Jumatano, Agosti 6
Kijia cha waadilifu ni kama nuru nyangavu ya asubuhi, inayong’aa zaidi na zaidi mpaka mchana kamili.—Met. 4:18.
Katika kipindi chote cha siku za mwisho, Yehova ametumia tengenezo lake kuendelea kuandaa chakula cha kiroho ili kutusaidia sisi sote tuendelee kutembea katika “Njia ya Utakatifu.” (Isa. 35:8; 48:17; 60:17) Tunaweza kusema kwamba kila mara mtu anapokubali kujifunza Biblia, anapata nafasi ya kutembea katika “Njia ya Utakatifu.” Baada ya kutembea kwa muda mfupi, baadhi yao huacha kutembea katika barabara hiyo kuu. Wengine wameazimia kuendelea kutembea katika barabara hiyo hadi watakapofika mwisho wa safari yao. Mwisho huo wa safari ni nini? Kwa wale ambao wana tumaini la kwenda mbinguni, “Njia ya Utakatifu” inaongoza kwenye “paradiso ya Mungu” huko mbinguni. (Ufu. 2:7) Kwa wale walio na tumaini la kuishi duniani, barabara hiyo kuu itaongoza kwenye ukamilifu mwishoni mwa ile miaka 1,000. Ikiwa leo unatembea katika barabara hiyo kuu, usitazame nyuma. Na usiondoke kwenye barabara hiyo hadi utakapomaliza safari yako na kuingia katika ulimwengu mpya! w23.05 17 ¶15; 19 ¶16-18
Alhamisi, Agosti 7
Sisi tuna upendo, kwa sababu alitupenda kwanza.—1 Yoh. 4:19.
Unapofikiria mambo yote ambayo Yehova amekufanyia utamthamini sana na utataka kujiweka wakfu kwake. (Zab. 116:12-14) Biblia inamwita kwa usahihi Yehova kuwa ndiye Mpaji wa “kila zawadi njema na kila tuzo kamilifu.” (Yak. 1:17) Zawadi bora zaidi kuliko zote ni dhabihu ya Yesu, Mwana wake. Hebu fikiria! Fidia imekuwezesha kuwa na uhusiano wa karibu pamoja na Yehova. Na imekupatia tumaini la kuishi milele. (1 Yoh. 4:9, 10) Kujiweka wakfu kwa Yehova ni njia ya kuonyesha shukrani kwa ajili ya upendo huo mkubwa zaidi ambao amekuonyesha, pamoja na baraka nyingine ambazo Yehova amekupatia.—Kum. 16:17; 2 Kor. 5:15. w24.03 5 ¶8
Ijumaa, Agosti 8
Mtu anayetembea kwa unyoofu wake anamwogopa Yehova.—Met. 14:2.
Kuhusu viwango vya maadili vilivyo katika ulimwengu huu, tunahisi kama Loti mwadilifu. ‘Alitaabishwa sana na mwenendo mpotovu wa waasi sheria,’ kwa sababu alijua kwamba Baba yetu wa mbinguni anachukia mwenendo mbaya. (2 Pet. 2:7, 8) Kumwogopa na kumpenda Mungu kulimchochea Loti akatae mwenendo mpotovu wa watu waliomzunguka. Sisi pia tumezungukwa na watu ambao wanapuuza viwango vya maadili vya Yehova. Ingawa hivyo, tunaweza kuendelea kuwa safi kiadili ikiwa tutaendelea kumpenda Mungu na kusitawisha woga unaofaa kumwelekea. Ili kutusaidia, Yehova anatutia moyo kwa upendo na kutuchochea kupitia kitabu cha Methali. Wakristo wote wanaume na wanawake, vijana na wazee, wanaweza kunufaika sana kwa kuchunguza ushauri wenye hekima ulio katika kitabu hicho. Ikiwa tunamwogopa Yehova, tutakuwa waangalifu na kuepuka kushirikiana na watu wanaotenda mabaya. w23.06 20 ¶1-2; 21 ¶5