Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w25 Aprili kur. 20-25
  • Kamwe Hatuko Peke Yetu

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kamwe Hatuko Peke Yetu
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2025
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • YEHOVA HUTUONGOZA
  • YEHOVA HUTUANDALIA MAHITAJI YETU
  • YEHOVA HUTULINDA
  • YEHOVA HUTUFARIJI
  • YEHOVA ATATUSAIDIA SIKUZOTE
  • Kumbuka Kwamba Yehova Ndiye “Mungu Aliye Hai”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2024
  • Yehova “Huwaponya Waliovunjika Moyo”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2024
  • Pata Furaha Kubwa Inayotokana na Kutoa
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2024
  • Uwe Mwenye Kiasi Inapohusu Mambo Usiyoyajua
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2025
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2025
w25 Aprili kur. 20-25

MAKALA YA 17

WIMBO 99 Ndugu Makumi ya Elfu

Kamwe Hatuko Peke Yetu

“Nitakusaidia.”—ISA. 41:10.

JAMBO KUU

Njia nne ambazo Yehova anatumia ili kututunza.

1-2. (a) Kwa nini tunaweza kusema kwamba hatutakabili kamwe majaribu tukiwa peke yetu? (b) Tutachunguza nini katika makala hii?

TUNAPOKABILI majaribu makubwa, huenda tukahisi kana kwamba tuko peke yetu katika mashua ndogo kwenye bahari yenye dhoruba. Hata hivyo, hatukabili majaribu tukiwa peke yetu. Baba yetu wa mbinguni anayetupenda anaona majaribu yetu na anaahidi pia kutusaidia kukabiliana nayo. Kwa upendo, Yehova anawahakikishia hivi watumishi wake washikamanifu: “Nitakusaidia.”—Isa. 41:10.

2 Katika makala hii, tutachunguza jinsi Yehova anavyotusaidia (1) kwa kutuongoza, (2) kwa kutuandalia mahitaji yetu, (3) kwa kutulinda, na (4) kwa kutufariji. Yehova anatuhakikishia kwamba hata tukikabili changamoto gani maishani, hatatusahau kamwe. Hatatuacha kamwe. Hivyo, kamwe hatuko peke yetu.

YEHOVA HUTUONGOZA

3-4. Yehova anatuongozaje? (Zaburi 48:14)

3 Soma Zaburi 48:14. Yehova hatarajii tujiongoze wenyewe. Anawaongozaje waabudu wake washikamanifu leo? Njia moja anayofanya hivyo ni kupitia Biblia. (Zab. 119:105) Kupitia Neno lake lililoongozwa na roho, Yehova anatusaidia kufanya maamuzi mazuri na kusitawisha sifa zinazotupatia furaha zaidi sasa na tumaini la kuishi milele wakati ujao.a Kwa mfano, anatufundisha jinsi ya kutoweka kinyongo, kuwa wanyoofu katika mambo yote, na kuwapenda sana wengine kutoka moyoni. (Zab. 37:8; Ebr. 13:18; 1 Pet. 1:22) Tunapoonyesha sifa hizo za Mungu, tunakuwa wazazi, wenzi wa ndoa, na marafiki wazuri zaidi.

4 Kwa kuongezea, katika Neno lake, Yehova alitia ndani masimulizi ya watu halisi ambao walikabili majaribu kama yetu na walikuwa na hisia kama zetu. (1 Kor. 10:13; Yak. 5:17) Tunaposoma masimulizi hayo ya watu halisi na kutumia maishani mambo tunayojifunza, tunanufaika kwa angalau njia mbili. Kwanza, tunatambua kwamba hatuko peke yetu—wengine wamekabili hali kama zetu na walivumilia kwa mafanikio. (1 Pet. 5:9) Na pili, tunajifunza jinsi ya kukabiliana na majaribu yetu.—Rom. 15:4.

5. Yehova anawatumia nani kutuongoza katika barabara ya uzima?

5 Pia, Yehova amefanya mipango ili waabudu wenzetu watuongoze.b Kwa mfano, waangalizi wa mzunguko hutembelea makutaniko kwa ukawaida ili kututia moyo. Hotuba zao huimarisha imani yetu na kutusaidia kudumisha umoja wetu wenye thamani. (Mdo. 15:40–16:5) Wazee wa kutaniko pia wanapendezwa kutoka moyoni na hali njema ya kila mhubiri. (1 Pet. 5:​2, 3) Wazazi huwapatia mwongozo wa kiroho watoto wao, kwa kuwasaidia wasitawishe uwezo mzuri wa kufikiri na mazoea yanayofaa. (Met. 22:6) Na akina dada Wakristo wakomavu wanawasaidia akina dada wenye umri mdogo zaidi kwa kuwawekea mfano mzuri, kuwapatia ushauri unaofaa, na kuwatia moyo.—Tito 2:​3-5.

6. Ni lazima tufanye nini ili tunufaike na mwongozo wa Yehova?

6 Yehova ametimiza sehemu yake kwa kutupatia mwongozo tunaohitaji. Tunawezaje kuonyesha kwamba tunathamini mambo aliyotufanyia? Methali 3:​5, 6 inasema: “Mtumaini Yehova kwa moyo wako wote, wala usitegemee uelewaji wako mwenyewe.” Tunapofanya hivyo, “atavinyoosha vijia [vyetu],” yaani, atatusaidia tuepuke matatizo mengi na kuwa na maisha yenye furaha zaidi. Tunashukuru sana kwamba Yehova anampatia kila mmoja wetu ushauri wenye upendo!—Zab. 32:8.

YEHOVA HUTUANDALIA MAHITAJI YETU

7. Taja baadhi ya njia ambazo Yehova anatuandalia mahitaji yetu. (Wafilipi 4:19)

7 Soma Wafilipi 4:19. Zaidi ya kutuongoza kiroho, Yehova hubariki jitihada zetu za kutafuta chakula, mavazi tunayohitaji, na mahali pa kuishi. (Mt. 6:33; 2 The. 3:12) Ingawa ni jambo la kawaida kuwa na mahangaiko kuhusu mahitaji yetu ya kimwili, Yehova anatutia moyo tusiwe na mahangaiko kupita kiasi kuhusu vitu hivyo. (Mt. 6:25) Kwa nini? Kwa sababu Baba yetu hatawaacha kamwe waabudu wake waaminifu wanapokuwa na uhitaji. (Mt. 6:8; Ebr. 13:5) Tunaweza kumtumaini kabisa Yehova anaposema kwamba atatuandalia mahitaji yetu.

8. Yehova alimfanyia nini Daudi?

8 Fikiria njia ambayo Yehova alimsaidia Daudi. Wakati Daudi alipokabili hali ngumu akiwa mkimbizi, Yehova alimwandalia yeye na wanaume wake mambo waliyohitaji ili waendelee kuwa hai. Alipokumbuka jinsi Yehova alivyomtunza katika miaka hiyo, Daudi aliandika hivi: “Nilikuwa kijana lakini sasa nimezeeka, lakini sijamwona mtu yeyote mwadilifu akiwa ameachwa, wala watoto wake wakitafuta mkate.” (Zab. 37:25) Inaelekea kwamba katika maisha yako, umejionea pia jinsi Yehova alivyowaandalia kwa upendo watumishi wake waaminifu mahitaji yao.

9. Leo, Yehova huwaandaliaje watu wake mahitaji yao wakati wa majanga? (Tazama pia picha.)

9 Yehova huwaandalia pia watu wake mahitaji yao wakati wa majanga. Kwa mfano, kulipokuwa na njaa katika karne ya kwanza, Wakristo kutoka maeneo mbalimbali waliwatumia msaada ndugu na dada zao waliokuwa na uhitaji. (Mdo. 11:​27-30; Rom. 15:​25, 26) Watu wa Mungu leo wanaonyesha pia sifa hiyo ya ukarimu. Janga linapotokea, kwa upendo Yehova huwachochea watu wake wawasaidie ndugu zao walio kwenye maeneo yaliyoathirika kwa kuwapatia mahitaji ya muhimu kama vile chakula, maji, mavazi, na dawa. Vikosi vya ujenzi hurekebisha nyumba zilizoharibika na Majumba ya Ufalme. Na watumishi wa Yehova huwapatia haraka faraja na kuwatia moyo wale waliopoteza wapendwa wao au nyumba zao.c

Mkusanyo wa picha: Wakipokea msaada wa kimwili na kiroho baada ya janga la asili nchini Malawi. 1. Mafuriko yaliyoathiri eneo kubwa. 2. Ndugu Gage Fleegle akizungumza na ndugu na dada. 3. Akina ndugu wakishusha mifuko ya chakula kutoka kwenye gari.

Yehova hutuandaliaje faraja wakati wa majanga? (Tazama fungu la 9)e


10-11. Unajifunza nini kutokana na kisa cha Borys?

10 Yehova huandaa pia mahitaji ya wale ambao bado hawajaanza kumwabudu. Vivyo hivyo, sisi pia tunatafuta fursa za kuwaonyesha fadhili wale ambao si waabudu wenzetu. (Gal. 6:10) Mara nyingi hilo hutokeza nafasi nzuri ya kutoa ushahidi. Fikiria kisa cha Borys, mwalimu mkuu wa shule anayeishi nchini Ukrainia. Ingawa Borys si Shahidi wa Yehova, sikuzote aliwatendea kwa fadhili wanafunzi Mashahidi na aliheshimu imani yao. Borys alipoamua kukimbia eneo la vita mahali ambapo alikuwa anaishi na kwenda katika eneo lingine la nchi lililokuwa salama zaidi, ndugu zetu walimsaidia. Baadaye, Borys alihudhuria Ukumbusho wa kifo cha Kristo. Anapokumbuka wakati huo, Borys anasema hivi: “Mashahidi walinijali na kunitunza sana. Ninawashukuru sana Mashahidi wa Yehova.”

11 Sisi pia tunaweza kumwiga Baba yetu wa mbinguni mwenye rehema kwa kuwaonyesha upendo wale wenye uhitaji, iwe ni waabudu wenzetu au la. (Luka 6:​31, 36) Tunatumaini kwamba jitihada zetu za kuwaonyesha watu upendo zitawachochea kuwa wanafunzi wa Kristo. (1 Pet. 2:12) Hata hivyo, iwe wataamua kumtumikia Yehova au la, tutapata furaha kubwa zaidi inayotokana na kutoa.—Mdo. 20:35.

YEHOVA HUTULINDA

12. Yehova anaahidi kuwapatia watu wake ulinzi gani wakiwa kikundi? (Zaburi 91:​1, 2, 14)

12 Soma Zaburi 91:​1, 2, 14. Leo, Yehova anaahidi kutupatia ulinzi wa kiroho. Hatamruhusu kamwe Shetani achafue ibada safi. (Yoh. 17:15) Na wakati wa “dhiki kuu,” tunaweza kuwa na uhakika kabisa kwamba Yehova atatimiza ahadi yake ya kuwalinda watu wake kiroho na pia kimwili.—Ufu. 7:​9, 14.

13. Yehova anatupatia ulinzi kwa njia gani tukiwa mtu mmoja-mmoja?

13 Yehova anatupatia ulinzi gani tukiwa mtu mmoja-mmoja? Yehova anatusaidia kutambua mema na mabaya kupitia Maandiko. (Ebr. 5:14) Tunapoishi kulingana na kanuni zinazopatikana katika Neno la Mungu, tunajilinda dhidi ya madhara ya kiroho na ya kimwili. (Zab. 91:4) Yehova anatupatia pia ulinzi kupitia kutaniko. (Isa. 32:​1, 2) Kwa kushirikiana na wale wanaompenda Yehova na kuishi kulingana na kanuni zake, tunatiwa moyo na kuimarishwa ili tujiepushe na mambo yanayoweza kutudhuru.—Met. 13:20.

14. (a) Kwa nini Mungu anaruhusu tukabili majaribu? (b) Zaburi 9:10 inatuhakikishia nini? (Tazama pia maelezo ya chini.)

14 Pindi fulani, Yehova aliwalinda waabudu wake kimwili. Hata hivyo, hakufanya hivyo kila mara. Nyakati nyingine, tunapatwa na “matukio yasiyotarajiwa.” (Mhu. 9:11) Pia, Yehova aliruhusu baadhi ya watumishi wake wakabili mateso na hata kifo ili kuthibitisha kwamba Shetani ni mwongo. (Ayu. 2:​4-6; Mt. 23:34) Hali iko hivyo leo pia. Ingawa huenda Yehova hataondoa majaribu yetu, tunaweza kuwa na uhakika kwamba hatawaacha kamwe wale wanaompenda.d—Zab. 9:10.

YEHOVA HUTUFARIJI

15. Sala, Neno la Mungu, na waabudu wenzetu wanatupatiaje faraja? (2 Wakorintho 1:​3, 4)

15 Soma 2 Wakorintho 1:​3, 4. Pindi fulani, sisi huwa na huzuni, mahangaiko, au hutaabika. Huenda kwa sasa unakabili hali inayokutaabisha na kufanya uhisi uko peke yako. Je, kuna mtu yeyote anayeelewa hisia zako? Yehova anaelewa jinsi unavyohisi. Hahisi tu maumivu yetu, bali pia “hutufariji katika majaribu yetu yote.” Jinsi gani? Tunapomtolea dua Yehova, anatupatia “amani ya Mungu inayozidi uelewaji wote.” (Flp. 4:​6, 7) Pia, tunapata faraja tunaposoma maneno ya Yehova katika Biblia. Maneno hayo yaliyoongozwa na roho yenye upendo, hekima, na tumaini, ambayo yanapatikana katika hazina hiyo, yanaweza kututia moyo. Na mikutano ya Kikristo hutufariji kwa kutupatia ushirika mchangamfu na kitia-moyo kutoka katika Biblia.

16. Unajifunza nini kutokana na kisa cha Nathan na Priscilla?

16 Tunaweza kuona jinsi ambavyo Yehova anatupatia faraja na kututia moyo kupitia Neno lake katika kisa cha Nathan na Priscilla, wanaoishi Marekani. Miaka kadhaa iliyopita, waliamua kuhamia katika eneo lenye uhitaji mkubwa wa wahubiri wa Ufalme. Nathan anasema hivi: “Tulikuwa na uhakika kwamba Yehova angebariki jitihada zetu.” Hata hivyo, baada ya kufika katika mgawo wao mpya, walikabili matatizo ya afya na ya kifedha ambayo hawakutarajia. Mwishowe, wenzi hao walilazimika kurudi nyumbani, ambapo waliendelea kuwa na matatizo ya kifedha. Nathan anasema hivi: “Nilijiuliza kwa nini Mungu hakutubariki kama tulivyofikiri angefanya. Hata nilianza kujiuliza ikiwa nilikuwa nimemkosea.” Hata hivyo, baada ya muda, Nathan na Priscilla walitambua kwamba Mungu hakuwa amewaacha walipokuwa na uhitaji. Nathan anaeleza hivi: “Katika nyakati hizo ngumu, Biblia ilikuwa kama rafiki mwenye hekima anayetutia moyo na kutuongoza. Kukazia fikira jinsi Yehova alivyotusaidia kuvumilia matatizo hayo, badala ya kukazia fikira tatizo lenyewe, kulitutayarisha kukabili kwa imani changamoto za wakati ujao.”

17. Dada anayeitwa Helga alifarijiwa jinsi gani? (Tazama pia picha.)

17 Ndugu na dada zetu wanaweza kutupatia faraja zaidi. Jinsi gani? Fikiria kisa cha Helga, anayeishi nchini Hungaria. Kwa miaka mingi, alikabiliana na changamoto mbalimbali zilizomfanya awe na mahangaiko na ahisi kwamba hafai. Lakini anapokumbuka wakati huo, anaona jinsi Yehova alivyomfariji kupitia kutaniko. Aliandika hivi: “Sikuzote Yehova amenisaidia alipoona kwamba nguvu zangu zimekuwa chache kwa sababu ya kazi ya kimwili, kumtunza mtoto wangu mgonjwa, na majaribu mengine. Katika miaka 30 iliyopita, hakuna hata siku moja ambayo Yehova hajatimiza ahadi yake ya kunifariji. Mara nyingi ananiimarisha kupitia maneno yenye fadhili, yenye kufikiriwa vizuri, na yanayoonyesha kwamba ninathaminiwa na wengine. Mara nyingi nimepokea ujumbe, kadi, au pongezi kwa wakati unaofaa.”

