Jumatano, Julai 23
Mmeniletea taabu kubwa.—Mwa. 34:30.
Yakobo alikabili matatizo mengi. Wana wawili ya Yakobo, Simoni na Lawi, waliletea familia yao aibu, na kuliletea suto jina la Yehova. Isitoshe, Raheli, mke mpendwa wa Yakobo, alikufa alipokuwa akijifungua mtoto wao wa pili. Na kwa sababu ya njaa kali, Yakobo alilazimika kuhamia nchini Misri alipokuwa amezeeka. (Mwa. 35:16-19; 37:28; 45:9-11, 28) Licha ya matatizo hayo yote, Yakobo hakupoteza imani yake katika Yehova na katika ahadi Zake. Naye Yehova, akamwonyesha Yakobo kwamba alikuwa na kibali chake. Kwa mfano, Yehova alimbariki Yakobo kwa kumpa mali nyingi. Na wazia jinsi Yakobo alivyomshukuru Yehova alipoungana tena na mwanaye Yosefu—mwana ambaye alidhani alikufa muda mrefu uliopita! Urafiki wa karibu kati ya Yakobo na Yehova, ulimsaidia kukabiliana na majaribu yake kwa mafanikio. (Mwa. 30:43; 32:9, 10; 46:28-30) Ikiwa tutadumisha urafiki wa karibu pamoja na Yehova, sisi pia tunaweza kukabiliana kwa mafanikio na majaribu tusiyotarajia. w23.04 15 ¶6-7
Alhamisi, Julai 24
Yehova ni Mchungaji wangu. Sitakosa chochote.—Zab. 23:1.
Zaburi ya 23 ni wimbo unaotuhakikishia kwamba Yehova anatupenda na kututunza kwa wororo. Daudi, mwandishi wa zaburi hii, anaeleza kuhusu uhusiano wa karibu uliopo kati yake na Mchungaji wake, Yehova. Daudi alihisi akiwa salama kwa kumruhusu Yehova amwongoze, na alimtegemea Yehova kikamili. Daudi alijua kwamba upendo wa Yehova ungemfuatia sikuzote za maisha yake. Kwa nini alikuwa na uhakika huo? Daudi alihisi anatunzwa vizuri kwa sababu sikuzote Yehova alimpatia mahitaji yake. Pia, Daudi alifurahia urafiki na kibali cha Yehova. Ndiyo maana alikuwa na uhakika kwamba hata nini kitokee wakati ujao, Yehova angeendelea kumwandalia mahitaji yake. Kwa kuwa Daudi aliamini kwamba Yehova anampenda na angemtunza, hilo lilimsaidia asiogope, bali awe na furaha na aridhike.—Zab. 16:11. w24.01 29 ¶12-13
Ijumaa, Julai 25
Mimi nipo pamoja nanyi sikuzote mpaka umalizio wa mfumo wa mambo.—Mt. 28:20.
Tangu Vita vya Pili vya Ulimwengu, watu wa Yehova katika nchi nyingi wamefurahia amani ya kadiri na uhuru wanapoendelea na kazi ya kuhubiri. Isitoshe, kazi hiyo imekuwa na matokeo makubwa. Leo, washiriki wa Baraza Linaloongoza wanaendelea kuutegemea mwongozo wa Kristo. Wangependa maagizo wanayowapatia akina ndugu yapatane na maoni ya Yehova na Yesu. Na wanawatumia waangalizi wa mzunguko na wazee ili kuyapatia makutaniko mwongozo. Wazee watiwa-mafuta wako kwenye ‘mkono wa kuume’ wa Kristo. (Ufu. 2:1) Bila shaka, wazee hao si wakamilifu na wanafanya makosa. Pindi fulani Musa na Yoshua walifanya makosa, kama ilivyokuwa kwa mitume pia. (Hes. 20:12; Yos. 9:14, 15; Rom. 3:23) Bado Kristo anamwongoza kwa makini mtumwa mwaminifu na wazee waliowekwa rasmi, na ataendelea kufanya hivyo. Hivyo, tuna kila sababu ya kutumaini mwongozo ambao anatupatia kupitia wale aliowaweka rasmi ili kuongoza. w24.02 23-24 ¶13-14