GEORGIY PORCHULYAN | SIMULIZI LA MAISHA
“Kumpenda Yehova Kumenitegemeza Maishani”
Nilipokuwa na umri wa miaka 23 tu, nilipelekwa kwenye kambi ya kazi ngumu katika eneo lenye hali ngumu la Magadan, huko Siberia. Wakati huo nilikuwa nimebatizwa mwaka mmoja tu uliopita na kuwa Shahidi wa Yehova. Kwa sababu mara nyingi nilitenda bila kufikiri na nilikuwa mpya sana katika kweli, mara ya kwanza nilipojaribu kumweleza mfungwa mwingine kuhusu imani yangu, karibu tupigane.
Ni nini kilichonichochea niache kuwa Mkomunisti na nianze kushirikiana na kikundi cha kidini kilichoonwa kuwa adui wa Serikali? Upendo wa Yehova na mazoezi kutoka kwake yalinisaidiaje kuboresha utu wangu katika miaka niliyokuwa katika kambi ya kazi ngumu na pia uhamishoni?
Kupigania Haki na Kutafuta Amani ya Akili
Nilizaliwa mwaka wa 1930, huko Tabani, kijiji kilichokuwa na umaskini kaskazini mwa Moldova. Wazazi wetu walifanya kwa bidii kazi ya kufuga wanyama ili watulishe sisi watoto sita. Hatukuwa na vitu vingi vya kimwili. Mama yangu alikuwa mshiriki wa Kanisa la Othodoksi la Urusi na baba yangu alikuwa Mkatoliki. Mara nyingi walibishana vikali kwa sababu ya mambo yenye kushtua ambayo makasisi walifanya.
Nilipohitimu kutoka shuleni nikiwa na umri wa miaka 18, nilijiunga na Komsomol, kikundi cha vijana kilichofundisha Ukomunisti. Lengo lao lilikuwa kuwafunza vijana ili wajiunge na Chama cha Kikomunisti. Baada ya muda nilichaguliwa kuwa katibu wa kikundi hicho kijijini mwetu. Walifunza kwamba watu wote ni ndugu na dada, wana haki sawa, na walipaswa kutendewa bila ubaguzi, na mambo hayo yalinipendeza. Lakini nilipoona ukosefu wa haki na ufisadi mwingi katika jamii nilikata tamaa.
Nikiwa mshiriki mwenye bidii wa Komsomol, sikuwa na budi ila kuunga mkono maagizo yaliyotolewa na serikali ya Muungano wa Sovietia walipokuwa wakifunga na kusambaratisha vikundi vya kidini. Kulikuwa na Mashahidi kadhaa wa Yehova kijijini mwetu. Nilitambua walikuwa watu wanyoofu na wenye amani, lakini bado niliwaona kuwa watu wenye misimamo mikali ya kidini. Sikujua kwamba baada ya muda mfupi mmoja wao angenijibu maswali mengi niliyokuwa nayo.
Dimitriy, mjomba wangu, aliyeishi kijijini kwetu alikuwa Shahidi wa Yehova. Siku moja mnamo Mei 1952, aliniuliza, “Georgiy, unataka kufanya nini maishani?” Alinijali sana kiasi cha kuuliza swali hilo. Kwa kweli, nilikuwa na maswali mengi akilini ambayo sikuweza kupata majibu. Kwa mfano, nilijiuliza mara kwa mara, ‘Ikiwa Mungu yuko, kwa nini anaruhusu watu wateseke sana?’ Dimitriy alitumia siku nane zilizofuata kujibu maswali yangu akitumia Biblia. Wakati mwingine tulizungumza kumhusu Mungu hadi saa tisa usiku!
Siku nyingine Georgiy na Dimitriy wangekesha usiku mzima wakizungumzia Biblia
Baada ya mazungumzo hayo niliamua kujifunza Biblia kwa makini. Nikaanza kutambua kwamba nilikuwa na Baba mbinguni ambaye alinipenda sana. (Zaburi 27:10) Ingawa sikuwa na ujuzi mwingi wa Biblia, nilimpenda Yehova sana kiasi cha kufanya mabadiliko makubwa. Niliacha Chama cha Ukomunisti licha ya vitisho kutoka kwa mwenyekiti wa chama hicho kijijini mwetu. Kisha baada ya kujifunza Biblia kwa miezi minne tu, nilijiweka wakfu kwa Yehova na kubatizwa mnamo Septemba 1952.
Upendo Wangu kwa Yehova Wajaribiwa
Wakati huo, utendaji wa Mashahidi wa Yehova ulikuwa umepigwa marufuku. Hata hivyo, nilitaka kumwonyesha Yehova upendo wangu kwa matendo, basi nilijitolea kuwapelekea machapisho ya Biblia Mashahidi wenzangu ambao waliiishi katika vijiji vingine. Ilikuwa hatari kufanya hivyo kwa sababu wanakijiji wangeweza kumripoti mgeni ikiwa wangemtilia shaka. Hata baadhi ya Mashahidi walinitilia shaka, wakihofia kwamba huenda nilikuwa moja kati ya polisi wengi wa siri ambao walijifanya kuwa Mashahidi na kujiunga na kutaniko. Lakini upesi ikawa wazi kwamba sikuwa mpelelezi. Miezi miwili tu baada ya kubatizwa, nilikamatwa na kufungwa kwa sababu ya kusambaza machapisho yaliyopigwa marufuku.
Nilipokuwa mahabusu kwa kipindi cha mwaka mmoja hivi, maofisa walinihoji mara nyingi na wakajaribu kuvunja uaminifu wangu. Lakini tayari nilikuwa nimesitawisha upendo mkubwa kwa Yehova Mungu. Hatimaye, kesi yangu ilisikilizwa katika mahakama ya jiji la Odessa nchini Ukrainia. Wazazi wangu na ndugu na dada zangu, ambao hawakuwa Mashahidi wa Yehova wakati huo, waliitwa mahakamani.
Nilifikishwa mahakamani kwa shtaka la kukubali kudanganywa na kujiunga na dhehebu hatari. Wenye mamlaka walitaka wazazi wangu na ndugu na dada zangu wafikiri kwamba nilikuwa nimerukwa na akili. Wazazi wangu waliogopa. Walilia na kuniomba niache kuwa Shahidi. Lakini niliendelea kuwa mtulivu. Nikamwambia mama yangu: “Usiwe na wasiwasi. Mimi sijadanganywa. Nimepata nilichokuwa nikitafuta na sitakiacha kamwe.” (Methali 23:23) Sikuwa na ujuzi mwingi wa Biblia, lakini nilijua mambo ya kutosha kumhusu Yehova yaliyonisaidia kushikamana naye. Miaka sita hivi baadaye, wazazi wangu walichunguza zaidi imani yangu na kugundua kwamba ndio ukweli, na wao pia wakawa Mashahidi wa Yehova.
Akiwa mbele ya wazazi wake, mahakama ilimshtaki Georgiy kwa kosa la kujiunga na dhehebu hatari
Nilihukumiwa kifungo cha miaka 15 ya kazi ya kulazimishwa na nikapelekwa kwa gari-moshi hadi eneo la Kolyma, lililojulikana kwa kuwa na kambi nyingi za kazi ya kulazimishwa. Ili kuwadhibiti kabisa wafungwa, walinzi na maofisa walitupiga na kutunyima chakula. Mwanzoni sikujua jinsi ambavyo ningeweza kustahimili hali hizo.
Nilijionea Mungu Akinitunza kwa Upendo na Kunizoeza
Baada tu ya kuwasili, baadhi ya Mashahidi 34 ambao tayari walikuwa wamefungwa kambini waliniuliza kwa tahadhari: “Je, katika kikundi chenu kuna Yonadabu yeyote?” Mara moja nikajua walikuwa ndugu zangu wa kiroho. Ni wao tu ambao wangetumia neno kama hilo la Biblia! Ndugu hao wenye uzoefu walinifunza kutumia kanuni za Biblia katika hali ngumu na pia kusitawisha sifa za Kikristo kama vile utambuzi.
Nilifanya kazi kambini nikiwa mwendesha mashine. Siku moja, Matphey mfanyakazi mwenzangu, alijivuna kwamba alikuwa amekariri majina ya watakatifu 50. Nilipozungumza vibaya kuhusu watakatifu hao, Matphey alijaribu kunipiga ngumi lakini nikatoroka. Baadaye, nilikasirika nilipowaona akina ndugu wakinicheka. Nikawauliza: “Kwa nini mnanicheka? Nilitaka kuhubiri!” Kwa fadhili walinikumbusha kwamba lengo letu ni kuwaeleza watu habari njema, si kuwaudhi. (1 Petro 3:15) Matphey hakuunga mkono wala kuheshimu sera za serikali, alivutiwa na jinsi Mashahidi walivyowaheshimu walinzi na wenye mamlaka. Baada ya muda alianza kupendezwa na ujumbe wa Biblia. Siku zote nitakumbuka usiku ambao alibatizwa kisiri kwenye pipa la maji baridi.
Muda mfupi baada ya kufika kambini, mimi pamoja na ndugu wengine wawili vijana tulialikwa kuhudhuria masomo ya nadharia za kisiasa. Mwanzoni, tulikataa kuhudhuria masomo hayo. Tulifikiria kwamba kwa kuhudhuria masomo hayo tungekuwa tunakiuka msimamo wetu wa kutounga mkono upande wowote wa kisiasa. (Yohana 17:16) Kwa sababu hiyo, tuliwekwa ndani ya chumba chenye giza zito kwa majuma mawili. Tuliporuhusiwa kutoka humo, akina ndugu waliotujali walitueleza kwamba kuhudhuria tu mikutano hiyo hakungevunja msimamo wetu wa kutounga mkono upande wowote. Kwa upande mwingine, kwa kuhudhuria tungeweza kupata fursa ya kutoa ushahidi. Ndugu hao wenye upendo walitusaidia kuwa na hekima na usawaziko zaidi tunapofanya maamuzi.
Mazoezi yao yenye subira yalionyesha wazi Yehova ananipenda na kunijali. Kwa mfano, mfungwa mmoja aliyekuwa kasisi alipewa kazi ya kuwa mhasibu mkuu. Kila tulipokutana wakati wa mlo, alinisalimu kwa kusema, “Habari yako wewe mwana wa Ibilisi!” Mfungwa mwingine aliniambia nimjibu kwa kejeli, “Mzima Baba yangu!” Kwa kusikitisha nilifanya hivyo na matokeo ni kwamba nilipigwa vibaya. Akina ndugu waliposikia kilichonipata, walinisaidia kuona kwamba nilikuwa nimekosea. (Methali 29:11) Hatimaye, nilimwomba kasisi yule msamaha.
Kabla ya kupelekwa kwenye kambi ya kazi ngumu, nilikuwa nikihudhuria mikutano ya Kikristo kisiri usiku au asubuhi sana. Lakini katika kambi hiyo, hakukuwa na mahali popote pa kujificha. Kwa hiyo, kila siku, sisi akina ndugu tulisimama pamoja katika duara, mahali ambapo walinzi wangetuona ili kuzungumzia baadhi ya maandiko tuliyonakili kwenye vipande vidogo vya karatasi. Lengo letu lilikuwa kukariri maandiko mengi iwezekanayo na kujikumbusha mara kwa mara. Ofisa alipotukaribia, tulimeza karatasi zetu upesi.
Hakukuwa na mahali pa kujificha katika kambi ya kazi ngumu, basi Mashahidi walisoma Biblia wakiwa mahali ambapo walinzi wangewaona
Upendo wa Mungu Ulitufikia Hata Tukiwa Uhamishoni
Mwaka wa 1960 hivi baada Georgiy kuachiliwa huru kutoka kwenye kambi ya kazi ngumu
Mwaka wa 1959, niliachiliwa huru kutoka kambini na nikahamishiwa eneo la Karaganda huko Kazakhstan. Ingawa bado nilikuwa chini ya masharti, niliwaomba wenye mamlaka waniruhusu niondoke kwa siku 20 ili nikafunge ndoa. Nilisafiri hadi Tomsk nchini Urusi, ambako nilimfahamu mapema dada fulani mwaminifu na mrembo anayeitwa Maria. Kama kawaida yangu, nilizungumza waziwazi. Nilimwambia: “Maria, sina muda wa kukuchumbia. Tuoane!” Alikubali, na tukafanya harusi ndogo. Maria alivutiwa na kwamba nilikuwa nimevumilia majaribu mengi, na alitaka kunisaidia niendelee kumtumikia Yehova.—Methali 19:14.
Katika miaka ya 1960, hatungeweza kwenda nyumba kwa nyumba hadharani, lakini tulitumia kila fursa kuwaeleza watu kuhusu imani yetu isivyo rasmi. Tulipoalikwa na watu au tulipokuwa likizo, mara nyingi tulizungumzia tumaini letu la kuishi milele duniani. Pia, tulitafuta fursa za kuzungumza na watu. Kwa mfano, tulijaribu kuanzisha mazungumzo ya kiroho na wauzaji wa nyumba. Kwa kutumia mbinu hii, mimi na Maria tulianzisha mafunzo sita ya Biblia ambao hatimaye walibatizwa na kuwa Mashahidi wa Yehova.
