Jumatatu, Julai 21
Endeleeni kufarijiana.—1 The. 4:18.
Kwa nini kuwafariji wengine ni njia muhimu ya kuwaonyesha kwamba tunawapenda? Kulingana na rejeo fulani la Biblia, neno “kufarijiana” ambalo Paulo alitumia linamaanisha “kusimama kando ya mtu na kumtia moyo anapopata majaribu makali.” Hivyo, tunapotoa faraja tunamsaidia mwabudu mwenzetu anayekabili hali ngumu, asimame na kuendelea kutembea katika barabara ya uzima. Kila mara tunapomfariji ndugu au dada yetu, tunamwonyesha upendo mwabudu mwenzetu. (2 Kor. 7:6, 7, 13) Kuonyesha huruma na kufariji ni sifa zinazohusiana kwa ukaribu. Kwa njia gani? Mtu mwenye huruma huchochewa kuwafariji wengine na kujitahidi kuwapunguzia mateso yao. Hivyo, kwanza tunaonyesha huruma; kisha tunawafariji wengine. Ona jinsi Paulo anavyohusianisha huruma ya Yehova na faraja anayotoa. Paulo anamfafanua Yehova kuwa “Baba wa rehema nyororo na Mungu wa faraja yote.”—2 Kor. 1:3. w23.11 9-10 ¶8-10
Jumanne, Julai 22
Tushangilie tukiwa katika dhiki.—Rom. 5:3.
Wafuasi wote wa Kristo wanaweza kutazamia kupata dhiki. Fikiria mfano wa mtume Paulo. Aliwaambia hivi Wathesalonike: “Tulipokuwa pamoja nanyi, tulikuwa tukiwaambia mapema kwamba tutapatwa na dhiki, na imekuwa hivyo.” (1 The. 3:4) Na aliwaandikia hivi Wakorintho: “Hatutaki mkose kujua, akina ndugu, kuhusu dhiki tuliyopata . . . Hatukuwa na uhakika hata kuhusu uhai wetu. (2 Kor. 1:8; 11:23-27) Leo pia, Wakristo wanaweza kutazamia kupatwa na dhiki ya aina fulani. (2 Tim. 3:12) Kwa sababu ya kumwamini Yesu na kumfuata, huenda marafiki na watu wa ukoo wakakutendea kwa ukatili. Je, unapata matatizo kazini kwa sababu ya azimio lako la kuendelea kuwa mnyoofu katika mambo yote? (Ebr. 13:18) Je, umekabili upinzani kutoka kwa serikali kwa sababu ya kuwaambia wengine tumaini lako? Hata tukabili dhiki ya aina gani, Paulo anasema tunapaswa kushangilia. w23.12 10-11 ¶9-10
Jumatano, Julai 23
Mmeniletea taabu kubwa.—Mwa. 34:30.
Yakobo alikabili matatizo mengi. Wana wawili ya Yakobo, Simoni na Lawi, waliletea familia yao aibu, na kuliletea suto jina la Yehova. Isitoshe, Raheli, mke mpendwa wa Yakobo, alikufa alipokuwa akijifungua mtoto wao wa pili. Na kwa sababu ya njaa kali, Yakobo alilazimika kuhamia nchini Misri alipokuwa amezeeka. (Mwa. 35:16-19; 37:28; 45:9-11, 28) Licha ya matatizo hayo yote, Yakobo hakupoteza imani yake katika Yehova na katika ahadi Zake. Naye Yehova, akamwonyesha Yakobo kwamba alikuwa na kibali chake. Kwa mfano, Yehova alimbariki Yakobo kwa kumpa mali nyingi. Na wazia jinsi Yakobo alivyomshukuru Yehova alipoungana tena na mwanaye Yosefu—mwana ambaye alidhani alikufa muda mrefu uliopita! Urafiki wa karibu kati ya Yakobo na Yehova, ulimsaidia kukabiliana na majaribu yake kwa mafanikio. (Mwa. 30:43; 32:9, 10; 46:28-30) Ikiwa tutadumisha urafiki wa karibu pamoja na Yehova, sisi pia tunaweza kukabiliana kwa mafanikio na majaribu tusiyotarajia. w23.04 15 ¶6-7