Barua Kutoka kwa Baraza Linaloongoza
Ndugu Zetu Wapendwa:
Tuna pendeleo kubwa la kuitwa kwa jina la Mwenye Enzi Kuu, Yehova! Jina hilo halina kifani nalo litadumu milele. Yehova ndiye aliyetuita kwa jina lake, na hasa tangu mwaka wa 1931, tumekuwa tukitambuliwa kwa jina hilo la pekee. (Isa. 43:10) Tunajivunia kuitwa Mashahidi wa Yehova.
Ibilisi amefanya juu chini kulifutilia mbali jina la Mungu. Chini ya utawala wake, mataifa yanalidharau jina la Yehova. Babiloni Mkubwa, milki ya ulimwengu ya dini ya uwongo, analichukia jina la Mungu naye ameliondoa katika tafsiri nyingi za Biblia. Tofauti nao, Yesu alilitukuza jina la Baba yake, na kulitanguliza katika sala ya kielelezo aliyowafundisha wafuasi wake. Alisema: “Basi, ninyi msali hivi: ‘Baba yetu uliye mbinguni, jina lako na litakaswe.’” (Mt. 6:9) Baadaye, akisali kwa hisia nyingi, alimwambia hivi Baba yake: “Nimelifunua jina lako kwa watu ulionipa kutoka ulimwenguni.” (Yoh. 17:6) Kama alivyofanya Yesu, tumeazimia hata zaidi kutangaza kwa bidii jina la Yehova kotekote duniani.
Andiko la mwaka wa 2009, ‘Toa ushahidi kamili kuhusu habari njema,’ lilituhimiza tutimize huduma yetu kwa ukamili. (Mdo. 20:24) Ni wazi kwamba Yehova amebariki jitihada zetu katika mwaka wa utumishi uliopita. Ushahidi mkubwa ulitolewa ulimwenguni pote kwa utukufu na heshima ya jina la Yehova. Kulikuwa na kilele kipya cha wahubiri 7,313,173. Wahubiri hao waliunganisha sauti zao katika kuhubiri na kuwafundisha wale wenye mioyo minyoofu ambao wanatafuta utatuzi wa matatizo yanayowakumba kila siku. Hudhurio la watu 18,168,323 kwenye Ukumbusho wa kifo cha Kristo linaonyesha kwamba huenda bado kuna mamilioni zaidi ya watu ambao wataliitia jina la Yehova kabla ya mwisho wa mfumo huu mbovu wa mambo.
Maadamu Yehova hajaleta mwisho huo, tutaendelea kuhubiri habari njema ya Ufalme kwa bidii, tukifanya yote tuwezayo ili kuwafikia watu katika maeneo yetu. (Mt. 24:14; Marko 13:10) Iwe tunahubiri nyumba kwa nyumba, kupitia barua na simu, au kwa njia zisizo rasmi, na tujitahidi kutangaza jina la Yehova, mapenzi yake, na makusudi yake kwa watu wengi iwezekanavyo.
Tuna kila sababu ya kuamini kwamba hivi karibuni Yehova atalitakasa jina lake. (Eze. 36:23) Siku ya kuwanyamazisha wote wanaolikashifu jina la Mungu inakaribia sana. Itakuwa siku tukufu kama nini kwa watumishi wote waaminifu wa Yehova, wanaotangaza jina Lake na kuunga mkono enzi yake kuu ya ulimwenguni pote!
Upendo wa Yehova ulionekana wazi kwenye Makusanyiko ya Wilaya na ya Kimataifa yenye kichwa “Endeleeni Kukesha!” yaliyofanyika sehemu mbalimbali ulimwenguni pote mwaka 2009. Makusanyiko hayo yalikuwa ya kihistoria, nayo yalituhimiza tuendelee kukesha tukiingojea siku ya Yehova.—Marko 13:37; 1 The. 5:1, 2, 4.
Kwa kweli, Yehova ni mwema; anaijaza mioyo yetu shangwe. Anatulaza katika malisho yenye majani mengi na kutuongoza mahali pa kupumzika palipo na maji mengi.—Zab. 23:1, 2; 100:2, 5.
Muwe na hakika kwamba Yehova ataendelea kuwabariki mnapoendelea kuwa na bidii katika kazi ya Ufalme siku za usoni!
Pokeeni salamu zetu za upendo wa Kikristo,
Ndugu zenu,
Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova