Ijumaa, Julai 25
Mimi nipo pamoja nanyi sikuzote mpaka umalizio wa mfumo wa mambo.—Mt. 28:20.
Tangu Vita vya Pili vya Ulimwengu, watu wa Yehova katika nchi nyingi wamefurahia amani ya kadiri na uhuru wanapoendelea na kazi ya kuhubiri. Isitoshe, kazi hiyo imekuwa na matokeo makubwa. Leo, washiriki wa Baraza Linaloongoza wanaendelea kuutegemea mwongozo wa Kristo. Wangependa maagizo wanayowapatia akina ndugu yapatane na maoni ya Yehova na Yesu. Na wanawatumia waangalizi wa mzunguko na wazee ili kuyapatia makutaniko mwongozo. Wazee watiwa-mafuta wako kwenye ‘mkono wa kuume’ wa Kristo. (Ufu. 2:1) Bila shaka, wazee hao si wakamilifu na wanafanya makosa. Pindi fulani Musa na Yoshua walifanya makosa, kama ilivyokuwa kwa mitume pia. (Hes. 20:12; Yos. 9:14, 15; Rom. 3:23) Bado Kristo anamwongoza kwa makini mtumwa mwaminifu na wazee waliowekwa rasmi, na ataendelea kufanya hivyo. Hivyo, tuna kila sababu ya kutumaini mwongozo ambao anatupatia kupitia wale aliowaweka rasmi ili kuongoza. w24.02 23-24 ¶13-14
Jumamosi, Julai 26
Iweni waigaji wa Mungu, kama watoto wapendwa.—Efe. 5:1.
Leo, tunaweza kumfurahisha Yehova kwa kuzungumza kumhusu kwa njia inayoonyesha kwamba tunamthamini na tunampenda sana. Tunapokuwa katika huduma, tunakumbuka kwamba lengo letu kuu ni kuwasaidia watu wamkaribie Yehova, na wahisi kama sisi tunavyohisi kumhusu Baba yetu mwenye upendo. (Yak. 4:8) Tunafurahi sana kuwaonyesha watu jinsi Biblia inavyomfafanua Yehova, inavyofunua upendo wake, haki, hekima, na sifa zake nyingine zenye kuvutia. Pia, tunamsifu Yehova na kumfurahisha kwa kujitahidi kumwiga. Tunapofanya hivyo, tunakuwa tofauti kabisa na watu katika ulimwengu huu mwovu. Huenda watu wakatambua kwamba tuko tofauti na kujiuliza kwa nini. (Mt. 5:14-16) Tunaposhughulika nao katika maisha ya kila siku, huenda tukapata fursa ya kuwaeleza kwa nini tunatenda kwa njia tofauti. Matokeo ni kwamba watu wanyoofu wanatamani kumkaribia Mungu wetu. Tunapomsifu Yehova kwa njia hizo, tunaufurahisha moyo wake.—1 Tim. 2:3, 4. w24.02 10 ¶7
Jumapili, Julai 27
[Uweze] kutia moyo . . . na pia kuwakaripia.—Tito 1:9.
Ili uwe mwanamume Mkristo mkomavu, utahitaji kujifunza stadi zinazofaa. Stadi hizo zitakusaidia kutimiza majukumu yako kutanikoni, kupata kazi itakayokutegemeza wewe au familia yako, na zitakusaidia kuwa na uhusiano mzuri na wengine. Kwa mfano, jifunze kusoma na kuandika vizuri. Biblia inasema kwamba mwanamume mwenye furaha na mwenye mafanikio hutumia muda kila siku kusoma Neno la Mungu na kulitafakari. (Zab. 1:1-3) Kwa kusoma Biblia kila siku, atajua njia ya Yehova ya kufikiri ambayo itamsaidia kufikiria mambo kwa njia nzuri, na kujifunza jinsi ya kutumia Maandiko vizuri. (Met. 1:3, 4) Ndugu na dada zetu wanahitaji msaada wa wanaume wenye uwezo wa kufundisha na kuwapa ushauri unaotegemea Biblia. Ikiwa unajua kusoma na kuandika vizuri, utaweza kuandaa hotuba na maelezo yenye habari zenye kujenga na kuimarisha imani. Pia, utaweza kuandika mambo makuu kwa njia nzuri itakayokusaidia kujenga imani yako na kuwatia moyo wengine. w23.12 26-27 ¶9-11