Mungu zaidi?
12 Ikiwa wewe ni Mkristo aliyebatizwa, tayari umemkaribia Yehova kwa kiwango kikubwa. Umejifunza kweli nyingi kumhusu Yehova Mungu na Kristo Yesu, umetubu dhambi zako za wakati uliopita, umeonyesha imani yenye nguvu katika Mungu, na unajitahidi kuishi kulingana na mapenzi yake. Hata hivyo, ili kumkaribia zaidi Mungu, ni lazima tuendelee kufanya mambo hayo.—Kol. 2:6.
13. Ni mambo gani matatu yanayoweza kutusaidia kuendelea kumkaribia zaidi Yehova?
13 Ni mambo gani yatakayotusaidia kuendelea kumkaribia zaidi Yehova? (1) Ni lazima tuendelee kusoma na kujifunza Biblia. Tunapofanya hivyo, lengo letu linapaswa kuwa kufanya mengi zaidi ya kujifunza mambo ya msingi kumhusu Mungu. Tunapaswa kujitahidi kuyafahamu mapenzi ya Mungu kutuelekea na kuongozwa na kanuni alizotuwekea katika Neno lake. (Efe. 5:15-17) (2) Ni lazima tuimarishe imani yetu kwa kutafakari kuhusu uthibitisho mwingi wa upendo wake kwetu. (3) Ni lazima tuendelee kuchukia mambo yanayomkasirisha Yehova na kutoshirikiana na watu wanaofanya mambo kama hayo.—Zab. 1:1; 101:3.
14. Kulingana na 1 Wakorintho 10:31, ni baadhi ya mambo gani tunayoweza kufanya katika maisha yetu ya kila siku ili kumfurahisha Yehova? (Tazama pia picha.)
14 Soma 1 Wakorintho 10:31. Ni jambo la muhimu tujitahidi kufanya mambo yanayomfurahisha Yehova. Hilo linahusisha mengi zaidi ya kuhubiri na kuhudhuria mikutano ya kutaniko. Matendo yanayomfurahisha Yehova yanatia ndani mambo tunayofanya katika maisha yetu ya kila siku. Kwa mfano, tunapokuwa wanyoofu katika mambo yote na kushiriki vitu tulivyo navyo na wengine, tunamfurahisha Yehova. (2 Kor. 8:21; 9:7) Pia, anataka tuonyeshe kwamba tunathamini sana zawadi ya uhai. Tunamkaribia zaidi Mpaji wa uhai kwa kudumisha kwa usawaziko mazoea mazuri ya kula na kunywa na kutunza afya zetu. Kila jitihada tunayofanya ili kumfurahisha Yehova, hata katika mambo yanayoonekana kuwa madogo, itamfanya Yehova atupende hata zaidi.—Luka 16:10.
Kuendesha gari kwa njia salama, kutunza miili yetu kwa kufanya mazoezi na kula vyakula vyenye lishe, na kuwa wakarimu ni baadhi ya njia ambazo tunaweza kumfurahisha Yehova (Tazama fungu la 14)
15. Yehova anatarajia tuwatendee wengine kwa njia gani?
15 Yehova ni mwenye fadhili kuelekea waadilifu na wasio waadilifu. (Mt. 5:45) Yehova anatarajia tuwaonyeshe wengine fadhili pia. Kwa mfano, ‘hatusemi vibaya kumhusu yeyote, hatuwi wagomvi, na tunaonyesha upole wote kwa watu wote.’ (Tito 3:2) Tukiwa na hilo akilini, hatuwadharau wengine eti kwa sababu hawaamini mambo tunayoamini. (2 Tim. 2:23-25) Tunamkaribia Yehova zaidi kwa kuwa wenye fadhili na ufikirio sikuzote tunaposhughulika na watu wote.
TUNAWEZA “KUMKARIBIA MUNGU” HATA TUNAPOJIKWAA
16. Mwandikaji wa Zaburi ya 73 alianza kuhisije baada ya muda fulani?
16 Lakini vipi ikiwa baada ya muda fulani, unaanza kuhisi kwamba hustahili upendo wa Yehova? Kama ilivyotajwa awali, jambo kama hilo lilimpata mwandikaji wa Zaburi ya 73. Alisema hivi: “Miguu yangu ilikuwa karibu kukengeuka; hatua zangu zilikuwa karibu kuteleza.” (Zab. 73:2) Alikiri kwamba alikuwa “mchungu” na “mpumbavu” “kama mnyama asiye na akili” mbele za Yehova. (Zab. 73:21, 22) Je, alifikia mkataa kwamba Yehova aliacha kumpenda na hangemsamehe kwa sababu ya kosa lake?
17. (a) Hata alipokuwa ameshuka moyo kabisa, mtunga zaburi alifanya nini? (b) Tunaweza kujifunza nini kutokana na kisa chake? (Tazama pia picha.)
17 Ikiwa mtunga zaburi huyo alihisi kwamba Yehova alimkataa, ni lazima hisia hizo zilikuwa za muda mfupi tu. Inaonekana kwamba alipokuwa ameshuka moyo kabisa, alitambua uhitaji wa kumkaribia zaidi Mungu. Alisema hivi: “Lakini sasa niko pamoja nawe [Yehova] sikuzote; umeushika mkono wangu wa kulia. Unaniongoza kwa ushauri wako, na baadaye utaniongoza kwenye utukufu.” (Zab. 73:23, 24) Sisi pia tunapaswa kumwona Yehova kuwa mwamba wetu imara tunapokuwa dhaifu au tunapovunjika moyo. (Zab. 73:26; 94:18) Hata ikiwa tutafanya makosa mazito, tunaweza kumrudia Yehova tukiwa na uhakika kwamba yuko “tayari kusamehe.” (Zab. 86:5) Hasa tunapokuwa tumeshuka moyo kabisa, tunapaswa kumkaribia zaidi Mungu wetu.—Zab. 103:13, 14.
Tunapokuwa dhaifu kiroho, tunapaswa kumkaribia zaidi Yehova kwa kufanya mengi zaidi katika ibada yetu kwake (Tazama fungu la 17)
“KUMKARIBIA MUNGU” MILELE
18. Kwa nini tunaweza kuendelea kumkaribia zaidi Yehova milele?
18 Tunaweza kuendelea kumkaribia zaidi Yehova milele na hatutaacha kamwe kujifunza kumhusu. Biblia inasema kwamba njia za Yehova, hekima yake, na ujuzi wake ‘hautafutiki.’—Rom. 11:33.
19. Maneno ya Zaburi yanatupatia uhakikisho gani?
19 Zaburi 79:13 inasema hivi: “Sisi, watu wako na kondoo wa malisho yako, tutakushukuru milele; nasi tutatangaza sifa yako kizazi mpaka kizazi.” Kadiri unavyoendelea kumkaribia Mungu, wewe pia unaweza kuwa na uhakika wa kupata baraka za milele na kusema hivi kwa usadikisho: “Mungu ni mwamba wa moyo wangu na fungu langu milele.”—Zab. 73:26.
WIMBO 32 Simama Upande wa Yehova!
a Baadhi ya watu ambao wanakabiliana kwa muda mrefu na mahangaiko au huzuni huenda wakahitaji msaada wa daktari. Kwa habari zaidi, tazama gazeti la Mnara wa Mlinzi, Na. 1 2023.