TAPANI VIITALA | SIMULIZI LA MAISHA
Kutimiza Tamaa Yangu ya Kuwasaidia Viziwi
Nilipokutana na Mashahidi wa Yehova kwa mara ya kwanza, walinionyesha ahadi ya Biblia kwamba “masikio ya viziwi yatazibuliwa.” (Isaya 35:5) Hata hivyo, nilizaliwa kiziwi kwa hiyo, ilikuwa vigumu kwangu kuwazia itakavyokuwa nikipata uwezo wa kusikia. Basi, ahadi hiyo haikunivutia. Niliguswa moyo sana waliponionyesha kutoka kwenye Biblia kwamba Ufalme wa Mungu utaondoa ukosefu wa haki, vita, magonjwa, na hata kifo. Matokeo ni kwamba nilisitawisha tamaa kubwa ya kushiriki na viziwi wengine mambo niliyokuwa nimejifunza.
Nilizaliwa mwaka wa 1941 na watu wote wa familia yetu walikuwa viziwi. Tuliishi Virrat, Finland. Wazazi wangu, ndugu yangu mdogo, dada yangu mdogo, na watu wengi wa ukoo ni viziwi. Sote tulitumia lugha ya ishara kuwasiliana.
Kujifunza Mambo Mazuri Kutoka Kwenye Biblia
Shule yetu ilikuwa ya bweni na ilikuwa umbali wa kilomita 240 kutoka nyumbani. Hatukuruhusiwa kutumia lugha ya ishara shuleni. Enzi hizo, shule za viziwi nchini Finland ziliwalazimisha viziwi kujifunza lugha inayozungumzwa na watu wanaosikia na pia kusoma midomo ya watu wanapoongea. Ikiwa walimu wetu wangetuona tukitumia lugha ya ishara wangetuadhibu kwa fimbo au rula hivi kwamba vidole vyetu vingevimba kwa siku kadhaa.
Nilipomaliza shule ya sekondari, nilienda kwenye chuo cha mafunzo ya ukulima. Wazazi wangu walikuwa na shamba hivyo nilihitaji kujifunza ukulima. Niliporudi nyumbani niliona magazeti ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni mezani. Baba aliniambia kwamba magazeti hayo yanaeleza mambo mazuri kutoka kwenye Biblia na kwamba kulikuwa na watu fulani wenye uwezo wa kusikia waliokuwa wakijifunza Biblia pamoja na yeye na mama. Waliwasiliana na wazazi wangu kwa kuandikiana ujumbe kwenye karatasi.
Baba aliniambia kwamba chini ya Ufalme wa Mungu, dunia itabadilika na kuwa paradiso maridadi na kwamba wafu watafufuliwa. Lakini nilikuwa nimefundishwa kwamba watu wanaokufa wanaenda mbinguni. Nilidhani kwamba baba hakuwa amewaelewa Mashahidi vizuri, hasa kwa sababu hawakuwasiliana naye katika lugha ya ishara.
Ndugu huyo na mke wake walipowatembelea wazazi wangu tena, niliwauliza kuhusu mambo ambayo baba alikuwa ameniambia. Waliniambia, “Baba yako yuko sahihi.” Kisha wakanionyesha maneno ambayo Yesu alisema kuhusu ufufuo katika Yohana 5:28, 29. Walinieleza jinsi Mungu atakavyosafisha dunia kwa kuondoa uovu na pia walinieleza kwamba watu wataishi milele wakiwa na afya kamilifu na amani.—Zaburi 37:10, 11; Danieli 2:44; Ufunuo 21:1-4.
Nilikuwa na hamu ya kujua mengi zaidi basi nikaanza kujifunza Biblia na Shahidi aliyeitwa Antero ambaye alikuwa na uwezo wa kusikia. Kwa kuwa hakufahamu lugha ya ishara, nilijibu maswali yaliyo katika chapisho la kujifunzia kwa kuandika majibu yangu kwenye karatasi. Kisha, Antero aliyasoma naye pia aliandika maelezo au maswali ya ziada. Kwa subira, alitumia saa mbili kila juma kujifunza nami kwa njia hii.
