Jumamosi, Julai 26
Iweni waigaji wa Mungu, kama watoto wapendwa.—Efe. 5:1.
Leo, tunaweza kumfurahisha Yehova kwa kuzungumza kumhusu kwa njia inayoonyesha kwamba tunamthamini na tunampenda sana. Tunapokuwa katika huduma, tunakumbuka kwamba lengo letu kuu ni kuwasaidia watu wamkaribie Yehova, na wahisi kama sisi tunavyohisi kumhusu Baba yetu mwenye upendo. (Yak. 4:8) Tunafurahi sana kuwaonyesha watu jinsi Biblia inavyomfafanua Yehova, inavyofunua upendo wake, haki, hekima, na sifa zake nyingine zenye kuvutia. Pia, tunamsifu Yehova na kumfurahisha kwa kujitahidi kumwiga. Tunapofanya hivyo, tunakuwa tofauti kabisa na watu katika ulimwengu huu mwovu. Huenda watu wakatambua kwamba tuko tofauti na kujiuliza kwa nini. (Mt. 5:14-16) Tunaposhughulika nao katika maisha ya kila siku, huenda tukapata fursa ya kuwaeleza kwa nini tunatenda kwa njia tofauti. Matokeo ni kwamba watu wanyoofu wanatamani kumkaribia Mungu wetu. Tunapomsifu Yehova kwa njia hizo, tunaufurahisha moyo wake.—1 Tim. 2:3, 4. w24.02 10 ¶7
Jumapili, Julai 27
[Uweze] kutia moyo . . . na pia kuwakaripia.—Tito 1:9.
Ili uwe mwanamume Mkristo mkomavu, utahitaji kujifunza stadi zinazofaa. Stadi hizo zitakusaidia kutimiza majukumu yako kutanikoni, kupata kazi itakayokutegemeza wewe au familia yako, na zitakusaidia kuwa na uhusiano mzuri na wengine. Kwa mfano, jifunze kusoma na kuandika vizuri. Biblia inasema kwamba mwanamume mwenye furaha na mwenye mafanikio hutumia muda kila siku kusoma Neno la Mungu na kulitafakari. (Zab. 1:1-3) Kwa kusoma Biblia kila siku, atajua njia ya Yehova ya kufikiri ambayo itamsaidia kufikiria mambo kwa njia nzuri, na kujifunza jinsi ya kutumia Maandiko vizuri. (Met. 1:3, 4) Ndugu na dada zetu wanahitaji msaada wa wanaume wenye uwezo wa kufundisha na kuwapa ushauri unaotegemea Biblia. Ikiwa unajua kusoma na kuandika vizuri, utaweza kuandaa hotuba na maelezo yenye habari zenye kujenga na kuimarisha imani. Pia, utaweza kuandika mambo makuu kwa njia nzuri itakayokusaidia kujenga imani yako na kuwatia moyo wengine. w23.12 26-27 ¶9-11
Jumatatu, Julai 28
Yule aliye katika muungano na ninyi ni mkuu kuliko yule aliye katika muungano na ulimwengu.—1 Yoh. 4:4.
Unapoogopa, tafakari mambo ambayo Yehova atafanya wakati ujao Shetani atakapoondolewa. Onyesho lililotolewa kwenye programu ya kusanyiko la eneo la mwaka wa 2014 lilionyesha baba akizungumza na familia yake kuhusu jinsi ambavyo maneno ya 2 Timotheo 3:1-5 yangesomwa ikiwa mistari hiyo iliyotabiriwa ingezungumzia hali zitakavyokuwa katika Paradiso. Alisema hivi: “Katika ulimwengu mpya, kutakuwa na nyakati zenye furaha sana. Maana watu watakuwa wenye kupendana, wenye kupenda mambo ya kiroho, wenye kiasi, wanyenyekevu, wenye kumsifu Mungu, wanaotii wazazi, wenye shukrani, washikamanifu, walio na upendo wa asili, wanaotaka makubaliano, wanaosema mema kuhusu wengine sikuzote, wanaojizuia, wapole, wanaopenda wema, wanaotumainika, wenye kutii, wanyenyekevu katika akili, wanaompenda Mungu badala ya kupenda raha, wakichochewa na upendo wa kweli kwa Mungu; nawe shikamana na watu hao.” Je, wewe huzungumza na watu wa familia yako au waabudu wenzako kuhusu jinsi maisha yatakavyokuwa katika ulimwengu mpya? w24.01 6 ¶13-14