Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • ijwyp makala 19
  • Kwa Nini Mimi Hujikata Kimakusudi?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kwa Nini Mimi Hujikata Kimakusudi?
  • Vijana Huuliza
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Kujikata ni nini?
  • Kwa nini watu hujikata kimakusudi?
  • Ikiwa una tatizo hilo, unawezaje kuliacha?
  • Kwa nini mimi hujiumiza?
    Amkeni!—2006
  • Aliathiri Maisha Nyingi
    Amkeni!—1995
  • Sababu Iliyonifanya Niache Kazi Yenye Pesa Nyingi
    Amkeni!—2010
  • Nitaachaje kujiumiza?
    Amkeni!—2006
Pata Habari Zaidi
Vijana Huuliza
ijwyp makala 19

VIJANA HUULIZA

Kwa Nini Mimi Hujikata Kimakusudi?

  • Kujikata ni nini?

  • Kwa nini watu hujikata kimakusudi?

  • Ikiwa una tatizo hilo, unawezaje kuliacha?

  • Mahojiano

  • Maswali ya kutafakari

  • Daftari yangu ya maandiko

Kujikata ni nini?

Kujikata ni tendo la kujidhuru kimakusudi kwa kutumia vitu vyenye ncha kali. Hiyo ni aina mojawapo tu ya kujiumiza kimakusudi. Aina nyingine za kujiumiza kimakusudi zinatia ndani kujiunguza, kujikwaruza, au kujipiga. Makala hii inazungumzia kujikata kimakusudi, lakini kanuni zinazozungumziwa zinatumika katika aina zote za kujiumiza kimakusudi.

Tahini ujuzi wako: Kweli au Si kweli.

  1. Ni wasichana peke ndio hujikata kimakusudi.

  2. Kujikata huvunja amri ya Biblia iliyo kwenye Mambo ya Walawi 19:28, inayosema: “Msijikatekate mwili wenu.”

Majibu sahihi:

  1. Si kweli. Ingawa inaonekana tatizo hilo limeenea miongoni mwa wasichana, pia wavulana fulani hujikata na hujihusisha katika ana nyingine za kujiumiza kimakusudi.

  2. Si kweli. Mambo ya Walawi 19:28 linarejelea desturi ya wapagani wa kale, na si tendo la kujiumiza kimakusudi linalozungumziwa katika makala hii. Hata hivyo, ni jambo linalopatana na akili kufikia mkataa kwamba Muumba wetu mwenye upendo hataki tujiumize.​—1 Wakorintho 6:​12; 2 Wakorintho 7:1; 1 Yohana 4:8.

Kwa nini watu hujikata kimakusudi?

Tahini ujuzi wako: Ni sababu gani unayofikiri ni sahihi zaidi?

Watu hujikata . . .

  1. kwa sababu wanajaribu kushinda maumivu yao ya kihisia.

  2. kwa sababu wanajaribu kujiua.

Jibu sahihi: A. Watu wengi wanaojikata kimakusudi hawataki kufa. Wanataka tu kumaliza maumivu yao ya kihisia.

Ona mambo ambayo vijana fulani wamesema kuhusu zoea lao ya kujikata kimakusudi.

Celia: “Liliniletea kitulizo.”

Tamara: “Ilionekana kwamba lilinipa kitulizo. Maumivu ya mwili yalikuwa afadhali kuliko maumivu ya kihisia.”

Carrie: “Sikupenda kuwa na huzuni. Kujikata kulinifanya niache kukazia fikira huzuni yangu na badala yake nikazie fikira maumivu ya mwili.”

Jerrine: “Kila mara nilipojikata kimakusudi, ni kana kwamba nilisahau matatizo yangu, na nikahisi kwamba sikuhitaji kuyashughulikia. Nilifurahia jambo hilo.”

Ikiwa una tatizo hilo, unawezaje kuliacha?

Kusali kwa Yehova Mungu kunaweza kuwa hatua muhimu ya kuacha zoea hilo. Biblia inasema: ‘Tupeni mahangaiko yenu yote juu yake, kwa sababu yeye anawajali ninyi.’​—1 Petro 5:7.

Pendekezo: Anza kwa kutoa sala fupifupi, labda ukimwambia Yehova hivi: “Naomba unisaidie.” Baada ya muda, utaweza kujieleza zaidi na kumwaga hisia zako kwa “Mungu wa faraja yote.”​— 2 Wakorintho 1:​3, 4.

Sala haipaswi kuonwa kuwa njia ya kutuliza tu hisia. Ni njia ya kuzungumza waziwazi na Baba yako wa mbinguni, ambaye anaahidi hivi: “Nitakusaidia kwelikweli. Nitakushika kwelikweli kwa mkono wangu wa kuume wa uadilifu.”​—Isaya 41:10.

Wengi wanaosumbuliwa na zoea la kujikata kimakusudi wamepata faraja pia kwa kuongea na mzazi au mtu mzima mwingine wanayemtumaini. Ona maelezo yafuatayo kutoka kwa vijana watatu ambao walifanya hivyo.

Mahojiano

  • Diana, miaka 21

  • Kathy, miaka 15

  • Lorena, miaka 17

Ulikuwa na umri gani ulipoanza kujikata kimakusudi?

Lorena: Nilianza kujikata kimakusudi nilipokuwa na umri wa karibu miaka 14.

Diana: Nilikuwa na umri wa miaka 18, na mara ambazo nilijikata zilitofautiana. Ningejikata kila siku kwa juma moja au mawili na halafu mwezi ungepita bila kujikata hata kidogo.

Kathy: Nilianza kujikata kimakusudi nilipokuwa na umri wa miaka 14. Na bado mara kwa mara ninashindwa kudhibiti zoea hilo.

Kwa nini ulitaka kujiumiza kimakusudi?

Kathy: Nilijichukia. Nilihisi kana kwamba hakuna mtu yoyote angeweza kutaka niwe rafiki yake.

Diana: Nyakati nyingine nililemewa na huzuni hivi kwamba nilijihisi hoi na kukata tamaa kabisa. Hisia hizo zilikuwa kama mnyama mkubwa tumboni mwangu na nilihisi ni lazima nijikate ili nimtoe.

Lorena: Ningeshuka moyo sana au ningekuwa na hasira au ningejihisi sifai. Na nilitaka kuondoa hisia hizo zote. Nyakati nyingine nilihisi nastahili kuumia.

Je, kujiumiza kulikuletea nafuu?

Diana: Ndiyo. Baada ya kujikata kimakusudi nilijihisi mwepesi, kana kwamba nimetua mzigo mzito.

Kathy: Kujiumiza kimakusudi ni kama tu kulia. Baada ya kujikata nilihisi nafuu kama vile baadhi ya watu wanavyopata nafuu baada ya kulia.

Lorena: Nilipojikata kimakusudi ilikuwa ni kana kwamba nilitoboa tundu ndogo kwenye puto lililojaa hisia zisizofaa. Hisia hizo zilitoka polepole badala ya kulipuka mara moja.

Je, uliogopa kuwaambia wengine kuhusu tatizo lako?

Lorena: Ndiyo. Niliogopa watu wangeniona kuwa mtu mwenye tabia za ajabu. Pia sikutaka wengine wajue kuhusu maisha yangu.

Diana: Kila mara watu waliniambia wananiona kuwa mtu thabiti, nilitaka waendelee kuniona hivyo. Nilihisi kwamba kuomba msaada kungekuwa ni kujishushia hadhi.

Kathy: Niliogopa watu wangefikiri kuwa nimevurugika kihisia, jambo hilo lingenifanya nijihisi vibaya hata zaidi. Isitoshe, nilihisi kwamba nastahili kujitendea kwa njia hiyo.

Nini kilichokusaidia kuacha kujikata kimakusudi?

Lorena: Nilimwambia mama yangu kuhusu zoea langu la kujikata kimakusudi. Pia nilipata msaada kutoka kwa daktari, ambaye alinisaidia kudhibiti hisia zangu zisizofaa. Nilishindwa kudhibiti zoea hilo mara kadhaa, lakini kuboresha mazoea yangu ya kujifunza Biblia kulinisaidia sana. Pia nina bidii katika huduma ya Kikristo. Labda mara kwa mara nitaendelea kupambana na hisia za kujiona kuwa sifai, hata hivyo zinapotokea, nitajaribu kuzidhibiti.

Kathy: Dada Mkristo ambaye alinizidi umri kwa miaka kumi hivi aligundua nina tatizo, hatimaye nikamweleza kuhusu tatizo langu. Nilishangaa aliponiambia kuwa hata yeye aliwahi kupambana na zoea la kujikata. Nilijihisi huru kuongea naye kwa sababu yeye pia alikuwa amepitia hali kama yangu. Pia nilipata msaada kutoka kwa daktari ambaye alinisaidia mimi na wazazi wangu kuelewa vizuri hali niliyokuwa napitia.

Diana: Usiku mmoja nilipokuwa nyumbani kwa wenzi wa ndoa ambao niliwatumaini, mume aligundua kuna jambo lililokuwa likinitatiza. Kwa fadhili aliniomba nimweleze tatizo langu. Mke wake alinikumbatia na kunibembeleza kama vile tu mama alivyokuwa akinifanyia nilipokuwa mtoto. Nilianza kulia, naye akalia pia. Haikuwa rahisi kuwaambia kuwa nilikuwa na zoea la kujiumiza kimakusudi, lakini nafurahi niliwaambia.

Biblia imekusaidiaje?

Diana: Biblia imenisaidia kutambua kwamba siwezi kushinda tatizo hili nikiwa peke yangu. Ninahitaji msaada wa Yehova Mungu.​—Methali 3:​5, 6.

Kathy: Kusoma Biblia​—na kujua kwamba ujumbe wake unatoka kwa Mungu​—kunanifariji sana!​—2 Timotheo 3:​16.

Lorena: Ninaposoma maandiko yanayohusu hali yangu, ninayaandika katika kijitabu changu ili niweze kuyatafakari baadaye.​—1 Timotheo 4:​15.

Je, kuna andiko hususa lililokusaidia?

Diana: Methali 18:1 inasema hivi: “Mtu anayejitenga na wengine atatafuta mapendezi yake mwenyewe; atashindana na hekima yote inayotumika.” Nyakati fulani mimi huona vigumu kuchangamana na watu, lakini andiko hilo limenisaidia kutambua kuwa kujitenga ni hatari.

Kathy: Mistari miwili ya Biblia ninayoipenda ni Mathayo 10:29 na 31. Katika andiko hilo, Yesu alisema kwamba hakuna hata shomoro mmoja anayekufa bila Yehova Mungu kujua. Kisha akaongezea hivi: “Msiogope: ninyi ni bora kuliko shomoro wengi.” Hata sasa, kusoma maneno hayo hunikumbusha kuwa nina thamani mbele za Yehova.

Lorena: Ninapenda maneno yaliyo kwenye Isaya 41:​9, 10, ambako Yehova anawaambia hivi watu wake: “Sikukukataa. Usiogope, kwa maana mimi nipo pamoja nawe. . . . Nitakutia nguvu.” Andiko hilo hunifanya nijihisi nimetiwa nguvu, nikijua kwamba Yehova ananipenda na siku zote atakuwa kando yangu.

Maswali ya kutafakari

  • Unapokuwa tayari kutafuta msaada, unaweza kumwendea nani?

  • Unaweza kusema nini unaposali kwa Yehova Mungu kuhusu tatizo lako?

  • Unaweza kuorodhesha njia mbili (ambazo hazihusishi kujiumiza kimakusudi) unazoweza kutumia kuondoa mkazo na mahangaiko yako?

Daftari yangu ya maandiko

Pendekezo: Unaposoma mstari wa Biblia unaokuhakikishia kuwa Yehova anakupenda au unaoweza kukusaidia kuwa na maoni yenye usawaziko kujihusu na kuhusu mapungufu yako, andika andiko hilo katika daftari yako. Pia andika sentensi moja au mbili ukieleza kwa nini maneno ya andiko hilo ni yenye maana kwako. Unaweza kuanza na maandiko yafuatayo ambayo Diana, Kathy, na Lorena waliyaona kuwa yenye msaada.

  • Waroma 8:​38, 39

    “Mistari hiyo inanionyesha kuwa Yehova ananipenda, hata ninapohisi kuwa hali ni mbaya sana.”​—Diana.

  • Zaburi 73:23

    “Maandiko kama hili hunihakikishia kuwa siko peke yangu. Ni kana kwamba Yehova yuko hapa kando yangu.”​—Kathy.

  • 1 Petro 5:​10

    “Huenda tusipate kitulizo mara moja; huenda tukalazimika kuteseka ‘kitambo kidogo.’ Lakini mwishowe, Yehova anaweza kutuimarisha ili tuweze kuvumilia kila jambo.”​—Lorena.

Maandiko zaidi ya kutafakari

  • Zaburi 34:18

  • Zaburi 54:4

  • Zaburi 55:22

  • Isaya 57:15

  • Mathayo 11:28, 29

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki