Wakati Amani ya Ndoa Inapotishika
“Mke asiachane na mumewe; . . . tena mume asimwache mkewe.”—1 WAKORINTHO 7:10, 11.
1. Kusudi la Yehova lilikuwa nini kuhusu ndoa?
YEHOVA MUNGU aliungamanisha wanadamu wawili wa kwanza katika kifungo cha ndoa na kukusudia kwamba kifungo hicho cha mnofu mmoja kidumu. Ulipasa kuwa muungano uliobarikiwa ambao ungetokeza furaha kwao na kuzaa watoto waadilifu, yote hayo yakiwa kwa utukufu wa Mungu.—Mwanzo 1:27, 28; 2:24.
2. Ni nini kisababishi kimoja ambacho huongoza kwenye utenganisho wa vifungo vya ndoa?
2 Mpango huo wa ndoa ulio bora sana ulikatishwa vibaya na fikira ya kujitegemea na dhambi. (Mwanzo 3:1-19; Warumi 5:12) Kwa uhakika, roho ya kujitegemea ni moja la mambo yanayoongoza kwenye utenganisho wa vifungo vya ndoa leo. Hivyo, katika United States wakati wa 1985, kulikuwa na talaka 5—zikilinganishwa na ndoa 10.2—kwa kila watu 1,000. Katika 1986 ripoti moja kutoka Moscow ilionyesha kwamba ni asilimia 37 tu ya ndoa zilizo katika Urusi ambazo zinaendelea kwa miaka mitatu, na kwamba asilimia 70 zinamalizika katika muda wa mwongo mmoja.
3. (a) Ni nini kinachoweza kusababisha kutosikilizana katika ndoa? (b) Kuhusiana na ndoa, ni nani aliye mvunja-amani mkuu?
3 Roho ya kujitegemea inaweza kusababisha kutosikilizana katika ndoa. Pia inafungia ukuzi wa kiroho, kwa maana “tunda la haki [uadilifu, NW] hupandwa katika amani.” (Yakobo 3:18) Lakini ni nani aliye mvunja-amani mkuu? Ni Shetani. Na loo, inahuzunisha kama nini wakati wowote kati ya watumishi wa Mungu ‘wanapompa Ibilisi nafasi’ na hivyo wanashindwa kufurahia maskani za pumziko na amani!—Waefeso 4:26, 27.
4. Wakati wenzi Wakristo wanapokuwa na matatizo makali ya ndoa, inawapasa wang’amue nini na inawapasa wafanye nini?
4 Wakati wenzi wa ndoa walio Wakristo wanapokuwa na rai ya kwamba mtengano ndilo suluhisho pekee kwa matatizo yao ya ndoa, wao wamo katika hatari ya kujiachilia walemewe na mbinu za Shetani, na hapo huwa pana kasoro fulani kubwa ya kiroho. (2 Wakorintho 2:11) Kanuni za Mungu huwa hazitumiwi kwa ukamili na mmoja au wote wawili. (Mithali 3:1-6) Kwa hiyo inawapasa wafanye kwa haraka jitihada zenye sala za kutatua tofauti zao. Ikiwa zinaonekana kama zisizopatanika, ushauri wa wazee wa kundi unaweza kutafutwa. (Mathayo 18:15-17) Ingawa wanaume hao hawakupewa mamlaka ya kuambia waitikadi wenzao vile hasa wanavyopaswa kufanya kuhusu matatizo yao ya ndoa, wanaweza kuelekeza fikira kwenye mambo ambayo Maandiko yanasema.—Wagalatia 6:5.
5. Ni juu ya msingi gani talaka yenye uwezekano wa kufunga ndoa tena pamoja na mtu mwingine inakubalika Kimaandiko?
5 Ikiwa hali ya ndoa ni mbaya sana hivi kwamba mume na mke Wakristo hata wanafikiria talaka, wazee wanaweza kuonyesha wazi kwamba talaka na kufunga ndoa upya ni mambo yenye kukubalika ikiwa mwenzi wa mtu katika ndoa amefanya “uasherati” tu. Neno hilo linahusisha ndani uzinzi na namna nyingine za ngono zisizo za adili na mipotosho ya ngono. (Mathayo 19:9; Warumi 7:2, 3; ona Mnara wa Mlinzi, Januari 1, 1984, kurasa 7, 8.) Hata hivyo, namna gani ikiwa “uasherati” umekuwa haukufanywa lakini amani ya ndoa imetishika kwa njia nzito? Maandiko yanasema nini juu ya mtengano wa halali au usio na uhalali kamili?
Shauri la Paulo Lililovuviwa
6. (a) Ni nini maana hasa ya shauri la Paulo kwenye 1 Wakorintho 7:10, 11? (b) Wenzi walio Wakristo wanapaswa kutatua matatizo yao ya ndoa jinsi gani?
6 Kwa jitihada ya kusaidia mume na mke Wakristo ambao vifungo vya ndoa yao vinatishika, wazee wanaweza kuelekeza fikira kwenye maneno ya mtume Paulo: “Wale waliokwisha kuoana nawaagiza; wala hapo si mimi, ila Bwana; mke asiachane na mumewe; lakini, ikiwa ameachana naye, na akae asiolewe, au apatane na mumewe; tena mume asimwache mkewe.” (1 Wakorintho 7:10, 11) Wenzi wa ndoa walio Wakristo wanapaswa waweze kutatua matatizo yao, wakifanya maruhusio ya kutokamilika kwa kibinadamu. Hakuna tatizo linalopasa kuwa kubwa sana hivi kwamba haliwezi kutatuliwa kwa kusali kwa moyo wa bidii, kutumia kanuni za Biblia, na kuonyesha upendo ulio tunda la roho ya Mungu.—Wagalatia 5:22; 1 Wakorintho 13:4-8.
7. (a) Ikiwa wenzi wa ndoa walio Wakristo wanatengana, msimamo wao wa Kimaandiko ni nini? (b) Huenda mtengano wa Wakristo wawili waliofunga ndoa ukawa nini kuhusu kuwa na mapendeleo ya utumishi?
7 Lakini namna gani wenzi wa ndoa walio Wakristo wakitengana? Ni lazima ‘wakae bila kuoa au kuolewa au wapatane.’ Isipokuwa kama suala linalohusika ni talaka iliyopatikana kwa msingi wa “uasherati,” hakuna yeyote kati yao aliye huru Kimaandiko kufunga ndoa tena. Kwa sababu ya jambo hilo na “mweneo wa uasherati,” ingekuwa vyema ‘wapatane’ bila kukawia. (1 Wakorintho 7:1, 2, NW) Si kazi ya wazee kudai kwamba mwanamume na mwanamke hao wamalize mtengano wao, lakini huenda watu hao wasistahili mapendeleo fulani ya utumishi kwa sababu ya matatizo yao ya ndoa. Mathalani, ikiwa mwanamume fulani ‘hajui jinsi ya kusimamia nyumba yake mwenyewe,’ ithibati iko wazi kwamba hana uwezo wa ‘kuangalia kundi la Mungu’ akiwa mwangalizi.—1 Timotheo 3:1-5, 12, NW.
8. Ni wazo gani kuu lililo katika shauri la Paulo kwenye 1 Wakorintho 7:12-16?
8 Mkazo unawekwa juu ya kuhifadhi ndoa hata ikiwa ni mwenzi wa ndoa mmoja tu aliye mwitikadi. Paulo aliandika hivi: “Iwapo ndugu mmoja ana mke asiyeamini, na mke huyo anakubali kukaa naye, asimwache. Na mwanamke, ambaye ana mume asiyeamini, na mume huyo anakubali kukaa naye, asimwache mumewe. . . . Lakini yule asiyeamini akiondoka, na aondoke. Hapo huyo ndugu mume au ndugu mke hafungiki. Lakini Mungu ametuita katika amani. Kwa maana wajuaje, wewe mwanamke, kama utamwokoa mumeo? au wajuaje, wewe mwanamume, kama utamwokoa mkeo?” (1 Wakorintho 7:12-16) Ikiwa yule asiye mwitikadi anachagua kuondoka, aliye Mkristo atamwacha aende zake. Lakini aliye mwitikadi, kwa kutumainia kwamba asiye mwitikadi huenda akavutwa kuja kwenye Ukristo, siye angekuwa wa kwanza kutokeza mvunjiko huo. Inaonekana kuwa Eunike, mama ya Timotheo, alikaa pamoja na mume wake asiye mwitikadi lakini akampa mwana wake maagizo ya kiroho.—2 Timotheo 1:5; 3:14, 15.
Misingi ya Mtengano
9, 10. (a) Kulingana na 1 Timotheo 5:8, ni nini msingi mmoja wa kutengana kwa wenzi wa ndoa? (b) Inawapasa wazee waliowekwa rasmi wafanye nini ikiwa mwanamume Mkristo anashtakiwa kukataa kuandaa riziki kwa mke na watoto wake?
9 Maneno ya Paulo kwenye 1 Wakorintho 7:10-16 yanawatia moyo wenzi wa ndoa wakae pamoja. Hata hivyo, baada ya kujaribu sana kuhifadhi uhusiano wao wa ndoa, hatimaye baadhi yao wameamua kwamba, kwa kujali kabisa dhamiri, wao hawana jingine la kufanya ila kutengana. Ni nini inayoweza kuwa misingi ya hatua hiyo?
10 Kutokutoa riziki kimakusudi ni msingi mmoja wa mtengano. Wakati wa kuingia katika kifungo cha ndoa, mume hujitwalia daraka la kuandaa riziki kwa ajili ya mke na watoto wowote ambao huenda wakapata. Mwanamume asiyeandalia washiriki wa nyumba yake “ameikana Imani, tena ni mbaya kuliko mtu asiyeamini.” (1 Timotheo 5:8) Kwa hiyo mtengano unawezekana ikiwa kuna ukosefu wa kimakusudi wa kutoa riziki. Bila shaka, wazee waliowekwa rasmi wanapaswa kufikiria kwa uangalifu shtaka la kwamba Mkristo anakataa kuruzuku mke na jamaa yake. Kukataa kwa ukaidi kuruzuku jamaa ya mtu huenda kukatokeza kutengwa na ushirika.
11. Ni nini msingi mwingine wa mtengano, lakini ni jambo gani huenda likafanya hali ile iwe yenye kuvumilika?
11 Kutendwa mabaya ya kupita kiasi mwilini ni msingi mwingine wa mtengano. Tuseme mwenzi asiye mwitikadi hulewa, anakasirika sana, na kumsababishia mwitikadi dhara la kimwili. (Mithali 23:29-35) Kupitia sala na kuonyesha tunda la roho ya Yehova, huenda mwitikadi akaweza kuzuia mifoko hiyo na kufanya hali ile ivumilike. Lakini ikiwa hatua imefikiwa ambapo afya na uhai wa mwenzi mwenye kutendwa vibaya imo hatarini, mtengano ungeruhusika Kimaandiko. Tena, wazee wa kundi wanapaswa wachunguze mashtaka ya kutendwa vibaya kimwili wakati Wakristo wawili wanapohusika katika ndoa yenye matata, na huenda ikawa lazima hatua ya kutenga na ushirika ichukuliwe.—Linganisha Wagalatia 5:19-21; Tito 1:7.
12. (a) Ni jinsi gani huenda hali ya kiroho ya mwitikadi ikahusika juu ya lile suala la mtengano? (b) Ni jambo gani linalodokezwa ikiwa hali ya afya mbaya kiroho imo katika maskani ya Kikristo?
12 Kuhatarishwa kabisa kabisa kwa hali ya kiroho kunaandaa pia msingi wa mtengano. Aliye mwitikadi katika maskani iliyogawanyika kidini anapaswa afanye kila jambo linalowezekana ayatumie kwa faida maandalizi ya kiroho ya Mungu. Lakini mtengano unaruhusika ikiwa upinzani wa mwenzi asiyeitikadi (labda kutia na kuzuiliwa kimwili) unafanya kwa uhalisi isiwezekane kufuatia ibada ya kweli na kwa uhakika unahatarisha hali ya kiroho ya mwitikadi. Hata hivyo, namna gani ikiwa hali ya afya mbaya sana ya kiroho ipo mahali ambapo wenzi wote wawili ni waitikadi? Wazee wanapaswa kutoa usaidizi, lakini mume aliyebatizwa hasa anapaswa kutia bidii nyingi aondoe hali ile. Bila shaka, ikiwa mwenzi wa ndoa aliyebatizwa hutenda kama mwasi-imani na hujaribu kuzuia mwenzi wake asitumikie Yehova, wazee wanapaswa kushughulikia mambo kulingana na Maandiko. Kutenga na ushirika kukitokea katika kisa kinachohusisha ndani kuhatarishwa kamili kwa hali ya kiroho, kutoandaa riziki kimakusudi, au kutendwa vibaya kimwili kwa njia ya kupita kiasi, Mkristo mwaminifu anayetafuta mtengano wa kisheria hangekuwa akienda dhidi ya shauri la Paulo juu ya kupeleka mwitikadi mahakamani.—1 Wakorintho 6:1-8.
13. Ni chini ya mastakimu gani huenda mtengano wa wenzi wa ndoa ukaruhusika?
13 Ikiwa mastakimu ni za kupita kiasi, hapo huenda mtengano ukawa unafaa. Lakini ni wazi kwamba visingizo ovyo havipasi kutumiwa ili kujipatia mtengano. Wakristo wowote wanaofanya mtengano lazima wahimili daraka la kibinafsi kwa kitendo hicho na wanapaswa kung’amua kwamba sisi sote tutatolea Yehova hesabu.—Waebrania 4:13.
Je! Ni Hatua ya Hekima?
14. (a) Ni tatizo gani ambalo mtengano unaelekea kufanyiza? (b) Huenda mtengano ukaathiri watoto jinsi gani?
14 Matatizo ambayo mtengano utaelekea kufanyiza yanapasa kufikiriwa kwa sala. Mathalani, ni mara haba ambapo jamaa ya mzazi mmoja huandaa mambo ambayo jamaa zenye wazazi wawili zinaweza kuandaa katika usawaziko na nidhamu. Na huenda mtengano ukawa na tokeo zito juu ya watoto kama lile la talaka, ambalo jarida India Today liliripoti juu yalo hivi: “Sheena, ambaye ana macho makubwa yanayokodolewa sana kama kwamba yanataka kuuona ulimwengu wote, ana miaka sita. Wazazi wa kisichana huyo walitalikiana miaka miwili iliyopita baada ya pambano la mahakamani lenye sifa mbaya. Muda mfupi baadaye, baba yake alioa mwanamke mwingine. Kwa mwaka mmoja kisichana huyo alipatwa-patwa na asthma mbaya na hunyonya kidole-gumba daima. Yeye anaishi pamoja na mama yake Delhi Kusini. Mama yule [asema]: ‘Huzuni yangu imenitoka mimi na kumwingia Sheena. . . . Yeye anasikitika kutokuwa na baba yake. . . . Yeye ni mkomavu kuliko walio wengi wa watoto wa umri wake. Lakini yeye hupatwa-patwa na vipindi vya kulia-lia, kama kwamba anataka kutokeza nje kitu fulani kilicho ndani yake. Shule ilikuwa tatizo. Watoto wanaweza kuwa wakatili sana. Mara nyingi, yeye huwazia-wazia mambo yasiyo ya kweli: yeye hujitungia hadithi kwa kuambia rafiki zake kwamba sisi sote tuko pamoja tukiendelea vizuri tu.’”
15. Ni athari gani ambayo huenda mtengano ukawa nayo juu ya mume au mke Mkristo?
15 Mara nyingi, mtengano hauwi na matokeo mazuri kwa mume wala mke Mkristo. Baada ya muda mfupi wao wanapata kujua kwamba bila mwenzi wa ndoa au watoto kunakuwa na uwazi wenye kusumbua-sumbua. Isiyo ya kupuuzwa ni ile mibano inayotokana na mtengano. Je! itawezekana kushughulikia mambo kwa msimamo wa kifedha au vinginevyo? Na namna gani ikiwa mgogoro wa kutengana unatokeza kutumbukia katika ukosefu wa adili? Yesu alisema: “Hekima inathibitishwa kuwa adilifu na kazi zake.” (Mathayo 11:19, NW) Hasa wakati wenzi wote wawili ni Wakristo, nyakati nyingine mipango ambayo inafanywa-fanywa kupitia mtengano imethibitika kuwa yenye kukosa sana hekima.
Jitahidini Kutatua Matatizo
16. Wenzi wa ndoa walio Wakristo ambao wanapata amani ya ndoa yao ikitishika wanapaswa kufanya nini?
16 Wenzi wa ndoa walio Wakristo ambao wanapata amani yao ya ndoa ikitishika kwa uzito wanapaswa kuzungumzia tofauti zao kwa njia inayowafaa wale wanaotumikia Mungu. Na kwa uhakika wanapaswa kufanya maruhusio kwa hali ya kutokamilika. (Wafilipi 2:1-4) Lakini ni jambo gani jingine linaloweza kufanywa?
17. Ni jinsi gani kuonyesha hekima kuhusiana na vitu vya kimwili kunaweza kuchangia amani ya ndoa?
17 Kuonyesha hekima kuhusiana na vitu vya kimwili kunaweza kuchangia amani ya ndoa. Kwa kutoa kielezi: Baada ya kufikiria rai ya mke wake iliyo ya mwelekeo hasi, huenda hata hivyo mwanamume akaamua kwamba ni jambo la hekima jamaa yake kuhamia mahali pengine. Huenda ikaonekana inashaurika kufanya hivyo kwa sababu za kiuchumi, lakini pia huenda hiyo ikawezesha jamaa kusogeza mbele masilahi ya Ufalme kwa kutumikia mahali ambako uhitaji ni mkubwa zaidi. (Mathayo 6:33) Huenda mke wake Mkristo asipendelee mhamo huo kwa sababu angekuwa akiacha nyuma wazazi wake au mazingira aliyoyazoea. Lakini mke huyo atakuwa mwenye hekima kufanya ushirikiano kamili pamoja na mume wake, ambaye ndiye kichwa cha nyumba ana ndiye mwenye daraka la kuamua ni wapi jamaa yake itaishi. Waaidha, kujitiisha kwa mke na kuonyesha ushirikiano wenye upendo kutachangia amani ya nyumbani.—Waefeso 5:21-24.
18. Ni fursa gani ambazo wenzi wa ndoa walio Wakristo wanazo kufanya mambo pamoja?
18 Amani ya jamaa husitawi na matatizo kuonekana kutokuwa mazito sana wakati wenzi wa ndoa wanapofanya mambo pamoja. Mathalani, wenzi wa ndoa walio Wakristo wana fursa nzuri sana za kufanya kazi mmoja pamoja na mwenzake katika huduma ya shambani. Wakifanya hivyo kwa ukawaida na kwenda pamoja na watoto wao, jamaa nzima itanufaika. Huenda pia kukawa kuna fursa mbalimbali za kuimarisha kifungo cha ndoa kwa kushiriki katika utendaji mwingine unaofaa ambao humfurahisha kwa njia ya pekee mwenzi huyu au huyu.
19. Ni ukichwa wa aina gani ambao utaendeleza amani ya jamaa?
19 Ukichwa unaozoewa ifaavyo utaimarisha vifungo vya ndoa. Bila shaka, mume Mkristo aliye mkomavu hatakuwa mtawala wa kidikteta. Badala ya hivyo, ‘yeye ataendelea kupenda mke wake na hatakuwa mwenye kasirani kali kwake.’ Yehova anamtarajia ajizoeze ukichwa wenye upendo. (Wakolosai 3:18, 19, NW) Hapo tena, ukichwa huo unaendeleza amani ya jamaa.
Katika Nyumba Zilizogawanyika
20, 21. Ni jinsi gani huenda kiasi katika kutenda mambo kikawa na manufaa wakati amani inapotishika katika nyumba iliyogawanyika kidini?
20 Kuwa na kiasi katika kutenda mambo husaidia kutatua matatizo ya ndoa kati ya wenzi wa ndoa walio Wakristo. (Wafilipi 4:5) Lakini kiasi katika kutenda mambo ni cha maana pia ikiwa amani inatishika katika nyumba iliyogawanyika kidini. Ikiwa mume asiye mwitikadi anajaribu kuzuia mke Mkristo asitumikie Yehova, mke angeweza kujaribu kusababu mambo pamoja naye, akionyesha wazi kwa nadhari kwamba yeye humpa mume wake uhuru wa kidini na ni jambo la kiakili kwamba yeye anapaswa kutendewa vile yeye hutendea mume wake. (Mathayo 7:12) Ingawa mke anapaswa kuwa katika ujitiisho wa kiasi kwa mume wake asiye mwitikadi, mapenzi ya Mungu lazima yafanywe ikiwa kuna hitilafiano. (1 Wakorintho 11:3; Matendo 5:29) Kwa uhakika, kuhudhuria mikutano ya Kikristo mara tatu kwa juma si jambo linalopita kiasi. Lakini mke mwenye kuitikadi huenda akaona ni hekima kuwa kwenye maskani yao jioni nyinginezo na kuratibu huduma yake ya shambani iwe ya saa ambazo mume wake yuko kazini na watoto wanapokuwa shuleni. Kwa kutenda mambo kwa kiasi na kufanya mipango myema, yeye hahitaji ‘kuchoka katika kutenda mema.’—Wagalatia 6:9.
21 Kiasi katika kutenda mambo kinanyooka kufikia mambo mengine pia. Mathalani, mtu ana haki ya kuzoea dini fulani. Lakini lingekuwa jambo lisilo la kiasi na lisilo la hekima mke Mkristo kuweka Biblia zake na misaada ya kujifunzia Biblia mahali ambapo pangeweza kutomfurahisha mume wake mwenye kupinga vikali. Hitilafiano linaweza kuepukwa ikiwa vichapo hivyo vinawekwa miongoni mwa vitu vya kibinafsi vya mke na ajifunze vichapo hivyo kwa faragha. Bila shaka, ni lazima yeye asikubali kuacha msimamo wake juu ya kanuni za uadilifu.—Mathayo 10:16.
22. Ni jambo gani huenda likafanywa ikiwa kukatishwa vibaya kwa amani ya nyumbani kunategemea hasa kuwapa watoto maagizo ya kidini?
22 Ikiwa kukatishika vibaya kwa amani ya nyumbani kunategemea hasa kuwapa watoto maagizo ya kidini, mke mwitikadi anaweza kupanga kwa nadhari ili wao waandamane naye kwenye mikutano na katika huduma ya shambani. Lakini ikiwa mume na baba asiye mwitikadi anazuia jambo hilo, mke anaweza kufundisha watoto kanuni za Biblia ili kwamba wakuapo na kutoka kwenye maskani yao, waelekee kufuatia ibada ya kweli. Ikiwa mume ndiye mwitikadi, kwa kuwa ndiye kichwa cha nyumba, ana wajibu wa Kimaandiko kulea watoto wake wakiwa Wakristo. Kwa hiyo inampasa ajifunze Biblia pamoja nao, awapeleke mikutanoni, na kuwafundisha katika huduma ya shambani. (Waefeso 6:4) Kama ilivyo kiasili, anapaswa kuwa mwenye fadhili, mwenye upendo, na mwenye kiasi katika kushughulika pamoja na mke wake asiye mwitikadi.
Dumisheni Amani Mkiwa Jamaa Yenye Muungamano
23. Ikiwa amani ya ndoa inatishika, ni jambo gani huenda likathibitika kuwa lenye msaada?
23 Kwa kuwa wenzi wa ndoa ni “mnofu mmoja,” inawapasa waishi pamoja kwa amani kulingana na mpango wa Mungu kwa watu waliofunga ndoa, hasa ikiwa wenzi wote wawili ni Wakristo. (Mathayo 19:5, NW; 1 Wakorintho 7:3-5) Lakini ikiwa amani ya ndoa inatishika katika kisa chako, yapitie kwa sala mawazo ya Kimaandiko yaliyotangulia kutajwa. Huenda pia likawa jambo lenye msaada kufikiria kule nyuma wakati wa uchumba wako. Nyinyi wote wawili mlijitahidi kama nini kutenda yaliyofaa na kuweka msingi wa muungano wenye furaha! Je! sasa nyinyi mtafanya jitihada kama hizo ili kushikanisha ndoa yenu?
24. Wakristo wanapaswa kuwa na mwelekeo gani kuhusu kifungo cha ndoa?
24 Wakristo walioungamana katika kifungo cha ndoa wana zawadi nzuri ajabu kutoka kwa Mungu—ndoa yao! Nyinyi mkiishi kulingana na nadhiri zenu za ndoa na kudumisha ukamilifu kwa Yehova, mbele yenu pana ulimwengu mpya wa uadilifu ambamo mtengano na talaka inayoleta kihoro kingi cha moyoni haitakumba tena aina ya binadamu. Kwa hiyo onyesheni shukrani kwa kifungo cha ndoa kikiwa “kamba ya nyuzi tatu” ya kitamathali, huku Yehova akiwa sehemu muhimu ya kifungo hicho. (Mhubiri 4:12) Na washiriki wote wa nyumba yenu yenye muungamano waone shangwe juu ya baraka ya kuwa na furaha ya jamaa katika maskani yenye pumziko na amani.
Majibu Yako Ni Nini?
◻ Ni jinsi gani wewe ungetoa muhtasari wa shauri la Paulo kwenye 1 Wakorintho 7:10-16?
◻ Ni nini sababu halali za mtengano wa wenzi wa ndoa?
◻ Ni jinsi gani huenda Wakristo wakatatua matatizo wakati amani ya ndoa inapotishika?
◻ Katika nyumba zilizogawanyika kidini, ni jinsi gani kiasi kinavyoweza kuchangia amani?
[Picha katika ukurasa wa 23]
Wenzi wa ndoa walio Wakristo ambao amani yao ya ndoa inatishika wanapaswa kuzungumzia matatizo yao kwa njia inayowafaa wale wanaotumikia Yehova