Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • yb04 kur. 3-5
  • Barua Kutoka Kwa Baraza Linaloongoza

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Barua Kutoka Kwa Baraza Linaloongoza
  • 2004 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehovah
  • Habari Zinazolingana
  • Barua Kutoka kwa Baraza Linaloongoza
    2009 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
  • Matukio Muhimu Ya Mwaka Uliopita
    2004 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehovah
  • Barua Kutoka Kwa Baraza Linaloongoza
    2005 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
  • Mikusanyiko Uthibitisho wa Udugu Wetu
    Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
Pata Habari Zaidi
2004 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehovah
yb04 kur. 3-5

Barua Kutoka Kwa Baraza Linaloongoza

Ndugu na Dada Wapendwa:

“NA MUWE na fadhili zisizostahiliwa na amani kutoka kwa Mungu Baba yetu na Bwana Yesu Kristo.” (1 Kor. 1:3) Tunatamani sana wakati ambapo kila kitu kinachopumua kitampa Yehova utukufu ambao anastahili! (Zab. 150:6) Tunapongojea siku hiyo kuu, tunaendelea kutangaza habari njema za Ufalme wa Mungu na kufanya wanafunzi.

Kazi ya Yehova inayokaziwa fikira sasa duniani ni kuhubiriwa kwa habari njema. (Marko 13:10) Kwa sababu tunajua kabisa kwamba Yehova anapendezwa na kazi hii, tunaomba atusaidie kuifanya huku tukitambua kwamba kila mwanadamu ana nafasi ya kufaidika na mpango wa fidia. (Ufu. 14:6, 7, 14, 15) Ni kweli kwamba tunakabili magumu, lakini tunashukuru sana kwamba ‘tumevikwa nguvu kutoka juu’ ili tutimize huduma yetu!—Luka 24:49.

Inaridhisha sana kuchanganua mwaka wa utumishi uliopita na kutafakari mambo ambayo Yehova ametimiza kupitia watumishi wake waaminifu. Kwa uwezo wa roho takatifu, watu wa Mungu wameonyesha upendo wa Kikristo na kushinda chuki ulimwenguni pote. Upendo huo ulionekana wazi kwenye makusanyiko yetu. Kuanzia Juni hadi Desemba 2003, ndugu kutoka nchi zaidi ya 100 walihudhuria makusanyiko 32 ya kimataifa yaliyofanywa katika mabara sita. Mishonari, watumishi wa kimataifa, na Wanabetheli wanaotumikia katika nchi nyingine walihojiwa kwenye makusanyiko ya wilaya na ya kimataifa.

Kwenye makusanyiko hayo, tulipokea broshua ‘Ona Nchi Nzuri’ na kitabu Jifunze Kutoka kwa Mwalimu Mkuu. Mbali na hayo, ilitangazwa kwamba kitabu kilichosahihishwa cha Shule ya Utumishi wa Painia kitaanza kutumiwa mwishoni mwa mwaka wa utumishi wa 2004. Mapainia wa zamani ambao wamehudhuria shule hiyo wataalikwa hatua kwa hatua kuhudhuria shule pamoja na mapainia wapya.

Majumba mengi ya Ufalme yamejengwa hasa katika nchi maskini kwa msaada wa Mungu na ukarimu wa wanadamu. Miradi ya kupanua ofisi za tawi inaendelea katika nchi nyingi kwa sababu ya mahitaji yanayoongezeka ya chakula cha kiroho. Broshua Furahia Milele Maisha Duniani! inapatikana sasa katika lugha 299, na jumla ya nakala milioni 139 zimechapishwa; kitabu Ujuzi Uongozao Kwenye Uhai Udumuo Milele kinapatikana katika lugha 161 na zaidi ya nakala milioni 93 zimechapishwa; nakala zaidi ya milioni 200 za broshua Mungu Anataka Tufanye Nini? zimechapishwa katika lugha 267.

Tunawakaribisha kwa uchangamfu wale 258,845 ambao walionyesha kwamba wamejiweka wakfu kwa kubatizwa katika mwaka wa utumishi uliopita! Ingawa Shetani anawachukia sana kwa sababu ya kuunga mkono Ufalme wa Mungu, Yehova anawabariki sana na kuwalinda kiroho mnapokimbia shindano la mbio lililowekwa mbele yenu. (Ebr. 12:1, 2; Ufu. 12:17) Naam, iweni na hakika kwamba ‘Yeye anayewalinda hawezi kamwe kusinzia.’—Zab. 121:3.

Andiko la mwaka wa 2004, “Endeleeni kukesha . . . Iweni tayari,” linafaa kabisa. (Mt. 24:42, 44) Neno la Mungu linasema kwamba Wakristo ni kama wakaaji wa muda katika ulimwengu huu unaoangamia. (1 Pet. 2:11; 4:7) Kwa hiyo, tunahitaji kukazia fikira mambo ya kiroho, kutojishughulisha na mambo yasiyo na maana maishani, na kuchunguza mioyo yetu kwa uangalifu. “Yule joka mkubwa” anataka kutumeza ili tuwe sehemu ya mfumo wake wa mambo.—Ufu. 12:9.

Kusoma Biblia kila siku kutatusaidia sana kuendelea kuwa macho. Kunaweza kutusaidia ‘kuacha Ndiyo yetu imaanishe Ndiyo’ kuhusiana na wakfu wetu na ‘kuushikilia sana uhakika tuliokuwa nao mwanzoni imara mpaka mwisho.’ (Yak. 5:12; Ebr. 3:14) Kusoma Biblia kila siku kunaweza kutusaidia kukumbuka kwamba ulimwengu umekengeuka sana kutoka kwa kanuni za Mungu zisizobadilika. (Mal. 3:6; 2 Tim. 3:1, 13) Ujuzi wa Biblia unaweza kutusaidia kuepuka “hadithi za uwongo zilizotungwa kwa ufundi” na kubaki waaminifu kwa Yehova.—2 Pet. 1:16; 3:11.

Wazazi, mnapoendelea kuwalea watoto wenu katika nidhamu na mwongozo wa akilini wa Yehova, je, mnawasaidia kuweka miradi ya kiroho na ‘kuendelea kukesha’? (Efe. 6:4) Je, mnawazoeza kuona wakati ujao kama Yesu, yule mtu mwenye hekima zaidi aliyepata kuishi duniani, alivyouona? Yesu angaliweza kuwa seremala, mbuni, au daktari bora zaidi aliyewahi kuishi duniani, lakini alichagua huduma ya wakati wote. Mfano wake na uwachochee ninyi kuwasaidia watoto wenu kutanguliza Ufalme maishani mwao.

Jamii ya mtumwa mwaminifu, kupitia Baraza Linaloongoza, inaushukuru sana “umati mkubwa” ambao umetusaidia kutimiza daraka letu la kuhakikisha kwamba ‘habari njema ya ufalme inahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa ili kuwa ushahidi kwa mataifa yote.’ (Ufu. 7:9; Mt. 24:14, 45) Enyi wapendwa, Yehova anawahakikishia kwamba anakumbuka “kazi yenu na upendo mlioonyesha kwa ajili ya jina lake, kwa kuwa mmewahudumia watakatifu nanyi mnaendelea kuhudumu.” (Ebr. 6:10) Mnaposoma masimulizi yenye kusisimua katika kitabu hiki na kuona matokeo ya jitihada zenu, mjue kwamba mmetimiza sehemu muhimu sana katika kutoa ushahidi ulimwenguni pote.

Muwe na tumaini hakika la wakati ujao mnapoendelea ‘kukaza macho kwenye malipo ya thawabu,’ na msimruhusu mwanadamu yeyote au mashetani wawanyang’anye thawabu hiyo. (Ebr. 11:26; Kol. 2:18) Ndiyo, mtumainini Yehova, mkiwa na uhakika kwamba atawasaidia wote ambao wanampenda wapate uzima wa milele.—Yoh. 6:48-54.

Mwe na hakika kwamba tunafurahi kutumikia pamoja nanyi ili kuleta sifa kwa utukufu wa Yehova.

Ndugu zenu,

Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki