Alhamisi, Julai 24
Yehova ni Mchungaji wangu. Sitakosa chochote.—Zab. 23:1.
Zaburi ya 23 ni wimbo unaotuhakikishia kwamba Yehova anatupenda na kututunza kwa wororo. Daudi, mwandishi wa zaburi hii, anaeleza kuhusu uhusiano wa karibu uliopo kati yake na Mchungaji wake, Yehova. Daudi alihisi akiwa salama kwa kumruhusu Yehova amwongoze, na alimtegemea Yehova kikamili. Daudi alijua kwamba upendo wa Yehova ungemfuatia sikuzote za maisha yake. Kwa nini alikuwa na uhakika huo? Daudi alihisi anatunzwa vizuri kwa sababu sikuzote Yehova alimpatia mahitaji yake. Pia, Daudi alifurahia urafiki na kibali cha Yehova. Ndiyo maana alikuwa na uhakika kwamba hata nini kitokee wakati ujao, Yehova angeendelea kumwandalia mahitaji yake. Kwa kuwa Daudi aliamini kwamba Yehova anampenda na angemtunza, hilo lilimsaidia asiogope, bali awe na furaha na aridhike.—Zab. 16:11. w24.01 29 ¶12-13
Ijumaa, Julai 25
Mimi nipo pamoja nanyi sikuzote mpaka umalizio wa mfumo wa mambo.—Mt. 28:20.
Tangu Vita vya Pili vya Ulimwengu, watu wa Yehova katika nchi nyingi wamefurahia amani ya kadiri na uhuru wanapoendelea na kazi ya kuhubiri. Isitoshe, kazi hiyo imekuwa na matokeo makubwa. Leo, washiriki wa Baraza Linaloongoza wanaendelea kuutegemea mwongozo wa Kristo. Wangependa maagizo wanayowapatia akina ndugu yapatane na maoni ya Yehova na Yesu. Na wanawatumia waangalizi wa mzunguko na wazee ili kuyapatia makutaniko mwongozo. Wazee watiwa-mafuta wako kwenye ‘mkono wa kuume’ wa Kristo. (Ufu. 2:1) Bila shaka, wazee hao si wakamilifu na wanafanya makosa. Pindi fulani Musa na Yoshua walifanya makosa, kama ilivyokuwa kwa mitume pia. (Hes. 20:12; Yos. 9:14, 15; Rom. 3:23) Bado Kristo anamwongoza kwa makini mtumwa mwaminifu na wazee waliowekwa rasmi, na ataendelea kufanya hivyo. Hivyo, tuna kila sababu ya kutumaini mwongozo ambao anatupatia kupitia wale aliowaweka rasmi ili kuongoza. w24.02 23-24 ¶13-14
Jumamosi, Julai 26
Iweni waigaji wa Mungu, kama watoto wapendwa.—Efe. 5:1.
Leo, tunaweza kumfurahisha Yehova kwa kuzungumza kumhusu kwa njia inayoonyesha kwamba tunamthamini na tunampenda sana. Tunapokuwa katika huduma, tunakumbuka kwamba lengo letu kuu ni kuwasaidia watu wamkaribie Yehova, na wahisi kama sisi tunavyohisi kumhusu Baba yetu mwenye upendo. (Yak. 4:8) Tunafurahi sana kuwaonyesha watu jinsi Biblia inavyomfafanua Yehova, inavyofunua upendo wake, haki, hekima, na sifa zake nyingine zenye kuvutia. Pia, tunamsifu Yehova na kumfurahisha kwa kujitahidi kumwiga. Tunapofanya hivyo, tunakuwa tofauti kabisa na watu katika ulimwengu huu mwovu. Huenda watu wakatambua kwamba tuko tofauti na kujiuliza kwa nini. (Mt. 5:14-16) Tunaposhughulika nao katika maisha ya kila siku, huenda tukapata fursa ya kuwaeleza kwa nini tunatenda kwa njia tofauti. Matokeo ni kwamba watu wanyoofu wanatamani kumkaribia Mungu wetu. Tunapomsifu Yehova kwa njia hizo, tunaufurahisha moyo wake.—1 Tim. 2:3, 4. w24.02 10 ¶7