Je! Wewe Waweza Kusaidia Wajane na Yatima “Katika Shida Zao”?
1, 2. (a) Kuna tofauti gani kati ya ‘kumtazama’ mtu aliye na taabu na ‘kumwangalia’? (b) Kulingana na Yakobo 1:27, ibada ya kweli inaleta daraka gani?
KUNA tofauti kubwa sana kati ya kumtazama mtu aliye na taabu na kumwangalia. Ibada ya kweli yapaswa kuwageuza watu waache kuwa watazamaji wasiopendezwa na kuwa wasaidiaji wenye kujali wa waamini wenzao, kwa sababu “dini iliyo safi na isiyo na hitilafu mbele ya Mungu Baba ni hii: Kuwasaidia [“kuwaangalia”, NW] yatima na wajane katika shida zao, na kujilinda mwenyewe usichafuliwe na ulimwengu.”—Yak. 1:27, HNWW.
2 Katika Yakobo 1:27 neno la asili la Kigiriki linalotafsiriwa “kuwaangalia” lafafanuliwa kuwa ‘kumjali (mtu), kumpa (mtu).’ Linatoa wazo la kutembelea mtu kumpelekea msaada unaohitajiwa. Msaada huo unathaminiwa sana.
WATOTO WANAWEZA KUTOA MSAADA WENYE THAMANI
3, 4. (a) Kulingana na 1 Timotheo 5:4, ni nani wanaopaswa kuhangaikia kusaidia wajane? (b) Watoto wa wazazi wasio na wenzi waweza kusaidia katika njia zipi, nao watoto hao waweza kutoa msaada gani ulio bora zaidi?
3 Mtume Paulo anaonyesha ni nani wanaopaswa kuhangaikia kuwasaidia wajane akisema hivi: “Lakini mjane aliye na watoto au wajukuu, hao wanapaswa kujifunza kutimiza wajibu wao wa kidini [“utawa,” NW] kwa jamaa zao wenyewe na hivyo kuwalipa wazazi wao na wazee wao, kwani hilo ni jambo la kupendeza mbele ya Mungu.” (1 Tim. 5:4, HNWW) Ijapokuwa usemi huo unahusu watoto ambao wamekuwa watu wazima, hata vijana wanaweza kujifunza kuonyesha kujitoa kwao kwa Mungu kwa “kuwalipa” wazazi wao, ambao wamewafanyia mengi. Lakini namna gani? Vijana wengine wanasaidia kwa njia ya fedha, kama vile alivyofanya kijana mmoja kwa kutoa fedha zote alizokuwa amepata kwa kufanya kazi ya muda zilipie gharama isiyotazamiwa. “Ukarimu wa namna hii kutoka kwa mwana wa miaka 14,” akasema mama yake kwa uchangamfu, “unanitia moyo kuliko vile ninavyoweza kueleza kwa maneno.”
4 Hata kama watoto hawawezi kusaidia kwa njia ya fedha, wanaweza kutoa mambo mengine ya maana hata zaidi—kuthamini na utii. (Mit.23: 22; Efe. 6:1-3) Wazazi wengi wasio na wenzi wanajiuliza hivi, “Je! mimi ninaifanya vizuri kazi yangu ya kulea mtoto wangu?” Ebu wazia furaha ya mzazi mmoja asiye na mwenzi wakati mtoto wake mchanga alipotengeneza kipande cha karatasi, akaandika: “Nakupenda sana nami najua unajaribu sana.” Basi, ikiwa wewe ni mtoto wa mzazi asiye na mwenzi, je! hivi karibuni umepata kumwambia huyo namna unavyothamini kujinyima kwake kwa ajili yako? Unakuwa mwepesi katika kutii? Unajua maana ya kusafisha vyombo vya kulia kwa utii, kutoa takataka nje, kujifunza masomo ya shule ambayo umepewa kufanyia nyumbani, kufika nyumbani bila kuchelewa, kusafisha, na zaidi ya yote, kujifunza masomo yako ya Biblia kwa ukawaida? Utii kama huo wa hiari ndio msaada bora zaidi unaoweza kumpa mzazi wako.
NAMNA KUNDI LINAVYOWEZA KUSAIDIA
5. (a) Kuonyesha ‘kuwafikiria wengine’ kunamaanisha nini, na ni kwa sababu gani jambo hilo ni la maana sana? (b) Ni katika njia zipi kundi letu laweza kuonyesha ‘kuwafikiria wengine’ kwa njia hiyo kuhusiana na wazazi wasio na wenzi?
5 “Imekuwa vigumu na nyakati nyingine ninachoka,” akasema mzazi mmoja asiye na mwenzi mwenye watoto sita, kutia na mapacha wa miezi 17. “Hata hivyo, pindi kwa pindi mmoja wa akina ndugu au akina dada [kundini] huniambia: ‘Joan, unafanya kazi nzuri. Itastahilisha hayo.’ Kujua tu kwamba wengine wanakufikiria na kwamba wanajali kunasaidia sana.” Hiyo yaonyesha namna wote wanavyoweza kusaidia. “Ninyi nyote,” anasihi mtume Petro, “iweni na nia iyo hiyo, mkionyesha kufikiriana, mkiwa na shauku ya kidugu, na kuhurumiana kwa upendo.” (1 Pet. 3:8, NW) Jiweke mahali pa yule mtu mwingine. Neno la fadhili, tabasamu ya kutoka moyoni, yaweza kumaanisha mengi. Uwe mwenye moyo wa huruma badala ya kuwa mwenye kulaumu.
6. Ni kwa sababu gani mtu anayetenda kama mtu anayeelezwa katika 1 Yohana 3:17 angekuwa na daraka kweli kweli mbele za Mungu?
6 Upendo halisi unatia mengi zaidi ya maneno ya fadhili tu. Kabla tu ya kuwaambia Wakristo waonyeshe upendo wao kwa matendo, mtume Yohana aliandika hivi: “Lakini mtu akiwa na riziki ya dunia [hii], kisha akamwona ndugu yake ni mhitaji, akamzuilia huruma zake, je’ upendo wa Mungu wakaaje ndani yake huyo?” (1 Yohana 3:17) Neno la asili la “akamwona” halimaanishi kutupia jicho tu vivi hivi bali kutazama kwa kusudi. Linatumiwa kuhusu jemadari akikagua jeshi. Bila shaka, yeye anaangalia hata mambo madogo madogo kwa kupendezwa. Kwa hiyo ebu wazia hali anayoeleza Yohana: Mtu aliye na uwezo wa kusaidia, baada ya kutazama ndugu yake kwa uangalifu anaona uhitaji, kisha anafunga kabisa mlango wa moyo wake. Anakataa kusaidia. Anakosa huruma kama nini! Tunashukuru kwamba, itikio kama hilo lisilofaa ni jambo lisilo la kawaida miongoni mwa Mashahidi wa Yehova. Ripoti nyingi zaonyesha ukarimu wao kuelekea wale ‘walio na uhitaji.’
7. Mara nyingi wakati jamaa zenye uhitaji za wazazi wasio na wenzi zinapokosa kuangaliwa, tatizo huwa nini, nalo laweza kumalizwaje?
7 Hata hivyo, kumekuwako visa vya kutosaidia. Mara nyingi hilo limetokea kwa sababu ya kushindwa ‘kuona’ uhitaji. ‘Kuangalia kwa uangalifu,’ pamoja na kupendezwa juu ya wenye uhitaji, kulikosekana. Kwa hiyo namna gani juu ya hali katika kundi lenu? Je wewe unaona kweli hali ya wajane na yatima? Ni lini ulipofanya zaidi ya kuwasalimu tu? Je! umepata kuwaalika kwenye chakula au kwenye kikusanyiko cha kirafiki ili upate kufahamiana nao vizuri zaidi? Maulizo kama hayo yanatusaidia kuona kama ‘tunaona’ kweli kweli hali ya jamaa zetu zenye wazazi wasio na wenzi.
8. Je! wengine kundini wamepata kusaidia jamaa zenye uhitaji za wazazi wasio na wenzi?
8 Haihitaji utajiri mwingi ili mtu aweze kusaidia. Wengi, kwa kuona uhitaji halisi, wameshiriki chakula cha ziada pamoja na hao wenye uhitaji au wakawapa mavazi yasiyowatosha watoto wao ambao wamekuwa wakubwa. Wengine hata wamewafundisha wazazi wasio na wenzi ufundi fulani, kama vile kushona nguo, ili waweze kujisaidia zaidi. Mithali ya kale inasema hivi: “Mpe mtu samaki nawe wampa chakula cha siku moja. Mfundishe kuvua samaki na utampa chakula cha wakati wa maisha yake yote.” Mzazi mmoja asiye na mwenzi aliandika hivi: “Dada mmoja alinipa mashine ya kushonea, vitambaa viwili vya kushonea nguo na kunifundisha kushona. Tangu wakati huo nimeokoa mamia mengi ya [fedha].”
9. Ni maoni gani yanayosawazika zinayopaswa kuwa nayo jamaa za wazazi wasio na wenzi kuhusu kupata msaada kutoka kwa wengine?
9 Walakini je! wazazi wasio na wenzi wanapaswa kutarajia kupewa msaada kwa wingi na kisha kuvunjika moyo usipopatikana? Lazima mtu awe na maoni yanayosawazika. Ijapokuwa mtu anapaswa kushukuru kwa ajili ya misaada inayotolewa, inampasa mtu ajiulize, “Je! mimi nafanya yote niwezayo kushindana na hali hiyo?” Kama vile mzazi mmoja asiye na mwenzi alivyosema: “Kwa kweli hakuna ye yote anayeweza kuchukua jamaa ya ziada. Usipojisaidia, wewe hukubali daraka lako lote. Inakupasa ujifunze kujitegemea mwenyewe.” Kuna mifano ya Biblia ya wajane waaminifu waliojitoa kusaidia, badala ya kutazamia watumikiwe na wengine. (Luka 2:36-38; Marko 12:42-44) Mzazi mmoja asiyekuwa na mwenzi na aliyekuwa maskini kwa habari ya fedha na ambaye kwa miaka mingi alijitahidi sana kulea watoto wawili alikuwa na kipande cha karatasi kwenye ukuta wake kilichokuwa na maneno haya: “Wale wanaosaidia wengine hawawezi kukosa kusaidiwa.” Kwa miaka 12, akiwa mhubiri wa Injili wa wakati wote, amefanya ilo hilo. Amejitoa kusaidia wengine, na sasa, akiwa na umri wa miaka 73, angali amejitoa asaidie wengine. Na kama matokeo, yeye hajakuwa na uhitaji kamwe.—Mit. 11:25.
10. Kuna ushuhuda gani kuonyesha kwamba dada waliokomaa walishiriki sehemu kubwa katika kusaidia wajane na yatima katika karne ya kwanza?
10 Pasipo shaka wanawake waliokomaa walishiriki sehemu kubwa katika kusaidia wajane na yatima katika karne ya kwanza. Wajane wengine wanaelezwa kuwa ‘walisaidia watu wenye taabu,’ pengine kutia na jamaa za wazazi wasio na wenzi. (1 Tim. 5:10, HNWW) Katika barua yake aliyowaandikia Wakristo katika Roma, robo moja ya wale waliosalimiwa na mtume Paulo walikuwa wanawake waliokuwa wametumikia kwa uaminifu pamoja na kundi au kwa ajili ya kundi. Baadhi yao wanasemekana waziwazi kuwa walifanya kazi kwa bidii au walijitaabisha “katika Bwana.” (Rum. 16:3-15) Yule mwanamke Fibi, ‘mhudumu wa [kundi]” (kwa wazi alitumikia katika njia isiyo rasmi akiangalia mahitaji ya kibinafsi ya wengine), anaelezwa kuwa “msaidizi wa watu wengi.” Bila shaka, alichukua hatua ya kwanza katika kusaidia “wengi, “jambo lililotia kundi nguvu. Leo, kama vile alivyofanya Fibi, wanawake Wakristo waliokomaa wanatoa kitia-moyo chenye upendo pamoja na msaada, kutia na mali zao ili wasaidie ‘walio na taabu.’—Rum. 16:1, 2.
11. (a) Ni msaada wa namna gani ambao akina dada waliokomaa waweza kuwapa wazazi wasio na wenzi? (b) Waweza kutoa mfano gani, je! unajua visa vingine?
11 Wanawake wengi Wakristo wazee wanatoa msaada wa kiroho na wa kimoyo kwa kuwa “wafundishao mema,” ili kwamba “wawatie wanawake vijana akili,” kwa kuwapa mashauri yenye ufahamu. (Tito 2: 3-5) Kama mfano, mama mmoja asiye na mwenzi alikuwa akilia baada ya kusikiliza hotuba ya Biblia juu ya ndoa. Mwanamke Mkristo mwenye umri mkubwa zaidi akauliza kuna ubaya gani. “Nadhani najisikitikia tu,” akajibu kwa machozi. Mwanamke huyo aliyekuwa na umri mkubwa zaidi alianza kuzungumza naye. Yeye alijua alivyokuwa akijisikia huyu aliyekuwa ameshuka moyo, kwa kuwa yeye mwenyewe alikuwa ameachwa na mumewe miaka 20 iliyokuwa imepita. Huyo mwanamke kijana alisema hivi: “[Mwanamke huyo] alikuwa ndiye msaada wangu mkubwa zaidi. Alizungumza nami mara nyingi akanialika nishiriki naye kazi ya kuhubiri. Amekuwa mpendwa sana kwangu.” Wanawake wengi Wakristo waliokomaa wamewaendea wenye hali hiyo wakawafariji, hata wakazungumza matatizo ya kipekee sana ambayo mwanamume Mkristo, akiwa peke yake, hangeweza kuyazungumza kwa kufaa.
WAZEE—‘WAFURAHISHA MOYO WA WAJANE’
12. Wazee wanawezaje ‘kufurahisha moyo wa wajane’?
12 ‘Naliufanya moyo wa wajane kuimba kwa furaha,’ akasema Ayubu wa nyakati zilizotangulia Ukristo. (Ayubu 29:13) Yeye “aliona” maumivu waliyoyaona wajane. Badala ya kuyaongezea kwa kunena au kutenda bila kufikiri, yeye alitenda kwa njia iliyowafurahisha kindani—moyoni. Wazee wa makundi ya Kikristo leo wanaweza kufanya vivyo hivyo kwa kuwahakikishia hao kwamba kundi ni jamaa changamfu, kwa kuwafanya wajisikie kweli kweli kuwa sehemu yake. Waangalizi hao wanaweza kushiriki andiko lenye kufariji na linaloonyesha baraka zinazotokana na uaminifu. ‘Maono ya kufikiriana’ yatawasaidia wajaribu kufahamu mikazo mikubwa ya moyoni na ya akilini inayowataabisha wazazi wengi wasio na wenzi. (1 Pet. 3:8, NW) Kama matokeo, wenye uhitaji watajiona kuwa huru kuwaendea wapate msaada. Kila mmoja wa wanaume hawa wa kiroho aweza kweli kweli kuwa kama “mahali pa kujisitiri na dhoruba; kama mito ya maji mahali pakavu.”—Isa. 32:1, 2.
13. Ni kwa sababu gani wazazi wasio na wenzi wanaweza kuwafikia wazee wapate msaada katika kufanya maamuzi ya maana, nao ni msaada wa namna gani unaopaswa kutolewa?
13 Biblia ilitabiri kwamba Mungu angerudisha “washauri” wenye uwezo miongoni mwa watu wake wa zamani. (Isa. 1:26) Hali moja na hiyo, leo wazazi wasio na wenzi wanaweza kuwategemea wazee wapate shauri katika kufanya maamuzi ya maana. Wanapofikiwa, wazee wapaswa kutoa “uongozi wa ustadi,” wakimsaidia mwulizaji atambue kanuni za Biblia zinazohusika katika habari inayofikiriwa. Hata hivyo, daraka la mzee au ye yote mwingine anayefikiwa atoe msaada ni ‘kushauri,’ wala si kuwafanyia wengine maamuzi.—Mit. 11:14, NW; Gal. 6:5.
14. (a) Kwa nini wazee wanapaswa wajaribu ‘kutengeneza upya’ mtu anayechukua hatua ya uongo (b) Neno la Kigiriki linalotafsiriwa kurekebisha upya’ lilitumiwaje katika karne ya kwanza, nako kujua hivyo kwapaswa kuhusuje namna ‘kurekebisha upya’ kwa namna hiyo kunavyopaswa kufanywe?
14 Huenda mzee akaona kwamba, kwa sababu ya mikazo, mzazi asiye na mwenzi anachukua “hatua fulani ya uongo,” kama vile kuwa na matembezi ya kirafiki pamoja na asiyeamini. Huenda mtu huyo asijue kabisa kabisa uzito wa hatua kama hiyo. “Ndugu, hata ingawa mtu huchukua hatua fulani ya uongo kabla hajajua,” yapendekeza Biblia, “ninyi mlio na sifa za kiroho jaribuni kumrekebisha upya mtu huyo katika roho ya upole.” (Gal. 6:1 NW) Hivyo wazee pamoja na wengine wanaweza kuzuia “hatua ya uongo” isiwe mwendo wa upotovu. Neno la Kigiriki la ‘kurekebisha upya’ vilevile linatafsiriwa kuwa ‘tengeneza.’ (Marko 1:19) Katika karne ya kwanza, lilitumiwa kuhusu kutengeneza mfupa uliovunjika. Ijapokuwa daktari la zima atumie nguvu kadiri fulani, angekuwa mpole weee katika kutengeneza mfupa! Lengo lingekuwa ‘kutengeneza’ jeraha, si kulifanya baya zaidi. Kwa hiyo wazee wanaotaka kufikia moyo wa watu kama hao watampa sababu mtu huyo kwa upole na kwa wazi “katika roho ya upole,” na kumsaidia aone sababu gani kutumia shauri la Neno la Mungu ni kwa faida yake, na hivyo kumtengeneza kiroho.
15. (a) Ni wakati gani inapoweza kuwa lazima wazee wafanye mpango wa kusaidia wajane walio na uhitaji? (b) Ni kwa sababu gani wazee wanahitaji msaada kutoka kwa wengine kundini?
15 Nyakati nyingine huenda wazee wakalazimika kufanya mpango wajane wenye upweke wasaidiwe. Huko Trinidad, mjane mmoja Mkristo mwenye umri wa miaka 79 aliugua sana ugonjwa wa donda baya akahitaji kuangaliwa kila wakati mchana na usiku. Ijapokuwa alipokea malipo fulani ya uzeeni kutoka kwa serikali, yeye hakuwa na watu wo wote wa ukoo wa kumsaidia. Ili kuzuia kazi hiyo ngumu isiwaangukie wachache tu, wazee walipanga kuweko vikundi vya wanawake Wakristo waliojitolea kusaidia. Kwa muda wa zaidi ya miezi sita wanawake hao walipika na kumsafishia vitu dada yao wa kiroho, wakampeleka alikohitaji kupelekwa, wakafua mavazi yake na hata wakamwogesha alipokuwa hajiwezi tena. Huo ulikuwa mfano wa upendo uliowavutia jirani kweli kweli. Kwa wazi wazee hawawezi kufanya kila kitu kinachohitajiwa kifanywe katika hali kama hiyo. Kwa kawaida wao wana jamaa zao wenyewe wanazopaswa kuangalia. Walakini wanafurahia kufanya lo lote wawezalo, na wanathamini sana wakati wengine wanapochukua hatua ya kwanza na kusaidia katika hali za namna hiyo.
AKINA NDUGU—‘WAOKOENI YATIMA’
16. (a) Hangaiko kubwa zaidi la wazazi wa kike wasio na wenzi ni hangaiko gani? (b) Ni nani wanaoweza kusaidia, na namna gani?
16 Mama katika jamaa ya mzazi asiye na mwenzi kwa kawaida anahangaishwa na ukosefu wa uongozi wa baba katika nyumba, sana sana juu ya wana. Wanaume kundini wanapaswa kuona kama alivyoona Ayubu, aliyesema hivi: “Nalimwokoa . . . yatima naye, na yule asiyekuwa na mtu wa kumsaidia.” (Ayubu 29:12) Mara nyingi linalohitajiwa ni kupendezwa kwa unyofu. Vijana hao wanaweza kualikwa washiriki pamoja nawe katika kutoa ushuhuda, katika utendaji fulani katika Jumba la Ufalme na hata katika tafrija inayofaa. Kuangaliwa kama huko kwaweza ‘kumwokoa’ kijana kutokana na mwendo wa kilimwengu na kumvuta kwenye kundi.
17. (a) Ni nani aliyekuwa mfano mzuri wa mtu ‘aliyeokoa yatima,’ kukawa na matokeo gani? (b) Anapotoa msaada kwa watoto wengine, ndugu ambaye ameoa apaswa kufikiria nini?
17 Mtume Petro ni mmoja ‘aliyewaokoa yatima.’ Yeye alifanya urafiki na Yohana Marko, hata akamwita “Marko mwanangu.” (1 Pet. 5:13) Huenda Maria, mama ya Marko, akawa alikuwa mzazi asiye na mwenzi, kwa sababu masimulizi yasema kwamba Petro alikwenda nyumbani kwake, si kwa mume wake. (Matendo 12:12, HNWW) Bila shaka ushirika mzuri wa kiroho aliokuwa nao Marko pamoja na Petro na wanaume wengine Wakristo ulimsaidia sana awe misionari ambaye hata alipata kuandika kitabu cha Biblia. Yeye ni mfano bora kwa vijana ambao wanalazimika kulelewa na mama akiwa peke yake. Kwa wazi, ndugu ye yote aliyeoa apaswa kutambua kwamba kulingana na Maandiko ana daraka la kwanza—kuangalia jamaa yake kwanza. Bila kukosa kuangalia “walio wake,” mambo mengi mema yaweza kutimizwa kwa kuonyesha kupendezwa na hao yatima kwa kadiri kufanya hivyo kunavyofaidi na kadiri hali za mtu zinavyoruhusu.—1 Tim. 5:8.
MSINGI WA MSAADA HUO—UPENDO WA KUJINYIMA
18. (a) Ni upendo wa namna gani unaotambulisha Ukristo wa kweli, naye Yesu aliuonyeshaje? (b) Twaweza kuuonyeshaje upendo huo?
18 Kitambulisho cha Mkristo wa kweli si upendo wa vivi hivi tu, bali upendo wa kujinyima. Yesu aliwaambia wanafunzi wake hivi: “Amri mpya nawapa, Mpendane. Kama vile nilivyowapenda ninyi, nanyi mpendane vivyo hivyo. Hivyo watu wote watatambua ya kuwa ninyi mmekuwa wanafunzi wangu, mkiwa na upendo ninyi kwa ninyi.” (Yohana 13:34, 35) Mfano wake wa kutoa ndio ungekuwa kanuni. Yeye “hakujipendeza mwenyewe.” “Alijifanya maskini kwa ajili yenu.” “Alijitoa nafsi yake [kupitia kwa kifo chenye maumivu makali] kwa ajili ya dhambi zetu.” Ni kwa kuiga tu mfano huo wa upendo kwamba wanafunzi wake wangeweza kuonyesha uangalizi na kujali ambako wajane na yatima wangehitaji wakati wa “dhiki yao.”—Rum. 15:3; 2 Kor. 8:9, HNWW; Gal. 1:4; Yak. 1:27
19, 20. (a) Je! ni jambo rahisi sikuzote kuonyesha upendo wa kujinyima? Kwa sababu gani ndivyo au kwa sababu gani sivyo? (b) Hasa twapaswa kuhangaikia kusaidia nani?
19 Kadiri mikazo inavyozidi na inavyokuwa vigumu zaidi kushughulika na matatizo yetu wenyewe, ni rahisi kukosa kujali hali mbaya ya mwingine na kujishughulisha tu na maisha yetu wenyewe. Hata wengine katika karne ya kwanza ambao walikuwa ‘wamefundishwa na Mungu kupendana’ walihitaji ‘kufanya hata zaidi.’ (1 The. 4:9, 10, HNWW) Je! haitupasi kuangalia kikweli maoni na matendo yetu kuelekea ndugu na dada zetu Wakristo walio katika hali mbaya? Upendo kama ule wa Yesu ungetuhitaji tutoe uhai wetu kwa ajili ya ndugu zetu. Walakini, ikiwa tuna nia ya kuutoa uhai wetu kwa ajili ya ndugu zetu, inatupasa kuonaje juu ya kushiriki “chakula” chetu ‘tunapomwona ndugu yetu akiwa mhitaji’?—1 Yohana 3:17.
20 Kuangalia madaraka yetu ya kimaandiko kunatufanya tuwe na kazi nyingi. Mara nyingi tunaona afadhali tungekuwa na uwezo wa kufanya mengi zaidi kusaidia wengine. Hata hivyo, ikiwa tunafanya kwa moyo wa kupenda yale tuwezayo iweni na hakika kwamba Yehova anajua kadiri ya uwezo wetu naye anathamini yale tunayofanya. “Kwa hiyo kadiri tupatavyo nafasi na tuwatendee watu wote mema; na hasa jamaa ya waaminio —Gal. 6:10.
WOTE WAFANYA KAZI PAMOJA KUVUMILIA SHIDA
21. (a) Ni mambo gani wanayoweza kufanya wazazi wasio na wenzi ili washindane na mikazo ya leo? (b) Wengine kundini waweza kusaidiaje, na je! msaada huo ni wa maana?
21 Hivyo, kwa ufupi, wazazi wasio n; wenzi wanaweza kuvumilia kwa kufanya yafuatayo: (1) Kutumaini Mungu wakati wote sasa na kulitegemea tumaini la uzima wa milele wakati Mungu atakapotosheleza tamaa za wote. (Zab. 37:3, 4) (2) Kuendeleza uhusiano wa karibu pamoja na Mungu kupitia kwa funzo Biblia na sala zenye bidii. (3) Kujishughulisha na kazi zenye kufaidi, kutia na kushuhudia Ufalme, kuangalia mambo ya nyumbani na kulea watoto. Upendo wa kujinyima utawaongoza wote kundini waone lazima ya kusaidia wazazi wasio na wenzi na walio na uhitaji. Namna gani? Kwa ‘kuonyesha kuwafikiria wengine,’ kwa kuonyesha kupendezwa na watoto wao na kwa kuwasaidia kiroho na kimwili hayo ni mambo machache tu wanayoweza kufanyiwa. Msaada kama huo ni wa thamani kadiri gani? Mzazi mmoja asiye na mwenzi alisema hivi: “Nimepatwa na mambo mengi sana yasiyopendeza ambayo naona afadhali niyasahau. Walakini, acha niseme hivi: Bila msaada kutoka kwa akina ndugu na dada waaminifu wenye upendo nisingeweza kufaulu kamwe!”
22. Ni nini yatakayokuwa matokeo ya kuwaangalia wajane na yatima wenye uhitaji?
22 Ndiyo, wale ‘wanaoangalia’ kikweli jamaa za wazazi wasio na wenzi katika taabu yao si kwamba watawaona wakivumilia kwa uaminifu tu. (Yak. 1:27, NW) Wataonyesha waziwazi vilevile utu wa Baba yetu wa kimbinguni, ambaye “humpa msaada mjane na mtoto ambaye hana baba.”—Zab. 146:9, The Bible in Basic English.
—Kutoka The Watchtower Sept. 15, 1980.
[Picha katika ukurasa wa 12]
Wanawake Wakristo waliokomaa waweza kutoa kitia-moyo chenye upendo pamoja na msaada kutia na usaidizi wa vitu vya kimwili
[Picha katika ukurasa wa 13]
Kujifunza ufundi fulani kwaweza kusaidia wazazi wasio na wenzi wakabiliane na gharama ya maisha
[Picha katika ukurasa wa 15]
Je! wewe umepata kualika jamaa ya mzazi asiye na mwenzi ishiriki chakula pamoja nawe, mfahamiane zaidi?