MAKALA YA 27
WIMBO 79 Wafundishe Kusimama Imara
Wasaidie Wanafunzi wa Biblia Wachukue Msimamo Upande wa Kweli
“Simameni imara katika imani . . . Iweni na nguvu.”—1 KOR. 16:13.
JAMBO KUU
Jinsi tunavyoweza kuwasaidia wanafunzi wa Biblia wasitawishe imani na ujasiri wanaohitaji ili wachukue msimamo upande wa kweli.
1-2. (a) Kwa nini baadhi ya wanafunzi wa Biblia wanasita kuchukua msimamo upande wa kweli? (b) Tutachunguza nini katika makala hii?
JE, ULISITA kuwa Shahidi wa Yehova? Huenda uliogopa kwamba wafanyakazi wenzako, marafiki, au watu wa familia wangekupinga. Au huenda ulihisi kwamba hungeweza kamwe kuishi kulingana na viwango vya Mungu. Ikiwa ndivyo, unaelewa hisia za wanafunzi wa Biblia wanaosita kuchukua msimamo upande wa kweli.
2 Yesu alitambua kwamba woga huo unaweza kwa urahisi kuzuia ukuzi wa kiroho. (Mt. 13:20-22) Lakini hakukata tamaa ilipohusu watu ambao walisita kumfuata. Badala yake, aliwaonyesha wanafunzi wake jinsi ya kuwasaidia watu hao (1) watambue mambo yanayowazuia kufanya maendeleo, (2) waimarishe upendo wao kwa Yehova, (3) watangulize mambo muhimu zaidi maishani, na (4) washinde changamoto wanazokabili. Tunawezaje kutumia mambo ambayo Yesu aliwaambia wanafunzi wake tunapotumia kitabu Furahia Maisha Milele! kumsaidia mwanafunzi wa Biblia achukue msimamo upande wa kweli?
MSAIDIE MWANAFUNZI WAKO ATAMBUE MAMBO YANAYOMZUIA KUFANYA MAENDELEO
3. Ni jambo gani ambalo huenda lilimzuia Nikodemo kuwa mwanafunzi wa Yesu?
3 Nikodemo, kiongozi mashuhuri wa Wayahudi, alikabili jambo fulani lililomzuia kuwa mwanafunzi wa Yesu. Miezi sita tu baada ya Yesu kuanza huduma yake, Nikodemo alitambua kwamba Yesu alikuwa mwakilishi wa Mungu. (Yoh. 3:1, 2) Hata hivyo, kwa kuwa ‘aliwaogopa Wayahudi,’ Nikodemo aliamua kukutana na Yesu kwa siri. (Yoh. 7:13; 12:42) Huenda alihisi kwamba angepoteza mamlaka na mali zake ikiwa angekuwa mwanafunzi wa Yesu.a
4. Yesu alimsaidiaje Nikodemo aelewe Mungu alitarajia nini kutoka kwake?
4 Nikodemo alikuwa na ujuzi wa Sheria, lakini alihitaji msaada ili aelewe Yehova alitarajia nini kutoka kwake. Yesu alimsaidiaje? Yesu alikuwa tayari kutumia wakati mwingi pamoja na Nikodemo, hata wakati wa usiku. Na Yesu alimwambia wazi Nikodemo mambo aliyopaswa kufanya ili awe mwanafunzi wake: atubu dhambi zake, abatizwe katika maji, na aonyeshe imani katika Mwana wa Mungu.—Yoh. 3:5, 14-21.
5. Tunawezaje kumsaidia mwanafunzi wa Biblia atambue mambo yanayozuia maendeleo yake?
5 Hata ikiwa mwanafunzi wa Biblia ana ujuzi mzuri wa Maandiko, huenda akahitaji kusaidiwa kutambua mambo yanayozuia maendeleo yake. Huenda kazi ya kimwili au upinzani kutoka kwa familia ukamkengeusha asitimize malengo yake ya kiroho. Hivyo, tenga wakati ili kumsaidia mwanafunzi wako. Unaweza kumkaribisha nyumbani kwa ajili ya chakula chepesi na mazungumzo. Katika mazingira hayo yenye kustarehesha, unaweza kumsaidia ajieleze kuhusu changamoto anazopitia. Mtie moyo mwanafunzi wako afanye mabadiliko yanayohitajika, si ili akupendeze wewe, bali ili aonyeshe upendo wake kwa Yehova.
6. Unaweza kumsaidiaje mwanafunzi wako apate ujasiri wa kuchukua msimamo upande wa kweli? (1 Wakorintho 16:13)
6 Mwanafunzi wa Biblia anapokuwa na uhakika kwamba Yehova atamsaidia kuishi kulingana na viwango vya Biblia, atapata ujasiri wa kutumia mambo anayojifunza. (Soma 1 Wakorintho 16:13.) Jukumu lako linaweza kufananishwa na jukumu la mwalimu wa shule. Mwalimu uliyempenda zaidi ulipokuwa shuleni alikuwa nani? Huenda ni mwalimu ambaye kwa subira alikusaidia utambue uwezo wako na ujiamini zaidi. Vivyo hivyo, mwalimu mzuri wa Biblia hafundishi tu wanafunzi wake mambo ambayo Mungu anataka wafanye, bali pia anawahakikishia kwamba kwa msaada wa Yehova wanaweza kufanya mabadiliko yanayohitajika maishani. Unawezaje kufanya hivyo?
MSAIDIE MWANAFUNZI WAKO AIMARISHE UPENDO WAKE KWA YEHOVA
7. Yesu aliwasaidiaje wasikilizaji wake waimarishe upendo wao kwa Yehova?
7 Yesu alijua kwamba upendo wao kwa Mungu ungewachochea wanafunzi wake watumie mambo waliyojifunza. Mara nyingi aliwafundisha mambo ambayo yangewasaidia wanafunzi wake waimarishe upendo wao kwa Baba yao wa mbinguni. Kwa mfano, alimlinganisha Yehova na mwanamume anayewapatia vitu vyema watoto wake. (Mt. 7:9-11) Huenda baadhi ya wasikilizaji wa Yesu hawakuwa na baba mwenye upendo huo. Wazia jinsi walivyohisi Yesu alipotoa mfano wa baba mwenye huruma aliyemkaribisha mwana wake ambaye alikuwa amefanya mambo mengi mabaya. Wangeweza kuona huruma ya Yehova kuelekea watoto wake duniani.—Luka 15:20-24.
8. Unaweza kumsaidiaje mwanafunzi wa Biblia aimarishe upendo wake kwa Yehova?
8 Wewe pia unaweza kumsaidia mwanafunzi wa Biblia aimarishe upendo wake kwa Yehova kwa kukazia sifa za Mungu unapomfundisha. Katika kila kipindi cha funzo, msaidie aelewe uhusiano kati ya mambo anayojifunza na upendo wa Yehova. Mnapozungumzia fidia, kazia jinsi inavyomhusu kibinafsi. (Rom. 5:8; 1 Yoh. 4:10) Huenda mwanafunzi akachochewa kumpenda Yehova anapotafakari kuhusu jinsi Yehova anavyompenda kibinafsi.—Gal. 2:20.
9. Ni nini kilichomsaidia mwanamume anayeitwa Michael kufanya mabadiliko maishani?
9 Mfikirie Michael kutoka nchini Indonesia. Alilelewa katika kweli lakini hakubatizwa. Alipokuwa na umri wa miaka 18, alihamia nchi nyingine na kufanya kazi ya kuendesha lori. Baadaye, alirudi nchini Indonesia na kufunga ndoa kisha akaiacha familia yake huko na kuendelea na kazi ya udereva katika nchi hiyo ya kigeni. Wakati huo, mke wake na binti yake walianza kujifunza Biblia na kufanya maendeleo. Baada ya mama yake kufa, Michael aliamua kurudi nyumbani ili amtunze baba yake na akakubali kuanza kujifunza Biblia. Walipokuwa wakichunguza sehemu ya “Chimba Zaidi” katika somo la 27 kwenye kitabu Furahia Maisha Milele!, Michael aliguswa moyo sana. Michael alitokwa na machozi alipotafakari kuhusu jinsi Yehova alivyohisi alipomwona Mwana Wake akiteseka. Aliithamini hata zaidi fidia na alichochewa kufanya mabadiliko maishani na kubatizwa.
MSAIDIE MWANAFUNZI WAKO ATANGULIZE MAMBO MUHIMU ZAIDI MAISHANI
10. Yesu aliwasaidiaje wanafunzi wake wa mapema wabadili mambo waliyotanguliza maishani? (Luka 5:5-11) (Tazama pia picha.)
10 Wanafunzi wa mapema walitambua haraka kwamba Yesu alikuwa Masihi aliyeahidiwa, hata hivyo walihitaji msaada ili watangulize huduma maishani. Petro na Andrea tayari walikuwa wanafunzi kwa kipindi fulani Yesu alipowaalika wamfuate wakati wote. (Mt. 4:18, 19) Walikuwa na biashara yenye mafanikio ya kuvua samaki, inaelekea pamoja na Yakobo na Yohana. (Marko 1:16-20) Inaelekea Petro na Andrea ‘walipoziacha nyavu zao’ na kumfuata Yesu, walifanya mipango ili kuziandalia familia zao. Ni jambo gani lililowachochea wabadili mambo waliyotanguliza maishani? Simulizi katika kitabu cha Luka linasema kwamba Yesu alifanya muujiza ili kuimarisha uhakika wao katika uwezo wa Yehova wa kutimiza mahitaji yao.—Soma Luka 5:5-11.
Tunaweza kujifunza nini kutokana na njia ambayo Yesu aliwasaidia wanafunzi wake watangulize mambo muhimu zaidi maishani? (Tazama fungu la 10)b
11. Tunawezaje kutumia mambo tuliyopitia maishani kuimarisha imani ya mwanafunzi wa Biblia?
11 Hatuwezi kufanya miujiza kama Yesu alivyofanya, lakini tunaweza kusimulia jinsi Yehova anavyowategemeza wale wanaomtanguliza maishani mwao. Kwa mfano, je, unakumbuka jinsi Yehova alivyokusaidia ulipoanza kuhudhuria mikutano? Huenda ulihitaji kumweleza mwajiri wako kwa nini hungeweza kuendelea kufanya kazi baada ya muda wa kazi ikiwa ingevuruga ratiba yako ya kuhudhuria mikutano. Unapomsimulia mambo hayo mwanafunzi wako, mweleze jinsi imani yako ilivyoimarishwa ulipoona Yehova akibariki uamuzi wako wa kutanguliza ibada yake.
12. (a) Kwa nini tunapaswa kuwaalika wahubiri tofauti-tofauti katika funzo la Biblia? (b) Unawezaje kutumia video kumfundisha mwanafunzi wako kwa njia yenye matokeo? Toa mfano.
12 Mwanafunzi wako atanufaika pia na masimulizi ya Wakristo wengine kuhusu jinsi walivyobadili mambo waliyotanguliza maishani. Hivyo, waalike waamini wenzako kutoka katika malezi mbalimbali ili washiriki katika funzo la Biblia. Waombe waeleze jinsi walivyopata kweli na mambo waliyofanya ili kutanguliza utumishi wa Yehova maishani mwao. Zaidi ya hilo, tazama pamoja na mwanafunzi wako video kutoka katika sehemu ya “Chimba Zaidi” au “Chunguza Zaidi” kwenye kitabu Furahia Maisha Milele! Kwa mfano, mnapochunguza somo la 37, unaweza kukazia kanuni zinazopatikana kwenye video, Yehova Atatutimizia Mahitaji Yetu.
MSAIDIE MWANAFUNZI WAKO ASHINDE CHANGAMOTO ANAZOKABILI
13. Yesu aliwatayarishaje wanafunzi wake kwa ajili ya upinzani?
13 Tena na tena, Yesu aliwaambia wanafunzi wake kwamba wangekabili upinzani kutoka kwa watu, kutia ndani watu wao wa ukoo. (Mt. 5:11; 10:22, 36) Yesu alipokuwa akikaribia mwisho wa huduma yake, aliwaonya wanafunzi wake kwamba wangeweza kukabili kifo. (Mt. 24:9; Yoh. 15:20; 16:2) Aliwahimiza wawe waangalifu katika huduma yao. Aliwashauri wasibishane na wale wanaowapinga na watende kwa busara ili waweze kuendelea kuhubiri.
14. Tunaweza kumsaidiaje mwanafunzi ajitayarishe kwa ajili ya upinzani? (2 Timotheo 3:12)
14 Tunaweza kumsaidia mwanafunzi wetu ajitayarishe kwa ajili ya upinzani kwa kumweleza mambo ambayo wafanyakazi, marafiki, na watu wake wa ukoo wanaweza kumwambia. (Soma 2 Timotheo 3:12.) Huenda baadhi ya wafanyakazi wenzake wakadhihaki njia yake mpya ya maisha. Huenda wengine, kutia ndani watu wake wa karibu wa ukoo, wakapinga mambo anayoamini yanayotegemea Biblia. Tunapowatayarisha wanafunzi wetu mapema iwezekanavyo kukabiliana na upinzani, ndivyo watakavyokuwa na uwezo mzuri zaidi wa kukabiliana nao utakapotokea.
15. Ni nini kinachoweza kumsaidia mwanafunzi wa Biblia kukabiliana na upinzani kutoka kwa watu wa familia?
15 Ikiwa mwanafunzi wako anapingwa na watu wake wa ukoo, msaidie afikirie kwa nini wanampinga. Huenda wanafikiri kwamba amepotoshwa, au huenda wanahisi kwamba Mashahidi wa Yehova ni watu wabaya. Yesu pia alikabili upinzani kutoka kwa watu wa familia. (Marko 3:21; Yoh. 7:5) Msaidie mwanafunzi wako aendelee kuonyesha subira na busara anaposhughulika na wengine, kutia ndani watu wa familia.
16. Tunaweza kumsaidiaje mwanafunzi wa Biblia ashiriki kwa busara mambo anayoamini?
16 Hata ikiwa watu wa ukoo wataonyesha upendezi, ni jambo la hekima kwa mwanafunzi kutowaeleza kila kitu anachojua kwa wakati mmoja. La sivyo, huenda wapendwa wake wakalemewa na habari hizo zote, na matokeo ni kwamba wanaweza kukataa kumsikiliza wakati mwingine. Hivyo, mtie moyo mwanafunzi wako awaeleze wengine mambo anayoamini kwa njia ambayo itawachochea kukubali kuzungumza naye kuhusu Biblia wakati mwingine. (Kol. 4:6) Anaweza kuwaalika watu wake wa ukoo watembelee tovuti ya jw.org. Hilo litawasaidia wajifunze kuhusu Mashahidi wa Yehova kulingana na kasi na ratiba yao.
17. Unawezaje kumzoeza mwanafunzi kushughulikia maoni yasiyo sahihi ambayo huenda wengine wanayo kuhusu Mashahidi wa Yehova? (Tazama pia picha.)
17 Unaweza kutumia mfululizo “Maswali Yanayoulizwa Mara Nyingi” kwenye jw.org kumsaidia mwanafunzi wako atayarishe majibu rahisi ya maswali ambayo huenda watu wake wa ukoo au wafanyakazi wenzake wakamuuliza. (2 Tim. 2:24, 25) Mwishoni mwa kila somo, pitia sehemu ya “Watu Fulani Husema” katika kitabu Furahia Maisha Milele! Mtie moyo mwanafunzi wako afanye mazoezi ili atoe maelezo kwa maneno yake mwenyewe. Usisite kumpatia mapendekezo ya jinsi anavyoweza kuboresha maelezo yake. Mazoezi hayo yatamsaidia kutetea imani yake kwa uhakika.
Mtie moyo mwanafunzi wako wa Biblia ahubiri hadharani kwa kufanya naye mazoezi mapema (Tazama fungu la 17)c
18. Unawezaje kumtia moyo mwanafunzi wako awaeleze watu katika huduma mambo anayoamini? (Mathayo 10:27)
18 Yesu aliwahimiza wanafunzi wake watangaze habari njema hadharani. (Soma Mathayo 10:27.) Kadiri mwanafunzi anavyoanza mapema kuhubiri pamoja na kutaniko, ndivyo atakavyojifunza haraka zaidi kumtegemea Yehova. Unawezaje kumsaidia mwanafunzi ajiwekee lengo hilo? Kampeni ya kuhubiri inapotangazwa kutanikoni, mtie moyo mwanafunzi wako afikirie kuhusu jinsi anavyoweza kustahili kuwa mhubiri. Mweleze kwa nini wahubiri wengine wameona ikiwa rahisi zaidi kuanza kuhubiri wakati wa kampeni hizo. Anaweza pia kunufaika kwa kujitahidi kustahili kutoa hotuba katika mkutano wa katikati ya juma, ili aweze kuzoezwa na kujifunza jinsi ya kuwaeleza wengine kwa usadikisho mambo anayoamini.
ONYESHA UHAKIKA KATIKA MWANAFUNZI WAKO
19. Yesu alionyeshaje kwamba alikuwa na uhakika katika wanafunzi wake, na tunawezaje kumwiga?
19 Kabla ya Yesu kwenda mbinguni, aliwaambia wanafunzi wake kwamba siku moja wangekuwa pamoja naye tena. Hawakuelewa kwamba Yesu alikuwa akizungumza kuhusu kwenda kwao mbinguni. Hata hivyo, Yesu alikazia fikira ushikamanifu wao, si shaka walizokuwa nazo. (Yoh. 14:1-5, 8) Alijua kwamba walihitaji muda ili waelewe baadhi ya mambo kama vile, tumaini la kwenda mbinguni. (Yoh. 16:12) Sisi pia tunaweza kuonyesha kuwa tuna uhakika kwamba mwanafunzi wetu anatamani kumfurahisha Yehova.
Kadiri mwanafunzi anavyoanza mapema kuhubiri pamoja na kutaniko, ndivyo atakavyojifunza haraka zaidi kumtegemea Yehova
20. Dada mmoja nchini Malawi alionyeshaje kwamba alikuwa na uhakika katika mwanafunzi wake?
20 Tunaendelea kutumaini kwamba mwanafunzi wetu anataka kufanya jambo lililo sawa. Fikiria mfano wa Chifundo, dada nchini Malawi. Alianza kujifunza Biblia kwa kutumia kitabu Furahia Maisha Milele! na mwanamke kijana Mkatoliki anayeitwa Alinafe. Walipokuwa wakimaliza kuzungumzia somo la 14, Chifundo alimuuliza Alinafe maoni yake kuhusu kutumia sanamu katika ibada. Alinafe alikasirika na kujibu, “Huo ni uamuzi wa kibinafsi!” Chifundo alijiuliza ikiwa huo ulikuwa mwisho wa Alinafe kujifunza Biblia. Lakini kwa subira aliendelea kujifunza na Alinafe, akitumaini kuwa baada ya muda ataelewa kwamba jambo hilo halifai. Miezi michache baadaye, Chifundo alimuuliza swali lililo katika somo la 34: “Kufikia sasa, umenufaikaje kwa kujifunza Biblia na kumhusu Mungu wa kweli, Yehova?” Chifundo anasema hivi kuhusu kile ambacho Alinafe alisema: “Alitaja mambo mengi mazuri, jambo moja lilikuwa kwamba Mashahidi hawajihusishi na mazoea ambayo Biblia inakataza.” Muda mfupi baadaye, Alinafe aliacha kutumia sanamu na akastahili kubatizwa.
21. Tunawezaje kuimarisha tamaa ya mwanafunzi ya kuchukua msimamo upande wa kweli?
21 Hata ingawa Yehova ndiye “anayeikuza,” tunaweza kumsaidia mwanafunzi afanye maendeleo. (1 Kor. 3:7) Tunafanya mengi zaidi ya kumfundisha mambo ambayo Mungu anataka afanye. Tunamsaidia kuimarisha upendo wake kwa Yehova. Pia, tunamtia moyo aonyeshe upendo wake kwa Yehova kwa kumtanguliza maishani. Na tunamfundisha jinsi ya kumtegemea Yehova anapokabili changamoto. Kwa kuonyesha kwamba tuna uhakika naye, tunaimarisha uhakika wake kwamba anaweza kuishi kulingana na viwango vya Yehova na kusimama imara upande wa kweli.
WIMBO 55 Msiwaogope!
a Miaka miwili na nusu baada ya kukutana na Yesu, Nikodemo bado alikuwa mshiriki wa mahakama kuu ya Wayahudi. (Yoh. 7:45-52) Wanahistoria fulani wanafikiri kwamba Nikodemo alikuja kuwa mwanafunzi baada ya Yesu kufa.—Yoh. 19:38-40.
b MAELEZO YA PICHA: Petro na wavuvi wengine wanaacha biashara yao ya uvuvi ili wamfuate Yesu.
c MAELEZO YA PICHA: Dada anamsaidia mwanafunzi wake wa Biblia kujitayarisha kwa ajili ya kuhubiri hadharani.