Jumanne, Julai 29
Nimekukubali.—Luka 3:22.
Tunafurahi sana kujua kwamba Yehova anawakubali watu wake wakiwa kikundi! Biblia inasema hivi: “Yehova anawafurahia watu wake.” (Zab. 149:4) Hata hivyo, wakati mwingine baadhi ya watu wanavunjika moyo na kujiuliza, ‘Je, Mungu ananikubali mimi binafsi?’ Watumishi wengi waaminifu wa Yehova walioishi nyakati za Biblia, pindi fulani walihangaishwa na mawazo kama hayo. (1 Sam. 1:6-10; Ayu. 29:2, 4; Zab. 51:11) Biblia inaonyesha wazi kwamba wanadamu wasio wakamilifu wanaweza kupata kibali cha Yehova. Jinsi gani? Ni lazima tuonyeshe kwamba tunamwamini Yesu Kristo na kubatizwa. (Yoh. 3:16) Hivyo, tunaonyesha hadharani kwamba tumetubu dhambi zetu na tumemwahidi Mungu kuwa tutafanya mapenzi yake. (Mdo. 2:38; 3:19) Yehova anafurahi tunapochukua hatua hizo ili kusitawisha uhusiano mzuri pamoja naye. Maadamu tunaendelea kufanya yote tuwezayo ili kuishi kulingana na ahadi tuliyotoa tulipojiweka wakfu, Yehova anatukubali na kutuona kuwa rafiki zake wa karibu.—Zab. 25:14. w24.03 26 ¶1-2
Jumatano, Julai 30
Hatuwezi kuacha kusema kuhusu mambo ambayo tumeyaona na kuyasikia.—Mdo. 4:20.
Tunaweza kuwaiga wanafunzi hao kwa kuendelea kuhubiri hata ikiwa wenye mamlaka watatuamuru tuache kuhubiri. Tunaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova atatusaidia kutimiza huduma yetu. Hivyo, sali ili upate ujasiri na hekima na umwombe Yehova akusaidie uvumilie licha ya matatizo. Wengi wetu tunakabiliana na changamoto za magonjwa au za kihisia, kufiwa na mpendwa wetu, hali fulani ngumu katika familia, mateso, au matatizo mengine. Na mambo kama vile mlipuko wa magonjwa na vita yamefanya iwe vigumu hata zaidi kushughulika na changamoto hizo. Mmiminie Yehova moyo wako. Mwambie kuhusu hali yako kama ambavyo ungemwambia rafiki wa karibu. Uwe na uhakika kwamba Yehova “atatenda kwa niaba yako.” (Zab. 37:3, 5) Kudumu katika sala kutatusaidia ‘kuvumilia chini ya dhiki.’ (Rom. 12:12) Yehova anajua mambo ambayo waabudu wake wanavumilia—yeye “husikia kilio chao cha kuomba msaada.”—Zab. 145:18, 19. w23.05 5-6 ¶12-15
Alhamisi, Julai 31
Endeleeni kuhakikisha jambo linalokubalika kwa Bwana.—Efe. 5:10.
Tunapotaka kufanya maamuzi muhimu, tunahitaji “kuyafahamu mapenzi ya Yehova” na kisha tutende kupatana nayo. (Efe. 5:17) Tunapotafuta kanuni za Biblia zinazohusu hali yetu, kwa kweli tutakuwa tukitafuta mawazo ya Mungu kuhusu jambo hilo. Kisha, kadiri tunavyotumia kanuni za Mungu, ndivyo tutakavyoweza kufanya maamuzi mazuri. “Yule mwovu,” adui yetu Shetani, angependa tutumie muda mwingi kufuatilia mambo ya ulimwengu huu, hivi kwamba tukose wakati wa kufanya utumishi wetu kwa Mungu. (1 Yoh. 5:19) Inaweza kuwa rahisi sana kwa Mkristo kutanguliza mali, elimu, au kazi yake badala ya kutafuta fursa za kumtumikia Yehova. Ikiwa jambo hilo litatokea, itaonyesha kwamba Mkristo huyo ameathiriwa na njia ya kufikiri ya ulimwengu. Kwa kweli, mali, elimu, au kazi si mambo mabaya, lakini hayapaswi kamwe kutangulizwa maishani mwetu. w24.03 24 ¶16-17