Mwaka wa 1960, nilihudhuria kusanyiko la Mashahidi wa Yehova na programu hiyo ilikuwa ikitafsiriwa katika lugha ya ishara. Ijumaa alasiri, tangazo lilitolewa kwamba ubatizo ungefanywa siku inayofuata. Kwa hiyo, Jumamosi asubuhi nikabeba nguo zangu za kuogelea na taulo yangu, kisha nikabatizwa!a Haukupita muda mrefu nao wazazi wangu na wadogo zangu wakabatizwa pia.
Hatimaye, watu wote wa familia yetu walibatizwa
Kutangaza Kweli za Biblia
Nilitamani kuwaeleza viziwi wengine mambo niliyokuwa nimejifunza na njia bora zaidi ya kufanya hivyo ilikuwa kutumia lugha ya ishara. Nilianza kwa kuwahubiria kwa bidii viziwi katika eneo tuliloishi.
Kisha nikahamia Tampere, jiji kubwa lenye viwanda. Nilienda nyumba kwa nyumba nikiwatafuta viziwi na niliwauliza wenye nyumba ikiwa walimfahamu kiziwi yeyote. Kwa njia hii, nilipata mafunzo ya Biblia na baada ya miaka michache tu, kulikuwa na zaidi ya viziwi kumi walioshiriki kazi ya kuhubiri jijini Tampere.
Mwaka wa 1965, nilikutana na dada mrembo aliyeitwa Maire. Kisha tukafunga ndoa mwaka uliofuata. Maire alijifunza lugha ya ishara upesi, na alikuwa mke mshikamanifu mwenye bidii. Tulimtumikia Yehova pamoja kwa miaka hamsini.
Harusi yetu, 1966
Miaka miwili baada ya kufunga ndoa, tulipata mwana, Marko, ambaye ana uwezo wa kusikia. Nyumbani, alijifunza lugha ya mama, Kifini, na pia Lugha ya Ishara ya Kifini. Marko alibatizwa akiwa na umri wa miaka 13.
Kadiri muda ulivyosonga, tulipata watu wengi wapya katika kikundi chetu cha lugha ya ishara cha Tampere. Basi, tukaamua kuhamia jiji la Turku, ambalo halikuwa na Mashahidi viziwi. Kwa mara nyingine tena, tulienda nyumba kwa nyumba tukitafuta viziwi. Tuliishi Turku kwa miaka kadhaa na katika kipindi hicho watu 12 niliojifunza nao Biblia walibatizwa.
Kuhubiri Katika Maeneo ya Baltiki
Mwaka wa 1987, Marko alialikwa Betheli. Kwa kuwa kikundi chetu cha lugha ya ishara jijini Turku kilikuwa imara, tulianza kufanya mipango ya kuhama tena.
Katika kipindi hicho, maeneo yaliyo Mashariki mwa Ulaya yalianza kuwa na uhuru wa ibada. Januari 1992, mimi na ndugu mwingine kiziwi tulisafiri hadi Tallinn, Estonia.
Tuliwasiliana na dada Mkristo ambaye alikuwa na kaka yake aliye kiziwi. Ingawa mwanamume hiyo hakupendezwa na ujumbe wa Ufalme, kwa fadhili alitusaidia kuwapata Waestonia wengi ambao walikuwa viziwi. Usiku wa mwisho wa ziara yetu, alitupeleka kwenye mkutano wa Shirika la Viziwi la Estonia uliofanywa jijini Tallinn. Tulifika mapema na kupanga mezani vitabu na magazeti mengi ya Kiestonia na Kirusi. Tulitoa zaidi ya vitabu 100 na magazeti 200 na pia tulipata anwani 70. Jioni hiyo, msingi wa kazi ya kuhubiri katika lugha ya ishara nchini Estonia uliwekwa!
Tukisafiri kwenda kwenye mojawapo ya nchi za Baltiki
Muda mfupi baadaye, mimi na Maire tulitembelea nchi ya Estonia mara kwa mara ili kuhubiri. Tulipunguza saa tulizotumia katika kazi za kimwili na tukaamua kuwa mapainia wa kawaida. Mwaka wa 1995, tulihamia karibu na jiji la Helsinki ili iwe rahisi zaidi kusafiri hadi Tallinn kwa meli. Utumishi wetu nchini Estonia ulikuwa na matokeo mazuri kuliko tulivyotarajia!
