Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • ijwhf makala 10
  • Jinsi ya Kutumia Teknolojia kwa Usawaziko

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Jinsi ya Kutumia Teknolojia kwa Usawaziko
  • Msaada kwa Ajili ya Familia
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Unachopaswa kujua
  • Unachoweza kufanya
  • Teknolojia Inaathirije Ndoa Yako?
    Amkeni!—2021
  • Jinsi ya Kuacha Kazi “Ibaki Kazini”
    Msaada kwa Ajili ya Familia
  • “Ndoa na Iheshimiwe”
    “Jitunzeni Katika Upendo wa Mungu”
  • Katika Makala Hii
    Amkeni!—2021
Pata Habari Zaidi
Msaada kwa Ajili ya Familia
ijwhf makala 10
Mume na mke wakitumia simu zao za mkononi wakati wa mlo.

MSAADA KWA AJILI YA FAMILIA | NDOA

Jinsi ya Kutumia Teknolojia kwa Usawaziko

Matumizi ya teknolojia yanaweza kuboresha au kudhoofisha ndoa yako. Teknolojia inaathirije ndoa yako?

  • Unachopaswa kujua

  • Unachoweza kufanya

  • Wenzi wengine wa ndoa wanasema nini

  • Mwongozo wa mazungumzo

Unachopaswa kujua

  • Kutumia teknolojia kwa hekima kunaweza kuwa na faida kubwa katika ndoa. Kwa mfano, wenzi fulani hutumia teknolojia kuwasiliana wakati ambapo hawapo pamoja.

    Mume akimtumia mke wake ujumbe wenye maneno matamu wakati ambapo hawapo pamoja.

    “Ujumbe mfupi tu unaosema ‘Nakupenda’ au ‘Ninakufikiria’ unaweza kugusa moyo sana.”—Jonathan.

  • Kutumia teknolojia bila hekima kunaweza kudhoofisha ndoa. Kwa mfano, baadhi ya watu hutumia vifaa vyao kila wakati, na hivyo wanakosa kumpa mwenzi wao wakati na uangalifu anaohitaji.

    “Nina hakika kuna pindi ambazo mume wangu alitaka kuzungumza nami lakini nilikuwa nikitumia simu yangu.”—Julissa.

  • Baadhi ya watu husema kwamba wanaweza kuwa na mazungumzo ya kina na wenzi wao huku wakitumia vifaa vyao. Mwanasosholojia Sherry Turkle anasema kwamba “watu fulani hufikiri wanaweza kufanya zaidi ya jambo moja kwa wakati mmoja, lakini hilo haliwezekani.” Na kwa kweli, hilo si jambo zuri. Anaongezea kusema, “ubora wa utendaji wetu hupungua tunapofanya zaidi ya jambo moja kwa wakati mmoja.”a

    “Kuzungumza na mume wangu ni jambo lenye kufurahisha sana, lakini sihisi hivyo anapofanya jambo lingine huku akizungumza nami. Akifanya hivyo ni kana kwamba ananiambia anaweza kuwa na furaha akiwa na vifaa vyake tu.”—Sarah.

Jambo kuu: Matumizi yako ya teknolojia yanaweza kusaidia au kuathiri ndoa yako.

Unachoweza kufanya

Fahamu mambo ya kutanguliza. Biblia inasema: “Mhakikishe mambo muhimu zaidi.” (Wafilipi 1:10) Jiulize, ‘Je, mimi na mwenzi wangu hutumia vifaa vyetu kwa muda mwingi kuliko tunaotumia pamoja?’

“Inasikitisha kuona mwanamume na mwanamke wakiwa mkahawani wakitumia simu zao badala ya kuzungumza pamoja—ni kana kwamba wametekwa na vifaa vyao. Hatungependa kuwa watumwa wa teknolojia na kusahau jambo muhimu zaidi—uhusiano wetu.”—Matthew.

Weka mipaka. Biblia inasema: “Endeleeni kuangalia sana jinsi mnavyotembea, si kama watu wasio na hekima bali kama watu wenye hekima, mkiutumia vizuri kabisa wakati wenu.” (Waefeso 5:15, 16) Jiulize, ‘Je, ninaweza kutenga muda hususa wa kusoma na kujibu jumbe ambazo hazina uharaka badala ya kuzijibu mara moja?’

“Nimeona kwamba inasaidia sana kuzima mlio wa simu yangu halafu kujibu jumbe zinazoingia kwa wakati mwafaka zaidi. Ni mara chache sana kwamba utakuta kuna simu, ujumbe, au barua-pepe ya dharura sana ambayo inahitaji kujibiwa mara moja.”—Jonathan.

