SIMULIZI LA MAISHA
Tumejifunza Kutoka kwa Mfundishaji Wetu Mkuu Maisha Yetu Yote
VIZUIZI barabarani vyenye wanajeshi wenye silaha, vizuizi vinavyowaka moto, vimbunga, vita vya wenyewe kwa wenyewe, na amri za kuondolewa nyumbani. Hizo ni baadhi ya changamoto ambazo mimi na mke wangu tumekabili tulipokuwa mapainia na wamishonari. Ingawa tumekuwa na changamoto nyingi maishani, hatujutii kamwe maamuzi tuliyofanya! Katika changamoto hizo zote, Yehova ametutegemeza na kutubariki. Akiwa Mfundishaji wetu Mkuu, Yehova ametufundisha pia masomo muhimu.—Ayu. 36:22; Isa. 30:20.
MFANO WA WAZAZI WANGU
Mwaka wa 1957, wazazi wangu walihama kutoka Italia kwenda Kindersley, Saskatchewan, Kanada. Muda mfupi baadaye walijifunza kweli, nayo ikawa jambo kuu maishani mwetu. Ninakumbuka nilipokuwa mtoto nilihubiri kwa saa nyingi pamoja na familia yetu, hivyo nyakati nyingine ninatania kwamba nilianza “upainia msaidizi” nilipokuwa na umri wa miaka minane!
Pamoja na familia yetu, mwaka wa 1966 hivi
Wazazi wangu walikuwa maskini; hata hivyo, waliweka mfano mzuri sana wa kujidhabihu kwa ajili ya Yehova. Kwa mfano, katika mwaka wa 1963, waliuza mali zao ili wapate pesa za kutosha kuhudhuria kusanyiko la kimataifa lililofanywa Pasadena, California, Marekani. Mwaka wa 1972, tulihamia eneo la Trail, British Columbia, Kanada, umbali wa kilomita 1,000 ili kusaidia katika kazi ya kuhubiri kwenye eneo la watu wanaozungumza Kiitaliano. Baba yangu alifanya kazi za usafishaji na udumishaji kwenye duka kubwa. Alikataa kupandishwa cheo ili aweze kukazia fikira mambo ya kiroho.
Ninathamini sana mfano mzuri ambao wazazi wangu waliniwekea mimi na ndugu zangu wa kimwili watatu. Hilo liliweka msingi imara wa mazoezi yangu ya kitheokrasi, yaliyotia ndani somo hili ambalo nimelitumia maisha yangu yote: Nikiutafuta kwanza Ufalme, Yehova atanitunza.—Mt. 6:33.
NAANZA UTUMISHI WA WAKATI WOTE
Mwaka wa 1980, nilifunga ndoa na Debbie, dada mrembo aliyekuwa na malengo ya kiroho. Tulitaka kuanza utumishi wa wakati wote, hivyo Debbie alianza upainia miezi mitatu baada ya kufunga ndoa. Mwaka mmoja baada ya kufunga ndoa, tulihamia katika kutaniko dogo lililokuwa na uhitaji, nami nikajiunga naye katika utumishi wa upainia.
Siku tuliyofunga ndoa, mwaka wa 1980
Baada ya muda, tulivunjika moyo na tukaamua kuhama. Lakini kwanza tulizungumza na mwangalizi wa mzunguko. Kwa upendo na unyoofu alituambia hivi: “Ninyi ni sehemu ya tatizo. Mnakazia fikira matatizo mliyo nayo. Badala yake, mkitafuta mambo mazuri, mtayapata.” Kwa kweli, tulihitaji shauri hilo. (Zab. 141:5) Mara moja tukalitumia na tukagundua kwamba kwa kweli kulikuwa na mambo mengi mazuri. Wengi katika kutaniko walitaka kufanya mengi zaidi kwa ajili ya Yehova, kutia ndani vijana na baadhi ya akina dada ambao walikuwa na waume wasio waamini. Tulijifunza somo muhimu sana. Tulijifunza kutafuta mambo mazuri na kumngojea Yehova arekebishe hali tunayoona kuwa ngumu. (Mika 7:7) Tulipata tena shangwe, na mambo yakawa mazuri zaidi.
Walimu waliotufundisha mara ya kwanza tulipohudhuria shule ya upainia walikuwa wametumikia katika nchi za kigeni. Walipokuwa wakionyesha picha na kuzungumzia changamoto na baraka walizopata, walichochea tamaa yetu ya kuwa wamishonari. Basi tukaamua kwamba tungependa kufanya utumishi huo.
Kwenye Jumba la Ufalme huko British Columbia, mwaka wa 1983
Ili kufikia lengo hilo, mwaka wa 1984 tulihamia katika eneo la Quebec ambapo watu wanazungumza Kifaransa, lililokuwa umbali wa kilomita 4,000 kutoka British Columbia. Hilo lilimaanisha kujifunza utamaduni na lugha mpya. Changamoto nyingine ni kwamba mara nyingi hatukuwa na pesa za kutosha. Pindi moja, chakula pekee tulichokuwa nacho ni mabaki ya viazi ambavyo mkulima mmoja alituruhusu tuokote kwenye shamba lake. Debbie alitumia ubunifu mwingi kuandaa mapishi mbalimbali ya viazi! Licha ya changamoto hizo, tulikazia fikira kuvumilia tukiwa na shangwe. Isitoshe, tulijionea kwamba Yehova alikuwa anatutunza.—Zab. 64:10.
Siku moja, tulipokea simu ambayo hatukutarajia. Ulikuwa mwaliko wa kutumikia katika Betheli ya Kanada. Tulikuwa tumejaza fomu ya kuhudhuria Shule ya Gileadi, hivyo tulihisi shangwe na pia huzuni tulipoalikwa Betheli. Lakini tulikubali mwaliko huo. Tulipofika Betheli, tulimuuliza hivi Ndugu Kenneth Little, mshiriki wa Halmashauri ya Tawi, “Namna gani kuhusu maombi yetu ya kwenda Shule ya Gileadi?” Akajibu, “Tutavuka daraja hilo tutakapolifikia.”
Juma moja baadaye, tulilifikia daraja hilo kwa sababu mimi na Debbie tulialikwa kuhudhuria Shule ya Gileadi. Hivyo tulihitaji kufanya uamuzi. Ndugu Little alituambia hivi: “Haidhuru mtafanya uamuzi gani, kuna siku ambazo mtahisi kwamba afadhali mngefanya uamuzi tofauti. Njia moja si bora kuliko nyingine; Yehova anaweza kuzibariki zote.” Tulikubali mwaliko wa kwenda kuhudhuria Shule ya Gileadi, na kwa miaka mingi, tumejionea ukweli wa ushauri wa Ndugu Little. Tumenukuu mara nyingi maneno yake tulipozungumza na wale ambao wamehitaji kuchagua ni mgawo gani watakaoukubali.
MAISHA YA UMISHONARI
(Kushoto) Ulysses Glass
(Kulia) Jack Redford
Tulisisimka kuwa miongoni mwa wanafunzi 24 wa darasa la 83 la Gileadi lililofanyika Brooklyn, New York, Aprili 1987. Ndugu Ulysses Glass na Jack Redford walikuwa walimu wetu wa msingi. Miezi mitano ilipita haraka, nasi tukahitimu Septemba 6, 1987. Tulipewa mgawo wa kwenda nchini Haiti, pamoja na John na Marie Goode.
Nchini Haiti, mwaka wa 1988
Wamishonari waliohitimu Gileadi hawakuwa wametumwa nchini Haiti tangu wamishonari walipofukuzwa mwaka wa 1962. Majuma matatu baada ya kuhitimu, tulianza mgawo wetu nchini Haiti katika kutaniko dogo lenye wahubiri 35 lililokuwa eneo la mbali katikati ya milima. Tulikuwa vijana wasio na uzoefu, peke yetu katika nyumba ya wamishonari. Watu wengi walikuwa maskini sana, na wengi walikuwa hawajui kusoma. Wakati wa siku hizo za mapema za umishonari tulikabiliana na misukosuko ya kijamii, mapinduzi, vizuizi vya barabarani vinavyowaka moto, na vimbunga.
Tuliweza kujifunza mengi kutoka kwa ndugu na dada walio imara na wenye shangwe nchini Haiti. Watu wengi walikuwa na maisha magumu, lakini walimpenda Yehova na huduma. Dada mmoja mwenye umri mkubwa hakujua kusoma, lakini alikuwa amekariri mistari 150 ya Biblia. Hali hizo ziliimarisha azimio letu la kuendelea kuhubiri habari njema ya Ufalme ambayo ni suluhisho pekee la matatizo ya wanadamu. Tunatiwa moyo kuona jinsi baadhi ya wanafunzi wetu wa mapema walivyokuja kutumikia wakiwa mapainia wa kawaida, mapainia wa pekee, na wazee wa kutaniko.
Tulipokuwa nchini Haiti, nilikutana na Trevor, kijana mmishonari wa Kanisa la Mormon, na tulipata fursa ya kuzungumzia Biblia mara kadhaa. Miaka mingi baadaye, nilipokea barua kutoka kwake. Aliandika hivi: “Nitabatizwa katika kusanyiko la mzunguko linalofuata! Ninataka kurudi Haiti na kutumikia nikiwa painia wa pekee katika eneo ambalo nilikuwa mmishonari wa Kanisa la Mormon.” Yeye na mke wake walifanya hivyo kwa miaka mingi.
KUTOKA ULAYA—MPAKA AFRIKA
Nikifanya kazi nchini Slovenia, mwaka wa 1994
Tulipewa mgawo wa kutumikia katika eneo la bara la Ulaya ambapo vizuizi katika kazi yetu ya kuhubiri vilianza kuondolewa. Mwaka wa 1992, tulifika katika jiji la Ljubljana, Slovenia, karibu na eneo ambalo wazazi wangu walilelewa kabla ya kuhamia Italia. Bado vita vilikuwa vikiendelea katika maeneo ya Yugoslavia ya zamani. Ofisi ya tawi ya Vienna, Austria, pamoja na ofisi ya Zagreb, Kroatia, na Belgrade, Serbia, zilikuwa zikisimamia kazi katika eneo hilo. Sasa kila jamhuri iliyojitegemea ingekuwa na Betheli yake yenyewe.
Hilo lilimaanisha kujifunza lugha na tamaduni mpya. Wenyeji wangesema, “Jezik je težek,” maneno yanayomaanisha kwamba “Lugha hii ni ngumu.” Na kwa kweli lugha hiyo ilikuwa ngumu! Tulipendezwa na ushikamanifu wa ndugu na dada waliokuwa tayari kukubali mabadiliko ya kitengenezo na tuliona jinsi Yehova alivyowabariki. Kwa mara nyingine, tulijionea jinsi ambavyo sikuzote Yehova hurekebisha mambo kwa upendo na kwa wakati unaofaa. Miaka tuliyotumikia nchini Slovenia ilikazia akilini mwetu mambo tuliyokuwa tumejifunza awali na pia tukajifunza mambo mapya.
Lakini bado tulipokea mabadiliko mengine. Mwaka wa 2000 tulipewa mgawo wa kutumikia nchini Côte d’Ivoire, Afrika Magharibi. Kisha Novemba 2002, kwa sababu ya vita vya wenyewe kwa wenyewe tulihamishiwa nchini Sierra Leone. Vita vya wenyewe kwa wenyewe vilivyodumu kwa miaka 11 nchini humo vilikuwa vimeisha. Haikuwa rahisi kuondoka ghafla nchini Côte d’Ivoire. Hata hivyo, mambo tuliyojifunza yalitusaidia kuendelea kudumisha shangwe yetu.
Tulikazia fikira matokeo mazuri tuliyopata katika eneo hilo na ndugu na dada zetu wenye upendo waliovumilia vita kwa miaka mingi. Ingawa walikuwa maskini, bado walitaka kushiriki na wengine vitu walivyokuwa navyo. Dada mmoja alimpatia Debbie nguo kadhaa. Debbie aliposita kukubali, dada huyo alisisitiza azichukue na kusema hivi: “Wakati wa vita, ndugu kutoka nchi nyingine walitutegemeza. Sasa ni zamu yetu kutoa msaada.” Tulijiwekea lengo la kuiga mfano wao.
Hatimaye tulirudi nchini Côte d’Ivoire, lakini misukosuko ya kisiasa ililipuka tena. Hivyo, Novemba 2004, tulihamishwa kwa helikopta, kila mmoja wetu akiwa na begi lenye uzito wa kilo 10 tu. Usiku huo tulilala kwenye sakafu katika kambi ya jeshi la Ufaransa, na kesho yake tulisafirishwa kwa ndege hadi Uswisi. Tulipofika kwenye ofisi ya tawi saa sita usiku, washiriki wa Halmashauri ya Tawi na walimu wa Shule ya Mazoezi ya Kihuduma na wake zao walitukaribisha kwa uchangamfu kwa kutukumbatia, kutupatia chakula, na chokleti nyingi za Uswisi. Tuliguswa moyo sana.
Nikitoa hotuba kwenye kusanyiko nchini Côte d’Ivoire, mwaka wa 2005
Tulipewa mgawo wa muda nchini Ghana na kisha tulirudi Côte d’Ivoire misukosuko ya kijamii ilipotulia. Fadhili tulizoonyeshwa na ndugu na dada zetu zilitusaidia kukabiliana na kuhamishwa-hamishwa na migawo yetu ya muda. Mimi na Debbie tulikubaliana kwamba ingawa ni kawaida katika tengenezo la Yehova kuonyeshwa upendo wa kindugu, kamwe hatungeuchukulia kivivi hivi. Kwa kweli, hata nyakati hizo ngumu zilikuja kuwa sehemu muhimu ya mazoezi yetu.
TUNAELEKEA MASHARIKI YA KATI
Tukiwa Mashariki ya Kati, mwaka wa 2007
Mwaka wa 2006 tulipokea barua kutoka makao makuu iliyosema kwamba tumepewa mgawo mpya Mashariki ya Kati. Kwa mara nyingine tena, tulipitia matukio yenye kusisimua, changamoto, lugha na utamaduni mpya. Tulikuwa na mengi ya kujifunza katika eneo hilo lilikuwa na misukosuko mingi ya kisiasa na kidini. Tulifurahia kushirikiana kutanikoni na ndugu na dada wanaozungumza lugha mbalimbali na tulijionea umoja uliotokana na kufuata mwongozo wa kitheokrasi. Tulivutiwa na akina ndugu na dada kwa sababu wengi wao walivumilia kwa ujasiri upinzani kutoka kwa watu wa familia, wanafunzi wenzao, wafanyakazi na majirani.
Mwaka wa 2012, tulihudhuria kusanyiko la pekee lililofanyika jijini Tel Aviv, Israel. Katika kusanyiko hilo la eneo, ilikuwa mara ya kwanza kwa watu wengi hivyo wa Yehova kukusanyika pamoja tangu Pentekoste 33 W.K. Lilikuwa tukio lenye kupendeza sana!
Katika miaka hiyo, tulitumwa kwenye nchi ambayo kazi yetu ilikuwa imewekewa vizuizi. Tulibeba machapisho kadhaa, tukashiriki katika huduma ya shambani, na tukahudhuria makusanyiko madogo. Kila mahali kulikuwa na wanajeshi wenye silaha na vituo vya ukaguzi, lakini tulihisi tukiwa salama tulipokuwa tukiandamana kwa tahadhari na wahubiri wachache.
TUNARUDI AFRIKA
Nikitayarisha hotuba nchini Kongo, mwaka wa 2014
Mwaka wa 2013, tulipokea mgawo tofauti kabisa—wa kutumikia katika ofisi ya tawi ya Kinshasa, Kongo, nchi yenye mandhari maridadi lakini yenye umaskini mwingi, na mara kwa mara ilikumbwa na vita. Mwanzoni tulisema, “Tunaijua Afrika; tuko tayari.” Lakini bado tulikuwa na mambo mengi ya kujifunza, hasa ilipohusu kusafiri katika maeneo ambayo hayana miundo mbinu mizuri. Kulikuwa na mambo mengi mazuri ya kukazia fikira, kama vile uvumilivu na shangwe ya ndugu na dada licha ya matatizo ya kiuchumi, upendo wao kuelekea kazi ya kuhubiri, na jitihada zao za kuhudhuria mikutano na makusanyiko. Tulijionea jinsi kazi ya Ufalme ilivyosonga mbele kwa sababu tu ya utegemezo na baraka kutoka kwa Yehova. Miaka tuliyotumikia nchini Kongo ilitufundisha masomo muhimu na kutupatia familia kubwa ya kiroho.
Nikihubiri nchini Afrika Kusini, mwaka wa 2023
Mwishoni mwa mwaka wa 2017, tulipewa mgawo mwingine—nchini Afrika Kusini. Ofisi hii ya tawi ndiyo ofisi kubwa zaidi tuliyowahi kutumikia, na hata migawo yetu ya Betheli ilikuwa mipya kwetu. Kwa mara nyingine tena, tulikuwa na mengi ya kujifunza, lakini masomo tuliyojifunza zamani yalitusaidia. Tunawapenda ndugu na dada zetu wengi ambao wamekuwa wakivumilia kwa miaka mingi. Na ni jambo lenye kupendeza sana kuona familia ya Betheli ikifanya kazi kwa umoja licha ya kutoka katika jamii na tamaduni mbalimbali. Tunajionea wazi kwamba Yehova anawabariki watu wake kwa kuwapatia amani, kadiri wanavyoendelea kuvaa utu mpya na kutumia kanuni za Biblia.
Kwa miaka mingi, mimi na Debbie tumepokea migawo yenye kusisimua, tumejifunza kuishi kulingana na tamaduni mbalimbali, na tumejifunza lugha mpya. Haikuwa rahisi mara zote kufanya hivyo, lakini sikuzote tumejionea upendo mshikamanifu wa Yehova kupitia tengenezo na undugu wetu. (Zab. 144:2) Tunatumaini kwamba mazoezi tuliyopata katika utumishi wetu wa wakati wote yametusaidia kuwa watumishi wazuri zaidi wa Yehova.
Ninathamini sana malezi niliyopata kutoka kwa wazazi wangu; msaada ninaopata kutoka kwa mke wangu mpendwa Debbie, na mifano bora inayopatikana katika familia yetu ya kiroho ya ulimwenguni pote. Tunapotafakari wakati wetu ujao, tumeazimia kuendelea kujifunza kutoka kwa Mfundishaji wetu Mkuu.