Alhamisi, Novemba 6
Toeni shukrani kuhusu kila jambo.—1 The. 5:18.
Tuna sababu nyingi za kumshukuru Yehova katika sala. Tunaweza kumshukuru kwa ajili ya kitu chochote kizuri tulicho nacho; kwa sababu kila zawadi njema hutoka kwake. (Yak. 1:17) Kwa mfano, tunaweza kumshukuru kwa dunia yetu maridadi na vitu vyenye kustaajabisha alivyoumba. Pia, tunaweza kumshukuru kwa uhai wetu, familia yetu, rafiki zetu, na tumaini letu. Na tungependa kumshukuru Yehova kwa kuturuhusu tufurahie urafiki wenye thamani pamoja naye. Huenda tukahitaji kufanya jitihada za pekee ili kufikiria sababu ambazo zinatufanya sisi binafsi tumshukuru Yehova. Tunaishi katika ulimwengu usio na shukrani. Mara nyingi watu hukazia fikira vitu wanavyotaka, badala ya kukazia fikira mambo wanayoweza kufanya ili kuonyesha shukrani kwa ajili ya vitu walivyo navyo. Ikiwa tutaathiriwa na mtazamo huo, sala zetu zinaweza kuwa orodha ya mambo tunayotaka. Ili jambo hilo lisitokee, tunapaswa kuendelea kusitawisha na kuonyesha shukrani kwa ajili ya mambo yote ambayo Yehova anatufanyia.—Luka 6:45. w23.05 4 ¶8-9
Ijumaa, Novemba 7
[Endeleeni] kuomba kwa imani, bila kuwa na shaka hata kidogo.—Yak. 1:6.
Akiwa Baba yetu mwenye upendo, Yehova hapendi kuona tukiteseka. (Isa. 63:9) Hata hivyo, hazuii majaribu yetu yote, ambayo yanaweza kulinganishwa na mito au miali ya moto. (Isa. 43:2) Lakini anaahidi atatusaidia ‘tunapopita katika’ majaribu hayo. Na hataruhusu majaribu yetu yatusababishie madhara ya kudumu. Pia, Yehova anatupatia roho yake takatifu yenye nguvu ili itusaidie kuvumilia. (Luka 11:13; Flp. 4:13) Hivyo, tunaweza kuwa na uhakika kwamba sikuzote atatupatia mambo tunayohitaji ili tuvumilie na kuendelea kuwa waaminifu kwake. Yehova anatarajia tumtumaini. (Ebr. 11:6) Wakati mwingine, tunaweza kulemewa na majaribu yetu. Huenda hata tukawa na shaka ikiwa Yehova atatusaidia. Lakini Biblia inatuhakikishia kwamba kwa nguvu za Mungu tunaweza “kuupanda ukuta.” (Zab. 18:29) Hivyo, badala ya kuwa na shaka, tunapaswa kusali tukiwa na imani kamili, tukiamini kwamba Yehova atajibu sala zetu.—Yak. 1:6, 7. w23.11 22 ¶8-9
Jumamosi, Novemba 8
Miale [ya upendo] ni moto mkali, mwali wa Yah. Maji yenye nguvu hayawezi kuuzima upendo, wala mito haiwezi kuufagilia mbali.—Wim. 8:6, 7.
Huo ni ufafanuzi maridadi sana wa upendo wa kweli! Maneno hayo yanawahakikishia hivi wenzi wa ndoa: Mnaweza kuwa na upendo wa kweli kati yenu. Wenzi wa ndoa wanahitaji kujitahidi ili kuwa na upendo unaodumu. Kwa mfano, moto wa kuni unaweza kuendelea kuwaka daima—ikiwa tu utaendelea kuongezwa kuni. Bila kuongeza kuni, mwishowe moto huo utazima. Vivyo hivyo, upendo kati ya mume na mke unaweza kuendelea kuwa wenye nguvu daima—ikiwa tu wataimarisha uhusiano wao. Nyakati fulani, huenda wakahisi upendo kati yao unapoa, hasa ikiwa wanakabili matatizo ya kifedha, matatizo ya kiafya, au mkazo wa kulea watoto. Hivyo, ili “mwali wa Yah” uendelee kuwaka, mume na mke wanapaswa kuwa na uhusiano wenye nguvu pamoja na Yehova. w23.05 20-21 ¶1-3