Jumamosi, Agosti 2
[Jitiishe] kwa mamlaka zilizo kubwa.—Rom. 13:1.
Tunaweza kujifunza kutokana na mfano wa Yosefu na Maria, ambao walikuwa tayari kutii mamlaka zilizo kubwa hata ilipokuwa vigumu kufanya hivyo. (Luka 2:1-6) Maria alipokuwa mjamzito kwa kipindi cha miezi tisa hivi, yeye na Yosefu walikabili jaribu la kutii. Augusto, ambaye alitawala Milki ya Roma, aliamuru watu wote waandikishwe. Yosefu na Maria walilazimika kusafiri kwenda Bethlehemu, safari ya kilomita 150 hivi wakipitia katika eneo lenye milima-milima. Safari hiyo haikuwa rahisi, hasa kwa Maria. Huenda wenzi hao walihofia usalama wao na wa mtoto wao ambaye bado hakuwa amezaliwa. Namna gani ikiwa Maria angepatwa na uchungu wa kuzaa wakiwa njiani? Tumboni mwake alikuwa amembeba Masihi wa wakati ujao. Je, wangetumia hali hiyo kuwa kisingizio cha kutotii serikali? Yosefu na Maria hawakuruhusu mahangaiko hayo yaamue ikiwa watatii sheria. Yehova aliwabariki kwa kutii. Maria aliwasili salama Bethlehemu, akajifungua mtoto mwenye afya, na hata akasaidia kutimiza unabii wa Biblia!—Mika 5:2. w23.10 8 ¶9; 9 ¶11-12
Jumapili, Agosti 3
Tutiane moyo.—Ebr. 10:25.
Namna gani ikiwa una wasiwasi wa kutoa maelezo katika mikutano? Unaweza kunufaika ikiwa utajitayarisha vizuri. (Met. 21:5) Kadiri unavyofahamu vizuri zaidi habari inayozungumziwa, ndivyo itakavyokuwa rahisi kwako kutoa maelezo. Pia, toa maelezo mafupi. (Met. 15:23; 17:27) Jibu fupi litakupunguzia wasiwasi. Unapotoa maelezo mafupi kwa maneno yako mwenyewe, utaonyesha kwamba umejitayarisha vizuri na kwamba unaelewa vizuri habari inayozungumziwa. Namna gani ikiwa utajaribu kutumia baadhi ya mapendekezo hayo, lakini bado uwe na wasiwasi kuhusu kutoa maelezo zaidi ya mara moja au mbili? Uwe na uhakika kwamba Yehova atathamini jitihada zako za kutoka moyoni za kufanya kile unachoweza. (Luka 21:1-4) Kutoa kilicho bora hakumaanishi kufanya jambo linalozidi uwezo wako. (Flp. 4:5) Amua jambo unaloweza kufanya, weka lengo la kulifanya, na usali ili uwe na moyo mtulivu. Mwanzoni, huenda lengo hilo likawa kutoa maelezo mafupi mara moja. w23.04 21 ¶6-8
Jumatatu, Agosti 4
[Vaa] bamba la kifuani . . . na . . . kofia ya chuma.—1 The. 5:8.
Mtume Paulo anatulinganisha na wanajeshi walio chonjo na waliovaa mavazi ya kivita. Mwanajeshi aliye kwenye zamu anatarajiwa kuwa tayari kwa ajili ya vita wakati wowote. Hali yetu iko hivyo pia. Tunaendelea kuwa tayari kwa ajili ya siku ya Yehova kwa kuvaa bamba la kifuani la imani na upendo na kofia ya chuma ya tumaini. Bamba la kifuani lililinda moyo wa mwanajeshi. Imani na upendo hulinda moyo wetu wa mfano. Sifa hizo zitatusaidia kuendelea kumtumikia Mungu na kumfuata Yesu. Imani inatuhakikishia kwamba Yehova atatuthawabisha tukiendelea kumtafuta kwa moyo wetu wote. (Ebr. 11:6) Itatuchochea kuendelea kuwa washikamanifu kwa Kiongozi wetu, Yesu, hata ikiwa tutakabili hali ngumu. Tunaweza kuimarisha imani yetu ili tukabiliane na hali ngumu maishani kwa kujifunza kutokana na mifano ya siku zetu ya watu waliodumisha utimilifu wao licha ya mateso au hali ngumu za kiuchumi. Na tunaweza kuepuka mtego wa kujikusanyia vitu vya kimwili kwa kuwaiga wale ambao walirahisisha maisha yao ili kutanguliza masilahi ya Ufalme. w23.06 10 ¶8-9