Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g92 8/8 kur. 14-16
  • Naweza Kumsaidiaje Mzazi Wangu Aliye Peke Yake?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Naweza Kumsaidiaje Mzazi Wangu Aliye Peke Yake?
  • Amkeni!—1992
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • ‘Kuwalipa Yanayowapasa’
  • Utii Unaufanya Mzigo Wake Kuwa Mwepesi
  • Kusaidia Kazi ya Nyumba
  • Kuchukua Hatua ya Kwanza
  • ‘Endelea Kutembea Katika Kweli’
  • Faida Mbalimbali
  • Nishughulikeje na Mzazi Wangu Aliyeondoka Nyumbani?
    Amkeni!—1992
  • Je, Unawajali Wazazi Wasio na Wenzi wa Ndoa?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2010
  • Familia za Mzazi Mmoja Zaweza Kufanikiwa!
    Siri ya Furaha ya Familia
  • Nini Ikiwa Mzazi Wangu ni Mraibu wa Dawa za Kulevya au Pombe?
    Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 2
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—1992
g92 8/8 kur. 14-16

Vijana Wanauliza . . .

Naweza Kumsaidiaje Mzazi Wangu Aliye Peke Yake?

“Kuwa mzazi mmoja ni kama kuwa mfanya kiinimacho. Baada ya miezi sita ya mazoezi, hatimaye umeweza kucheza kiinimacho na mipira minne kwa wakati mmoja. Lakini baada tu ya wewe kufanya hivyo, mtu anakurushia mpira mwingine!”—Mzazi mmoja.

KAZI ya mzazi mmoja ni yenye kuchokesha na kwa kawaida ni ngumu sana. Na ikiwa mama yako ni mzazi mmoja, bila shaka unatambua kwamba anahitaji msaada.a Lakini ukiwa tineja, unakabili lile mwandikaji mmoja aliita “kipindi cha wakati chenye mikazo sana na kitisho cha maisha.” Huenda ikaonekana kwamba una mengi ya kufanya hasa ukishindana tu na ujana.

Ingawa hivyo, kama yule mzazi mmoja aliyenukuliwa mwanzoni, mama yako mara kwa mara anaweza kujisikia amelemewa, akijaribu kuwa mama na baba kwako. Kweli, Yehova hatazamii mambo yasiyowezekana kutoka kwa yeyote. Kama vile kanuni moja ya Biblia huonyesha: “Jambo la maana ni kuwa na nia ya kutoa kile tunachoweza—hicho ndicho Mungu hukubali.” (2 Wakorintho 8:12, Phillips) Lakini bado anaweza kujisikia mwenye mkazo mkubwa. Je! udharau hali yake, au kuna sababu nzuri ya kujaribu kusaidia?

‘Kuwalipa Yanayowapasa’

Kwenye 1 Petro 3:8, NW, Wakristo wanaambiwa: “Kwa kumalizia, ninyi nyote mwe na akili iyo hiyo, mkionyesha hisia-mwenzi.” Kwa hivyo je, hisia-mwenzi kwa mzazi wako haipasi kukusukuma umsaidie? Naam, ni lenye “kukubalika mbele za Mungu” kwa vijana Wakristo “kuendelea kuwalipa wazazi wao yanayowapasa.”—1 Timotheo 5:4, NW.

Ingawa andiko hilo bila shaka linarejezea kutolea mzazi mpweke msaada wa kifedha, linafundisha kanuni ya maana: Twadaiwa na wazazi wetu zaidi ya yale tungelipa. Na wakati wana uhitaji, ni wajibu na pendeleo letu kujaribu kuwalipa. Kwa mfano, vijana wengine watatumia sehemu au mshahara wao wote wa kazi isiyo ya wakati wote kusaidia kulipa vitu vya nyumbani. Hilo laonyesha shukrani kweli kweli na uthamini!

Msaada wa kifedha, hata hivyo, ni njia moja tu ya kulipa mzazi wako ‘malipo yanayowapasa.’ Si kwamba ujaribu kufanya mahali pa mzazi asiyekuwako—hilo halitawezekana—wala huhitaji kujichosha kihisia-moyo kuona kwamba wewe ndiwe mwenye daraka la mambo yote katika nyumba. Hiyo bado ni kazi ya mama yako akiwa mzazi. (Linganisha Mithali 31:27.) Lakini kuna njia nyingi zenye kutumika ambazo waweza kuthibitisha kuwa msaada wa kweli kwa mama yako ikiwa yeye ni mzazi mmoja.

Utii Unaufanya Mzigo Wake Kuwa Mwepesi

Njia moja ni kufuata amri kwenye Wakolosai 3:20: “Ninyi watoto, watiini wazazi wenu katika mambo yote; maana jambo hili lapendeza katika Bwana.” Unaweza kusema kimoyomoyo andiko hilo. Lakini je! wakati mwingine wewe hukosa kulitii?

Mzazi mmoja aliye peke yake na mvulana mmoja tineja hufanya kazi saa nyingi ili kuandalia familia yake. Lakini asema kwa kupiga kite: “Mvulana wangu hufanya maisha yawe magumu wakati anakosa kunitii.” Mvulana wake akinza: “Mimi ndiye mwanamume peke yake katika nyumba. Mimi ni mkubwa kuliko mama yangu, kwa hivyo wakati mwingine ni vigumu sana kwangu kumtii na kumheshimu kama kichwa cha familia.”

Wala kimo wala jinsia yako haikuwachilii kutoka kwenye amri ya Yehova: “Wala usiiache sheria ya mama yako.” (Mithali 6:20) Mama yako amepewa idhini na Mungu kufanyiza sheria, au kanuni za nyumbani. Anakudai heshima na utii. Ikiwa wewe ni wa kiume, Mama anaweza kukuita kwa shauku mwanamume wa nyumbani. Lakini yeye ni kichwa cha nyumba! Na kwa kumtii yeye—si kubishana naye wakati wote anapokuuliza ufanye jambo—unafanya mzigo wake uwe mwepesi na kufanyiza amani katika familia yenu.

Kusaidia Kazi ya Nyumba

Njia nyingine ya kuufanya mwepesi mzigo wa mzazi wako ni kusaidia katika kazi za nyumbani—si kungoja hadi unung’unikiwe kuzifanya. ‘Lakini mama haniulizi kufanya chochote,’ unateta. Kwa kushangaza, mara nyingi hilo hutendeka. Kama vile Carol V. Murdock aandika: “Mama aliye peke yake au baba aliye peke yake anajikokota kupitia sebule na mzigo mkubwa wa nguo za kufua kiasi cha kushinda yule aliye na nguvu zaidi—huku macho ya watoto watatu hayaachi kamwe kiwambo cha televisheni.”—Single Parents Are People, Too!

Kwa nini wazazi wengi walio peke yao huhitaji machache kutoka kwa uzao wao? Mama mmoja aliye peke yake alitoa sababu: “Sitaki msichana wangu akose kujifurahisha kwa sababu ni lazima nifanye kazi. Naogopa atanichukia kwa ajili ya hilo.” Mwingine alisema: “Unataka kufanya mahali pa mzazi yule asiyekuwapo kwa kufanya iwe rahisi kwa watoto.” Hata hivyo, katika kiini cha hisia hizo, mzazi aweza kujisikia mwenye hatia isivyostahiliwa. Anaweza kuhisi kuwa mwenye hatia kwa sababu ya kazi yake inayomfanya awe mbali na wewe. Au huenda akahisi kuwa mwenye hatia kwa sababu ya ndoa yake iliyokosa kufanikiwa, akitoa sababu kwamba yeye ndiye anayelaumiwa kwa kuwa wewe unaishi katika nyumba ya mzazi mmoja.

Kulingana na Dakt. Richard A. Gardner, mtungaji wa The Boys and Girls Book About Divorce, vijana wengine huona mafaa ya hali hiyo. Wanadai huruma na kukataa kushiriki kazi za nyumbani. Hilo latukumbusha, basi, mwelekeo wa kikatili ulioonyeshwa na viongozi wa kidini katika siku za Yesu. Yesu alisema juu yao: ‘Wanaweka mizigo mizito, walakini hawawezi hata kuinua kidole kusaidia kubeba hiyo mizigo.’—Mathayo 23:4, Todays English Version.

Onyesha mwelekeo tofauti. Kataa kuongezea mama yako mzigo; usijiepushe na kazi za nyumbani.

Kuchukua Hatua ya Kwanza

Hili lamaanisha kufanya linalohitajiwa bila kuulizwa. Fikiria jinsi kijana Tony anavyorahisisha mzigo wa mama yake. Anasema: “Mama yangu anafanya kazi katika hospitali, na nguo zake za kazini lazima zinyooshwe. Kwa hivyo mimi humpigia pasi.” Lakini Je! hiyo si kazi ya wanawake? “Wengine hufikiri hivyo,” ajibu Tony. “Lakini inasaidia mama yangu, kwa hiyo naifanya.”

Mbali na msaada wa kutumika, unaweza kuchangamsha mama yako kwa kutoa maneno ya kuthamini. Mzazi mmoja aliye peke yake aliandika: “Mara nyingi ninapata kwamba wakati mimi ni mnyonge na mwepesi wa kuudhika kwa ajili ya siku yenye kutahini kazini na ninakuja nyumbani—hiyo ndiyo siku binti yangu amechagua kutayarisha meza na chakula cha jioni.” Anaongeza: “Mvulana wangu huweka mikono kunizunguka na kunikumbatia na kusema, ‘wewe ni mama mzuri zaidi katika ulimwengu.’” Je! anaathiriwaje na tendo hilo lenye maana? Yeye anaendelea: “Hali yangu yote inabadilika kuwa nzuri tena.”

‘Endelea Kutembea Katika Kweli’

“Sina furaha iliyokuu kuliko hii, kusikia ya kwamba watoto wangu wanakwenda [wanatembea, NW] katika kweli.” (3 Yohana 4) Mtume Yohana hapo aliongea kuhusu watoto wake wa kiroho. Ikiwa mama yako ni Mkristo, bila shaka anahisi vivyo hivyo kukuelekea; anataka wewe utembee katika kweli. Kwa sababu hiyo anaweza kupanga funzo la Biblia la familia la kawaida pamoja na wewe.

Kuongoza funzo hilo huenda kusiwe rahisi baada ya siku ya kazi yenye kuchosha. Na ikiwa wewe si mwenye kushirikiana na ni mwenye kunung’unika, funzo la familia laweza kuwa jaribu kwa kila mtu mwenye kuhusika. Kwa hiyo shirikiana! Uwe tayari kujifunza wakati uliopangwa unapofika. Tayarisha mapema. Ushirikiano wako huenda ukawa kichochezi anachohitaji mzazi wako ili kuendeleza funzo hilo kwa kawaida. Wakati unapohudhuria mikutano ya Kikristo na kushiriki katika kazi ya kuhubiri nyumba kwa nyumba bila kusukumwa, unaonyesha pia kwamba unatembea katika kweli. (Mathayo 24:14; Waebrania 10:24, 25) Kwa kufanya hivyo wamhakikishia mama yako kwamba jitihada yake si ya bure!

Faida Mbalimbali

Mithali 3:27 husema: “Usiwanyime watu mema yaliyo haki yao, ikiwa katika uwezo wa mkono wako kuyatenda.” Kwa wazi, unadaiwa na mzazi wako ufikirio huo. Na ukiutoa, unampendeza si yeye tu bali Yehova Mungu mwenyewe. Faida nyingine: Mzazi wako atakuwa katika hali nzuri na kukutolea msaada unapouhitaji.

Mwishowe, kusaidia wengine kunafanyiza sifa nzuri. Kama vile mwandikaji mmoja alivyoandika: “Vijana wanahitaji kupewa nafasi ili wahisi ni wenye msaada na kujitolea kwa wengine. Wakati wanakosa mambo hayo, hawawezi kutambua nguvu zao na udumifu ambao huja kwa kujua wewe ni mtu mzuri kwa kusaidia wengine.” Kama vile Yesu mwenyewe alisema: “Ni heri kutoa kuliko kupokea.” (Matendo 20:35) Na furaha kubwa yaweza kuwa yako ikiwa utajali sana kusaidia mzazi wako aliye peke yake.

[Maelezo ya Chini]

a Kwa vile wazazi wengi walio peke yao ni wanawake, tutatumia jinsia ya kike. Hata hivyo, kanuni zinazozungumzwa hapa zatumika kwa jinsia zote za mzazi mmoja.

[Picha katika ukurasa wa 15]

Kijana mvivu au asiyejali huongezea mkazo maisha ya mzazi wake . . . Yule anayesaidia kazi ya nyumbani huufanya mzigo wake uwe mwepesi

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki