Zaidi ya Miaka 40 Chini ya Marufuku ya Ukomunisti
KAMA ILIVYOSIMULIWA NA MIKHAIL VASILEVICH SAVITSKII
Gazeti la Mnara wa Mlinzi la Aprili 1, 1956 (la Kiingereza), liliripoti kwamba “uhamisho mkubwa” wa Mashahidi wa Yehova ulifanywa Aprili tarehe 1, 7, na 8, 1951. “Hizo ni tarehe ambazo Mashahidi wa Yehova huko Urusi hawawezi kusahau,” gazeti hilo la Mnara wa Mlinzi likaeleza. “Katika siku hizo tatu Mashahidi wa Yehova wote ambao wangeweza kupatikana katika Ukrainia ya Magharibi, White Russia [Belarus], Bessarabia, Moldavia, Latvia, Lithuania na Estonia—zaidi ya wanaume na wanawake elfu saba . . . waliwekwa katika mikokoteni, na kupelekwa kwenye stesheni za reli ambako walipakiwa katika mabehewa ya kubebea ng’ombe na kupelekwa mbali sana.”
APRILI 8, 1951, mke wangu, mwana wangu mwenye umri wa miezi minane, wazazi wangu, ndugu yangu mdogo, na Mashahidi wengine wengi walichukuliwa kutoka katika nyumba zao zilizokuwa ndani na nje ya jiji la Ternopol’, huko Ukrainia. Baada ya kupakiwa katika mabehewa ya kubebea ng’ombe, walisafiri kwa muda wa majuma mawili hivi. Hatimaye, walishushwa katika sehemu iitwayo Siberian taiga (mwitu ulio karibu na Aktiki) magharibi mwa Ziwa la Baikal.
Kwa nini mimi sikuwa kati ya waliohamishwa? Kabla ya kusimulia nilikokuwa wakati huo na kilichotupata sisi sote baadaye, acheni niwaambie jinsi nilivyokuja kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova.
Kweli ya Biblia Yatufikia
Katika Septemba 1947, nilipokuwa na umri wa miaka 15 tu, Mashahidi wa Yehova wawili walituzuru nyumbani kwetu katika kijiji kidogo cha Slaviatin, kilometa 50 hivi kutoka Ternopol’. Mimi na Mama tulipoketi huku tukiwasikiliza vijana hao—mmoja ambaye aliitwa Maria—nilijua hiyo haikuwa dini nyingine tu. Walieleza imani yao na kujibu maswali yetu ya Biblia waziwazi.
Niliamini kwamba Biblia ni Neno la Mungu, lakini nilikuwa nimetamaushwa na kanisa. Babu yangu alikuwa akisema: “Makasisi huogopesha watu kwa mazungumzo kuhusu kuteswa katika moto wa helo, lakini makasisi wenyewe hawaogopi chochote. Wao huwapokonya tu na kuwadanganya maskini.” Ninakumbuka matendo ya jeuri na uchomaji makusudi wa mali za wakazi Wapoland wa kijiji chetu mwanzoni mwa Vita ya Ulimwengu ya Pili. Kwa kushtusha, mashambulio hayo yalipangwa na kasisi wa Katoliki ya Kigiriki. Baadaye niliona wengi wa wahasiriwa waliouawa, nami nilikuwa na hamu nyingi ya kutaka kujua sababu za kufanya ukatili kama huo.
Nilipojifunza Biblia pamoja na Mashahidi, nilianza kuelewa. Nilijifunza kweli za msingi za Biblia, kutia na uhakika wa kwamba hakuna helo yenye kuwaka moto na kwamba Shetani Ibilisi hutumia dini ya uwongo kuendeleza vita na umwagaji wa damu. Pindi kwa pindi, nilikuwa nikitua kidogo wakati wa funzo langu la kibinafsi na kutoa sala yenye kuhisiwa moyoni ya kumshukuru Yehova kwa yale niliyokuwa nikijifunza. Nilianza kumfunza ndugu yangu mdogo, Stakh, kweli hizi za Biblia nami nikafurahi sana alipozikubali.
Kujizoeza Kufanya Niliyojifunza
Nilitambua uhitaji wa kufanya mabadiliko ya kibinafsi na mara moja nikaacha kuvuta sigareti. Nilielewa pia uhitaji wa kukutana kwa ukawaida pamoja na wengine kwa ajili ya funzo la Biblia lenye mpango. Ili kufanya hivyo, nilitembea kwa miguu umbali wa kilometa kumi hivi kupitia msituni ili kufika mahali pa siri ambapo mikutano ilikuwa ikifanyiwa. Nyakati nyingine, ni wanawake wachache tu walioweza kufika kwenye mkutano, na hata ingawa nilikuwa bado sijabatizwa, niliombwa niuongoze.
Lilikuwa jambo hatari kuwa na fasihi ya Biblia, na kupatikana nayo kungeweza kusababisha hukumu ya kufungwa gerezani hadi kufikia miaka 25. Hata hivyo, nilitamani kuwa na maktaba yangu mwenyewe. Mmoja wa majirani wetu alikuwa akijifunza na Mashahidi wa Yehova, lakini kwa sababu ya woga, akaacha na kuficha fasihi yake katika bustani yake. Nilimshukuru Yehova kama nini wakati mwanamume huyo alipofukua vitabu vyake vyote pamoja na magazeti na kunipa! Nilivificha katika mizinga ya nyuki ya Baba, ambapo wengine hawangeelekea kuvitafuta.
Katika Julai 1949, nilijiweka wakfu kwa Yehova na kubatizwa ili kuonyesha wakfu wangu. Hiyo ilikuwa siku yenye furaha zaidi maishani mwangu. Shahidi aliyenibatiza kisiri alikazia kwamba haikuwa rahisi kuwa Mkristo wa kweli na kwamba majaribu mengi yaliningoja. Punde si punde, nilijua jinsi maneno yake yalivyokuwa ya kweli! Hata hivyo, maisha yangu nikiwa Shahidi aliyebatizwa yalianza kwa shangwe. Miezi miwili baada ya kubatizwa, nilimwoa Maria, mmoja wa wale Mashahidi wawili ambao walitujulisha mimi na Mama kweli kwa mara ya kwanza.
Jaribu Langu la Kwanza Lilikuja Ghafula
Katika Aprili 16, 1950, nilikuwa nikirudi nyumbani kutoka mji mdogo wa Podgaitsi wakati askari waliponikabili ghafula na kunipata na fasihi ya Biblia niliyokuwa nikipelekea kikundi chetu cha kujifunza Biblia. Nilikamatwa. Katika siku chache za kwanza nikiwa rumande, nilipigwa kwa fimbo na sikuruhusiwa kula wala kulala. Niliamuriwa pia kufanya zoezi la kuchuchumaa na kuinuka mara mia moja, huku mikono yangu ikiwa juu ya kichwa changu, zoezi ambalo lilinichosha kabisa nisiweze kumaliza. Baadaye nilitiwa katika chumba cha chini ya ardhi kilichokuwa baridi, na chenye unyevunyevu kwa saa 24.
Walinitenda vibaya hivyo wakiwa na kusudi la kupunguza uwezo wangu wa kukinza na kufanya hali iwe rahisi zaidi kupata habari kutoka kwangu. “Ulipata wapi hiyo fasihi, na ulikuwa ukiipelekea nani?” wakataka kujua. Nilikataa kufunua chochote. Kisha nikasomewa fungu la sheria ambalo lingetumiwa kunishtaki. Fungu hilo lilisema kwamba kusambaza na kuweka fasihi iliyopinga Sovieti kulistahili adhabu ya kifo au kifungo cha miaka 25.
“Ungependelea adhabu gani?” wakaniuliza.
“Singependelea yoyote,” nikajibu, “lakini ninamtumaini Yehova, na kwa msaada wake mimi nitakubali chochote atakachoruhusu.”
Nilishangaa kwamba waliniachilia baada ya siku saba. Jambo hilo lililonipata lilinisaidia kuthamini ukweli wa ahadi hii ya Yehova: “Hakika sitakuacha kwa vyovyote wala kukuachilia mbali kwa vyovyote.”—Waebrania 13:5.
Niliporudi nyumbani, nilikuwa mgonjwa sana, lakini Baba akanipeleka kwa daktari, nami nikapona upesi. Baba alituunga mkono katika ibada yetu ingawa hakushiriki imani ya wengine katika familia.
Kifungo na Uhamisho
Miezi kadhaa baadaye niliitwa nitumikie katika jeshi la Sovieti. Nilieleza kukataa kwangu kwa sababu ya dhamiri yangu. (Isaya 2:4) Hata hivyo, katika Februari 1951, nilihukumiwa kifungo cha miaka minne na kupelekwa katika gereza moja jijini Ternopol’. Baadaye nilihamishwa kupelekwa katika gereza huko L’viv, jiji kubwa zaidi lililoko umbali wa kilometa 120 hivi. Nilipokuwa gerezani huko, nilipata habari kwamba Mashahidi wengi walikuwa wamehamishwa kupelekwa Siberia.
Katika kiangazi cha mwaka wa 1951, baadhi yetu tulipelekwa ng’ambo ya Siberia, hadi Mashariki ya Mbali. Tulisafiri kwa mwezi mmoja—kilometa zipatazo 11,000—tukivuka kanda 11 za majira! Baada ya kuwa katika garimoshi kwa zaidi ya majuma mawili, hilo garimoshi lilisimama mara moja tu mahali ambapo tuliruhusiwa kuoga. Lilisimama Novosibirsk, Siberia, mahali palipokuwa na bafu ya umma.
Hapo, katikati ya umati mkubwa wa wafungwa, nilisikia mwanamume fulani akisema kwa sauti kubwa: “Ni nani hapa ambaye ni wa familia ya Yonadabu?” Neno “Yonadabu” lilitumiwa wakati huo kutambulisha wale waliokuwa na tumaini la uhai wa milele duniani. (2 Wafalme 10:15-17; Zaburi 37:11, 29) Wafungwa kadhaa walijitambulisha mara moja kuwa Mashahidi. Tulisalimiana kwa shangwe iliyoje!
Utendaji wa Kiroho Gerezani
Tulipokuwa Novosibirsk tulikubaliana kutumia neno la siri ambalo lingetuwezesha kutambuana tulipofika tulikokuwa tukienda. Sote tulipelekwa katika kambi moja ya gereza kwenye Bahari ya Japani, karibu na Vladivostok. Huko tulipanga kukutana kwa ukawaida ili kujifunza Biblia. Kuwa na ndugu hao wazee walio wakomavu, ambao walikuwa wamehukumiwa vifungo virefu gerezani, kwa kweli kuliniimarisha kiroho. Waliongoza mikutano yetu kwa zamu, wakitumia maandiko ya Biblia na mambo mengine yaliyohusiana na Biblia ambayo walikumbuka kutoka katika magazeti ya Mnara wa Mlinzi.
Maswali yaliulizwa, na ndugu hao wakajibu. Wengi wetu tulikata visehemu vya makaratasi kutoka kwa mifuko mitupu ya sementi na kuandika maelezo waliyotoa. Tulihifadhi maandishi hayo na kuyafunga pamoja ili kuyatumia kama maktaba ya marejezo ya kibinafsi. Baada ya miezi miwili, wale waliokuwa wamehukumiwa vifungo virefu walipelekwa kwenye kambi zilizokuwa kaskazini ya mbali ya Siberia. Sisi ndugu watatu tuliokuwa na umri mdogo zaidi, tulihamishwa kupelekwa Nakhodka, jiji lililokuwa karibu, kilometa zisizozidi 650 kutoka Japani. Huko, nilikaa gerezani kwa muda wa miaka miwili.
Mara kwa mara tulipata nakala ya Mnara wa Mlinzi. Gazeti hilo lilitumika likiwa chakula chetu cha kiroho kwa miezi mingi. Baada ya muda, tulipokea barua pia. Barua ya kwanza niliyopokea kutoka kwa familia yangu (sasa ikiwa uhamishoni) ilinifanya nilie. Ilisimulia kwamba, kama ilivyofafanuliwa katika Mnara wa Mlinzi ulionukuliwa katika utangulizi, nyumba za Mashahidi zilikuwa zimevamiwa nazo familia zikapewa muda wa saa mbili tu kuondoka.
