Jumatano, Julai 30
Hatuwezi kuacha kusema kuhusu mambo ambayo tumeyaona na kuyasikia.—Mdo. 4:20.
Tunaweza kuwaiga wanafunzi hao kwa kuendelea kuhubiri hata ikiwa wenye mamlaka watatuamuru tuache kuhubiri. Tunaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova atatusaidia kutimiza huduma yetu. Hivyo, sali ili upate ujasiri na hekima na umwombe Yehova akusaidie uvumilie licha ya matatizo. Wengi wetu tunakabiliana na changamoto za magonjwa au za kihisia, kufiwa na mpendwa wetu, hali fulani ngumu katika familia, mateso, au matatizo mengine. Na mambo kama vile mlipuko wa magonjwa na vita yamefanya iwe vigumu hata zaidi kushughulika na changamoto hizo. Mmiminie Yehova moyo wako. Mwambie kuhusu hali yako kama ambavyo ungemwambia rafiki wa karibu. Uwe na uhakika kwamba Yehova “atatenda kwa niaba yako.” (Zab. 37:3, 5) Kudumu katika sala kutatusaidia ‘kuvumilia chini ya dhiki.’ (Rom. 12:12) Yehova anajua mambo ambayo waabudu wake wanavumilia—yeye “husikia kilio chao cha kuomba msaada.”—Zab. 145:18, 19. w23.05 5-6 ¶12-15
Alhamisi, Julai 31
Endeleeni kuhakikisha jambo linalokubalika kwa Bwana.—Efe. 5:10.
Tunapotaka kufanya maamuzi muhimu, tunahitaji “kuyafahamu mapenzi ya Yehova” na kisha tutende kupatana nayo. (Efe. 5:17) Tunapotafuta kanuni za Biblia zinazohusu hali yetu, kwa kweli tutakuwa tukitafuta mawazo ya Mungu kuhusu jambo hilo. Kisha, kadiri tunavyotumia kanuni za Mungu, ndivyo tutakavyoweza kufanya maamuzi mazuri. “Yule mwovu,” adui yetu Shetani, angependa tutumie muda mwingi kufuatilia mambo ya ulimwengu huu, hivi kwamba tukose wakati wa kufanya utumishi wetu kwa Mungu. (1 Yoh. 5:19) Inaweza kuwa rahisi sana kwa Mkristo kutanguliza mali, elimu, au kazi yake badala ya kutafuta fursa za kumtumikia Yehova. Ikiwa jambo hilo litatokea, itaonyesha kwamba Mkristo huyo ameathiriwa na njia ya kufikiri ya ulimwengu. Kwa kweli, mali, elimu, au kazi si mambo mabaya, lakini hayapaswi kamwe kutangulizwa maishani mwetu. w24.03 24 ¶16-17
Ijumaa, Agosti 1
Mwadilifu ana matatizo mengi, lakini Yehova humwokoa kutoka katika matatizo hayo yote.—Zab. 34:19.
Ona mambo mawili muhimu katika Zaburi hiyo: (1) Watu waadilifu hukabili matatizo. (2) Yehova hutukomboa kutoka katika majaribu yetu. Yehova hutukomboa jinsi gani? Njia moja ni kwa kutusaidia kuona mambo kihalisi kwenye mfumo huu wa mambo. Ingawa Yehova anatuahidi kwamba tutapata shangwe tunapomtumikia, hajatuhakikishia kwamba hatutapatwa na matatizo sasa. (Isa. 66:14) Anatuhimiza tukazie fikira wakati ujao—wakati ambapo tutaishi maisha anayotaka tufurahie milele. (2 Kor. 4:16-18) Kwa sasa, anatusaidia kuendelea kumtumikia kila siku. (Omb. 3:22-24) Tunaweza kujifunza nini kutokana na mifano ya waabudu waaminifu wa Yehova wanaotajwa katika Biblia na wa nyakati zetu? Huenda tukakabili matatizo tusiyotarajia. Lakini tunapomtegemea Yehova, atatutegemeza sikuzote.—Zab. 55:22. w23.04 14-15 ¶3-4