Kulikuwa na watu wengi waliotamani kujifunza Biblia lakini tulijifunza na idadi ya watu ambao tungeweza kusaidia. Kati yao, wanafunzi 16 walifanya maendeleo na kubatizwa kutia ndani wanawake wawili wa familia moja. Wote wawili hawakuwa na uwezo wa kusikia wala kuona. Nilijifunza Biblia nao kwa kufanya ishara mikononi mwao—njia ambayo inaitwa lugha ya ishara ya vipofu.
Haikuwa rahisi kujifunza na viziwi. Wakati huo, hakukuwa na machapisho ya lugha ya ishara katika eneo letu. Kwa hiyo, nilikusanya picha zenye kuvutia kutoka kwenye machapisho yetu na kuzibandika kwenye daftari na nilizitumia sana katika huduma.
Ofisi ya tawi ya Finland iliniomba nitembelee Latvia na Lithuania nichunguze mambo yaliyohitaji kufanywa ili kuendeleza kazi ya kuhubiri katika lugha ya ishara kwenye nchi hizo za Baltiki. Tulitembelea nchi hizo mara kadhaa na tukawasaidia Mashahidi katika maeneo hayo kuwatafuta viziwi. Karibu kila nchi ina lugha yake ya ishara. Kwa hiyo, nilijifunza lugha ya ishara ya Estonia, ya Latvia, ya Lithuania, pamoja na Lugha ya Ishara ya Urusi, inayotumiwa na Warusi ambao ni viziwi wanaoishi katika maeneo ya Baltiki.
Kwa kusikitisha, baada ya miaka nane ya kuhubiri Estonia na katika nchi nyingine za Baltiki, iligunduliwa kwamba Maire ana ugonjwa wa kutetemeka (Parkinson’s disease) kwa hiyo, tulishindwa kuendelea na safari hizo.
Mipango ya Kuwasaidia Viziwi
Mwaka wa 1997, kikundi cha utafsiri cha lugha ya ishara kilianzishwa kwenye Ofisi ya Tawi ya Finland. Kwa kuwa tuliishi karibu na ofisi hiyo, mimi na Maire tulipata nafasi ya kusaidia katika kazi ya kuandaa machapisho ya lugha ya ishara, na bado ninaendelea kusaidia mara kwa mara. Tulifanya kazi pamoja na mwana wetu, Marko. Baadaye, Marko na mke wake Kirsi, walisaidia kazi ya kuwazoeza watafsiri wa lugha ya ishara katika nchi nyingine.
Tukisaidia katika kazi ya kutokeza video za Lugha ya Ishara ya Kifini
Kwa kuongeza, ofisi ya tawi ilipanga madarasa kwa ajili ya kuwasaidia wahubiri wenye uwezo wa kusikia kujifunza lugha ya ishara. Madarasa hayo yamewasaidia wengi kujiunga na makutaniko na vikundi vya lugha ya ishara. Ndugu na dada hao wanaunga mkono kazi ya kuhubiri na hata wanasaidia katika majukumu mbalimbali kutanikoni.
Tamaa Yangu ya Kuwasaidia Viziwi Bado Inawaka
Mwaka wa 2004, mimi na Maire tulisaidia kuanzisha kutaniko la kwanza la lugha ya ishara jijini Helsinki. Baada ya miaka mitatu, kutaniko hilo likawa imara na lilikuwa na mapainia wengi wenye bidii.
Kwa mara nyingine tena, tulianza kufanya mipango ya kuhamia eneo lenye uhitaji mkubwa zaidi. Mwaka wa 2008, tulihamia karibu na jiji la Tampere na tukarudi kwenye kikundi cha lugha ya ishara tulichokuwa tumeacha huko miaka 34 mapema. Baada ya mwaka mmoja, kikundi hicho kikawa kutaniko la pili la lugha ya ishara nchini Finland.
Kufikia wakati huo, afya ya Maire ilikuwa ikizorota kwa kasi. Nilifurahia kumtunza mke wangu hadi alipokufa mwaka wa 2016. Ninamkosa sana Maire lakini ninatazamia kwa hamu kumwona katika ulimwengu mpya ambapo magonjwa hayatakuwepo.—Isaya 33:24; Ufunuo 21:4.
Maishani mwangu, nimetanguliza kazi ya kuwahubiria viziwi kwa miaka 60 na tamaa yangu ya kuwaeleza habari njema bado inaendelea kuwaka!
a Wakati huo mpango wa wazee kuzungumza na watu wanaotaka kubatizwa haukuwa umeanzishwa.