Wakati mwingine, tulitoa ushahidi wakati wa uchaguzi. Siku moja, polisi wa siri walikuja kiwandani ambako mimi na ndugu wengine tulikuwa tukifanya kazi. Mbele ya wafanyakazi wenzetu 1,000 hivi walituuliza kwa nini Mashahidi wa Yehova hawajihusishi katika siasa. Mhandisi mkuu na wafanyakazi wengine kadhaa walitutetea. Waliwaambia maofisa hao kwamba tulikuwa wafanyakazi wenye kutegemeka na wenye bidii. Msaada wao ulitupatia nguvu za kueleza msimamo wetu na tukanukuu maandiko tuliyokuwa tumekariri. Kwa sababu ya ushahidi tuliotoa kwa ujasiri, wafanyakazi wanne walipendezwa na kweli ya Biblia na wakabatizwa ndani ya mwaka mmoja.
Katika miaka ya mwanzoni ya 1970, watu wengi wanyoofu nchini Kazakhstan walibatizwa na kuwa Mashahidi wa Yehova, basi tuliona uhitaji wa kupanga kusanyiko la kwanza. Lakini tungewezaje kufanya hivyo bila wenye mamlaka kujua? Tuliamua kufanya kusanyiko la siku moja pamoja na harusi wakati uleule katika kijiji kimoja karibu na jiji la Almaty. Kwa kweli, tulifanya harusi na kusanyiko la Kikristo pia, kulikuwa na wageni 300 waliojiunga pamoja na bwana na bibi harusi! Mke wangu alishirikiana na akina dada kadhaa kupamba mahali hapo na kutayarisha chakula kitamu. Wageni walifurahia hata zaidi mafundisho yanayotegemea Biblia ambayo yalitolewa na wasemaji kadhaa. Kwa mara ya kwanza maishani mwangu, siku hiyo nilitoa hotuba ya Biblia mbele ya wasikilizaji wengi.
Upendo wa Mungu Umetutegemeza Katika Majaribu Yetu
Georgiy na Maria mke wake, wakiwa na binti yao, Lyudmila
Maria, mke wangu mpendwa, alikuwa msaidizi mwaminifu maisha yake yote. Alikuwa mpole na mtiifu, na sikuzote alitanguliza masilahi ya Ufalme. Ingawa alikuwa mwenye nguvu, ghafla alipata ugonjwa mbaya sana unaodhoofisha mifupa, yaani, osteoporosis na ugonjwa huo ulimfanya alale kitandani kwa karibu miaka 16. Kwa msaada Lyudmila, binti yetu mwenye huruma, tulimtunza vizuri mpaka alipokufa mwaka wa 2014.
Mke wangu mpendwa Maria alipokuwa akiteseka, nilihisi sina nguvu. Licha ya hilo, tuliendelea kusoma pamoja Biblia na makala zenye kutia moyo hadi siku alipokufa. Mara nyingi tulizungumzia maisha katika ulimwengu mpya. Nyakati nyingine, nikiwa karibu naye nililia kwa sauti ya chini. Lakini kila mara tuliposoma kuhusu ahadi nzuri za Yehova, tulitulia na kupata nguvu za kuvumilia.—Zaburi 37:18; 41:3.
Georgiy na Lyudmila wakiwa katika mkutano wa Kikristo
Tangu siku ya kwanza nilipohisi kwamba Yehova ananipenda, sikuzote nimejionea jinsi anavyonitegemeza na kunitunza. (Zaburi 34:19) Nilipokuwa kijana asiye na uzoefu, niliona upendo wake kupitia ndugu walionisaidia kwa subira kuboresha utu wangu. Nilipokabili mateso katika kambi ya kazi ngumu na nilipokuwa uhamishoni, nilihisi Yehova akinitegemeza kupitia Neno lake. Pia alinipa nguvu ya kumtunza mke wangu mpendwa Maria, hadi alipokufa. Na sasa, ninaweza kusema kwa uhakika kwamba upendo wa Yehova umenitegemeza maisha yangu yote.—Zaburi 31:19.
a Kazakhstan, Moldova, na Ukrainia zilikuwa sehemu ya Muungano wa Sovieti hadi mwaka wa 1991.