MAKALA YA 32
WIMBO 38 Atakupa Nguvu
Jinsi Yehova Anavyotusaidia Kuvumilia
“Mungu wa fadhili zote zisizostahiliwa . . . atawafanya muwe imara, atawatia nguvu, atawapa msingi imara.”—1 PET. 5:10.
JAMBO KUU
Maandalizi ambayo Yehova anatupatia ili kutusaidia tuwe na uvumilivu na jinsi tunavyoweza kutumia maandalizi hayo.
1. Kwa nini tunahitaji kuwa na sifa ya uvumilivu, na tuna msaada gani? (1 Petro 5:10)
KATIKA siku hizi za mwisho zilizo ngumu kushughulika nazo, watu wa Yehova wanahitaji kuwa wavumilivu. Baadhi yao wamekuwa wakiugua kwa muda mrefu. Wengine wamefiwa na mpendwa wao. Wengine pia wanakabili upinzani, iwe kutoka kwa watu wa familia au maofisa wa serikali. (Mt. 10:18, 36, 37) Uwe na hakika kwamba hata iwe unakabili hali gani ngumu, Yehova anaweza kukusaidia kuvumilia.—Soma 1 Petro 5:10.
2. Uwezo wetu wa kuvumilia tukiwa Wakristo unatoka wapi?
2 Uvumilivu ni uwezo wa kustahimili na kudumisha tumaini tunapokabili vizuizi, mateso, majaribu, au vishawishi. Tukiwa Wakristo, uwezo wa kuvumilia hautokani na nguvu zetu wenyewe; badala yake, unatoka kwa Yehova, yule anayeweza kutupatia “nguvu zinazopita zile za kawaida.” (2 Kor. 4:7) Katika makala hii, tutazungumzia maandalizi manne ambayo Yehova ametupatia ili kutusaidia kuvumilia. Pia, tutaona jinsi tunavyoweza kutumia maandalizi hayo.
SALA
3. Kwa nini tunaweza kusema kwamba sala ni muujiza?
3 Yehova ametupatia uandalizi wa kimuujiza unaoweza kutusaidia kuvumilia. Ingawa sisi ni watenda dhambi, amefanya iwezekane kwetu kuwasiliana naye. (Ebr. 4:16) Fikiria jambo hili: Tunaweza kusali kwa Yehova wakati wowote na kuhusu jambo lolote. Anaweza kutusikia tukisali kwake katika lugha yoyote na mahali popote, hata ikiwa tuko peke yetu au tuko gerezani. (Yona 2:1, 2; Mdo. 16:25, 26) Ikiwa tutakuwa na mahangaiko mengi hivi kwamba tukashindwa kujieleza, bado Yehova anaweza kuelewa jambo tunalotaka kusema. (Rom. 8:26, 27) Kwa kweli, sala ni muujiza!
4. Kwa nini tunaweza kusema kwamba sala zetu za kuomba uvumilivu zinapatana na mapenzi ya Yehova?
4 Katika Neno lake, Yehova anatuhakikishia kwamba “tukiomba chochote kulingana na mapenzi yake, yeye hutusikia.” (1 Yoh. 5:14) Je, tunaweza kumwomba Yehova atusaidie kuvumilia? Ndiyo! Kufanya hivyo kunapatana na mapenzi yake. Kwa nini tunaweza kusema hivyo? Tunapovumilia majaribu, Yehova anaweza kumjibu Shetani Ibilisi, mdhihaki wake. (Met. 27:11) Kwa kuongezea, Biblia inasema kwamba Yehova anatamani “[kudhihirisha] nguvu zake kwa niaba ya wale ambao moyo wao ni kamili kumwelekea yeye.” (2 Nya. 16:9) Hivyo, tunaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova ana nguvu na anatamani kutusaidia kuvumilia.—Isa. 30:18; 41:10; Luka 11:13.
5. Sala inawezaje kutupatia amani ya akili? (Isaya 26:3)
5 Biblia inasema kwamba tunaposali kwa bidii kuhusu mambo yanayotuhangaisha, “amani ya Mungu inayozidi uelewaji wote itailinda mioyo [yetu] na nguvu [zetu] za akili.” (Flp. 4:7) Fikiria hilo linamaanisha nini. Watu wasiomtumikia Yehova wanapatwa na matatizo, na huenda wakajaribu njia mbalimbali ili kupata amani ya akili. Kwa mfano, ili wapate utulivu, baadhi ya watu wanazoea la kukaza fikira kwa kina ili kuondoa mawazo yote akilini. Watu wanaofanya hivyo, wanaweza kuwapatia nafasi roho waovu waathiri akili zao. Jambo hilo ni hatari sana. (Linganisha Mathayo 12:43-45.) Isitoshe, amani ambayo Yehova anatupatia haiwezi kulinganishwa na amani yoyote ambayo mtu anaweza kupata kupitia zoea hilo. Tunaposali kwa Yehova, tunaonyesha kwamba tunamtegemea kikamili, naye anatupatia “amani inayodumu.” (Soma Isaya 26:3.) Njia moja ambayo Yehova anafanya hivyo, ni kwa kutusaidia kukumbuka kweli zinazotufariji ambazo tumejifunza katika Neno lake. Kweli hizo hutuliza akili na mioyo yetu kwa sababu tunajua kwamba Yehova anatujali na anataka tufanikiwe.—Zab. 62:1, 2.
6. Unawezaje kutumia kikamili uandalizi wa sala? (Tazama pia picha.)
6 Unaweza kufanya nini? Unapovumilia jaribu la imani, “mtupie Yehova mzigo wako” na sali ili akupatie amani yake. (Zab. 55:22) Sali pia ili upate hekima unayohitaji kukabiliana na changamoto yako. (Met. 2:10, 11) Zaidi ya kutoa dua ili upate uvumilivu, usisahau pia kutoa shukrani. (Flp. 4:6) Tafuta mambo yanayoonyesha kwamba Yehova anakutegemeza wakati wa jaribu lako, na umshukuru kwa msaada wake. Usiruhusu jaribu lako likupofushe usione baraka ambazo tayari umepokea.—Zab. 16:5, 6.
Unaposali, unazungumza na Yehova. Unaposoma Biblia, Yehova anazungumza nawe (Tazama fungu la 6)b
NENO LA MUNGU
7. Kujifunza Biblia kunawezaje kutusaidia kuvumilia?
7 Yehova ametupatia Neno lake ili kutusaidia kuvumilia. Biblia ina maandiko mengi ambayo yanatuhakikishia kwamba Yehova atatusaidia. Fikiria mfano mmoja. Mathayo 6:8 inasema hivi: “Baba yenu anajua kile mnachohitaji hata kabla hamjamwomba.” Yesu ndiye aliyesema maneno hayo na anamjua Yehova vizuri kuliko mtu yeyote mwingine. Hivyo, hatuna sababu ya kutilia shaka kwamba Yehova anajua mahitaji yetu tunapopitia hali ngumu, naye atatusaidia. Biblia ina maandiko mengi yenye mawazo kama hayo yanayoweza kuimarisha azimio letu la kuvumilia.—Zab. 94:19.
8. (a) Toa mfano wa kanuni ya Biblia inayoweza kutusaidia kuvumilia. (b) Ni nini kinachoweza kutusaidia kukumbuka kanuni za Biblia tunapozihitaji?
8 Kanuni za Biblia zinaweza kutusaidia kuvumilia. Kwa kweli, zina hekima inayotumika inayoweza kutusaidia kufanya maamuzi yanayofaa. (Met. 2:6, 7) Kwa mfano, Biblia inatutia moyo kushughulikia siku moja baada ya nyingine, badala ya kuwa na wasiwasi kupita kiasi kuhusu mambo ya wakati ujao ambayo huenda yakatokea au yasitokee. (Mt. 6:34) Ikiwa tuna zoea la kusoma na kutafakari Maandiko, tutakuwa na uwezekano mkubwa zaidi wa kukumbuka kanuni tunazohitaji wakati tutakapozihitaji.
9. Masimulizi ya Biblia yanaimarishaje uhakika wetu kwamba Yehova atatusaidia?
9 Pia, Biblia ina masimulizi ya watu wa kawaida ambao walimtumaini Yehova, naye aliwasaidia. (Ebr. 11:32-34; Yak. 5:17) Tunapotafakari kuhusu masimulizi hayo, tunaimarisha uhakika wetu kwamba Yehova ni “kimbilio letu na nguvu zetu, msaada unaopatikana kwa urahisi nyakati za taabu.” (Zab. 46:1) Tunapofikiria kuhusu jinsi ambavyo watumishi wa zamani wa Yehova walionyesha uaminifu, tunachochewa kuiga imani na uvumilivu wao.—Yak. 5:10, 11.
10. Unawezaje kutumia kikamili uandalizi wa Neno la Mungu?
10 Unaweza kufanya nini? Soma Biblia kila siku, na hifadhi orodha ya mistari ambayo unaona itakusaidia kihususa. Watu wengi wameona kwamba kusoma andiko la siku ni njia bora ya kuanza siku kwa kuchunguza wazo lenye kutia moyo kutoka katika Biblia. Dada anayeitwa Mariea alijionea ukweli wa jambo hilo ilipogunduliwa kwamba wazazi wake wote wawili wana kansa. Ni jambo gani lililomsaidia kuvumilia alipokuwa akiwatunza katika miezi ya mwisho ya maisha yao? Anasema hivi: “Kila asubuhi, nilisoma na kutafakari andiko kutoka katika kijitabu, Kuyachunguza Maandiko Kila Siku. Ratiba hiyo ilinisaidia kujaza akili yangu mawazo ya Kimaandiko yaliyonisaidia kumkazia fikira Yehova, badala ya kukazia tu fikira tatizo lililokuwa likinihangaisha.”—Zab. 61:2.
WAABUDU WENZAKO
11. Kwa nini tunatiwa moyo kujua kwamba hatuko peke yetu tunapovumilia majaribu?
11 Yehova anatupatia ndugu na dada zetu Wakristo wanaotusaidia kuvumilia. Kujua tu kwamba “mateso yaleyale yanaupata ushirika mzima wa ndugu [zetu]” kunatuhakikishia kwamba hatuko peke yetu. (1 Pet. 5:9) Kwa kweli, tunaweza kuwa na uhakika kwamba hata ikiwa tunakabili hali gani, wengine pia wamekabili hali kama hiyo, na wamevumilia. Hilo linamaanisha kwamba sisi pia tunaweza kuvumilia!—Mdo. 14:22.
12. Waabudu wenzetu wanaweza kutusaidiaje, nasi tunaweza kuwafanyia nini? (2 Wakorintho 1:3, 4)
12 Waabudu wenzetu wanaweza kututia moyo tunapovumilia majaribu. Mtume Paulo alijionea ukweli huo. Mara nyingi, aliwashukuru wale waliomsaidia alipokuwa katika kifungo cha nyumbani, akiwataja kwa majina. Walimfariji Paulo, walimtia moyo, na kumsaidia kwa njia hususa. (Flp. 2:25, 29, 30; Kol. 4:10, 11) Leo, tunaweza kupitia hali kama hiyo. Tunapohitaji msaada ili kuvumilia jaribu, ndugu na dada zetu wako tayari kutusaidia; na watakapohitaji msaada, tuko tayari kuwasaidia.—Soma 2 Wakorintho 1:3, 4.
13. Ni nini kilichomsaidia dada anayeitwa Maya kuvumilia?
13 Ndugu na dada walimtia moyo sana Dada Maya kutoka nchini Urusi. Nyumba yake ilipekuliwa mwaka wa 2020, na baadaye alishtakiwa mahakamani kwa sababu ya kushiriki imani yake na wengine. Maya anasema hivi: “Wakati ambapo nilikuwa nimechoka sana kihisia, ndugu na dada walinipigia simu, wakaniandikia barua, na kuniambia jinsi wanavyonipenda. . . . Sikuzote nilijua nina familia kubwa inayonipenda. Lakini kuanzia 2020, nimetambua hilo hata zaidi.”
14. Tunaweza kufanya nini ili tunufaike kutokana na msaada wa waabudu wenzetu? (Tazama pia picha.)
14 Unaweza kufanya nini? Endelea kuwa karibu na ndugu na dada zako unapovumilia majaribu. Usisite kuwaomba wazee wa kutaniko msaada. Wanaweza kuwa “kibanda cha kujificha kutokana na upepo, na mahali pa kukimbilia kutokana na dhoruba ya mvua.” (Isa. 32:2, maelezo ya chini) Kumbuka kwamba Wakristo wenzako wanavumilia pia majaribu. Kumtendea kwa fadhili mtu mwenye uhitaji kutakusaidia kudumisha mtazamo unaofaa na kuwa mwenye usawaziko unapovumilia jaribu lako.—Mdo. 20:35.
Endelea kuwa karibu na ndugu na dada zako Wakristo (Tazama fungu la 14)c
TUMAINI LETU
15. Tumaini limewasaidiaje waaminifu, kutia ndani Yesu? (Waebrania 12:2)
15 Yehova ametupatia tumaini thabiti ili kutusaidia kuvumilia. (Rom. 15:13) Kumbuka jinsi tumaini lilivyomsaidia Yesu kuvumilia siku ngumu zaidi katika maisha yake alipokuwa duniani. (Soma Waebrania 12:2.) Yesu alijua kwamba uaminifu wake ungechangia katika kutetewa kwa jina la Yehova. Yesu alitazamia pia kuungana tena na Baba yake na baadaye kutumikia pamoja na ndugu zake katika Ufalme wa mbinguni. Vivyo hivyo, tumaini letu la kuishi milele katika ulimwengu mpya wa Mungu linatusaidia kuvumilia tatizo lolote tunalopata katika ulimwengu wa Shetani.
16. Tumaini lilimsaidiaje dada mmoja kuvumilia, na unajifunza nini kutokana na maelezo yake?
16 Fikiria jinsi tumaini la Ufalme lilivyomsaidia Dada Alla kutoka nchini Urusi, ambaye mume wake aliwekwa mahabusu kabla ya kesi yake kusikilizwa. Jambo hilo lilipotokea, Alla alisema hivi: “Kusali na kutafakari kuhusu tumaini letu la wakati ujao kumenisaidia nisikate tamaa. Ninajua kwamba majaribu haya yataisha. Yehova atakuwa mshindi, na sisi pia tutashinda.”
17. Tunawezaje kuonyesha kwamba tunathamini tumaini ambalo Yehova ametupatia? (Tazama pia picha.)
17 Unaweza kufanya nini? Tenga wakati na utafakari kuhusu wakati ujao maridadi ambao Yehova ameahidi. Wazia ukiwa katika ulimwengu mpya wa Mungu na utafakari kuhusu baraka tutakazokuwa nazo. Kisha, majaribu yoyote ambayo huenda tunakabili sasa yataonekana “ni ya muda mfupi na ni [mepesi].” (2 Kor. 4:17) Pia, fanya yote unayoweza ili kuwaeleza wengine kuhusu imani yako. Wazia jinsi ambavyo si rahisi kwao kukabiliana na changamoto za ulimwengu wa Shetani bila kujua kusudi la Mungu la wakati ujao. Huenda ukachochea upendezi wao kuelekea tumaini la Ufalme hata kwa kuwaambia mambo machache.
Tenga wakati na utafakari kuhusu wakati ujao maridadi ambao Yehova ameahidi (Tazama fungu la 17)d
18. Kwa nini tunaweza kuwa na uhakika katika ahadi za Yehova?
18 Baada ya kuvumilia majaribu mengi kwa mafanikio, Ayubu alimwambia hivi Yehova: “Sasa ninajua kwamba unaweza kufanya mambo yote na kwamba hakuna jambo lolote unalokusudia lisilowezekana kwako.” (Ayu. 42:2) Kama Ayubu alivyojifunza, hakuna jambo lolote linaloweza kuzuia kutimizwa kwa kusudi la Yehova. Ukweli huo unaweza kutuimarisha tunapovumilia. Kwa mfano, mwazie mwanamke mgonjwa aliyevunjika moyo kwa sababu madaktari wengi wameshindwa kumtibu. Lakini daktari mzoefu na anayetumainika anapogundua ugonjwa wake na kumweleza jinsi atakavyomtibu, mwanamke huyo anapata kitulizo, ingawa itachukua muda fulani hadi apone. Sasa anaweza kuvumilia, kwa kuwa anajua kwamba ana tumaini zuri—tumaini la kwamba atapona. Vivyo hivyo, uhakika tulio nao kuhusu tumaini letu la Paradiso inayokuja unatusaidia kuvumilia.
19. Tunahitaji nini ili tuweze kuvumilia?
19 Kama tulivyoona, Yehova anatusaidia kuvumilia majaribu kupitia sala, Neno lake, waabudu wenzetu, na tumaini letu. Ikiwa tutatumia kikamili maandalizi hayo, Yehova atatusaidia kukabiliana na changamoto maishani hadi ulimwengu wa Shetani utakapoondolewa.—Flp. 4:13.
WIMBO 33 Mtupie Yehova Mzigo Wako
a Baadhi ya majina katika makala hii yamebadilishwa.
b MAELEZO YA PICHA: Ndugu mwenye umri mkubwa akivumilia kwa uaminifu, msimu mmoja baada ya mwingine.
c MAELEZO YA PICHA: Ndugu mwenye umri mkubwa akivumilia kwa uaminifu, msimu mmoja baada ya mwingine.
d MAELEZO YA PICHA: Ndugu mwenye umri mkubwa akivumilia kwa uaminifu, msimu mmoja baada ya mwingine.