Ikiwezekana, acha kazi ibaki kazini. Biblia inasema hivi: “Kuna wakati uliowekwa wa kila jambo.” (Mhubiri 3:1) Jiulize maswali haya: ‘Je, ninaruhusu shughuli za kazi ziathiri maisha ya nyumbani kwa kutumia simu kufanyia kazi nyumbani? Kama ndivyo, jambo hilo linaathirije ndoa yangu? Mwenzi wangu angejibuje swali hilo?’

“Kwa sababu ya teknolojia, tuna uwezo wa kufanya kazi wakati wowote. Nilihitaji kujitahidi sana ili niepuke kutazama simu yangu kila wakati au kushughulikia mambo yanayohusu kazi ninapokuwa na mke wangu.”—Matthew.

Zungumzia matumizi ya teknolojia pamoja na mwenzi wako. Biblia inasema: “Kila mmoja na aendelee kutafuta, si faida yake mwenyewe, bali faida ya yule mtu mwingine.” (1 Wakorintho 10:24) Zungumza na mwenzi wako kuhusu jinsi kila mmoja wenu anavyotumia teknolojia na ikiwa kuna mabadiliko yoyote mnayohitaji kufanya. Mnaweza kuanza kwa kutumia mwongozo wa mazungumzo ulio katika makala hii.

“Mimi na mume wangu huambiana ukweli sikuzote, na tunajulishana ikiwa tunahisi kwamba mmoja wetu anatumia simu au tablet yake kupita kiasi. Sisi sote tunatambua kwamba hili linaweza kuwa tatizo, hivyo tunazingatia sana maoni ya kila mmoja.”—Danielle.

Jambo kuu: Hakikisha wewe si mtumwa wa teknolojia.

Wenzi wengine wa ndoa wanasema nini

Trista na Georgel.

“Muda tunaotumia jioni kuzungumza kuhusu jinsi siku yetu ilivyokuwa unaweza kuvurugwa ikiwa kila wakati tunatazama simu zetu. Tayari kuna mambo mengi maishani yanayochukua muda wetu, kwa hiyo tusingependa kupoteza muda wenye thamani wa kuwa na mwenzi wetu kwa kutazama vifaa vyetu.”—Trista, akiwa na mume wake, Georgel.

Jonathan na Katelyn.

“Mwenzi wako anahitaji umpe uangalifu wako. Sikuzote kutakuwa na ujumbe, barua-pepe, au habari mpya ya kuangalia. Lakini mara nyingi si jambo la dharura. Ikiwa kawaida unaepuka kutuma ujumbe unapoendesha gari kwa sababu hilo linaweza kusababisha madhara, kwa nini utumie kifaa chako kwa njia ambayo itaathiri ndoa yako?”—Jonathan, akiwa na mke wake, Katelyn.

Mwongozo wa mazungumzo

Kwanza, kila mmoja wenu anaweza kuchunguza maswali haya akiwa peke yake. Kisha, zungumzieni majibu pamoja.

  • Je, kuna njia zozote ambazo teknolojia imeboresha ndoa yenu?

  • Je, unahisi kwamba njia ambayo mwenzi wako anatumia teknolojia inasababisha mkazo katika ndoa yako? Ikiwa ndivyo, jinsi gani?

  • Je, unafikiri mwenzi wako atasema kwamba matumizi yako ya teknolojia yanasababisha mkazo katika ndoa yenu? Ikiwa ndivyo, jinsi gani?

  • Je, kuna sababu zozote zinazofanya iwe lazima kwako kupokea na kujibu jumbe zote zinazoingia? Ikiwa ndivyo, unaweza kufanya nini ili kuhakikisha jambo hilo halileti mkazo katika ndoa yenu?

  • Wewe na mwenzi wako mngependa kufanya mabadiliko gani kuhusiana na jinsi mnavyotumia teknolojia?

Muhtasari: Jinsi ya Kutumia Teknolojia kwa Usawaziko

Fahamu mambo ya kutanguliza. Usisahau kwamba jambo muhimu zaidi ni ndoa yako.

Weka mipaka. Je, unaweza kutenga muda fulani hususa wa kusoma na kujibu jumbe ambazo hazina uharaka badala ya kuzijibu mara tu zinapoingia?

Ikiwezekana acha kazi ibaki kazini. Hata kama unaweza kupatikana kufanya kazi wakati wote, je, ni lazima?

Zungumzia matumizi ya teknolojia pamoja na mwenzi wako. Matumizi ya teknolojia yanaathirije uhusiano wenu? Je, kuna mabadiliko yoyote mnayopaswa kufanya?

a Kutoka kwenye kitabu Reclaiming Conversation—The Power of Talk in a Digital Age.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki