Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g 7/10 kur. 10-13
  • Je, Niko Tayari Kuondoka Nyumbani?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Je, Niko Tayari Kuondoka Nyumbani?
  • Amkeni!—2010
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Nina Nia Gani?
  • Je, Niko Tayari?
  • Nina Miradi gani?
  • Niko Tayari Kuondoka Nyumbani?
    Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 1
  • Je, Niko Tayari Kuondoka Nyumbani?
    Vijana Huuliza
  • Maisha Yako Yanaelekea Wapi?
    Endeleeni Kukesha!
  • Unapolazimika Kurudi Nyumbani
    Amkeni!—2015
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—2010
g 7/10 kur. 10-13

Vijana Huuliza

Je, Niko Tayari Kuondoka Nyumbani?

“Nyakati nyingine mimi huhisi kwamba watu wananidharau kwa sababu nina umri wa miaka 19 na bado ninaishi nyumbani, ni kana kwamba siwezi kuonwa kuwa mtu mzima hadi niondoke nyumbani.” —Katie.a

“Ninakaribia umri wa miaka 20, nami huchukizwa kwamba wazazi wangu hawaniruhusu nifanye maamuzi yangu mwenyewe. Nimefikiria kuhama kwa sababu wao hunipuuza na kuniambia wanajua kinachonifaa.”—Fiona.

MUDA mrefu kabla ya kuwa tayari kuondoka nyumbani unaweza kuanza kuhisi kuwa unatamani kujitegemea. Hisia kama hiyo ni ya kawaida. Isitoshe, kusudi la awali la Mungu lilikuwa kwamba vijana wakue na mwishowe wawaache baba na mama yao na kuanzisha familia yao. (Mwanzo 2:23, 24; Marko 10:7, 8) Lakini kwa kuwa tu unahisi kwamba unataka kujitegemea, je, hiyo inamaanisha uko tayari kuondoka nyumbani? Huenda. Hata hivyo, utajua jinsi gani kwamba uko tayari kuondoka nyumbani? Fikiria maswali matatu muhimu ambayo unapaswa kujibu. Swali la kwanza ni . . .

Nina Nia Gani?

Ili uweze kuelewa nia yako ya kuondoka nyumbani, tazama orodha ifuatayo. Andika nambari ukianza na sababu unayoona kuwa muhimu.

․․․ Niepuke matatizo nyumbani

․․․ Nipate uhuru zaidi

․․․ Niheshimiwe zaidi na rafiki zangu

․․․ Nimsaidie rafiki anayehitaji mtu wa kuishi naye

․․․ Nijitolee kazi katika eneo lingine

․․․ Nijifunze kuishi peke yangu

․․․ Niwapunguzie wazazi wangu mzigo

․․․ Sababu nyingine ․․․․․

Hakuna sababu yoyote mbaya kati zile zilizoorodheshwa. Hata hivyo, nia yako ya kuondoka nyumbani inaweza kuamua ikiwa utakuwa mwenye furaha unapoondoka. Kwa mfano, ikiwa unaoondoka ili tu uepuke matatizo nyumbani au ili ujipatie uhuru zaidi, huenda ukashangaa kuona mambo ni tofauti na ulivyotarajia!

Danielle, aliyeondoka nyumbani kwa muda akiwa na umri wa miaka 20, alijifunza mambo mengi kutokana na kuchukua hatua hiyo. Anasema: “Sote tunahitaji kuishi chini ya vizuizi fulani. Unapoishi peke yako, huenda hutafanya mambo fulani kwa sababu ya ratiba yako ya kazi na kukosa pesa.” Carmen, aliyehamia nchi nyingine kwa muda wa miezi sita anasema: “Nilifurahia wakati huo, lakini kila mara nilihisi sikuwa na wakati wa ziada wa kutosha! Nilihitaji kufanya kazi za nyumbani kama kusafisha nyumba, kurekebisha vitu vilivyoharibika, kulimia bustani, kuosha nguo, kusugua sakafu, na kadhalika.”

Ni kweli kwamba kuhama kunaweza kukupa uhuru zaidi na kunaweza pia kukufanya uheshimiwe zaidi na rafiki zako. Lakini wewe ndiye utakayelipia gharama zote za nyumba, kupika, kusafisha nyumba, na kutafuta mambo ya kufanya wakati ambapo marafiki na watu wa familia hawako nyumbani. Kwa hiyo, usiwaruhusu watu wengine wakuharakishe ufanye uamuzi wa haraka. (Methali 29:20) Hata ikiwa una sababu nzuri za kuondoka nyumbani, mengi zaidi yanahitajika mbali na kuwa na nia nzuri tu. Unahitaji kuwa na uwezo wa kujitunza na hilo linatuleta kwenye swali letu la pili . . .

Je, Niko Tayari?

Kuondoka nyumbani ni sawa na kutembea msituni. Je, unaweza kutembea jangwani bila kujua jinsi ya kusimamisha hema, kuwasha moto, kupika, au hata kusoma ramani? Huenda usifanye hivyo! Lakini vijana wengi sana huondoka nyumbani bila kuwa na uwezo wa kujitunza.

Mfalme Sulemani mwenye hekima alisema kwamba “mtu mwerevu huzifikiria hatua zake.” (Methali 14:15) Ili kukusaidia kufikiria ikiwa uko tayari kuondoka nyumbani, chunguza habari iliyo chini ya vichwa vifuatavyo. Tia alama hii ✔ kando ya sifa ambazo tayari uko nazo na alama hii X kando ya zile unazohitaji kufanyia kazi.

◯ Kupangia matumizi ya pesa “Sijawahi kulipia chochote,” anasema Serena mwenye umri wa miaka 19. “Ninaogopa kuondoka nyumbani na kupangia pesa zangu.” Ni katika njia gani unaweza kujifunza jinsi ya kupangia matumizi ya pesa zako?

Methali moja ya Biblia inasema hivi: “Mtu mwenye hekima atasikiliza na kupata mafundisho zaidi.” (Methali 1:5) Kwa hiyo, mbona usiwaulize wazazi wako mtu anahitaji pesa ngapi kila mwezi ili kulipia kodi ya nyumba, kununua chakula, na kutumia gari, au kulipia gharama nyingine za usafiri? Kisha waombe wazazi wako wakufundishe jinsi ya kupangia pesa zako na kulipia gharama. Kwa nini ni muhimu kujifunza kufuata bajeti? Kevin, mwenye umri wa miaka 20 anasema hivi: “Unapoanza kuishi peke yako, unaanza kuwa na gharama nyingi ambazo hukutarajia. Usipokuwa mwangalifu, huenda ukafanya kazi nyingi sana ili tu ulipe madeni.”

Je, unataka kujua ukweli wa mambo? Ikiwa unafanya kazi na bado unaishi nyumbani, kwa muda fulani wape wazazi wako kiasi cha pesa kinacholingana na kile unachotumia kila mwezi kwa ajili ya chakula, malazi, na gharama zako nyingine. Ikiwa huwezi au hutaki kulipia gharama zako ukiwa bado nyumbani, basi hujajitayarisha vya kutosha kuondoka nyumbani.—2 Wathesalonike 3:10, 12.

◯ Kazi za nyumbani Brian, mwenye umri wa miaka 17, anasema kwamba hataki kuondoka nyumbani kwa sababu hataki kufua nguo zake mwenyewe. Utajua jinsi gani kwamba uko tayari kuishi peke yako? Aron, mwenye umri wa miaka 20 anatoa dokezo hili: “Kwa juma moja jaribu kuishi ni kana kwamba uko peke yako. Kula chakula ambacho umejinunulia mwenyewe dukani kwa pesa zako mwenyewe na ukajipikia. Vaa nguo ambazo umefua mwenyewe na kupiga pasi. Jifanyie kazi zote za nyumbani. Unapotaka kusafiri, jaribu kufanya hivyo mwenyewe bila msaada wa wazazi wako.” Ukifuata dokezo hili utapata faida mbili: (1) Utapata ujuzi wenye thamani na (2) utathamini zaidi kazi ambayo wazazi wako wanafanya.

◯ Kushirikiana na wengine Je, una uhusiano mzuri pamoja na wazazi na ndugu na dada zako? Ikiwa sivyo, huenda ukadhani kuwa maisha yatakuwa rahisi utakapoishi na rafiki yako. Labda. Lakini fikiria yale ambayo Eve mwenye umri wa miaka 18 anasema: “Rafiki zangu wawili walianza kuishi pamoja. Walikuwa marafiki wa chanda na pete kabla hawajaanza kuishi pamoja, lakini hawakuweza kuishi pamoja. Mmoja alikuwa nadhifu na mwingine alikuwa shaghala-baghala. Mmoja alijali mambo ya kiroho na mwingine hakuyajali. Hawakufaulu!”

Erin, mwenye umri wa miaka 18, anataka kuondoka nyumbani. Lakini anasema hivi: “Unaweza kujifunza mengi kuhusu jinsi ya kuishi na watu ukiwa bado nyumbani. Unajifunza jinsi ya kutatua matatizo na kukubali maoni ya wengine. Nimetambua kuwa wale wanaoondoka nyumbani ili tu waepuke kugombana na wazazi wao, hukuza tabia ya kukimbia matatizo badala ya kuyatatua.”

◯ Ratiba yako ya kiroho Wengine huondoka nyumbani wakiwa na kusudi la kutoroka utendaji wa kidini wa wazazi wao. Wengine huondoka wakiazimia kuendelea na ratiba nzuri ya kujifunza Biblia na ya ibada lakini baada ya muda mfupi wanakuza mazoea mabaya. Unaweza kuzuia jinsi gani ‘imani yako isivunjike’?—1 Timotheo 1:19.

Usifuate tu kile ambacho wazazi wako wanaamini bila kufikiri. Yehova Mungu anataka sisi sote tujihakikishie wenyewe mambo tunayoamini. (Waroma 12:1, 2) Panga ratiba nzuri ya funzo la Biblia na ya ibada na uhakikishe kwamba unaifuata. Kwa nini usiandike ratiba hiyo kwenye kalenda na uone ikiwa utaifuata kwa mwezi mmoja bila wazazi wako kukusukuma?

Kisha, swali la tatu ambalo unahitaji kufikiria ni . . .

Nina Miradi gani?

Vijana wengine wanaondoka nyumbani ili kutoroka matatizo au kuepuka kuwa chini ya wazazi wao. Wanakazia fikira mambo wanayotoroka badala ya kule wanakoelekea. Lakini kufanya hivyo ni kama kujaribu kuendesha gari ukiangalia nyuma. Dereva anapokazia fikira kile anachoacha nyuma, hataona kile kilicho mbele. Tunajifunza nini? Ili ufanikiwe usikazie fikira tu kuondoka nyumbani bali kazia mradi unaofaa.

Vijana fulani ambao ni Mashahidi wa Yehova wameondoka nyumbani ili kuhubiri katika maeneo yenye uhitaji katika nchi zao au katika nchi nyingine. Wengine wanaondoka ili kusaidia katika ujenzi wa mahali pa ibada au kufanya kazi katika ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova. Wengine wanahisi kuwa wanapaswa kuishi peke yao kwa muda kabla ya kufunga ndoa.b

Andika hapa mradi ambao ungependa kutimiza utakapoondoka nyumbani. ․․․․․

Katika visa fulani inawezekana kuishi nyumbani kwa muda mrefu sana na ukose kukomaa au kuwa na ujuzi unaohitaji ili kuishi peke yako. Hata hivyo, usiwe na haraka ya kutaka kuondoka nyumbani. Fikiria hilo kwa makini. Methali moja ya Biblia inasema hivi: “Mipango ya mwenye bidii bila shaka huleta faida, lakini kila mtu anayetenda haraka-haraka bila shaka huuelekea uhitaji.” (Methali 21:5) Sikiliza mashauri ya wazazi wako. (Methali 23:22) Sali kuhusu jambo hilo. Na unapofanya uamuzi fikiria kanuni za Biblia zilizozungumziwa katika habari hii.

Swali halipaswi kuwa Je, niko tayari kuondoka nyumbani? bali linapaswa kuwa Je, niko tayari kusimamia nyumba yangu mwenyewe? Ikiwa unaweza kusema ndiyo kwa swali la mwisho, basi huenda uko tayari kuondoka nyumbani.

[Maelezo ya Chini]

a Baadhi ya majina katika makala hii yamebadilishwa.

b Katika tamaduni fulani, ni kawaida kwa watoto, hasa wasichana, kuishi na wazazi wao hadi watakapoolewa. Biblia haitoi mashauri hususa kuhusu jambo hili.

MAMBO YA KUFIKIRIA

● Hata ingawa kuna matatizo katika familia yenu, kuishi nyumbani kwa muda kutakunufaisha jinsi gani?

● Ukiwa nyumbani, ni mambo gani unayoweza kufanya yatakayonufaisha familia yenu na kukusaidia kujitayarisha kuishi peke yako?

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 11]

VIJANA WENZAKO WANASEMA NINI?

“Wazazi wako wanapokupa madaraka, kama yale ungekuwa nayo ikiwa ungekuwa unaishi peke yako, basi kuishi nyumbani ni njia nzuri ya kujifunza jinsi ya kujitegemea baadaye.”

“Ni kawaida kutaka kujitegemea. Lakini ikiwa nia yako ya kuondoka nyumbani ni kuhepa sheria unazowekewa, basi hilo linaonyesha kwamba hauko tayari kuondoka nyumbani.”

[Picha]

Sarah

Aron

[Sanduku katika ukurasa wa 13]

TAARIFA KWA WAZAZI

Serena, aliyetajwa katika habari iliyotangulia, anaogopa kuondoka nyumbani. Kwa nini? Anasema hivi: “Hata ninapotaka kununua kitu kwa kutumia pesa zangu, Baba yangu haniruhusu. Anasema kwamba hiyo ni kazi yake. Kwa hiyo, wazo la kulipia gharama zangu huniogopesha.” Bila shaka, baba ya Serena anafikiri kwamba anafanya jambo linalofaa, lakini je, unafikiri kwamba anamtayarisha binti yake kusimamia nyumba yake mwenyewe?—Methali 31:10, 18, 27.

Je, umewalinda watoto wako kupita kiasi hivi kwamba hawako tayari kuishi peke yao? Utajua jinsi gani ikiwa wako tayari? Ukiwa mzazi, fikiria mambo manne yaliyotajwa katika habari iliyotangulia.

Kupangia matumizi ya pesa. Je, watoto wako wanajua jinsi ya kujaza fomu ya malipo ya kodi au sheria zinazohusiana na kodi? (Waroma 13:7) Je, wanajua jinsi ya kutumia kadi za mkopo vizuri? (Methali 22:7) Je, wanaweza kupanga bajeti na kuifuata? (Luka 14:28-30) Je, wanafahamu faida ya kununua kitu kwa pesa walizofanyia kazi? Je, wamejionea furaha inayopatikana kwa kutumia wakati na mali zao ili kuwasaidia wengine?—Matendo 20:35.

Kazi za nyumbani. Je, binti na wana wako wanajua kupika? Je, umewafundisha jinsi ya kuosha na kupiga nguo pasi? Ikiwa wanajua kuendesha gari, je, wanajua jinsi ya kulirekebisha kwa kufanya mambo madogo kama vile kubadili fyuzi, mafuta, au gurudumu lililotoboka?

Kushirikiana na wengine. Watoto wako wakubwa wanapokosana, je, kila wakati wewe huingilia na kuwatatulia tatizo lao? Au je, umewazoeza kusuluhisha tatizo kwa amani kisha wakueleze jinsi walivyolisuluhisha?—Mathayo 5:23-25.

Ratiba yako ya kiroho. Je, wewe huwaambia watoto wako kile wanachopaswa kuamini, au unawashawishi kuamini? (2 Timotheo 3:14, 15) Badala ya kuwajibu maswali yao kuhusu dini na maadili kila wakati, je, unawafundisha kusitawisha “uwezo wa kufikiri” na ‘kuzoeza nguvu zao za ufahamu kutofautisha yaliyo sawa na yaliyo makosa pia’? (Methali 1:4; Waebrania 5:14) Je, ungependa waige mfano wako wa kujifunza Biblia, au ungependa wawe na ratiba nzuri zaidi?

Bila shaka, kuwazoeza watoto wako katika mambo yaliyotajwa kunahitaji wakati na jitihada nyingi. Lakini jitihada hizo huwa na faida kubwa wakati wanapoondoka nyumbani.

[Picha katika ukurasa wa 12]

Kuondoka nyumbani ni sawa na kutembea msituni—unahitaji kuwa na uwezo wa kujitunza kabla ya kuanza safari

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki