Alhamisi, Agosti 7
Sisi tuna upendo, kwa sababu alitupenda kwanza.—1 Yoh. 4:19.
Unapofikiria mambo yote ambayo Yehova amekufanyia utamthamini sana na utataka kujiweka wakfu kwake. (Zab. 116:12-14) Biblia inamwita kwa usahihi Yehova kuwa ndiye Mpaji wa “kila zawadi njema na kila tuzo kamilifu.” (Yak. 1:17) Zawadi bora zaidi kuliko zote ni dhabihu ya Yesu, Mwana wake. Hebu fikiria! Fidia imekuwezesha kuwa na uhusiano wa karibu pamoja na Yehova. Na imekupatia tumaini la kuishi milele. (1 Yoh. 4:9, 10) Kujiweka wakfu kwa Yehova ni njia ya kuonyesha shukrani kwa ajili ya upendo huo mkubwa zaidi ambao amekuonyesha, pamoja na baraka nyingine ambazo Yehova amekupatia.—Kum. 16:17; 2 Kor. 5:15. w24.03 5 ¶8
Ijumaa, Agosti 8
Mtu anayetembea kwa unyoofu wake anamwogopa Yehova.—Met. 14:2.
Kuhusu viwango vya maadili vilivyo katika ulimwengu huu, tunahisi kama Loti mwadilifu. ‘Alitaabishwa sana na mwenendo mpotovu wa waasi sheria,’ kwa sababu alijua kwamba Baba yetu wa mbinguni anachukia mwenendo mbaya. (2 Pet. 2:7, 8) Kumwogopa na kumpenda Mungu kulimchochea Loti akatae mwenendo mpotovu wa watu waliomzunguka. Sisi pia tumezungukwa na watu ambao wanapuuza viwango vya maadili vya Yehova. Ingawa hivyo, tunaweza kuendelea kuwa safi kiadili ikiwa tutaendelea kumpenda Mungu na kusitawisha woga unaofaa kumwelekea. Ili kutusaidia, Yehova anatutia moyo kwa upendo na kutuchochea kupitia kitabu cha Methali. Wakristo wote wanaume na wanawake, vijana na wazee, wanaweza kunufaika sana kwa kuchunguza ushauri wenye hekima ulio katika kitabu hicho. Ikiwa tunamwogopa Yehova, tutakuwa waangalifu na kuepuka kushirikiana na watu wanaotenda mabaya. w23.06 20 ¶1-2; 21 ¶5
Jumamosi, Agosti 9
Mtu yeyote akitaka kunifuata, lazima ajikane mwenyewe, aubebe mti wake wa mateso siku baada ya siku na aendelee kunifuata.—Luka 9:23.
Huenda umekabili upinzani kutoka kwa watu wa familia, au labda umeacha kufuatilia mambo fulani ya kimwili ili utangulize masilahi ya Ufalme. (Mt. 6:33) Ikiwa ndivyo, uwe na uhakika kwamba Yehova anatambua mambo yote unayofanya kwa ajili yake. (Ebr. 6:10) Inawezekana umejionea ukweli wa maneno haya ya Yesu: “Hakuna mtu aliyeacha nyumba au ndugu au dada au mama au baba au watoto au mashamba kwa ajili yangu na kwa ajili ya habari njema ambaye hatapata mara 100 sasa katika kipindi hiki—nyumba, ndugu, dada, mama, watoto, mashamba, pamoja na mateso—na katika mfumo wa mambo unaokuja, uzima wa milele.” (Marko 10:29, 30) Kwa kweli, baraka ambazo umepata ni nyingi zaidi ukilinganisha na jambo lolote ulilojidhabihu.—Zab. 37:4. w24.03 9 ¶5