Ijumaa, Agosti 8
Mtu anayetembea kwa unyoofu wake anamwogopa Yehova.—Met. 14:2.
Kuhusu viwango vya maadili vilivyo katika ulimwengu huu, tunahisi kama Loti mwadilifu. ‘Alitaabishwa sana na mwenendo mpotovu wa waasi sheria,’ kwa sababu alijua kwamba Baba yetu wa mbinguni anachukia mwenendo mbaya. (2 Pet. 2:7, 8) Kumwogopa na kumpenda Mungu kulimchochea Loti akatae mwenendo mpotovu wa watu waliomzunguka. Sisi pia tumezungukwa na watu ambao wanapuuza viwango vya maadili vya Yehova. Ingawa hivyo, tunaweza kuendelea kuwa safi kiadili ikiwa tutaendelea kumpenda Mungu na kusitawisha woga unaofaa kumwelekea. Ili kutusaidia, Yehova anatutia moyo kwa upendo na kutuchochea kupitia kitabu cha Methali. Wakristo wote wanaume na wanawake, vijana na wazee, wanaweza kunufaika sana kwa kuchunguza ushauri wenye hekima ulio katika kitabu hicho. Ikiwa tunamwogopa Yehova, tutakuwa waangalifu na kuepuka kushirikiana na watu wanaotenda mabaya. w23.06 20 ¶1-2; 21 ¶5
Jumamosi, Agosti 9
Mtu yeyote akitaka kunifuata, lazima ajikane mwenyewe, aubebe mti wake wa mateso siku baada ya siku na aendelee kunifuata.—Luka 9:23.
Huenda umekabili upinzani kutoka kwa watu wa familia, au labda umeacha kufuatilia mambo fulani ya kimwili ili utangulize masilahi ya Ufalme. (Mt. 6:33) Ikiwa ndivyo, uwe na uhakika kwamba Yehova anatambua mambo yote unayofanya kwa ajili yake. (Ebr. 6:10) Inawezekana umejionea ukweli wa maneno haya ya Yesu: “Hakuna mtu aliyeacha nyumba au ndugu au dada au mama au baba au watoto au mashamba kwa ajili yangu na kwa ajili ya habari njema ambaye hatapata mara 100 sasa katika kipindi hiki—nyumba, ndugu, dada, mama, watoto, mashamba, pamoja na mateso—na katika mfumo wa mambo unaokuja, uzima wa milele.” (Marko 10:29, 30) Kwa kweli, baraka ambazo umepata ni nyingi zaidi ukilinganisha na jambo lolote ulilojidhabihu.—Zab. 37:4. w24.03 9 ¶5
Jumapili, Agosti 10
Rafiki wa kweli hupenda nyakati zote naye ni ndugu ambaye amezaliwa kwa ajili ya nyakati za taabu.—Met. 17:17.
Wakristo huko Yudea walipokabili njaa kali, akina ndugu katika kutaniko la Antiokia “wakaamua kila mmoja kulingana na uwezo wake, watume msaada kwa akina ndugu walioishi Yudea.” (Mdo. 11:27-30) Ingawa akina ndugu waliokabili njaa waliishi eneo la mbali, Wakristo huko Antiokia waliazimia kuwasaidia. (1 Yoh. 3:17, 18) Leo, sisi pia tunaweza kuonyesha huruma tunapopata habari kwamba waabudu wenzetu wamepatwa na msiba. Tunaitikia upesi—labda kwa kuwauliza wazee ikiwa tunaweza kusaidia katika kazi ya kutoa msaada, kwa kutoa mchango kwa ajili ya kazi ya ulimwenguni pote, au kwa kusali kwa ajili ya wale walioathiriwa na msiba. Huenda ndugu na dada zetu wakahitaji pia msaada ili kupata mahitaji yao ya msingi. Mfalme wetu, Kristo Yesu, atakapokuja kutekeleza hukumu, tungependa atupate tukionyesha huruma, kisha atupatie mwaliko wa ‘kuurithi Ufalme.’—Mt. 25:34-40. w23.07 4 ¶9-10; 6 ¶12