Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g99 4/22 kur. 20-25
  • Twapelekwa Uhamishoni Siberia!

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Twapelekwa Uhamishoni Siberia!
  • Amkeni!—1999
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Twapelekwa Uhamishoni
  • Kazi Uhamishoni
  • Maisha Yetu ya Kiroho
  • Kuvumilia Hali Zilipobadilika
  • Maendeleo Yangu ya Kiroho
  • Jinsi Kazi Ilivyositawi
  • Kushangilia Upanuzi Mkubwa Zaidi
  • Shabaha ya Mashambulizi ya Sovieti
    Amkeni!—2001
  • Nilimtumikia Mungu Licha ya Magumu
    Amkeni!—2005
  • Hangaiko Langu Kuu—Kudumu Mwaminifu
    Amkeni!—2000
  • Zaidi ya Miaka 40 Chini ya Marufuku ya Ukomunisti
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1999
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—1999
g99 4/22 kur. 20-25

Twapelekwa Uhamishoni Siberia!

KAMA ILIVYOSIMULIWA NA VASILY KALIN

Kama ungemwona mtu akisoma Biblia kwa utulivu katikati ya kelele za mizinga, je, hungetaka kujua angewezaje kuwa mtulivu jinsi hiyo? Baba yangu aliona jambo hilo hasa zaidi ya miaka 56 iliyopita.

ILIKUWA Julai 1942, Vita ya Ulimwengu ya Pili ilipokuwa imechacha. Jeshi la Ujerumani lilipopita katika kijiji cha Vilshanitsa, anakotoka baba, huko Ukrainia, baba yangu alipitia kwenye nyumba ya watu fulani wazee-wazee. Mizinga ilikuwa ikilipuka kila mahali, na bado mwanamume huyo alikuwa ameketi kando ya jiko akichemsha mahindi na kusoma Biblia.

Nilizaliwa miaka mitano baadaye, karibu na jiji lenye kupendeza la magharibi ya Ukrainia la Ivano-Frankivs’k, ambalo wakati huo lilikuwa sehemu ya Muungano wa Sovieti. Baadaye baba yangu alinisimulia jinsi anavyokumbuka kukutana kwake na mtu huyo, aliyekuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova na pia juu ya miaka yenye kutisha ya vita. Watu walikuwa wamechoka na kutatanishwa na yote hayo, na wengi walijiuliza, ‘Kwa nini kuna ukosefu mwingi wa haki? Kwa nini maelfu ya watu wasio na hatia wanakufa? Kwa nini Mungu anaruhusu hayo? Kwa nini? Kwa nini? Kwa nini?’

Baba alizungumza waziwazi na kwa muda mrefu na mwanamume huyo mzee kuhusu maswali hayo. Mwanamume huyo akifungua Biblia yake kwenye andiko baada ya andiko, alimwonyesha Baba majibu ya maswali yaliyokuwa yamemtatanisha kwa muda mrefu. Alimweleza kwamba Mungu alikusudia kukomesha vita vyote kwa wakati wake aliouweka na kwamba dunia itakuwa paradiso yenye kupendeza.—Zaburi 46:9; Isaya 2:4; Ufunuo 21:3, 4.

Baba aliharakisha kwenda nyumbani na kusema kwa mshangao: “Je, mnaweza kuamini jambo hili? Baada ya kuzungumza mara moja tu na Mashahidi wa Yehova, macho yangu yamefunguka! Nimeipata kweli!” Baba alisema kwamba ijapokuwa alikuwa amehudhuria Kanisa Katoliki kwa ukawaida, makasisi hawakuwahi kujibu maswali yake. Kwa hiyo Baba akaanza kujifunza Biblia, na mama yangu akajiunga naye. Pia walianza kufundisha watoto wao watatu—dada yangu, aliyekuwa na umri wa miaka 2 tu, na ndugu zangu, ambao mmoja alikuwa na umri wa miaka 7 na yule mwingine miaka 11. Muda mfupi baada ya hapo, makao yao yaliharibiwa vibaya sana na bomu, ikiacha chumba kimoja tu cha kuishi.

Mama alitoka kwenye familia kubwa yenye dada sita na ndugu mmoja. Baba yake alikuwa mmojawapo wa watu matajiri katika eneo hilo, naye alithamini sana mamlaka yake na cheo chake. Kwa hiyo, mwanzoni, watu wa jamaa walipinga imani mpya ya familia yetu. Hata hivyo, baada ya muda fulani wengi wa wapinzani hawa walitupilia mbali mazoea mengine ya kidini yasiyo ya kimaandiko, kama vile matumizi ya sanamu, na kujiunga na wazazi wangu katika ibada ya kweli.

Makasisi walichochea watu waziwazi wapinge Mashahidi. Tokeo likawa kwamba wakazi wa mahali hapo walivunja madirisha yao na kuwatisha. Yajapokuwa yote hayo, wazazi wangu waliendelea kujifunza Biblia. Hivyo, kufikia wakati nilipozaliwa mwaka wa 1947, familia yetu ilikuwa inamwabudu Yehova katika roho na kweli.—Yohana 4:24.

Twapelekwa Uhamishoni

Ningali naikumbuka kabisa asubuhi ya Aprili 8, 1951, hata ingawa nilikuwa na umri wa miaka minne tu wakati huo. Wanajeshi wenye mbwa waliingia nyumbani kwetu. Walitupatia amri ya kuhamishwa na kuanza msako. Askari-jeshi wenye bunduki za kumimina risasi na mbwa, walisimama mlangoni, nao wanaume waliovalia nguo za kijeshi waliketi kwenye meza yetu, wakitungojea tulipokuwa tukijitayarisha haraka ili kuondoka kwa muda wa saa mbili tulizokuwa tumepewa. Sikuweza kuelewa kilichokuwa kikiendelea, nikalia.

Wazazi wangu waliamriwa kutia sahihi hati iliyosema kwamba hawakuwa Mashahidi wa Yehova tena na kwamba hawangeendelea kujishughulisha nao. Kama wangetia sahihi, wangeachwa waishi katika nyumba yao na nchi yao ya nyumbani. Lakini Baba alijulisha hivi waziwazi: “Nina uhakika kwamba popote pale mtakapotupeleka, Mungu wetu Yehova, atakuwa pamoja nasi.”

“Fikiria familia yako, watoto wako,” ofisa huyo akasihi. “Kwani, hampelekwi mahali pa kustarehe. Mwapelekwa kaskazini ya mbali, ambako kuna theluji daima na dubu wengi.”

Wakati huo neno “Siberia” lilikuwa baya na lisilojulikana kwa kila mtu. Hata hivyo, imani na upendo mwingi kwa Yehova ulithibitika kuwa wenye nguvu kuliko hofu ya mahali pasipojulikana. Mali zetu zilipakiwa kwenye bogi, nasi tulipelekwa jijini na kuingizwa katika mabehewa, pamoja na familia nyinginezo 20 hadi 30. Kisha tukaanza safari yetu hadi kwenye pori au nyika ya mbali, ya Siberia.

Katika stesheni za reli njiani, tulikutana na treni nyingine zikibeba wale waliokuwa wakihamishwa, na tuliona ishara zilizoangikwa kwenye magari ya reli: “Mashahidi wa Yehova Garini.” Hiyo ilikuwa aina ya pekee ya ushahidi, kwa kuwa katika njia hii wengi walipata kujua kwamba maelfu ya Mashahidi na familia zao walikuwa wakipelekwa maeneo mbalimbali ya kaskazini na mashariki ya mbali.

Kuna uthibitisho mwingi unaoonyesha kwamba Mashahidi wa Yehova walikusanywa na kuhamishwa katika Aprili 1951. Mwanahistoria Walter Kolarz aliandika kuhusu hilo katika kitabu chake Re­lig­ion in the Soviet Union: “Huo haukuwa mwisho wa ‘Mashahidi’ katika Urusi, bali tu mwanzo wa enzi mpya ya utendaji wao wa kushawishi watu kubadili itikadi. Hata walijaribu kutangaza imani yao waliposimama kwenye stesheni mbalimbali wakiwa njiani kwenda uhamishoni. Katika kuwahamisha Serikali ya Sovieti haingeweza kufanya chochote kuhusu kusambazwa kwa imani yao. Wakitolewa katika kijiji chao kilicho peke yake ‘Mashahidi’ waliletwa kwenye ulimwengu mpana, hata kama huu ulikuwa tu ulimwengu mbaya wa kambi za mateso na kazi ngumu.”

Familia yangu ilikuwa na hali nzuri, kwa kuwa tuliruhusiwa kubeba chakula—unga, mahindi, na maharagwe. Babu yangu hata aliruhusiwa kuchinja nguruwe, na ikawa chakula kwetu na kwa Mashahidi wengine. Tukiwa njiani tuliweza kusikia nyimbo zilizoimbwa kutoka moyoni zikija kutoka kwenye mabehewa. Yehova alitupa nguvu ya kuvumilia.—Mithali 18:10.

Tulisafiri kuvuka Urusi kwa majuma matatu hivi na hatimaye tukafika Siberia yenye baridi, upweke, na iliyo mbali sana. Tulipelekwa hadi stesheni ya Toreya katika eneo la Chunsk la wilaya ya Irkutsk. Kutoka huko, tulipelekwa mbali zaidi katika pori hadi kwenye kijiji kidogo, ambacho hati zetu zilikifafanua kuwa “makao [yetu] ya milele.” Mali za familia 15 zilitoshea vizuri katika gari la mizigo la kuendea kwenye barafu, na trakta ililivuruta kwenye matope ya masika. Familia 20 hivi zilikaa katika kambi za muda, zilizokuwa na korido ndefu zisizokuwa na migawanyo. Wenye mamlaka walionya watu wa hapo mapema kwamba Mashahidi wa Yehova walikuwa watu wabaya sana. Kwa hiyo mwanzoni, watu walituogopa nao hawakuthubutu kufahamiana nasi.

Kazi Uhamishoni

Mashahidi wa Yehova walifanya kazi ya kukata miti, na kazi hiyo ilifanywa chini ya hali ngumu zaidi. Kazi yote ilifanywa kwa mikono—kukata magogo kwa msumeno, kuyapasua, kuyapakia kwenye magari yaliyokokotwa na farasi, na baadaye, kuyapakia kwenye mabehewa. Hali ilifanywa iwe mbaya sana na inzi wengi zaidi wenye kuuma ambao haikuwa rahisi kujificha wasikuume. Baba yangu aliteseka sana. Mwili wake ulifura kabisa, akamwomba Yehova sana amsaidie ili avumilie. Lakini kujapokuwa magumu hayo yote, imani ya Mashahidi wa Yehova walio wengi ilibaki imara.

Punde baada ya hapo tulipelekwa kwenye jiji la Irkutsk, ambamo familia yetu iliishi katika kambi ya zamani ya gereza na kufanya kazi katika kiwanda cha kutengenezea matofali. Matofali yalipakuliwa moja kwa moja kutoka katika majoko makubwa, kwa mkono, na kiasi cha kazi kiliongezwa daima, hivi kwamba watoto walilazimika kusaidia wazazi wao ili kuimaliza. Tulikumbuka kazi ngumu ya utumwa ya Waisraeli katika Misri ya kale.—Kutoka 5:9-16.

Ilijulikana wazi kwamba Mashahidi walikuwa watu wenye kufanya kazi kwa bidii na wenye kufuatia haki, wala si “adui za watu,” kama ilivyodaiwa. Ilionwa kwamba hakuna Shahidi hata mmoja aliyetukana wenye mamlaka, wala Mashahidi hawakupinga maamuzi yaliyotolewa na wenye mamlaka. Hata imani yao ilikuja kupendwa na wengi.

Maisha Yetu ya Kiroho

Ijapokuwa Mashahidi walisakwa mara nyingi—kabla ya kupelekwa uhamishoni, walipokuwa njiani kuelekea uhamishoni, na walipokuwa uhamishoni—wengi walifaulu kuficha magazeti ya Mnara wa Mlinzi na hata Biblia. Baadaye, vichapo hivyo vilitokezwa upya kwa kuandikwa kwa mkono na kwa njia nyinginezo. Mikutano ya Kikristo ilifanywa kwa ukawaida katika kambi za muda. Mkuu wa kambi za muda alipokuja na kukuta baadhi yetu tukiimba, angetuamuru tunyamaze. Nasi tunge­nyamaza. Lakini alipokwenda kwenye kambi ya muda iliyofuata, tungeanza kuimba tena. Haikuwa rahisi kutunyamazisha.

Wala kazi yetu ya kuhubiri haikupata kukoma. Mashahidi wangeongea na kila mtu, kila mahali. Kaka zangu na wazazi wangu waliniambia kila mara jinsi walivyoweza kueleza wengine kweli za Biblia. Kwa sababu hiyo, kweli ya Biblia ilianza kuvutia watu wenye mioyo myeupe. Hivyo, mnamo miaka ya mapema ya 1950, Ufalme wa Yehova, ulijulishwa katika Irkutsk na eneo lenye kuizunguka.

Mwanzoni Mashahidi walionwa kuwa maadui wa kisiasa, lakini baadaye ilitambuliwa kirasmi kwamba tengenezo letu lilikuwa la kidini kabisa. Hata hivyo, wenye mamlaka walijaribu kukomesha utendaji wetu. Kwa hiyo tulikusanyika kwa ajili ya funzo la Biblia katika vikundi vidogo-vidogo vya familia mbili au tatu tukijaribu kuepuka kugunduliwa. Msako mmoja ulifanywa kwa uangalifu mapema asubuhi moja ya Februari mwaka 1952. Baadaye, Mashahidi kumi walikamatwa, na sisi tuliobaki tulipelekwa mahali mbalimbali. Familia yetu ilipelekwa kwenye kijiji cha Iskra, ambacho kilikuwa na idadi ya watu mia moja hivi na umbali wa kilometa 30 hivi kutoka jiji la Irkutsk.

Kuvumilia Hali Zilipobadilika

Wasimamizi wa kijiji walituonyesha ukarimu tusiotazamia. Watu wa huko walikuwa wa kawaida na wenye urafiki—hata watu kadhaa walitoka nyumbani mwao kuja kutusaidia. Familia yetu ilikuwa ya tatu kuwekwa katika chumba kilekile kidogo chenye ukubwa wa meta 17 za mraba. Tulikuwa tukitumia tu taa za mafuta.

Asubuhi iliyofuata kulikuwa na uchaguzi. Wazazi wangu walisema kwamba tayari walikuwa wamepigia kura Ufalme wa Mungu, ambao bila shaka, watu hawakuuelewa. Kwa hiyo wale waliokuwa watu wazima katika familia yetu walitiwa mbaroni siku nzima. Baadaye, watu kadhaa waliuliza juu ya itikadi zao, na hilo lilitokeza fursa nzuri kwa familia yetu kuongea juu ya Ufalme wa Mungu kuwa tumaini pekee la wanadamu.

Kwa miaka minne tuliyoishi katika kijiji cha Iskra, hakukuwa na Mashahidi wengine karibu ambao tungeweza kushirikiana nao. Ili tuondoke kijijini ilitupasa kupata ruhusa ya pekee kutoka kwa mkuu, naye mara nyingi hakukubali, kwa kuwa sababu kuu ya kuhamishwa kwetu ilikuwa kututenga na watu wengine. Hata hivyo, Mashahidi walijaribu sikuzote kuwasiliana ili kushiriki chakula chochote kipya cha kiroho ambacho walikuwa wamepata.

Baada ya kifo cha Stalin mwaka wa 1953, Mashahidi wote waliokuwa wamefungwa walipunguziwa vifungo vyao kutoka miaka 25 hadi miaka 10. Wale walioishi Siberia hawakuhitajiwa kuwa na hati ya pekee tena ili kutembea. Hata hivyo, wenye mamlaka walianza misako upesi, kisha kutia mbaroni Mashahidi kama wangewapata wakiwa na Biblia au fasihi za Biblia. Kambi za pekee zilijengwa kwa ajili ya Mashahidi, na akina ndugu wapatao 400 na dada wapatao 200 waliwekwa katika kambi hizo huko Irkutsk.

Habari za kunyanyaswa kwetu katika Muungano wa Sovieti zilifikia Mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote. Hivyo, katikati ya 1956 na Februari 1957, ombi la bidii kwa niaba yetu lilifanywa kwenye mikusanyiko ya wilaya 199 iliyofanywa katika sehemu zote za ulimwengu. Jumla ya watu 462,936 waliohudhuria walikubali ombi hilo lililoelekezwa kwa aliyekuwa waziri mkuu wa Sovieti Nikolay A. Bulganin. Miongoni mwa mambo mengine, ombi hilo la bidii liliomba kwamba tuachiliwe huru na kwamba “tuidhinishwe kupokea na kuchapisha gazeti Mnara wa Mlinzi katika Kirusi, Kiukrainia na lugha nyinginezo ihitajiwapo, na vilevile vichapo vinginevyo vya Biblia vinavyotumiwa na mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote.”

Wakati huohuo, familia yetu ilikuwa imepelekwa kwenye kijiji cha mbali cha Khudyakovo, karibu kilometa 20 kutoka Irkutsk. Tuliishi huko kwa miaka saba. Mwaka wa 1960 kaka yangu Fyodor alikwenda Irkutsk, na mwaka uliofuata kaka yangu akaoa na dada yangu akahama. Kisha, mwaka wa 1962, Fyodor alikamatwa na kufungwa gerezani kwa sababu ya kuhubiri.

Maendeleo Yangu ya Kiroho

Kutoka katika kijiji chetu cha Khudyakovo, tulisafiri mwendo wa kilometa 20 hivi kwa miguu au baiskeli ili kukutana na wengine kwa ajili ya funzo la Biblia. Kwa hiyo tulijaribu kuhamia Irkutsk ili tukaribie zaidi Mashahidi wengine. Hata hivyo, msimamizi wa eneo ambamo tuliishi hakutaka tuhame, naye alifanya yote aliyoweza kuzuia jambo hilo. Ingawa hivyo, baada ya muda fulani, mtu huyo alianza kutupendelea, nasi tukaweza kuhamia kijiji cha Pivovarikha, kilometa kumi hivi kutoka Irkutsk. Kulikuwa na kutaniko la Mashahidi wa Yehova huko, na nikaanza maisha mapya. Huko Pivovarikha kulikuwa na vikundi vya Funzo la Kitabu la Kutaniko vilivyopangwa na kulikuwa na akina ndugu waliosimamia utendaji wa kiroho. Nilifurahi kama nini!

Kufikia wakati huu nilikuwa nimependa kweli ya Biblia kwelikweli, nami nilitaka kubatizwa. Mnamo Agosti 1965 tamaa yangu ilitimia nilipobatizwa katika mto mdogo uitwao Mto Olkhe, ambapo Mashahidi wengi wapya walibatizwa kipindi hicho. Kwa mtazamaji mwenye kupita tu, ilionekana kana kwamba tulikuwa tukifurahia mandari na kuogelea mtoni. Upesi baadaye nilipokea mgawo wangu wa kwanza kuwa mwangalizi wa Shule ya Huduma ya Kitheokrasi. Kisha, mnamo Novemba 1965, tulifurahia sana Fyodor aliporudi kutoka gerezani.

Jinsi Kazi Ilivyositawi

Mnamo mwaka wa 1965 wahamishwa wote walikusanyika, ikatangazwa kwamba tulikuwa na haki ya kuhamia kokote tulikotaka, hivyo ikikomesha “makao [yetu] ya milele.” Je, unaweza kuwazia shangwe tuliyopata? Ingawa wakati huo wengi kati yetu waliondoka kwenda sehemu nyinginezo nchini, wengine waliamua kubaki pale ambapo Yehova alikuwa amebariki na kutegemeza maendeleo yetu na utendaji wetu wa kiroho. Wengi wao wamelea watoto wao, wajukuu wao, na vitukuu wao katika Siberia, ambayo baada ya muda fulani, ikawa kumbe si mahali pa kutisha.

Mnamo mwaka wa 1967, nilikutana na Maria, msichana ambaye familia yao pia ilikuwa imehamishwa kwenda Siberia kutoka Ukrainia. Tulipokuwa wachanga, sote tulikuwa tumeishi katika kijiji cha Ukrainia cha Vilshanitsa. Tulioana mnamo mwaka wa 1968, na hatimaye, tulibarikiwa kuwa na mwana, Yaroslav, na baadaye binti, Oksana.

Tuliendelea kutumia maziko na arusi kukutana tukiwa vikundi vikubwa-vikubwa kwa ushirika wa kiroho. Pia tulikuwa tukitumia vipindi hivyo kueleza kweli za Biblia watu wa jamaa wasio Mashahidi na marafiki waliokuja. Mara nyingi maofisa wa usalama walihudhuria mikusanyiko hiyo, ambapo tulihubiri waziwazi tukitumia Biblia juu ya tumaini la ufufuo au kuhusu uandalizi wa Yehova wa ndoa na baraka za wakati ujao katika ulimwengu mpya.

Wakati mmoja, nilipokuwa nikimalizia hotuba ya maziko, gari lilikuja na kusimama kando, milango ikafunguliwa, na mwanamume mmoja akatoka nje na kuniamuru niingie ndani ya gari. Sikuogopa. Kwa vyovyote, sisi hatukuwa wahalifu, tulikuwa waamini wa Mungu tu. Hata hivyo, mfukoni mwangu nilikuwa na ripoti za huduma za wahubiri wa kutaniko letu. Ningeweza kutiwa mbaroni kwa sababu hiyo. Kwa hiyo niliomba kama ningeweza kumpa mke wangu fedha kabla ya kwenda nao. Papo hapo nikampa kwa utulivu kibeti changu na ripoti za kutaniko.

Kuanzia 1974, mimi na Maria tulianza kutayarisha fasihi za Biblia kwa siri nyumbani kwetu. Kwa kuwa tulikuwa na mwana mdogo, tulifanya hivyo usiku sana ili asiweze kujua tulichokuwa tukifanya. Hata hivyo, kwa sababu ya udadisi, alijisingizia kuwa amelala na kuchungulia aone tulichokuwa tukifanya. Baadaye alisema: “Najua ni nani ambaye hutengeneza magazeti kuhusu Mungu.” Tuliogopa kidogo, lakini sikuzote tulimwomba Yehova alinde familia yetu inapofanya kazi hii ya maana.

Hatimaye, wenye mamlaka walipendelea Mashahidi wa Yehova zaidi, kwa hiyo tukafanya mipango ya kuwa na mkusanyiko mkubwa katika jumba la sanaa na tafrija la Mir katika jiji la Usol’ye-Sibirskoye. Tulihakikishia wakuu wa jiji kwamba mikutano yetu hufanywa kwa ajili ya funzo la Biblia na ushirika wa Kikristo pekee. Zaidi ya watu 700 walikusanyika mnamo Januari 1990, wakijaza jumba na kuvutia watu wengi sana.

Baada ya mkutano ripota mmoja aliuliza hivi, “Mliweza kuwazoeza watoto wenu lini?” Yeye na vilevile wageni wengine, walishangaa kwamba waliketi kwa makini kwa muda wa saa nne za mkutano wa kwanza wa watu wote. Punde makala nzuri juu ya Mashahidi wa Yehova ilichapishwa katika gazeti la habari la hapo. Ilisema hivi: “Kwa kweli mtu aweza kujifunza jambo fulani kutoka kwa [Mashahidi wa Yehova].”

Kushangilia Upanuzi Mkubwa Zaidi

Mnamo mwaka wa 1991 tulikuwa na mikusanyiko saba katika Muungano wa Sovieti, iliyohudhuriwa na watu 74,252. Baadaye, baada ya jamhuri za Muungano wa Sovieti za zamani kuwa huru, nilipokea mgawo kutoka kwa Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova kwenda Moscow. Nikiwa huko niliulizwa kama ningeweza kupanua ushiriki wangu katika kazi ya Ufalme. Wakati huo Yaroslav alikuwa ameoa na alikuwa na mtoto naye Oksana alikuwa tineja. Kwa hiyo, mnamo mwaka wa 1993, mimi na Maria tulianza huduma ya wakati wote katika Moscow. Mwaka huohuo, niliwekwa rasmi kuwa mratibu wa Administrative Center of the Regional Religious Organization of Jehovah’s Witnesses katika Urusi.

Sasa mimi na Maria tunaishi na kufanya kazi kwenye majengo yetu mapya ya ofisi ya tawi yaliyo nje ya St. Petersburg. Naiona kuwa heshima kuweza kushiriki na ndugu wengine waaminifu kushughulikia ukuzi unaosonga haraka-haraka wa idadi ya wapiga-mbiu wa Ufalme katika Urusi. Leo kuna Mashahidi zaidi ya 260,000 katika zile zilizokuwa jamhuri za Muungano wa Sovieti, zaidi ya 100,000 katika Urusi peke yake!

Mara nyingi mimi na Maria hufikiria jamaa na rafiki zetu ambao wanaendelea kwa uaminifu katika utumishi wao wa Ufalme huko Siberia, mahali palipokuwa makao yetu tuliyoyapenda. Leo mikusanyiko mikubwa hufanywa kwa ukawaida huko, na Mashahidi wapatao 2,000 ni watendaji katika Irkutsk yote. Kwa kweli, unabii wa Isaya 60:22 pia unatimizwa katika sehemu hiyo ya ulimwengu: “Mdogo atakuwa elfu, na mnyonge atakuwa taifa hodari.”

[Picha katika ukurasa wa 20]

Nikiwa na baba yangu, familia yetu, na wahamishwa wengine huko Irkutsk mnamo mwaka wa 1959

[Picha katika ukurasa wa 23]

Watoto uhamishoni Iskra

[Picha katika ukurasa wa 25]

Mwaka ambao tulioana

[Picha katika ukurasa wa 25]

Nikiwa na Maria leo

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki