Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • fy sura 9 kur. 103-115
  • Familia za Mzazi Mmoja Zaweza Kufanikiwa!

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Familia za Mzazi Mmoja Zaweza Kufanikiwa!
  • Siri ya Furaha ya Familia
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • KUPATA USTADI WA UTARATIBU WA NYUMBA
  • UGUMU WA KUPATA RIZIKI
  • NI NANI ANAYEMTUNZA MWINGINE?
  • KUDUMISHA NIDHAMU
  • KUSHINDA VITA DHIDI YA UPWEKE
  • JINSI WENGINE WAWEZAVYO KUSAIDIA
  • Wazazi Wasio na Wenzi Wanashinda na Matatizo ya Ulimwengu wa Leo
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1981
  • Je, Unawajali Wazazi Wasio na Wenzi wa Ndoa?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2010
  • Je! Wewe Waweza Kusaidia Wajane na Yatima “Katika Shida Zao”?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1981
  • Mzazi Mmoja, Matatizo Mengi
    Amkeni!—2002
Pata Habari Zaidi
Siri ya Furaha ya Familia
fy sura 9 kur. 103-115

SURA YA TISA

Familia za Mzazi Mmoja Zaweza Kufanikiwa!

1-3. Ni nini limechangia ukuzi katika idadi ya familia za mzazi mmoja, na wale wanaohusika huathiriwaje?

FAMILIA za mzazi mmoja zimeitwa “mtindo wa familia wenye kukua upesi zaidi” Marekani. Hali iko hivyohivyo katika nchi nyinginezo nyingi. Idadi kubwa zaidi iliyopata kurekodiwa ya talaka, kuacha familia, kutengana, na watoto haramu imekuwa na matokeo yenye kuathiri sana mamilioni ya wazazi na watoto.

2 “Mimi ni mjane mwenye umri wa miaka 28 aliye na watoto wawili,” akaandika mama mmoja aliye mzazi pekee. “Nimeshuka moyo sana kwa kuwa sitaki kuwalea watoto wangu bila baba. Yaonekana kama hakuna hata mtu mmoja anayenijali. Watoto wangu huniona nikilia machozi na hilo huwaathiri.” Zaidi ya kushindana na hisia kama vile hasira, hatia, na upweke, wazazi pekee walio wengi hukabili ugumu wa kuwa na kazi nje ya nyumbani na kufanya wajibu mbalimbali wa nyumbani. Mmoja alisema hivi: “Kuwa mzazi aliye pekee ni kama kuwa mwenye ustadi wa kurusha vitu hewani na kuvishika kimoja-kimoja. Baada ya miezi sita ya mazoezi, hatimaye umeweza kurusha na kushika mipira minne mara moja. Lakini mara tu uwezapo kufanya hivyo, mtu fulani akutupia mpira mpya!”

3 Mara nyingi vijana katika familia za mzazi mmoja huwa na ming’ang’ano yao wenyewe. Huenda wakalazimika kushindana na hisiamoyo zenye nguvu baada ya kuondoka kwa ghafula kwa mzazi au kifo chake. Kwa vijana wengi kutokuwako kwa mzazi mmoja kwaonekana kuwa na tokeo hasi sana.

4. Twajuaje kwamba Yehova ni mwenye ufikirio kuhusu familia za mzazi mmoja?

4 Familia za mzazi mmoja zilikuwako katika nyakati za Biblia. Maandiko hurudia-rudia kutaja “yatima [“mvulana asiye na baba,” NW]” na “mjane.” (Kutoka 22:22; Kumbukumbu la Torati 24:19-21; Ayubu 31:16-22) Yehova Mungu hakuwa mwenye kutojali hali yao. Mtunga-zaburi alimwita Mungu “baba wa yatima na mwamuzi wa wajane.” (Zaburi 68:5) Kwa hakika, Yehova ana ufikirio uo huo kwa familia za mzazi mmoja leo! Kwa kweli, Neno lake hutoa kanuni ziwezazo kuzisaidia zifanikiwe.

KUPATA USTADI WA UTARATIBU WA NYUMBA

5. Walio wazazi pekee wanalazimika kukabili tatizo jipi mwanzoni?

5 Fikiria kazi ya kusimamia nyumba. “Kuna pindi nyingi unapotamani ungekuwa na mwanamume nyumbani,” akiri mwanamke mmoja aliyetalikiwa, “kama wakati gari lako linapoanza kufanya makelele nawe hujui yanakotoka.” Wanaume ambao wametalikiwa au kufiwa na mke juzijuzi huenda vilevile wakafadhaishwa na wingi wa kazi za nyumbani ambazo ni lazima wafanye sasa. Kwa watoto, mchafuko nyumbani huongezea hisi za kukosa uthabiti na usalama.

Picha katika ukurasa wa 109

Watoto, shirikianeni na mzazi wenu aliye pekee

6, 7. (a) Ni kielelezo gani chema kilichowekwa na “mke mwema” wa Mithali? (b) Kuwa mwenye bidii ya kuendelea kuhusu madaraka ya nyumbani husaidiaje katika nyumba za mzazi mmoja?

6 Ni nini kiwezacho kusaidia? Ona kielelezo kilichowekwa na yule “mke mwema” afafanuliwaye kwenye Mithali 31:10-31. Upana wa matimizo yake ni wenye kutokeza—kununua, kuuza, kushona, kupika, kununua nyumba na shamba, kufanya ukulima, na kusimamia biashara. Siri yake ilikuwa nini? Alikuwa mwenye bidii ya kuendelea, akifanya kazi hadi usiku sana na kuamka mapema ili kuanza utendaji wake mbalimbali. Alikuwa mwenye utaratibu, akikabidhi wengine kazi fulani na kutumia mikono yake mwenyewe kushughulikia nyinginezo. Haishangazi kwamba alipokea pongezi!

7 Ikiwa wewe ni mzazi aliye pekee, uwe mwenye kudhamiria kuhusu madaraka yako ya nyumbani. Pata uradhi katika kazi hizo, kwa kuwa hizo huongezea sana furaha ya watoto wako. Hata hivyo, kupanga mambo ifaavyo na utaratibu ni muhimu. Biblia husema: “Mawazo [“mipango,” NW] ya wenye bidii huuelekea utajiri tu.” (Mithali 21:5) Baba mmoja aliye mzazi pekee alikiri hivi: “Naelekea kutofikiria milo hadi ninaposikia njaa.” Lakini milo iliyopangwa huelekea kuwa yenye lishe na yenye kuvutia zaidi kuliko ile iliyofanyizwa haraka-haraka. Huenda pia ukalazimika kujifunza jinsi ya kutumia mikono yako katika njia mpya. Kwa kuwaendea marafiki wenye ujuzi, kutumia vitabu vinavyofundisha jinsi ya kufanya mambo, na kuwaendea wataalamu wenye kusaidia, mama fulani walio wazazi pekee wamewezeshwa kupiga rangi, kufanya ufundi wa mabomba, na kufanya marekebisho sahili ya magari.

8. Watoto wa walio wazazi pekee wanaweza kusaidiaje nyumbani?

8 Je, yafaa kuwaomba watoto wasaidie? Mama mmoja aliye mzazi pekee alisababu hivi: “Wataka kulipia kutokuwako kwa yule mzazi mwingine kwa kufanya mambo yawe rahisi kwa watoto.” Hilo huenda likaeleweka lakini labda si kwa masilahi bora zaidi ya mtoto sikuzote. Vijana wenye kumhofu Mungu katika nyakati za Biblia waligawiwa kazi za nyumbani zilizofaa. (Mwanzo 37:2; Wimbo Ulio Bora 1:6) Kwa hiyo, ingawa yafaa kuwa mwangalifu kutowapa watoto wako mzigo mkubwa mno, utakuwa mwenye hekima kuwagawia kazi kama vile kushughulikia vyombo na kuweka vyumba vyao vikiwa safi. Kwa nini msifanye kazi fulani pamoja? Hilo laweza kuwa lenye kufurahisha sana.

UGUMU WA KUPATA RIZIKI

Picha katika ukurasa wa 107

Tumia wakati mwingi iwezekanavyo pamoja na watoto wako

9. Kwa nini mara nyingi akina mama walio wazazi pekee hukabili magumu ya kifedha?

9 Wazazi pekee walio wengi huliona kuwa jambo gumu kutimiza mahitaji yao ya kifedha, na kwa kawaida akina mama wasioolewa huwa na hali ngumu hasa.a Katika nchi ambako msaada wa umma unapatikana, huenda wakawa na hekima kuutumia kwa manufaa yao, angalau mpaka wapate kazi ya kuajiriwa. Biblia huwaruhusu Wakristo watumie maandalizi hayo inapokuwa lazima. (Waroma 13:1, 6) Wajane na wanawake waliotalikiwa hukabili magumu ayo hayo. Wengi, wakiwa wamelazimika kufanya kazi ya kuajiriwa tena baada ya miaka kadhaa ya kufanya kazi za nyumbani, mara nyingi huweza kupata tu kazi zenye malipo ya chini. Watu fulani huweza kuboresha maisha yao kwa kujiandikisha katika programu za mazoezi ya kazi au mitaala mifupi ya shule.

10. Mama aliye mzazi pekee aweza kuwaelezaje watoto wake ni kwa nini ni lazima atafute kazi ya kuajiriwa ya kimwili?

10 Usishangae ikiwa watoto wako wanakosa furaha unapotafuta kazi ya kuajiriwa, na usihisi kuwa na hatia. Bali, waeleze ni kwa nini ni lazima ufanye kazi, na uwasaidie waelewe kwamba Yehova akutaka uwaandalie. (1 Timotheo 5:8) Muda si muda, watoto walio wengi hubadilikana na hali. Hata hivyo, jaribu kutumia wakati mwingi iwezekanavyo pamoja nao kadiri ratiba yako yenye shughuli iruhusuvyo. Uangalifu huo wenye upendo waweza pia kusaidia kupunguza pigo la vizuizi vyovyote vya kifedha ambavyo huenda familia ikapata.—Mithali 15:16, 17.

NI NANI ANAYEMTUNZA MWINGINE?

Picha katika ukurasa wa 110

Kutaniko halipuuzi “wajane” na “wavulana wasio na baba”

11, 12. Ni lazima walio wazazi pekee wahifadhi mipaka gani, nao waweza kufanyaje hivyo?

11 Ni jambo la asili kwa walio wazazi pekee kuwa karibu hasa na watoto wao, hata hivyo lazima kuwe na uangalifu kwamba mipaka iliyowekwa na Mungu kati ya wazazi na watoto hairukwi. Kwa kielelezo, magumu mazito yaweza kutokea ikiwa mama aliye mzazi pekee amtazamia mwana wake kuchukua madaraka ya kichwa cha nyumba au amtendea binti yake kama msiri wake, akimlemeza huyo msichana na matatizo ya kindani. Kufanya hivyo hakufai, kunaleta mkazo, na labda kumtatanisha mtoto.

12 Hakikishia watoto wako kwamba wewe, ukiwa mzazi, utawatunza—si wao wakutunze. (Linganisha 2 Wakorintho 12:14.) Nyakati nyingine, huenda ukahitaji shauri au utegemezo fulani. Utafute kutoka kwa wazee Wakristo au labda kutoka kwa wanawake Wakristo walio wakomavu, si kutoka kwa watoto wako wadogo.—Tito 2:3.

KUDUMISHA NIDHAMU

13. Huenda mama aliye mzazi pekee akakabili tatizo gani kuhusiana na nidhamu?

13 Huenda mwanamume asiwe na tatizo sana kuonwa kwa uzito kuwa mwenye kutia nidhamu, lakini huenda mwanamke akawa na matatizo kwa habari hii. Asema mama aliye mzazi pekee: “Wana wangu wana miili ya wanaume na sauti za wanaume. Nyakati nyingine ni vigumu kutosikika kuwa mwenye kusitasita kuamua au dhaifu kwa kulinganishwa.” Zaidi ya hayo, huenda bado ukawa waombolezea kifo cha mwenzi mpendwa, au labda huenda ukawa unahisi kuwa na hatia au hasira juu ya kuvunjika kwa ndoa. Ikiwa nyote wawili mna haki ya kisheria ya kulea watoto, huenda ukahofu kwamba mtoto wako hupendelea kuwa na yule aliyekuwa mwenzi wako awali. Hali hizo zaweza kufanya iwe vigumu kutia nidhamu yenye usawaziko.

14. Walio wazazi pekee waweza kudumishaje maoni yenye usawaziko juu ya nidhamu?

14 Biblia husema kwamba “mwana aliyeachiliwa humwaibisha mamaye.” (Mithali 29:15) Una utegemezo wa Yehova Mungu katika kufanya na kutekeleza sheria za familia, kwa hiyo usiruhusu hisia ya hatia, majuto, au hofu ikushinde. (Mithali 1:8) Usiache kamwe kanuni za Biblia. (Mithali 13:24) Jaribu kuwa mwenye kiasi, bila ugeugeu, na imara. Muda si muda, watoto walio wengi wataitikia. Hata hivyo, utataka kufikiria hisia za watoto wako. Asema baba aliye mzazi pekee: “Nidhamu yangu ilihitaji kusawazishwa na uelewevu kwa sababu ya mshtuo wa kupoteza mama yao. Mimi huongea nao kwa kila fursa. Tunakuwa na wakati wa maongezi machangamfu tunapotayarisha mlo wa jioni. Ndipo wanaponiambia yote kikweli.”

15. Mzazi aliyetalikiwa aepuke nini anaposema juu ya yule aliyekuwa mwenzi wake awali?

15 Ikiwa umetalikiwa, hakuna mema yoyote yanayotimizwa kwa kumshushia staha mwenzi wako wa awali. Kupigana kwa wazazi ni jambo lenye kuumiza kwa watoto na hatimaye kutadhoofisha staha yao kwenu wawili. Kwa sababu hiyo, epuka kusema maneno yenye kudhuru kama vile: “Uko sawa na babako tu!” Hata iwe mwenzi wako wa awali alikusababishia umivu jinsi gani, yeye angali mzazi wa mtoto wako, anayehitaji upendo, uangalifu, na nidhamu ya wazazi wote wawili.b

16. Ni mipango gani ya kiroho ipaswayo kuwa sehemu ya kawaida katika nyumba ya mzazi mmoja?

16 Kama ilivyozungumziwa katika sura zilizotangulia, nidhamu hutia ndani mazoezi na mafunzo, si adhabu tu. Matatizo mengi yaweza kuepukwa kwa programu nzuri ya mazoezi ya kiroho. (Wafilipi 3:16) Kuhudhuria mikutano ya Kikristo kwa ukawaida ni muhimu. (Waebrania 10:24, 25) Ndivyo lilivyo funzo la Biblia la familia kila juma. Ni kweli, si rahisi kufanya funzo hilo kwa ukawaida. “Baada ya siku ya kazi, kwa kweli unataka kupumzika,” asema mama mmoja mwenye kudhamiria. “Lakini mimi hujitayarisha kiakili ili kujifunza na binti yangu, nikijua ni jambo linalohitaji kufanywa. Yeye kwa kweli hufurahia funzo letu la familia!”

17. Twaweza kujifunza nini kutokana na malezi mema ya Timotheo mwandamani wa Paulo?

17 Ni wazi kwamba Timotheo mwandamani wa mtume Paulo alipewa mazoezi katika kanuni za Biblia na mama yake na nyanya yake—lakini yaonekana hakupewa na baba yake. Hata hivyo, Timotheo alikuwa Mkristo mwenye kutokeza kama nini! (Matendo 16:1, 2; 2 Timotheo 1:5; 3:14, 15) Waweza vilevile kutumaini matokeo yafaayo unapojitahidi kuwalea watoto wako “katika nidhamu na rekebisho la akilini la Yehova.”—Waefeso 6:4.

KUSHINDA VITA DHIDI YA UPWEKE

18, 19. (a) Upweke waweza kujidhihirishaje kwa mzazi aliye pekee? (b) Ni shauri gani linalotolewa ili kusaidia kudhibiti tamaa za kimwili?

18 Mzazi mmoja aliye pekee alipiga kite hivi: “Nirudipo nyumbani na kuona zile kuta nne, na hasa baada ya watoto kwenda kitandani, upweke hunikumba kwelikweli.” Ndiyo, mara nyingi upweke ndilo tatizo kubwa zaidi ambalo mzazi aliye pekee hukabili. Ni jambo la asili kutamani ushirika mchangamfu na mahusiano ya karibu-karibu ya ndoa. Lakini je, mtu ajaribu kutatua tatizo hilo bila kujali nini? Katika siku ya mtume Paulo, wajane fulani wachanga zaidi waliruhusu “misukumo yao ya kingono [ije] kati yao na Kristo.” (1 Timotheo 5:11, 12) Kuruhusu tamaa za kimwili zichukue mahali pa masilahi ya kiroho lingekuwa jambo liletalo madhara.—1 Timotheo 5:6.

19 Mwanamume mmoja Mkristo alisema: “Misukumo ya kingono ni yenye nguvu sana, lakini waweza kuidhibiti. Wazo linapoingia akilini mwako, ni lazima usilikazie fikira. Ni lazima uliondolee mbali. Yasaidia pia kumfikiria mtoto wako.” Neno la Mungu hushauri hivi: ‘Fisheni viungo vya mwili wenu kwa habari ya hamu ya ngono.’ (Wakolosai 3:5) Ikiwa ulikuwa ukijaribu kufisha hamu yako ya chakula, je, ungesoma magazeti yanayoonyesha picha za chakula kitamu, au je, ungeshiriki na watu ambao wangeongea daima kuhusu chakula? Hasha! Ndivyo ilivyo kuhusiana na tamaa za kimwili.

20. (a) Ni hatari gani inayootea wale wanaotafuta uchumba na wasioamini? (b) Watu waseja katika karne ya kwanza na leo pia wamepigaje vita dhidi ya upweke?

20 Wakristo fulani wametafuta uchumba na watu wasioamini. (1 Wakorintho 7:39) Je, hilo lilitatua tatizo lao? La. Mwanamke Mkristo aliyetalikiwa alionya hivi: “Kuna jambo moja lililo baya zaidi sana kuliko kuwa mseja. Ni kufunga ndoa na mtu asiyefaa!” Bila shaka wajane Wakristo wa karne ya kwanza walikuwa na hali za upweke, lakini wale wenye hekima waliendelea kuwa na shughuli ‘wakipokea wageni, wakiosha miguu ya watakatifu, na kutuliza wale wenye kuwa katika dhiki.’ (1 Timotheo 5:10) Wakristo waaminifu leo ambao wamengoja miaka mingi ili kupata mwenzi anayemhofu Mungu wameendelea vivyo hivyo kuwa na shughuli. Mjane Mkristo mwenye umri wa miaka 68 alianza kuzuru wajane wengine wakati wowote alipokuwa mpweke. Alisema hivi: “Naona kwamba kwa kufanya ziara hizi, kuendelea na kazi zangu za nyumbani na kutunza hali yangu ya kiroho sina wakati wa kuwa mpweke.” Kufundisha wengine kuhusu Ufalme wa Mungu ni kazi njema yenye mafaa hasa.—Mathayo 28:19, 20.

21. Sala na mashirika mema yaweza kusaidia kwa njia gani kushinda upweke?

21 Ni kweli, hakuna ponyo la kimuujiza kwa upweke. Lakini huo waweza kuvumiliwa kwa nguvu kutoka kwa Yehova. Nguvu hizo hutokea wakati ambapo Mkristo “hudumu katika dua na sala usiku na mchana.” (1 Timotheo 5:5) Dua ni sihi zenye bidii, ndiyo, kule kuomba msaada, labda kwa vilio vyenye kupaaza kwa nguvu na machozi. (Linganisha Waebrania 5:7.) Kummwagia Yehova yote yaliyo moyoni “usiku na mchana” kwaweza kusaidia kikweli. Zaidi, mashirika yanayofaa yaweza kuchangia sana kujazia utupu wa upweke. Kupitia mashirika mema, mtu aweza kupata “neno jema” la kitia-moyo linalofafanuliwa kwenye Mithali 12:25.

22. Ni mambo gani ya kufikiriwa yatakayosaidia wakati hisia za upweke zinapotokea mara kwa mara?

22 Hisia za upweke zikitokea mara kwa mara—kama vile yaelekea kuwa zitatokea—kumbuka kwamba hakuna yeyote asiye na matatizo maishani. Kwa kweli, “ushirika mzima wa ndugu [zako]” unateseka kwa njia moja au nyingine. (1 Petro 5:9) Epuka kukaza fikira juu ya wakati uliopita. (Mhubiri 7:10) Fikiria manufaa unazofurahia. Zaidi ya yote, azimia kushika uaminifu-maadili wako na kuufanya moyo wa Yehova utereme.—Mithali 27:11.

JINSI WENGINE WAWEZAVYO KUSAIDIA

23. Wakristo wenzetu wana daraka gani kuelekea walio wazazi pekee kutanikoni?

23 Utegemezo na msaada wa Wakristo wenzetu ni wenye thamani sana. Yakobo 1:27 husema: “Namna ya ibada iliyo safi na isiyo na unajisi kwa maoni ya Mungu wetu na Baba ni hii: kutazama mayatima na wajane katika dhiki yao.” Ndiyo, Wakristo hawana budi kusaidia familia za mzazi mmoja. Ni nini baadhi ya njia zenye kutumika ambazo hili huenda likafanywa?

24. Familia za mzazi mmoja zilizo na uhitaji zaweza kusaidiwa kwa njia zipi?

24 Msaada wa kimwili waweza kutolewa. Biblia husema hivi: “Yeyote yule aliye na njia ya ulimwengu huu ya kutegemeza maisha na amwona ndugu yake akiwa na uhitaji na bado amfungia mlango wa huruma zake nyororo, ni katika njia gani kumpenda Mungu hukaa katika yeye?” (1 Yohana 3:17) Neno la asili la Kigiriki kwa “ona” humaanisha, si kutupa macho kivivi hivi tu, bali kukodolea macho kimakusudi. Hilo laonyesha kwamba huenda Mkristo mwenye fadhili akapata kwanza kuzoelea hali na mahitaji ya familia fulani. Labda wanahitaji fedha. Huenda watu fulani wakahitaji msaada na urekebishaji wa vitu nyumbani. Au huenda wakathamini tu kualikwa kula mlo au kwenye kikusanyiko cha kirafiki.

25. Wakristo wenzetu waweza kuonyeshaje huruma kuelekea walio wazazi pekee?

25 Kwa kuongezea, 1 Petro 3:8 husema: “Nyinyi nyote mwe wenye akili zenye kufanana, mkionyesha hisia-mwenzi, mkiwa na shauku ya kidugu, wenye huruma kwa njia ya wororo.” Mzazi mmoja aliye pekee mwenye watoto sita alisema hivi: “Hali imekuwa ngumu na nyakati nyingine mimi hulemewa. Hata hivyo, mara kwa mara akina ndugu au dada huniambia: ‘Joan, unafanya kazi njema. Hatimaye yote yatastahili jitihada.’ Kujua tu kwamba wengine wanakufikiria na kwamba wanajali kwasaidia sana.” Wanawake Wakristo wenye umri mkubwa zaidi huenda wakawa na matokeo hasa katika kusaidia wanawake vijana walio wazazi pekee, wakiwasikiliza wanapokuwa na matatizo ambayo huenda yasiwe rahisi kwao kuzungumza na mwanamume.

26. Wanaume Wakristo walio wakomavu waweza kusaidiaje watoto wasio na baba?

26 Wanaume Wakristo waweza kusaidia katika njia nyinginezo. Yule mwanamume mwadilifu Ayubu alisema hivi: “Nalimwokoa . . . yatima [“mvulana asiye na baba,” NW] naye, na yule asiyekuwa na mtu wa kumsaidia.” (Ayubu 29:12) Wanaume fulani Wakristo leo vilevile hupendezwa ifaavyo na watoto wasio na baba na huonyesha “upendo [wa kweli] kutokana na moyo safi,” wakiwa bila makusudio mabaya. (1 Timotheo 1:5) Bila kupuuza familia zao wenyewe, huenda mara kwa mara wakapanga kushiriki pamoja na vijana hao katika huduma ya Kikristo na huenda pia wakawaalika kushiriki katika funzo la familia au katika tafrija. Fadhili hiyo ingeweza sana kumwokoa mtoto asiye na baba na mwendo wa ukaidi.

27. Walio wazazi pekee waweza kuhakikishiwa juu ya utegemezo upi?

27 Hatimaye, bila shaka, walio wazazi pekee hawana budi ‘kuuchukua mzigo wao wenyewe’ wa daraka. (Wagalatia 6:5) Hata hivyo, wao waweza kuwa na upendo wa ndugu na dada Wakristo na wa Yehova Mungu mwenyewe. Biblia husema hivi juu yake: “Huwategemeza yatima na mjane.” (Zaburi 146:9) Kwa utegemezo Wake wenye upendo, familia za mzazi mmoja zaweza kufanikiwa!

a Mkristo mchanga akipata mimba kwa sababu ya mwenendo usio wa adili, kutaniko la Kikristo haliachilii kwa vyovyote jambo ambalo amefanya. Lakini akiwa mwenye toba, huenda wazee wa kutaniko na wengine kutanikoni wakataka kumtolea msaada.

b Haturejezei hali ambamo huenda mtoto akahitaji kulindwa dhidi ya mzazi mwenye kutenda watoto vibaya. Pia, ikiwa yule mzazi mwingine ajaribu kudhoofisha mamlaka yako, labda akiwa na kusudi la kuwashawishi watoto wakuache, huenda ikafaa kusema na marafiki wenye uzoefu, kama vile wazee katika kutaniko la Kikristo, wakupe shauri kuhusu jinsi ya kushughulikia hiyo hali.

KANUNI HIZI ZA BIBLIA ZAWEZA KUSAIDIAJE . . . WAZAZI NA WATOTO KUSHUGHULIKIA MATATIZO YA FAMILIA ZA MZAZI MMOJA?

Yehova Mungu ndiye “baba wa yatima na mwamuzi wa wajane.” —Zaburi 68:5.

Kupanga ifaavyo ni muhimu kwa mafanikio.—Mithali 21:5.

Yehova hutegemeza haki ya mzazi ya kutoa nidhamu ifaayo.—Mithali 1:8.

Wajane Wakristo wenye hekima huendelea kuwa wenye shughuli katika kazi njema nao hudumu katika sala.—1 Timotheo 5:5, 10.

Kupendezwa ifaavyo na “mayatima na wajane” ni sehemu ya ibada ya kweli.—Yakobo 1:27.

WANALOWEZA KUFANYA VIJANA

Je, mama au baba yako ndiye mzazi pekee? Ikiwa ndivyo, wewe waweza kufanya nini ili usaidie? Kwanza, uwe mtiifu. Wala ukubwa wala jinsia haimpi mtoto ruhusa ‘aiache sheria ya mama yake.’ (Mithali 1:8) Yehova akuamuru uwe mtiifu, na hatimaye, kufanya hivyo kutakuletea furaha.—Mithali 23:22; Waefeso 6:1-3.

Chukua hatua ya kwanza kusaidia, na uwe mwenye kuthamini. “Mama yangu hufanya kazi katika hospitali, na vazi lake la kazi lazima lipigwe pasi. Kwa hiyo mimi humpigia pasi,” asema Tony. “Hilo humsaidia mamangu, kwa hiyo hulifanya.” Mama mmoja aliye mzazi pekee asema hivi: “Mara nyingi mimi huona kwamba ninaposhuka moyo sana au kuwa mwenye kuudhika kwa sababu ya kuwa na siku ngumu hasa kazini na ninarudi nyumbani—hiyo ndiyo siku binti yangu amechagua kuandaa meza na kutayarisha mlo wa jioni.”

Kumbuka kwamba kushirikiana kwako ni jambo la maana. Baada ya siku ngumu kazini, huenda ikawa vigumu kwa mzazi wako kuongoza funzo la Biblia la familia. Usipokuwa mwenye kushirikiana, unafanya mambo yawe mabaya zaidi. Jaribu kuwa tayari wakati ulioratibiwa ufikapo. Tayarisha masomo yako kimbele. Kwa kuwa mtiifu, mwenye kuthamini, na mwenye kushirikiana, utampendeza mzazi wako, na la maana zaidi, utampendeza Mungu.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki