-
Talaka Huwa na MajeruhiAmkeni!—1991 | Oktoba 8
-
-
Talaka Huwa na Majeruhi
KAMA ungeamini yote ambayo “wataalamu” wameandika juu ya talaka katika muda wa miongo kadhaa iliyopita, labda ungekata shauri kwamba katika talaka ya kisiku-hizi, hakuna mtu aliye na kosa na hakuna yule anayeumizwa.
Wazazi wengi wameingzwa kwa wepesi kwenye njia ya talaka kutokana na misemo yenye kurudiwarudiwa na wengi, kama vile: Talaka ni afadhali kwa watoto kuliko ndoa isiyo na furaha; ebu ngoja mpaka watoto wawe ‘na umri ufaao,’ ili kuwaepusha na uchungu wowote; watoto hurudia tena hali yao ya kawaida kutoka kwa mkazo ule baada ya miaka michache tu.
Wengine wameunga mkono maoni hayo ya mtazamo mwema. Kwa mfano, waandishi Susan Gettleman na Janet Markowitz wanakataa “ile hekaya ya mtoto aliyeharibiwa.” Wao wakazia kwamba talaka haihitaji kuleta mkazo wa akili kwa watoto ikiwa wazazi ‘wanaishughulikia kikomavu.’ Hata wanasababu kwamba talaka ya wazazi huenda ikasaidia watoto kuwezana na talaka zao wenyewe siku fulani! Wao wadai: “Hasa malengo ya mabadilisho yapasa kuwa mfanyizo wenyewe wa ndoa na hekaya ya mambo ya kinyumbani.”—The Courage to Divorce.
Lakini je, semi kama hizo za ujasiri na mkazo huwa za kweli, kweli? Katika ulumwengu wenye hesabu zinazoongezeka za talaka, ni nini huwa gharama halisi za talaka kwa watoto? Je, ni kweli kwamba hakuna mtu anayeumia?
Matokeo Yenye Kuogofya
Katika mwaka 1971, wachunguzi wa U.S. Judith Wallerstein na Joan Berlin Kelly walianzisha uchunguzi wenye kutia alama juu ya matokeo ya muda mrefu ya talaka kwa familia. Walichagua familia 60 zilizokuwa katika taabu ya talaka. Yote pamoja, familia hizi zilikuwa na watoto 131 wenye umri wa kati ya miaka 2 na 18. Kwa kuwashangaza, wachunguzi hao walipata kwamba karibu wakati wote, talaka haikuwa kamwe kama kitulizo kwa watoto. Hii ilikuwa kweli hata wakati ambapo wazazi wao walikuwa na ndoa isiyo na furaha. Badala yake, talaka iliacha watoto wakiwa wamefadhaika.
Je, matokeo yalikuwa mkazo wa kiakili wa muda tu? kwa kuhuzunisha, la. Baada ya miaka mitano, asilimia 37 ya watoto hao walikuwa wamepata mshuko wa moyo kwa kadiri ndogo au kubwa. Wengi wao bado walitazamia kwamba wazazi wao wangeafikiana tena—hata ikiwa tayari walikuwa wameoa au kuolewa tena! Baada ya miaka 10 au hata 15, karibu nusu ya watoto waliochunguzwa “walifikia kuwa watu wazima wenye wasiwasi, wasiotimiza mambo kikamili, wenye kujilaumu, na wakati mwingine wakiwa vijana wanaume na wanawake wenye hasira.”
Matokeo kama hayo yako dhidi ya hekima ya kikawaida. Kama vile Wallerstein aandikavyo: “Yale tuliyopata yalikuwa kinyume kabisa cha yale tuliyotazamia. Habari hii haikupendwa na wengi, na tulipata barua zenye kuonyesha ghadhabu kutoka kwa watabibu, wazazi, na mawakili wakisema kwamba tulikosea bila shaka yoyote.”
Hata hivyo, watoto hao hawakuwa wanadanganya; baadhi ya uchunguzi mwingine umethibitisha uamuzi wa Wallerstein na Kelly. Journal of Social Issues ilisema kwamba wataalamu wengi, kama vile wanasayansi wa tabia, “wanaamini kwamba mtengano wa wazazi na mvunjiko wa ndoa una matokeo mabaya sana kwa watoto na wabalehe pia.” Jarida hilo liliongezea kwamba itikadi kama hizo “zimedhihirishwa kwa kiwango kikubwa,” zikionyesha matokeo kama haya: Watoto wa talaka wana viwango vya juu zaidi vya utovu wa nidhamu na tabia zisizokubalika kijamii kuliko vile watoto kutoka familia zilizoungana; kiwango cha watoto wa talaka wanaolazwa katika hospitali za kutibu ugonjwa wa akili ni kama mara mbili ya wale wanaotoka katika familia zilizoungana; talaka labda ndiyo sababu inayoongoza ya mshuko wa moyo kwa watoto.
Namna Gani Watoto Wakubwa?
Watoto wakubwa hushughulika na talaka kwa njia ile ile kama wale wachanga. Wakati wabalehe washuhudiapo talaka ya wazazi wao, huenda wakaugua kutokana na jambo hilo ambalo huharibu maoni yao juu ya ndoa na taasisi nyinginezo kama shule. Wengine hukata maneno kwamba mahusiano yote hayategemeki, yakielekea kufunuka siku fulani katika usaliti na ukosefu wa uaminifu.
Kwa kukosa usawaziko hivi, vijana fulani hupita kiasi kwa upande ule mwingine baada ya wazazi wao kutaliki. Wengine hugeukia dawa za kulevya, wengine huangukia upotovu wa ngono, na wengine hutoroka nyumbani. Wengine huonekana kuwa wanachukuliana vema na talaka, lakini baadaye mwitikio wao uliocheleweshwa huanza kutenda. Labda si upatano wa kivivi hivi tu kwamba, kulingana na The Washingtonian, ongezeko la talaka limeandamwa na ongezeko lile lile katika matatizo ya ulaji na kujiua kwa matineja.
Hivyo wazazi wanaongojea wakati wao, wakingoja mpaka watoto wao wawe ‘na umri ufaao’ kabla ya kufanya talaka, huenda wakangoja kwa muda mrefu. Hakuonekani kukiwa na ‘umri ufaao’ wa kimizungu ambao watoto waweza kupitia talaka bila ya kuumizwa.a Mwanasoshiolojia Norval D. Glenn hata alidokeza katika gazeti Psychology Today kwamba watoto waweza kuugua kutokana na matokeo mabaya ya talaka ambayo “huendelea bila kuisha muda wote wa maisha yao.” Yeye alimalizia hivi: “Lazima mtu afikirie kwa uzito juu ya kisio la kwamba idadi inayoongezeka ya watoto wa talaka inaongoza kwenye mbomoko wa polepole lakini wenye kuendelea wa hali njema ya idadi kubwa ya watu.”
Lakini mavumbuzi, michunguzo, na takwimu hizo, ingawa ni za kuogofya, hazimaanishi kwamba kila mtoto wa talaka ataelekea kuongoza maisha yenye matatizo. Hata hivyo, zinaonyesha kwamba talaka hutolea watoto hatari halisi kikweli. Swali ni: Watoto wawezaje kulindwa kutokana na matokeo ya talaka?
Tumaini Gani kwa Watoto?
Hakuna ulinzi bora zaidi kuliko kukinga. Kama vile Dakt. Diane Medved alivyoweka jambo hilo katika kitabu chake The Case Against Divorce: “Ni lazima sisi tuache kukubali hangaiko la kibinafsi liwe ndiyo kanuni pekee ya kufaa kwa talaka.” Hakuwezi kuwa na shaka lolote kwamba kujipenda mwenyewe, na ule mwelekeo wa mimi-kwanza ambao umeenea sana katika jamii ya kisiku-hizi umeharibu ndoa zisizohesabika. Wenzi wa ndoa wanawezaje kukinza uvutano huu na kufanya ndoa zao zidumu?
Biblia yadai kwamba mwandishi wayo ndiye Mbuni wa ndoa. Katika kuthibitisha dai hilo, shauri la Biblia juu ya ndoa hufanya kazi kwa hakika. Imesaidia mamilioni ya wanaume na wanawake kufanya maendeleo katika ubora wa maisha ya familia. Biblia imeokoa ndoa zisizohesabika kutokana na talaka. Inaweza kufanya kazi kwako pia.b
Hata hivyo kwa kuhuzunisha, si mara zote kwamba talaka inaweza kuepukwa au kuzuiwa. Talaka ni jambo halisi la ulimwengu wa kisasa. Wazazi fulani hujifunza juu ya viwango vya Mungu vya ndoa baada ya kutalikiana. Na hali wengine huishi kwa viwango hivyo kishikamanifu, kuja tu baadaye kusalitiwa na mwenzi mwenye ubinafsi na asiye na adili. Biblia yenyewe hukubali kwamba katika hali zenye kupita mipaka, talaka inakubalika. (Mathayo 19:9) Lakini, kama vile Yesu alifunza, ni jambo lisilowezekana kufanya uamuzi wenye hekima bila ya ‘kuhesabu gharama’ kwanza.—Luka 14:28.
Ikiwa tayari talaka imeshafanywa kihalisi, kwa kweli huu sio wakati wa kuzama katika hisia za hatia na majuto. Huu ndio wakati wa kuzimisha mpigo huo kwa ajili ya watoto. Inawezekana! Dakt. Florence Bienenfeld, mshauri na mpatanishi wa talaka mwenye kuheshimiwa na watu wengi, anahakikishia wazazi waliotalikiana: “Si lazima talaka iwe msiba wa Kigiriki ambapo kila mtu anakufa. Kila mtu aweza kuishi, na mwishowe kurudia hali yake ya kwanza na kufanya vema sana.”—Helping Your Child Succeed After Divorce.
Lakini jinsi gani? Wazazi, watu wa ukoo, na marafiki wanaweza kufanyaje ili kusaidia watoto wa talaka?
-
-
Kusaidia Watoto wa TalakaAmkeni!—1991 | Oktoba 8
-
-
Kusaidia Watoto wa Talaka
“Wakati mmoja, nilipokuwa na umri wa miaka mitatu, baba yangu alikuja kunichukua twende kuzuru. Tulienda na akanirudisha nyumbani kwa gari. Tulikaa ndani ya gari pamoja kwa kipindi kidogo. Lakini mara tu mama yangu alipotokea nje kuja kunichukua, yeye na baba yangu walianza kugombezana na kubishana kupitia dirisha la gari—mimi nikiwa katikati.
“Kwa ghafula baba yangu akafungua mlango na kunisukuma nje ya gari. Halafu akaendesha gari kwa kasi sana na kutoweka. Mimi sikujua kilichokuwa kinatendeka. Mama yangu hata hakuniruhusu nimfungue mwanasesere wangu. Sikumwona kamwe baada ya hapo. Na sikumwona baba yangu tena mpaka nilipokuwa na umri wa miaka 19.”—Heidi.
“WAKATI huponya jameraha yote,” ndivyo husema mithali moja. Je, mithali hiyo ni ya kweli? Au watoto huharibiwa kabisa na talaka bila matumaini ya kurudia hali yao ya kwanza?
Kulingana na The Journal of Social Issues, mengi yanategemea yale yanayotukia baada ya talaka. Jarida hilo linasema: “Mahusiano ya kifamilia ambayo hutokea baada ya talaka huathiri watoto kwa njia ile ile ambayo talaka huwaathiri au hata kwa ubaya zaidi.”
Katika kisa cha Heidi, talaka ya wazazi wake ilikuwa tu ndio mwanzo wa matatizo yake. Kama vile itukiavyo kwa kawaida, ndoa ya pili ya mama yake haikufanikiwa kupita ile ya kwanza, na hata ile iliyofuata. Maisha ya Heidi akiwa mtoto yaliokuwa kama kusafiri kwenye basi lenye vishindo ambako vita vingi vyenye mayowe na kuvunjwa kwa vyombo vya jikoni na hali kadhalika siku za kiangazi zenye upweke katika nyumba iliyo tupu, akifikiria kwa hofu ni wakati gani—na kama—mama yake angekuja nyumbani.
Kuna mengi ambayo wazazi waweza kufanya ili kuepusha watoto wao kutokana na matokeo haya yenye msukosuko ya talaka. Talaka, kwa vyovyote vile, hukomesha ndoa, si kuwa mzazi.
Wazazi—Daraka Lao Lenye Maana
“Kile kitendo cha uzazi kinastahilisha watoto kuwa na mama na baba,” wakaandika wanasaikolojia wawili katika Psychology Today. Maneno hayo huenda yakaonekana kwako kama ni yenye kujithibitisha yenyewe. Na bado, talaka hunyima mtoto wazazi wote wawili katika njia fulani kama kwa dhoruba moja.
Kwa mfano, fikiria juu ya United States, ambayo kwa takwimu yaweza kuitwa kitovu kikuu cha talaka ulimwenguni. Huko, zaidi ya asilimia 90 ya watoto wa talaka wanaishi na mama na wana uhusiano wa kiziara na baba. Zaidi ya nusu ya watoto hao huona baba zao mara moja tu kwa mwaka au hata hukosa kumwona kabisa! Na ule wakati ambao mama hutumia na watoto wake hushuka pia baada ya talaka, kwa kadiri ya saa 21 kwa juma, kulingana na uchunguzi mmoja.
Kama wachunguzi hukubaliana kwa chochote kingine, wao wanakubali kwamba watoto huelekea kujipatanisha vema na maisha baada ya talaka ikiwa wao wanaendelea kuwa na uhusiano unaofaa na wenye uendelevu na wazazi wote wawili. Ikiwa hilo haliwezekani, uhusiano mwema na angalau mzazi mmoja bado husaidia kuzimisha mpigo huo wa talaka. Lakini wazazi wawezaje kusitawisha ukaribu huo na watoto wao baada ya talaka?
Kutumia Wakati kwa Kufaa
Ikiwa wewe ni mama uliyetalikiwa, kudumisha ukaribu huenda kukawa jambo gumu la ushindani. Mara nyingi, huenda ukapatwa na kile ambacho jamii nyingi huona kuwa ni alama mbili za aibu: talaka na umaskini. Huku ukiingia katika hali ya kufanya kazi bila ya kuwa umejitayarisha, hali ukijitahidi kujazia malipo ya utegemezo kutoka kwa aliyekuwa mwenzi wako ambayo huwa hayategemeki au hayatoshi, huenda ukahisi kwamba una wakati mchache unaobaki kwa ajili ya watoto wako.
Jibu lenyewe: jitihada na ratiba. Nunua wakati wowote ule unaoweza kuupata, na upange na mtoto wako kile mtakachofanya wakati huo. Hata wakati mchache kila siku wa akili isiyogawanyika ni afadhali zaidi kuliko kukosa kabisa. Kupangia kimbele tafrija yenye maana mkiwa pamoja pia humpa mtoto wako jambo la kutazamia.
Halafu kuna uhitaji wa muhimu wa kumpa mtoto wako mwongozo wa kiroho, nidhamu, na mazoezi. Wakati ulio dhahiri kabisa kwa ajili ya makusudi haya huenda uwe vigumu kuupata. Hivyo Biblia hushauri: “Nawe uwafundishe watoto wako kwa bidii, na kuyanena, uketipo katika nyumba yako, na utembeapo njiani, na ulalapo, na uondokapo.”—Kumbukumbu la Torati 6:7.
Je, huwa mmo “njiani” pamoja kamwe, labda mkisafiri kwa gari lako au mkitumia usafiri wa umma? Nini huvutia uangalifu wako—mtoto wako, au gazeti au redio ya gari? Wakati mnapokula pamoja, je, televisheni huzamisha maongezi yote, au mlo huo huwa ndio wakati wa familia yako kuzungumza kwa amani? Je, kuna kazi mbalimbali unazoweza kushiriki pamoja na mtoto wako, kama vile kutayarisha chakula au kufua nguo?
Bila shaka hiyo haimaanishi kwamba wewe unyakue vipindi hivi ili kuhutubia mtoto wako. Kwa kuwa pamoja tu na mtoto wako na kuzungumza kirafiki na kwa uwazi, pasipo shaka utatia ndani yake baadhi ya sifa zako. Nyakati kama hizi zaweza pia kuwa fursa zifaazo kwako kuwapa watoto wako uhakikisho wanaohitaji sana sasa. Watoto fulani huhisi kwa usiri kuwa wenye lawama kwa mvunjiko wa wazazi wao. Wengine huhisi wamekataliwa na mzazi aliyeondoka nyumbani. Ikiwa unawahakikishia mara kwa mara juu ya upendo wako kwao, ukiwasifu kwa tabia zao nzuri na mambo wanayotimiza, na kuwafanya wahisi kuwa salama vya kutosha kuweza kusema yaliyo akilini kwa unyofu, utakuwa umefanya mengi katika kuzimisha mpigo wa talaka.
Wazazi wengine huachilia nidhamu baada ya talaka, mara nyingi ikiwa ni kutokana na hisia za hatia. ‘Mwanangu ameona magumu ya kutosha siku za hivi karibuni,’ wao waonekana wakisababu. Lakini kupatia watoto wako uhuru wa kufanya watakavyo si kuwaonyesha upendo. Mkurugenzi wa programu ya wabalehe na watoto katika hopitali ya kutibu ugonjwa wa akili aliambia The Washingtonian hivi: “Watoto mara nyingi huniambia hivi, ‘wazazi wangu huniruhusu nifanye nitakavyo. Wao hawanijali.’” Kama vile Biblia isemavyo: “Usipotia mtoto wako nidhamu, wewe humpendi. Iwapo kweli wampenda, utamsahihisha.”—Mithali 13:24, Todays English Version.
Mtoto Aliyegawanywa
Wakati mvulana mmoja mchanga alipoulizwa achore picha katika kliniki ya talaka, alijichora mwenyewe akiwa kama chombo cha kuvutaniwa kati ya wazazi wake wawili wenye hamaki; alikuwa anakongonyolewa kwenye vifundo akitokwa na damu humo. Hivyo ndivyo baadhi ya watoto wa wazazi waliotalikiana huhisi. Hali mtoto anawapenda wazazi wote wawili, hakuna mzazi anayetaka mtoto ampende yule mwingine.
Katika uchungu mkali wa moyo na maneno ambao huambatana na talaka, ni vigumu sana watoto wasitiwe ndani na wazazi wao katika pigano hilo. Wallerstein na Kelly waliripoti kwamba theluthi mbili ya wazazi katika uchunguzi wao walishindania kwa udhahiri upendo na utii wa watoto wao. Dakt. Bienenfeld aonya wazazi kwamba kumfanya mtoto ahisi kuwa amegawanywa kati ya wazazi kunaweza kutokeza hisia za kujichukia na za kuwa na hatia na “kutapunguza nafasi zake za kuwa na furaha, kutosheka na kufanikiwa.”
Biblia hushauri hivi kwa hekima: “Nanyi, akina baba [au akina mama], msiwachokoze watoto wenu; bali waleeni katika adabu na maonyo ya Bwana [Yehova, NW]. (Waefeso 6:4.) Kwa wazi, kumfanya mtoto wako achukie yule mzazi mwingine si kumlea katika njia ya Kikristo.
Kila mtoto ana wazazi wawili. Kifo chaweza kubadilisha hilo, lakini talaka haiwezi. Na isipokuwa korti liwe limezuia mzazi yule mwingine asiwaone watoto (au yule mzazi mwingine anaepa daraka kimakusudi), huenda ukahitaji kushirikiana na aliyekuwa mwenzi wako katika kutunza watoto.
Ni kweli, huenda ukawa na sababu ya haki ya kuwa na uchungu kuelekea aliyekuwa mwenzi wako. Lakini ukitumia watoto wako ili kumwadhibu, ni watoto wako ndio hasa huumia. Dakt. Bienenfeld adokeza kwamba kwa kukubali wewe mwenyewe kwamba huenda ulihusika pia katika matatizo yenu ya ndoa kwaweza kusaidia kuondoa uchungu wako. Gazeti Parents lasema juu ya mwanamke mmoja aliyejaribu kusali kwa niaba ya aliyekuwa mwenzi wake wakati wowote alipokuwa na fikira zisizofaa kumwelekea. Alipata kwamba mbinu hiyo ilimpa hisia ya hali njema na udhibiti iliyokuwa mpya kabisa kwake na iliyomweka huru kutokana na ‘kuganda katika hali ya kudumu ya vita.’—Linganisha Mathayo 5:43-45.
Je, Wengine Waweza Kusaidia?
Wanasaikolojia Julius na Zelda Segal waandika katika gazeti Parents kwamba “watoto katika familia zilizovunjika hutiwa nguvu ikiwa angalau nyuzi fulani za uendelevu zabaki bila kudhuriwa” baada ya dhoruba ya talaka. Kwa kuhuzunisha, kulingana na wanasaikolojia hawa, “kuna mwelekeo wa majirani na marafiki kujiepusha, na ndivyo ilivyo na mababu na nyanya fulani kwa sababu wanajishugulisha kuchukua upande fulani wa ule mzozo wa wazazi.”
Naam, talaka ni yenye ukatili hasa kwa watoto wakati watu wa ukoo wanapowatoweka maishani mwao. Hiyo huongeza hisia zao za kuachwa tupu. Hivyo ikiwa wewe ni shangazi, mjomba, babu au nyanya ya watoto wowote wa talaka, kaza fikira kwenye kuwapa uhakikishio wanohitaji sana sasa badala ya kushiriki katika mzozo wa wazazi wao. Wakati mwingine, hakuna mtu awezaye kutia mtoto nguvu kuliko babu au nyanya mwenye upendo.
Heidi, aliyenukuliwa mwanzoni mwa makala hii, hakupokea utegemezo kama huo. Na bado, hadithi yake ni yenye mafanikio. Leo, akiwa na umri wa miaka 26, yeye ni mwanamke aliyeolewa katika ndoa yenye furaha, mwenye ukunjufu wa moyo, na bidii. Ni nini kimechangia kufaulu kwake?
Kwa neno moja: urafiki. Akiwa tineja, Heidi alianza kujifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova. Kwenye Jumba la Ufalme ambako alihudhuria mikutano, yeye alipata marafiki wa kweli. “Nilikuwa ninafikiri kwamba hali yangu ilikuwa bila matumanini kabisa,” yeye akumbuka. “Lakini kuwa na watu unaoweza kuzungumza nao husaidia. Nilikuwa na rafiki mmoja ambaye ningeweza kumwambia lolote. Yeye wakati wote alijua kama kulikuwa na chochote chenye kasoro, na mwishowe ningemweleza. Yeye alikuwa kama mama kwangu. Lakini kulikuwa na wengine ambao ningeweza kufanya vitu pamoja nao pia.” Heidi alipata ukweli wa ahadi ya Yesu kwamba kundi la Kikristo lingeandaa familia kubwa kwa wale waliopoteza yao.—Marko 10:29, 30.
Lakini si Heidi aliyeanzisha urafiki huo. “Walinitafuta,” yeye asema. Na hilo ni jambo lenye kutukia mara nyingi kati ya watoto wa talaka katika kundi la Kikristo. Kwa mfano, mwanamke mchanga jina lake Meg hukumbuka kwa uchangamshi jinsi wenzi wawili wa ndoa walivyofanya urafiki naye baada ya wazazi wake kuachana: “Wao walijua tu kwamba niliwahitaji, na wao walikuwa karibu nami. Wewe hutaki kusema, ‘Ona, ninakuhitaji. Ninataka unipende sasa.’”
Namna gani wewe? Je, waweza kuwa kama ndugu, dada, mama, baba, babu au nyanya kwa mtoto wa talaka? Huyo kijana labda hatakuuliza ufanye hivyo, lakini hiyo haimaanishi kwamba yeye hakuhitaji.
Bila shaka, wewe hutaweza kamwe kurudisha hali zote za familia iliyounganika. Lakini waweza kuwa rafiki, msikilizaji mzuri, mwenye huruma. Wewe waweza pia kumsaidia mchanga huyo kwa kumwongoza kwenye uhusiano mwema ma Muumba wetu—“Baba wa yatima” aliye wa kweli kweli na Rafiki mkuu zaidi ambaye yeyote angetaka.—Zaburi 68:5.
Hata hivyo je, kuna tumaini la wakati ambapo idadi za talaka zitabadilika, wakati ambapo watoto watakuwa na uhakika wa kukua katika familia nzima nzima zenye furaha?
Wakati Familia Itakapopona
Ikiwa ni lazima tutegemee binadamu kwa suluhisho, basi jibu ni la, hakuna tumaini halisi kwa watoto. Binadamu hawezi hata kuanza kutengeneza familia ya kibinadamu ya tufe lote iliyogawanyika na isiyo na matumaini yoyote, achia mbali familia zisizohesabika ambazo zimegawanyika zinazoifanyiza. Kama vile Linda Bird Francke alivyoandika katika Growing Up Divorced: “Mengi sana yametendeka haraka sana. Korti zinatatanika. Mashule yanatatanika. Familia zinatatanika. Hakuna mtu ajuaye cha kutazamia kutoka kwa mwingine katika hizi siku za wingi wa talaka kwa vile hakuna sheria, hakuna violezo vya kufuatwa.”
Lakini Muumba wa binadamu hatataniki. Yeye anaelewa ulimwengu wetu uliogawanyika, na anaona kwamba hauhitaji “wataalamu” wa kibinadamu ili kuutuliza. Unahitaji kubadilishwa. Naye anaahidi kufanya hivyo. Yeye anaahidi kwamba wale wanaofanya mapenzi yake wataokoka wakati mfumo huu mwovu upitapo na waishi kuona paradiso iliyorudishwa ya tufe lote. (Luka 23:43; 1 Yohana 2:17) Akiishi chini ya utawala wa Mungu, mwanadamu ataponywa kutokana na dhambi ambayo huambukiza asili yake. Ubinafsi na kutokamilika kunakoleta migawanyiko, chuki, na kutokuwa na umoja mwishowe kutapitilia mbali. Familia ya kibinadamu itapona.—Ufunuo 21:3, 4.
Talaka wakati huo itakuwa sazo la wakati uliopita wenye kudidimia.
-