JINSI MICHANGO YAKO INAVYOTUMIWA
Kutoa Msaada Katika 2021—Hatuwaachi Ndugu na Dada Zetu
JANUARI 1, 2022
Ulimwengu uliendelea kuteseka kwa sababu ya janga la COVID-19 katika mwaka wa utumishi wa 2021.a Kama ilivyoelezwa katika makala “Msaada Ulimwenguni Pote kwa Ajili ya Janga la Ulimwenguni Pote,” tumetumia mamilioni ya dolab ili kutoa msaada wakati wa janga, na Halmashauri za Kutoa Msaada zaidi ya 950 zilianzishwa.
Hata hivyo, janga hilo lilipokuwa limepamba moto, bado misiba mingine ya asili na misiba iliyosababishwa na wanadamu, iliwaathiri ndugu na dada zetu katika sehemu mbalimbali ulimwenguni. Ili kushughulikia misiba mbalimbali zaidi ya 200, Halmashauri ya Waratibu ya Baraza Linaloongoza iliidhinisha kutumia dola milioni 8, bila kuhesabu msaada uliotolewa kwa ajili ya COVID-19. Ona jinsi michango yako ilivyotumiwa ili kuwasaidia waathiriwa wa misiba miwili iliyotokea hivi karibuni.
Mlipuko wa Mlima Nyiragongo
Mei 22, 2021, Mlima Nyiragongo, volkano, katika Jamhuri ya Demokrasia ya Kongo, ulianza kulipuka. Mtiririko wa lava uliharibu nyumba, shule, na hifadhi ya maji. Kulikuwa na hatari nyingine zaidi ya lava. Siku kadhaa baada ya mlipuko huo, bado kulikuwa na vumbi lenye sumu kutoka kwenye volkano lililofunika jiji la Goma, na pia kulikuwa na mitetemeko mingi ya ardhi midogo-midogo. Zaidi ya nusu ya watu wanaoishi jijini humo walilazimika kuhama. Mamia ya maelfu ya watu walitoroka, na baadhi yao wakavuka mpaka na kuingia Rwanda.
Halmashauri ya kutoa msaada ya eneo hili inaandaa uji kwenye eneo la Jumba la Ufalme
Mashahidi wa Yehova 5,000 hivi, walikuwa kati ya watu waliolazimika kuhama. Baadhi yao, nyumba zao ziliharibiwa na mlipuko, ilhali za wengine ziliporwa baada ya wao kutoroka. Halmashauri za kutoa msaada nchini Rwanda na Jamhuri ya Demokrasia ya Kongo zilifanya kazi pamoja ili kutoa msaada. Halmashauri ya tawi ya Kongo (Kinshasa) inaripoti hivi kuhusiana na halmashauri moja ya kutoa msaada: “Hata ingawa kulikuwa na vurugu jijini, hata kabla ya watu kuamuriwa kuhama, halmashauri hiyo ilikuwa imeanza kugawa chakula, maji, mashuka na blanketi, na nguo.” Katika jiji moja ambapo zaidi ya ndugu zetu 2,000 walikuwa wamekusanyika, halmashauri ya kutoa msaada iliweka mahema, wakawapa watu barakoa, na kuwaeleza jinsi ya kupunguza hatari ya kuambukizwa COVID-19 na ugonjwa wa kipindupindu.
Mifuko ya chakula ikipimwa kabla ya kupelekwa kwa Mashahidi waliolazimika kuhama makao yao
Miezi mitatu baada ya msiba huo kutokea, tayari ndugu zetu walikuwa wamegawa zaidi ya tani sita za mchele, tani sita za unga wa mahindi, tani tatu za mafuta ya kupikia, na tani tatu za maji. Ili kuokoa pesa, ofisi ya tawi ilipanga kununua chakula kingi katika maeneo ya karibu, badala ya kuagiza chakula ghali kutoka ng’ambo.
Dada mmoja ambaye nyumba yake mpya iliharibiwa na mlipuko huo, anasema hivi: “Tulikuwa na huzuni na uchungu mwingi.” Lakini familia yake ikapata msaada wa kimwili na wa kiroho pia. Sasa anasema: “Kwa msaada wa Yehova, bado tunapata mahitaji yetu. Tumeona kwamba Yehova anatubebea mizigo yetu na anafanya iwe rahisi kwetu kustahimili.”
Kuzorota kwa Uchumi Nchini Venezuela
Nchi ya Venezuela imekuwa na matatizo makubwa ya kiuchumi, kwa miaka mingi. Ndugu zetu huko wanakabili hali ngumu za maisha, upungufu wa chakula, na kuongezeka kwa uhalifu. Hata hivyo, tengenezo la Yehova halijawaacha.
Kupakia magunia ya mchele yatakayopelekwa sehemu mbalimbali za Venezuela
Katika mwaka wa utumishi uliopita, zaidi ya dola milioni 1.5, zilitumiwa kununua chakula na sabuni kwa ajili ya familia zilizokuwa na uhitaji. Ofisi ya tawi ya Venezuela inaripoti hivi: “Si rahisi kusafirisha tani 130 za chakula nchini kote kila mwezi, na kuhakikisha kwamba ndugu zetu wanaohitaji chakula hicho wamekipata.” Ili kuhakikisha kwamba chakula hakiozi, kwa kawaida akina ndugu hutuma chakula ambacho kinaweza kudumu muda mrefu. Ofisi hiyo ya tawi inaongezea hivi: “Tunanunua chakula kwa wingi wakati wa mavuno, na pia wakati bei za chakula zimeshuka. Kisha tunakisafirisha katika njia isiyotumia pesa nyingi.
Kwa sababu ya ukosefu mkubwa wa mafuta na hata magari ya kutumia, akina ndugu vijana husafiri kilomita 18, kwenda na kurudi, kwa baiskeli, ili kuwapelekea chakula ndugu na dada katika kutaniko lao
Leonel, ambaye ni mshiriki wa Halmashauri ya Kutoa Msaada nchini Venezuela, anapenda mgawo wake. Anasema hivi: “Kazi ya kutoa msaada ni ya pekee. Pendeleo hili limenitia moyo sana hasa baada ya kumpoteza mke wangu kutokana na COVID-19. Ninakuwa na mengi ya kufanya na ninafurahi kuwatumikia akina ndugu walio na uhitaji. Nimejionea jinsi Yehova anavyotimiza ahadi yake ya kutowaacha watu wake.”
Ndugu mmoja aliyepokea msaada, hapo awali alitumikia katika halmashauri ya kutoa msaada. Anasema hivi: “Sasa ni wakati wangu wa kupata msaada. Hatukupata tu msaada wa kimwili. Pia, akina ndugu walinisaidia mimi na mke wangu kubaki watulivu. Walitujali, wakatufariji, na kututia moyo.”
Misiba mingine hutokea ghafula. Lakini, mara nyingi tengenezo la Yehova linapata na kupeleka misaada upesi. Hilo linawezekana kwa sababu ya michango unayotoa kwa ajili ya kazi ya ulimwenguni pote. Baadhi ya njia za kutoa michango zimeelezwa katika donate.jw.org. Tunathamini ukarimu wako.
a Mwaka wa utumishi wa 2021 ulianza Septemba 1, 2020, na kuisha Agosti 31, 2021.
b Makala hii inapotaja dola, inarejelea dola za Marekani.