Mkusanyo wa picha: Ndugu mwenye umri mkubwa akipata faraja. 1. Anatazama picha ambazo watoto wamemchorea. 2. Ndugu anamtumia ujumbe mfupi. 3. Wenzi wa ndoa wanamletea mfuko wenye bidhaa na pizza. 4. Ndugu anampigia simu. 5. Msichana mdogo anachora picha ya simba akiwa katika Paradiso ili ampatie.

Yehova anaweza kukutumia jinsi gani kuwafariji wengine? (Tazama fungu la 17)


18. Tunawezaje kuwafariji wengine?

18 Tuna pendeleo la kumwiga Mungu wetu kwa kuwafariji wengine. Tunawezaje kufanya hivyo? Tunaweza kuwasikiliza kwa subira, kuzungumza nao kwa njia itakayowafariji, na kuwasaidia kwa njia hususa. (Met. 3:27) Tunajitahidi kuwafariji watu wote wanaoteseka kutia ndani wale ambao hawajaanza kumtumikia Mungu. Jirani zetu wanapokuwa na huzuni, wanapokuwa wagonjwa, au wanapokuwa na mahangaiko, tunawatembelea, tunawasikiliza, na tunawatia moyo kwa kutumia maandiko yaliyo katika Biblia. Tunapomwiga Yehova, “Mungu wa faraja yote,” tunawasaidia waabudu wenzetu wavumilie majaribu na pia tunawasaidia wale ambao si waabudu wake waanze kuikubali ibada safi.—Mt. 5:16.

YEHOVA ATATUSAIDIA SIKUZOTE

19. Yehova anafanya nini kwa ajili yetu, na tunawezaje kumwiga?

19 Yehova anawahangaikia sana wale wote wanaompenda. Hivyo, hatuachi tunapokabili matatizo. Kama mzazi anavyomjali kwa upendo mtoto wake, Yehova anawajali waabudu wake waaminifu. Anatuongoza, anatuandalia mahitaji yetu, anatulinda, na anatufariji. Tunamwiga Baba yetu wa mbinguni mwenye upendo, tunapowasaidia na kuwatia moyo wengine wanapokabili majaribu. Ingawa tutapatwa na matatizo na huzuni, tunaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova yuko pamoja nasi. Kwa kweli, ametuahidi hivi: “Usiogope, kwa maana mimi niko pamoja nawe.” (Isa. 41:10) Ahadi hiyo inatuhakikishia kwamba tukiwa na Yehova, kamwe hatuko peke yetu!

NI KWA NJIA GANI YEHOVA . . .

  • anatuongoza?

  • anatuandalia mahitaji yetu?

  • anatulinda na kutufariji?

WIMBO 100 Wakaribisheni

a Tazama makala “Fanya Maamuzi Ambayo Yanamletea Mungu Heshima” katika gazeti la Mnara wa Mlinzi la Aprili 15, 2011.

b Tazama fungu la 11-14 kwenye makala “Endelea Kufuata Mwongozo wa Yehova” katika gazeti la Mnara wa Mlinzi la Februari 2024.

c Unaweza kupata mifano ya hivi karibuni katika jw.org kwa kuandika “kutoa msaada” kwenye sehemu ya Tafuta.

d Tazama “Maswali Kutoka kwa Wasomaji” katika gazeti la Mnara wa Mlinzi la Februari 2017.

e MAELEZO YA PICHA: Ndugu nchini Malawi, wakipokea msaada wa kimwili na kiroho baada ya kupatwa na janga la asili.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki