Barua Kutoka kwa Baraza Linaloongoza
Ndugu Zetu Wapendwa:
Inafurahisha kama nini kuwaandikia enyi ndugu wapendwa! Tunahisi kama alivyohisi mtume Yohana aliyesema kwamba ‘aliwapenda kweli’ waamini wenzake na kushangilia kwamba walikuwa “wanatembea katika kweli.” (2 Yoh. 1, 4) Lo! Ni baraka iliyoje kwetu sote kuijua kweli! Kweli imetuweka huru kutoka katika Babiloni Mkubwa na mafundisho yake na mapokeo yanayomvunjia Mungu heshima. Kutii yale ambayo Biblia inafundisha kumetusaidia kuwa watu wenye upendo, fadhili, na rehema. Kweli imetusaidia kuwa na msimamo safi mbele za Mungu na pia kuwa na taraja la kupata uzima wa milele.
Pia, tunafurahi sana kupokea roho ya Yehova ambayo inatuongoza kila siku na kutuimarisha. Tuna hakika kwamba ulifurahia kuchunguza sehemu mbalimbali za maandalizi hayo kutoka kwa Yehova katika Makusanyiko ya Wilaya ya hivi karibuni yenye kichwa “Kuongozwa na Roho ya Mungu.” Hali za ulimwengu zinapoendelea kuzorota, ni muhimu tutegemee roho ya Yehova yenye nguvu ituongoze katika nyakati hatari zilizo mbele yetu.
Tuna hakika kwamba mioyo yenu iliguswa mliposoma masimulizi yenye kusisimua katika Kitabu cha Mwaka kuhusu ndugu zetu ambao wamevumilia mateso mengi sana kwa sababu ya imani yao. Inashangaza kujua kwamba wengi kati ya ndugu hao waaminifu walikuwa wamebatizwa kwa muda mfupi tu au hawakuwa wamebatizwa matatizo yalipotokea. Tunawapenda sana kwa ushikamanifu wao na kwa msimamo wao kwa ajili ya uadilifu! Kwa kweli, mfano wao bora unaimarisha azimio letu la kuwa washikamanifu kwa Ufalme hata tukipata shida gani.—1 The. 1:6-8.
Ndugu na dada zetu wapendwa, tunajua kwamba mnahitaji kukabiliana na matatizo mengi ya kiuchumi na matatizo mengineyo ili familia zenu ziendelee kuwa na upendo. Si rahisi kwa baadhi yenu kutegemeza kazi ya kuhubiri Ufalme na utendaji mwingine wa kutaniko kwa ukawaida na kwa ushikamanifu. Kwa sababu hiyo, baada ya kuzungumza na kusali mara nyingi, tumefanya mabadiliko fulani kuhusiana na mikutano ya kutaniko kuanzia Januari 1, 2009 (1/1/2009). Tunatumaini kwamba mabadiliko hayo yatawawezesha kuwa na muda mrefu zaidi kwa ajili ya funzo la kibinafsi na la familia.
Tumekuwa na shangwe nyingi kuona watu wengi wakibatizwa katika makusanyiko mbalimbali mwaka uliopita. Baadhi ya waliobatizwa walikuwa na umri mdogo. Ninyi wazazi mnastahili pongezi kwa kuwalea watoto wenu waithamini kweli na kwa kuwatia moyo wajiweke wakfu kumtumikia Yehova wakiwa wachanga. Uhakika wa kwamba watoto hao wapendwa wanakabili vipingamizi vingi shuleni na bado wamestahili kubatizwa, unaonyesha kwamba wamefundishwa vizuri nyumbani.—Zab. 128:1-6.
Pia, tungependa kutaja kwamba kumekuwa na ongezeko kubwa katika mafunzo ya Biblia—na wamishonari na mapainia wetu wanaohubiri kwa bidii wamechangia sana ongezeko hilo. Sote katika Baraza Linaloongoza tunathamini sana sehemu muhimu ambayo ndugu na dada zetu ulimwenguni pote wanachangia katika kuwaambia “Njoo!” watu wenye mioyo minyoofu, na kuwaalika wote wanaoona kiu ‘wachukue maji ya uzima bure.’ (Ufu. 22:17) Tungependa kuwakaribisha kwa uchangamfu kwenye kutaniko la ulimwenguni pote ndugu 289,678 waliojiweka wakfu na kubatizwa mwaka uliopita!
Kila wakati tunapaswa kukumbuka maneno ya mtume Yohana, aliyeandika: “Ulimwengu unapitilia mbali na pia tamaa yake, lakini yeye anayefanya mapenzi ya Mungu anadumu milele.” (1 Yoh. 2:17) Kwa sasa, tunaishi karibu sana na wakati ambapo ulimwengu huu ‘utapitilia mbali’! Ni jambo la hekima kuzingatia kufanya mapenzi ya Mungu na ‘kuendelea kukesha.’ (Mt. 24:42) Hatutajuta kamwe tukifanya hivyo, na tutanufaika na fadhili zenye upendo za Yehova.—Isa. 63:7.
Tunatumaini kwamba masimulizi yenye kugusa moyo kutoka nchi nyingi yaliyo katika Kitabu cha Mwaka huu yatawatia moyo ninyi nyote mtangulize mambo ya Ufalme maishani. Tungependa kuwahakikishia kwamba nyakati zote tunawafikiria na kusali kuwahusu na tunawapenda sana. Yehova na awamiminie baraka zake kwa wingi.
Ndugu zenu,
Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova