Jumapili, Agosti 3
Tutiane moyo.—Ebr. 10:25.
Namna gani ikiwa una wasiwasi wa kutoa maelezo katika mikutano? Unaweza kunufaika ikiwa utajitayarisha vizuri. (Met. 21:5) Kadiri unavyofahamu vizuri zaidi habari inayozungumziwa, ndivyo itakavyokuwa rahisi kwako kutoa maelezo. Pia, toa maelezo mafupi. (Met. 15:23; 17:27) Jibu fupi litakupunguzia wasiwasi. Unapotoa maelezo mafupi kwa maneno yako mwenyewe, utaonyesha kwamba umejitayarisha vizuri na kwamba unaelewa vizuri habari inayozungumziwa. Namna gani ikiwa utajaribu kutumia baadhi ya mapendekezo hayo, lakini bado uwe na wasiwasi kuhusu kutoa maelezo zaidi ya mara moja au mbili? Uwe na uhakika kwamba Yehova atathamini jitihada zako za kutoka moyoni za kufanya kile unachoweza. (Luka 21:1-4) Kutoa kilicho bora hakumaanishi kufanya jambo linalozidi uwezo wako. (Flp. 4:5) Amua jambo unaloweza kufanya, weka lengo la kulifanya, na usali ili uwe na moyo mtulivu. Mwanzoni, huenda lengo hilo likawa kutoa maelezo mafupi mara moja. w23.04 21 ¶6-8
Jumatatu, Agosti 4
[Vaa] bamba la kifuani . . . na . . . kofia ya chuma.—1 The. 5:8.
Mtume Paulo anatulinganisha na wanajeshi walio chonjo na waliovaa mavazi ya kivita. Mwanajeshi aliye kwenye zamu anatarajiwa kuwa tayari kwa ajili ya vita wakati wowote. Hali yetu iko hivyo pia. Tunaendelea kuwa tayari kwa ajili ya siku ya Yehova kwa kuvaa bamba la kifuani la imani na upendo na kofia ya chuma ya tumaini. Bamba la kifuani lililinda moyo wa mwanajeshi. Imani na upendo hulinda moyo wetu wa mfano. Sifa hizo zitatusaidia kuendelea kumtumikia Mungu na kumfuata Yesu. Imani inatuhakikishia kwamba Yehova atatuthawabisha tukiendelea kumtafuta kwa moyo wetu wote. (Ebr. 11:6) Itatuchochea kuendelea kuwa washikamanifu kwa Kiongozi wetu, Yesu, hata ikiwa tutakabili hali ngumu. Tunaweza kuimarisha imani yetu ili tukabiliane na hali ngumu maishani kwa kujifunza kutokana na mifano ya siku zetu ya watu waliodumisha utimilifu wao licha ya mateso au hali ngumu za kiuchumi. Na tunaweza kuepuka mtego wa kujikusanyia vitu vya kimwili kwa kuwaiga wale ambao walirahisisha maisha yao ili kutanguliza masilahi ya Ufalme. w23.06 10 ¶8-9
Jumanne, Agosti 5
Anayetazama mawingu hatavuna.—Mhu. 11:4.
Sifa ya kujizuia inamaanisha uwezo wa kudhibiti hisia na matendo yetu. Tunahitaji sifa ya kujizuia ili tuchochewe kufikia malengo yetu, hasa ikiwa lengo tunalotaka kufikia ni gumu au tumekosa kichocheo. Kumbuka, sifa ya kujizuia ni sehemu ya tunda la roho, basi mwombe Yehova akupatie roho takatifu ili ikusaidie kusitawisha sifa hiyo muhimu. (Luka 11:13; Gal. 5:22, 23) Usisubiri mpaka hali ziwe nzuri kabisa. Katika ulimwengu huu, inaelekea kwamba hatutakuwa kamwe na hali zinazofaa kabisa. Ikiwa tutasubiri hali zinazofaa, huenda tusitimize kamwe lengo letu. Huenda tukakosa kichocheo kwa sababu inaonekana kwamba ni vigumu sana kutimiza lengo letu. Ikiwa unakabili hali hiyo, je, unaweza kugawa lengo lako ili liwe malengo madogo-madogo? Ikiwa una lengo la kusitawisha sifa fulani, kwa nini usianze kujitahidi kuionyesha kwa njia ndogo? Ikiwa lengo lako ni kusoma Biblia nzima, je, unaweza kuanza kwa kupanga vipindi vifupi zaidi vya kusoma? w23.05 29 ¶11-13