Jumanne, Agosti 5
Anayetazama mawingu hatavuna.—Mhu. 11:4.
Sifa ya kujizuia inamaanisha uwezo wa kudhibiti hisia na matendo yetu. Tunahitaji sifa ya kujizuia ili tuchochewe kufikia malengo yetu, hasa ikiwa lengo tunalotaka kufikia ni gumu au tumekosa kichocheo. Kumbuka, sifa ya kujizuia ni sehemu ya tunda la roho, basi mwombe Yehova akupatie roho takatifu ili ikusaidie kusitawisha sifa hiyo muhimu. (Luka 11:13; Gal. 5:22, 23) Usisubiri mpaka hali ziwe nzuri kabisa. Katika ulimwengu huu, inaelekea kwamba hatutakuwa kamwe na hali zinazofaa kabisa. Ikiwa tutasubiri hali zinazofaa, huenda tusitimize kamwe lengo letu. Huenda tukakosa kichocheo kwa sababu inaonekana kwamba ni vigumu sana kutimiza lengo letu. Ikiwa unakabili hali hiyo, je, unaweza kugawa lengo lako ili liwe malengo madogo-madogo? Ikiwa una lengo la kusitawisha sifa fulani, kwa nini usianze kujitahidi kuionyesha kwa njia ndogo? Ikiwa lengo lako ni kusoma Biblia nzima, je, unaweza kuanza kwa kupanga vipindi vifupi zaidi vya kusoma? w23.05 29 ¶11-13
Jumatano, Agosti 6
Kijia cha waadilifu ni kama nuru nyangavu ya asubuhi, inayong’aa zaidi na zaidi mpaka mchana kamili.—Met. 4:18.
Katika kipindi chote cha siku za mwisho, Yehova ametumia tengenezo lake kuendelea kuandaa chakula cha kiroho ili kutusaidia sisi sote tuendelee kutembea katika “Njia ya Utakatifu.” (Isa. 35:8; 48:17; 60:17) Tunaweza kusema kwamba kila mara mtu anapokubali kujifunza Biblia, anapata nafasi ya kutembea katika “Njia ya Utakatifu.” Baada ya kutembea kwa muda mfupi, baadhi yao huacha kutembea katika barabara hiyo kuu. Wengine wameazimia kuendelea kutembea katika barabara hiyo hadi watakapofika mwisho wa safari yao. Mwisho huo wa safari ni nini? Kwa wale ambao wana tumaini la kwenda mbinguni, “Njia ya Utakatifu” inaongoza kwenye “paradiso ya Mungu” huko mbinguni. (Ufu. 2:7) Kwa wale walio na tumaini la kuishi duniani, barabara hiyo kuu itaongoza kwenye ukamilifu mwishoni mwa ile miaka 1,000. Ikiwa leo unatembea katika barabara hiyo kuu, usitazame nyuma. Na usiondoke kwenye barabara hiyo hadi utakapomaliza safari yako na kuingia katika ulimwengu mpya! w23.05 17 ¶15; 19 ¶16-18
Alhamisi, Agosti 7
Sisi tuna upendo, kwa sababu alitupenda kwanza.—1 Yoh. 4:19.
Unapofikiria mambo yote ambayo Yehova amekufanyia utamthamini sana na utataka kujiweka wakfu kwake. (Zab. 116:12-14) Biblia inamwita kwa usahihi Yehova kuwa ndiye Mpaji wa “kila zawadi njema na kila tuzo kamilifu.” (Yak. 1:17) Zawadi bora zaidi kuliko zote ni dhabihu ya Yesu, Mwana wake. Hebu fikiria! Fidia imekuwezesha kuwa na uhusiano wa karibu pamoja na Yehova. Na imekupatia tumaini la kuishi milele. (1 Yoh. 4:9, 10) Kujiweka wakfu kwa Yehova ni njia ya kuonyesha shukrani kwa ajili ya upendo huo mkubwa zaidi ambao amekuonyesha, pamoja na baraka nyingine ambazo Yehova amekupatia.—Kum. 16:17; 2 Kor. 5:15. w24.03 5 ¶8