Kolombia
MATUKIO MUHIMU YA MWAKA ULIOPITA
Kutanguliza Kazi ya Kuhubiri Ulimwenguni Pote
JUMATANO, Septemba 23, 2015, Baraza Linaloongoza lilizijulisha familia za Betheli ulimwenguni pote kuhusu mabadiliko kadhaa ambayo yangefanywa ili kutumia kwa hekima zaidi michango kwa ajili ya kazi ya Mungu. Kisha, Jumamosi ya Oktoba 3, 2015, tangazo la Baraza Linaloongoza lilifafanua hivi: “Katika Wafilipi 1:10, tunaambiwa ‘tuhakikishe mambo yaliyo ya maana zaidi.’ Kupatana na ushauri huu wenye hekima, sisi [Baraza Linaloongoza] tunatamani kutanguliza utendaji unaochangia hali bora ya kiroho ya watu wa Mungu na maendeleo ya kazi ya kuhubiri ya ulimwenguni pote.”
Stephen Lett wa Baraza Linaloongoza alifafanua zaidi kwenye JW Broadcasting, akisema: “Baraza Linaloongoza limefikiria kwa uzito kuongeza utendaji katika kazi ya kuhubiri Ufalme, hivyo tumechanganua njia ambazo tunaweza kupunguza gharama katika ofisi zote za tawi ili kuelekeza michango hiyo katika kazi ya kuhubiri. Kwa mfano, huduma nyingi ambazo zimekuwepo Betheli kwa muda mrefu zinapunguzwa au kuondolewa. Hii itafanya kuwe na washiriki wachache wa familia ya Betheli wanaohitajika.”
Hivyo, kuanzia Septemba 2015, washiriki wa familia ya Betheli 5,500 hivi wamepewa mgawo wa kwenda shambani. Ingawa mabadiliko haya yanahitaji marekebisho makubwa, baraka za Yehova zimeonekana wazi, na mabadiliko hayo yamechochea kazi ya kuhubiri na kufundisha.
Wenzi wa ndoa nchini Sri Lanka ambao waliondolewa Betheli na kupelekwa shambani wameona jambo hilo kuwa fursa ya kuonyesha imani yao kwa Yehova na tengenezo lake. Waliandika hivi: “Hatukujua maisha yetu yangekuwaje. Lakini tulikuwa na uhakika kwamba Yehova hangetuacha. Kwa hiyo tulisali, ‘Tafadhali, Yehova, hali yoyote ile tutakayokabili, tusaidie kufanya mabadiliko ili tuweze kukutumikia tukiwa mapainia wa kawaida.’ Mwezi wa kwanza, tulikuwa na vitu vichache sana vya kimwili. Hata hivyo, tulihisi kuwa Yehova anatujali na kutupenda, na sasa tuna kipato cha kawaida kinachotuwezesha kulipia gharama za maisha. Tuna ratiba yenye mambo mengi kutia ndani kazi za nyumbani, kazi ya kimwili, na upainia. Lakini tunaweza kupanga muda wetu vizuri kwa sababu ya mazoezi tuliyopata tulipokuwa Betheli. Hakuna jambo lenye kuridhisha zaidi kuliko kuwasaidia watu kujua ukweli, na tunafurahi kwa kuwa tunaweza kufanya hivyo tukiwa mapainia.”
Nchini Kolombia, baadhi ya Wanabetheli waliopewa migawo mingine wamejifunza lugha mpya na kwenda katika maeneo ya mbali ili kuhubiri ujumbe wa Ufalme. Ndugu na dada hawa wamekuwa baraka kwa makutaniko yao mapya. Mwangalizi wa mzunguko aliandika hivi kuhusu wenzi fulani wa ndoa ambao walipangiwa kutaniko lililo kwenye mzunguko anaozungukia: “Ndugu na dada katika kutaniko wanathamini sana msaada wao. Kutaniko limeongeza bidii katika utumishi wa shambani, na ndugu wenyeji wanazoezwa jinsi ya kushughulikia majukumu mbalimbali ya kutaniko.” Wengi wa wale waliokuwa Wanabetheli, wamekuwa tayari kujitolea kusaidia kazi za Betheli kwa siku moja au zaidi katika juma.
Ndugu fulani aliyetumikia Betheli ya Japani kwa miaka 31, alipangiwa kutaniko ambalo lilikuwa na wazee wawili. Kwa kuwa kutaniko hilo lilikuwa na ratiba ya kurekebisha Jumba la Ufalme, aliamua kwamba hatafanya kazi ya kimwili kwa majuma mawili. Lakini kabla ya marekebisho hayo, tetemeko la ardhi lenye kipimo cha 7.0 lilikumba eneo la Kumamoto, mahali ambapo kutaniko lake lilikuwa. Kwa kuwa hakuwa amepanga kufanya kazi ya kimwili, aliweza kusimamia kazi ya kutoa misaada na kufanya ziara za uchungaji baada ya tetemeko hilo. Anasema hivi: “Kwa sasa, ninaweza kusema kwamba Yehova ameniweka mahali ambapo pana uhitaji mkubwa zaidi.”
Phil na Sugar, ambao walitumikia katika ofisi ya tawi ya Australasia, wanaeleza hivi: “Tulipopewa mgawo mpya, tuliazimia kudumisha maisha rahisi. Tulisali kwa Yehova atupe mwongozo utakaotusaidia kufanya maamuzi mazuri na kubariki uamuzi tutakaofanya. Tulichotaka hasa ni kuwa na ratiba itakayotuwezesha kushiriki kwa ukamili utumishi katika kutaniko la nchi ya kigeni. Kwa hakika Yehova amebariki uamuzi wetu na kutusaidia kurahisisha maisha ili tuweze kumtumikia kwa nafsi yote!” Sasa wanatumikia katika kikundi cha lugha ya Kiingereza chenye wahubiri 34 na mapainia wa kawaida 9, kilichopo katika Kisiwa cha Samal, Davao, nchini Filipino. Kwa sasa wana anwani 120 za watu wanaopendezwa ambao wanahitaji kufuatiliwa. “Kuna kazi nyingi na ya kufurahisha inayopaswa kufanywa. Tunafurahi kwamba tulimtegemea Yehova kwa ukamili. Kwa kweli hilo limeongeza imani na upendo wetu kwake!”
Dada mseja nchini Urusi ambaye alipewa mgawo wa kuwa painia wa pekee, alisema hivi: “Upainia umenipa fursa ya kushiriki katika kazi muhimu zaidi ambayo haitarudiwa tena, kazi ya kuhubiri kuhusu Ufalme wa Mungu. Ninafurahi sana kutumiwa na Yehova.” Sasa, anaongoza mafunzo sita ya Biblia. Watu hao wanatoka katika nchi ya Iraki, Nigeria, Sri Lanka, Syria, na Zambia.
Zambia: Washiriki wa zamani wa familia ya Betheli wakikaribishwa kwa uchangamfu katika makutaniko yao mapya
Washiriki wengi wa familia ya Betheli nchini Zambia, walipewa mgawo wa kuwa mapainia wa kawaida. Wanafurahia kushiriki zaidi katika utumishi wa shambani. Andrew ambaye anatumikia akiwa painia pamoja na mke wake alisema hivi: “Muda mfupi tu baada ya kuondoka Betheli, tuliwasaidia watu wawili kujua kusoma na kuandika. Mwanafunzi wetu mmoja ambaye ni mvulana mwenye umri wa miaka kumi, atatoa mgawo wake wa kwanza hivi karibuni katika mkutano wa katikati ya juma. Wenzi fulani wa ndoa ambao tuliwahubiria, walihudhuria Ukumbusho na tangu siku hiyo hawajakosa mkutano hata mmoja. Wanafanya maendeleo mazuri sana katika funzo lao la Biblia. Tunahisi kwamba mambo yote hayo hayangewezekana ikiwa hatungefuata mwongozo wa Yehova, kukubali msaada, na kusubiri baraka zake.”
Edson na Artness, ambao pia wanaishi nchini Zambia, walikuwa wameoana miezi michache tu kabla ya kupewa mgawo wa kwenda shambani. Artness anasema hivi: “Mazoezi mazuri tuliyopata Betheli yametusaidia kutumia mali zetu chache vizuri na kubaki tukiwa wenye furaha na bila madeni. Hatujutii kamwe uamuzi wetu wa kutumikia Betheli. Tumejifunza kubadili malengo yetu ya kiroho na kuyatimiza kwa kutegemea msaada wa Yehova. Imani yetu kwa Yehova imeimarishwa zaidi, na tuko tayari kuendelea kuwa washikamanifu kwa Yehova.”