Ijumaa, Agosti 1
Mwadilifu ana matatizo mengi, lakini Yehova humwokoa kutoka katika matatizo hayo yote.—Zab. 34:19.
Ona mambo mawili muhimu katika Zaburi hiyo: (1) Watu waadilifu hukabili matatizo. (2) Yehova hutukomboa kutoka katika majaribu yetu. Yehova hutukomboa jinsi gani? Njia moja ni kwa kutusaidia kuona mambo kihalisi kwenye mfumo huu wa mambo. Ingawa Yehova anatuahidi kwamba tutapata shangwe tunapomtumikia, hajatuhakikishia kwamba hatutapatwa na matatizo sasa. (Isa. 66:14) Anatuhimiza tukazie fikira wakati ujao—wakati ambapo tutaishi maisha anayotaka tufurahie milele. (2 Kor. 4:16-18) Kwa sasa, anatusaidia kuendelea kumtumikia kila siku. (Omb. 3:22-24) Tunaweza kujifunza nini kutokana na mifano ya waabudu waaminifu wa Yehova wanaotajwa katika Biblia na wa nyakati zetu? Huenda tukakabili matatizo tusiyotarajia. Lakini tunapomtegemea Yehova, atatutegemeza sikuzote.—Zab. 55:22. w23.04 14-15 ¶3-4
Jumamosi, Agosti 2
[Jitiishe] kwa mamlaka zilizo kubwa.—Rom. 13:1.
Tunaweza kujifunza kutokana na mfano wa Yosefu na Maria, ambao walikuwa tayari kutii mamlaka zilizo kubwa hata ilipokuwa vigumu kufanya hivyo. (Luka 2:1-6) Maria alipokuwa mjamzito kwa kipindi cha miezi tisa hivi, yeye na Yosefu walikabili jaribu la kutii. Augusto, ambaye alitawala Milki ya Roma, aliamuru watu wote waandikishwe. Yosefu na Maria walilazimika kusafiri kwenda Bethlehemu, safari ya kilomita 150 hivi wakipitia katika eneo lenye milima-milima. Safari hiyo haikuwa rahisi, hasa kwa Maria. Huenda wenzi hao walihofia usalama wao na wa mtoto wao ambaye bado hakuwa amezaliwa. Namna gani ikiwa Maria angepatwa na uchungu wa kuzaa wakiwa njiani? Tumboni mwake alikuwa amembeba Masihi wa wakati ujao. Je, wangetumia hali hiyo kuwa kisingizio cha kutotii serikali? Yosefu na Maria hawakuruhusu mahangaiko hayo yaamue ikiwa watatii sheria. Yehova aliwabariki kwa kutii. Maria aliwasili salama Bethlehemu, akajifungua mtoto mwenye afya, na hata akasaidia kutimiza unabii wa Biblia!—Mika 5:2. w23.10 8 ¶9; 9 ¶11-12
Jumapili, Agosti 3
Tutiane moyo.—Ebr. 10:25.
Namna gani ikiwa una wasiwasi wa kutoa maelezo katika mikutano? Unaweza kunufaika ikiwa utajitayarisha vizuri. (Met. 21:5) Kadiri unavyofahamu vizuri zaidi habari inayozungumziwa, ndivyo itakavyokuwa rahisi kwako kutoa maelezo. Pia, toa maelezo mafupi. (Met. 15:23; 17:27) Jibu fupi litakupunguzia wasiwasi. Unapotoa maelezo mafupi kwa maneno yako mwenyewe, utaonyesha kwamba umejitayarisha vizuri na kwamba unaelewa vizuri habari inayozungumziwa. Namna gani ikiwa utajaribu kutumia baadhi ya mapendekezo hayo, lakini bado uwe na wasiwasi kuhusu kutoa maelezo zaidi ya mara moja au mbili? Uwe na uhakika kwamba Yehova atathamini jitihada zako za kutoka moyoni za kufanya kile unachoweza. (Luka 21:1-4) Kutoa kilicho bora hakumaanishi kufanya jambo linalozidi uwezo wako. (Flp. 4:5) Amua jambo unaloweza kufanya, weka lengo la kulifanya, na usali ili uwe na moyo mtulivu. Mwanzoni, huenda lengo hilo likawa kutoa maelezo mafupi mara moja. w23.04 21 ¶6-8