Pamoja na Familia Yangu Tena
Niliachiliwa Desemba 1952, baada ya kutumikia miaka miwili kati ya miaka minne ya hukumu yangu. Nilijiunga na familia yangu katika kijiji kidogo cha Gadaley karibu na Tulun, Siberia, ambako ilikuwa imehamishiwa. Bila shaka, lilikuwa jambo lenye kupendeza sana kuwa nao tena—mwana wangu Ivan alikuwa na umri wa karibu miaka mitatu, naye binti yangu Anna alikuwa na umri upatao miaka miwili. Hata hivyo, uhuru wangu ulikuwa wa kadiri. Pasipoti yangu ilitwaliwa na wenye mamlaka wa mahali hapo, nami nikawekwa chini ya uangalizi mkali. Singeweza kusafiri umbali unaozidi kilometa tatu kutoka nyumbani. Baadaye, niliruhusiwa kusafiri kwa farasi kwenda sokoni Tulun. Huku nikiwa mwenye hadhari, nilikutana na Mashahidi wenzangu huko.
Kufikia wakati huo, tulikuwa na wasichana wawili, Anna na Nadia, na wavulana wawili, Ivan na Kolya. Katika mwaka wa 1958 tulipata mwana mwingine, Volodya. Na baadaye, katika mwaka wa 1961, tukapata binti mwingine, Galia.
Shirika la KGB (shirika la zamani la usalama wa taifa) liliniweka kizuizini mara nyingi na kunihoji. Kusudi lao halikuwa tu kunifanya nifunue habari kuhusu kutaniko, bali pia kutokeza shaka kwamba nilikuwa nikishirikiana nao. Kwa hiyo walikuwa wakinipeleka kwenye mkahawa mzuri na kujaribu kunipiga picha nikiwa ninatabasamu huku nikionekana kufurahia kuwa pamoja nao. Lakini nilitambua nia yao, na kwa jitihada yenye uangalifu, niliendelea kuwa na uso wenye kukunjamana. Kila wakati nilipowekwa kizuizini, niliwaambia akina ndugu chochote kilichotukia. Hivyo, hawakushuku kamwe uaminifu-mshikamanifu wangu.
Kuwasiliana na Kambi
Katika miaka iliyofuata, mamia ya Mashahidi walitiwa katika kambi za gereza. Wakati huo, tuliwasiliana kwa ukawaida na ndugu zetu waliokuwa gerezani na kuwapelekea fasihi. Hilo lilifanywaje? Ndugu au dada walipoachiliwa kutoka kambini, tulipata kujua kutoka kwao njia ambazo fasihi ingeweza kuingizwa kisiri licha ya vizuizi vikali. Kwa miaka kumi hivi, tuliweza kuwapelekea ndugu zetu katika kambi hizo nakala za magazeti na vitabu ambavyo tulipata kutoka Poland na nchi nyingine.
Wengi wa dada zetu Wakristo walitumia muda wa saa nyingi wakifanya kazi yenye kuchosha ya kunakili fasihi katika maandishi madogo sana hivi kwamba gazeti zima lingeweza kufichwa katika kitu kidogo kama vile ganda la kiberiti! Katika mwaka wa 1991, marufuku ilipokuwa imeondolewa na tukiwa tunapokea magazeti mazuri yenye rangi nne, mmoja wa dada zetu alisema: “Sasa tutasahauliwa.” Alikosea. Hata ingawa wanadamu huenda wakasahau, Yehova hatasahau kazi ya waaminifu-washikamanifu hao!—Waebrania 6:10.
Kuhamia Makao Mapya na Misiba
Mwishoni mwa mwaka wa 1967 nyumba ya ndugu yangu iliyokuwa Irkutsk ilipekuliwa. Filamu na nakala za fasihi ya Biblia zilipatikana. Alipatikana na hatia na kuhukumiwa kifungo cha miaka mitatu gerezani. Hata hivyo, hakuna kitu kilichopatikana nyumba yetu ilipopekuliwa. Na bado, wenye mamlaka walikuwa na hakika kwamba tulihusika, kwa hiyo familia yangu ililazimika kuondoka eneo hilo. Tulisafiri umbali wa kilometa 5,000 hivi kuelekea magharibi hadi jiji la Nevinnomyssk, huko Caucasus. Huko tulikuwa na shughuli nyingi za kutoa ushahidi wa vivi hivi.
Tulipatwa na msiba siku ya kwanza ya likizo ya shule katika Juni 1969. Alipokuwa akijaribu kuupata tena mpira uliokuwa karibu na transfoma ya umeme yenye volteji nyingi, mwana wetu, Kolya, mwenye umri wa miaka 12, alipata mshtuko mkali wa umeme. Asilimia 70 ya mwili wake ilichomeka. Akiwa hospitalini, alinigeukia na kuniuliza: “Je, tutaweza kwenda tena kisiwani pamoja?” (Alikuwa akizungumzia kisiwa tulichofurahia kuzuru.) “Ndiyo, Kolya,” nikasema, “tutaenda kwenye kisiwa hicho tena. Yesu Kristo atakapokufufua, kwa hakika tutaenda kwenye kisiwa hicho.” Akiwa na fahamu kidogo, aliendelea kuimba mmojawapo wa nyimbo za Ufalme alizopenda sana, mmoja ambao alipenda kuimba kwa kupiga tarumbeta katika okestra ya kutaniko. Alikufa siku tatu baadaye, akiwa na uhakika katika tumaini la ufufuo.
Mwaka uliofuata, mwana wetu, Ivan, mwenye umri wa miaka 20, aliitwa ajiunge na utumishi wa kijeshi. Alipokataa utumishi huo, alikamatwa na kukaa miaka mitatu gerezani. Katika mwaka wa 1971, niliitwa nijiunge na utumishi wa kijeshi na kwa mara nyingine nikatishwa kufungwa kwa kukataa utumishi huo. Kesi yangu ilikawia kwa miezi mingi. Wakati huohuo mke wangu akaugua kansa na kuhitaji uangalifu mwingi. Kwa sababu hiyo wakafutilia mbali kesi yangu. Maria alikufa mwaka wa 1972. Alikuwa mwandamani mwaminifu, aliyekuwa mwaminifu-mshikamanifu kwa Yehova hadi kifo chake.
Familia Yetu Yasambazwa Kotekote
Nilimwoa Nina mwaka wa 1973. Baba yake alikuwa amemfukuza nyumbani kwake mwaka wa 1960 kwa sababu Nina alikuwa Shahidi. Alikuwa mhudumu mwenye bidii ambaye alikuwa miongoni mwa wale dada waliojitahidi sana kunakili magazeti kwa ajili ya wale waliokuwa kambini. Watoto wangu walimpenda pia.
Wenye mamlaka walisumbuliwa na utendaji wetu huko Nevinnomyssk na kutuhimiza tuondoke. Kwa hiyo, mwaka wa 1975, nilihamia eneo la Caucasus huko Georgia, nikiwa na mke wangu na binti zangu. Wakati huohuo, wana wangu Ivan na Volodya walihamia Dzhambul kwenye mpaka wa kusini wa Kazakstan.
Huko Georgia utendaji wa Mashahidi wa Yehova ulikuwa ndio unaanza tu. Tulitoa ushahidi wa vivi hivi ndani na karibu na miji ya Gagra na Sukhumi, kwenye Pwani ya Bahari Nyeusi, na baada ya mwaka, Mashahidi wapya kumi wakabatizwa katika mto ulioko mlimani. Punde si punde, wenye mamlaka walisisitiza kwamba tuondoke eneo hilo, nasi tukahamia mashariki mwa Georgia. Huko tulizidisha jitihada zetu za kutafuta watu wenye mfano wa kondoo, naye Yehova akatubariki.
Tulikutana pamoja tukiwa vikundi vidogo-vidogo. Lugha ilikuwa tatizo, kwa kuwa hatukujua Kigeorgia na baadhi ya Wageorgia hawakuzungumza Kirusi vizuri. Mwanzoni, tulijifunza na Warusi pekee. Ingawa hivyo, kuhubiri na kufundisha katika Kigeorgia kulipiga hatua upesi, na sasa kuna maelfu ya wahubiri wa Ufalme huko Georgia.
Katika mwaka wa 1979, chini ya mkazo wa shirika la KGB mwajiri wangu alisema kwamba sikutakikana tena nchini mwake. Wakati huo ndio binti yangu Nadia alipohusika katika aksidenti ambamo yeye na binti yake mdogo walikufa. Mwaka uliotangulia mama yangu alifia huko Nevinnomyssk akiwa mwaminifu kwa Yehova na kumwacha baba na ndugu yangu. Kwa hiyo, tuliamua kurudi huko.
Kubarikiwa kwa Ajili ya Kuvumilia
Huko Nevinnomyssk tuliendelea kutoa fasihi ya Biblia kisiri. Wakati mmoja katika miaka ya katikati ya 1980 nilipoitwa na wenye mamlaka, niliwaambia kwamba nilikuwa nimeota kwamba ninaficha magazeti yetu. Walicheka. Nilipokuwa nikiondoka, mmoja wao alisema: “Na usiote tena kuhusu jinsi ya kuficha fasihi yako.” Alimalizia kwa kusema: “Karibuni hiyo fasihi itawekwa hadharani kwenye rafu zenu, nawe utakuwa ukienda mikutanoni umeshikana mikono na mke wako na ukiwa na Biblia yako mkononi.”
Katika mwaka wa 1989 tulihuzunika wakati binti yangu Anna alipokufa kwa uvimbe wa ubongo. Alikuwa na umri wa miaka 38 tu. Mwaka huohuo, mwezi wa Agosti, Mashahidi kutoka Nevinnomyssk walikodisha garimoshi na kusafiri hadi Warsaw, Poland, ili kuhudhuria mkusanyiko wa kimataifa. Kulikuwepo na wahudhuriaji 60,366, waliotia ndani maelfu kutoka Muungano wa Sovieti. Kwa kweli tulifikiri tulikuwa tukiota! Muda unaopungua miaka miwili baadaye, Machi 27, 1991, nilikuwa na pendeleo la kuwa mmoja kati ya wazee watano, wenye kutumikia kwa muda mrefu katika Muungano wa Sovieti, kutia sahihi hati ya kihistoria jijini Moscow ambayo ilitambulisha kisheria tengenezo la kidini la Mashahidi wa Yehova!
Ninafurahi kwamba watoto wangu waliosalia wanamtumikia Yehova kwa uaminifu. Nami natazamia kwa hamu ulimwengu mpya wa Mungu nitakapoweza kumwona tena Anna, Nadia, na binti yake, na vilevile Kolya. Kolya atakapofufuliwa, nitatimiza ahadi yangu ya kumpeleka kwenye kisiwa ambacho tulifurahia sana pamoja miaka mingi iliyopita.
Wakati huohuo, imekuwa shangwe iliyoje kuona ukuzi wa haraka wa kweli ya Biblia katika bara hili kubwa! Ninafurahia kwelikweli fungu langu katika maisha, na ninamshukuru Yehova kwa kuniruhusu kuwa mmoja wa Mashahidi wake. Mimi ninasadiki ukweli wa andiko la Zaburi 34:8: “Onjeni mwone ya kuwa BWANA yu mwema; heri mtu yule anayemtumaini.”
[Picha katika ukurasa wa 25]
Mwaka nilipojiunga na familia yangu huko Tulun
[Picha katika ukurasa wa 26]
Juu: Baba yangu na watoto wangu nje ya nyumba yetu huko Tulun, Siberia
Juu kulia: Binti yangu Nadia na binti yake, ambao walikufa katika aksidenti ya motokaa
Kulia: Picha ya familia ya mwaka wa 1968