Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Wakristo wa Kweli Wanaheshimu Watu Wenye Umri Mkubwa!
    Mnara wa Mlinzi—1987 | Juni 1
    • Wakristo wa Kweli Wanaheshimu Watu Wenye Umri Mkubwa!

      “WATU wazee,” asema mchunguzi Suzanne Steinmetz, “wako katika mwisho wa maisha yao yenye kutokeza mazao ya kiuchumi, jambo ambalo ndio msingi unaotumiwa na utamaduni wetu kuthamini watu mmoja mmoja na kuheshimu maoni yao, kuwapa cheo, heshima na thawabu mbalimbali.” Hivyo maoni ya jamii ya kisasa juu ya watu wazee-wazee ni yenye kuhuzunisha, yasiyo mazuri. Haishangazi kwamba mara nyingi tunasoma juu ya kutotunzwa kwao na kutendwa vibaya.

      Hata hivyo, Biblia ina maoni gani juu ya watu wazee-wazee? Neno la Mungu linakubali kwa uhakika kwamba kuzeeka si jambo rahisi. Akasali hivi mtunga zaburi: “Usinitupe wakati wa uzee, nguvu zangu zipungukapo usiniache.” (Zaburi 71:9) Katika umri wake wa uzee, wakati huo yeye alihisi uhitaji wa tegemezo la Yehova zaidi ya wakati mwinginewo wote. Maoni ya Biblia ni mazuri katika kuonyesha kwamba sisi, pia, tunapaswa tuyaangalie mahitaji ya watu wazee.

      Kweli, Sulemani aliita umri mzee “siku zilizo mbaya” ambazo katika hizo mtu hangekuwa na “furaha.” (Mhubiri 12:1-3) Lakini “wingi wa siku” unahusianishwa katika Biblia na baraka kutoka kwa Mungu. (Mithali 3:1, 2) Kwa mfano, Yehova alimwahidi Abrahamu: “Lakini wewe . . . utazikwa katika uzee mwema.” (Mwanzo 15:15) Kwa uhakika Mungu hakuwa akimhukumia Abrahamu mwaminifu “siku zilizo mbaya” zisizo na tumaini, ambazo katika hizo yeye hangekuwa na “furaha.” Abrahamu alipata amani na utulivu katika miaka yake ya baadaye, akitazama nyuma kwa kuridhika na maisha aliyokuwa ametumia katika utumishi wa Yehova. Yeye angeweza pia kutazama mbele kwenye “mji wenye misingi ya kweli,” Ufalme wa Mungu. (Waebrania 11:10) Hivyo yeye angeweza kufa ‘katika uzee mwema akiwa ameshiba siku.’​—Mwanzo 25:8.

      Basi, mbona Sulemani aliuita uzee “siku zilizo mbaya”? Sulemani alielekeza kwenye kuchakaa kugumu sana kwa afya kunakotokea katika uzee. Hata hivyo, mtu yule aliyeshindwa ‘kumkumbuka Muumba wake siku za ujana wake’ anaipata miaka yake yenye kupunguka kuwa mibaya sana. (Mhubiri 12:1) Kwa sababu amepoteza maisha yake, mtu mzee kama huyo ‘hana furaha’ katika siku zake za baadaye za maisha. Njia yake ya maisha isiyo ya kimungu huenda hata ikawa imetokeza matatizo ya kimwili ambayo yanaongezea maumivu ya uzeeni. (Linganisha Mithali 5:3-11.) Hivyo anapotazama mbele, haoni akiwa na wakati ujao isipokuwa kaburi. Yule ambaye ametoa maisha yake kumtumikia Mungu anaona pia “siku zilizo mbaya” mwili wake unapodhoofika. Lakini kama Abrahamu, anaweza kupata furaha na uradhi katika maisha ambayo yalitumiwa vizuri na katika kutumia nguvu zake zinazobaki katika utumishi wa Mungu. “Kichwa chenye mvi ni taji ya uzuri wa sura wakati kunapopatikana katika njia ya uadilifu,” yasema Biblia.—Mithali 16:31, NW.

      Kwa kweli, hata uzee una faida fulani. “Ujana ni ubatili, na utu uzima pia,” akasema Sulemani. Ingawa vijana wanaweza kufurahia afya ya nguvu nyingi, mara nyingi wao hawa-na ujuzi wa maisha wala maamuzi mazuri. Ingawaje, uzee unaambatana na muda wa maisha ya kujionea mambo. Mtu aliye mzee-mzee ‘anauondolea mbali ubaya,’ tofauti na kijana anayesisimuka bila kufikiri ambaye mara nyingi anajitupa ndani moja kwa moja. (Mhubiri 11:10; 2 Timotheo 2:22) Kwa sababu hiyo, Sulemani angeweza kusema: “Fahari ya vijana ni nguvu zao, na uzuri wa wazee ni kichwa chenye mvi.”—Mithali 20:29.

      Basi Biblia inaheshimu watu wazee-wazee! Jambo hilo lina matokeo gani juu ya njia ambayo Wakristo wanashughulika nao?

      ‘Kuondokea’ Watu Wazee-Wazee

      Mungu alifanya heshima kwa wazee katika Israeli liwe shauri la kitaifa. Sheria ya Musa ilieleza: “Mwondokeeni mtu mwenye mvi; heshimuni uso wa mtu mzee.” (Walawi 19:32) Kwa wazi Wayahudi katika miaka ya baadaye walichukua sheria hii kwa njia halisi kabisa. Anasema Dakt. Samuel Burder katika kitabu chake Oriental Customs: “Waandikaji wa Kiyahudi wanasema kwamba amri ilikuwa, kuinuka wakiwa umbali wa dhiraa nne; na mara tu walipopita, kuketi tena, ili ionekane kwamba wenye kuinuka walifanya hivyo kwa sababu ya kuwaheshimu hasa.” Si watu mashuhuri peke yao walioonyeshwa heshima hiyo. “Heshimu hata mwanamume mzee ambaye ameishiwa na masomo aliyokuwa nayo,” ikatangaza Talmudi. Rabi mmoja alibisha kwamba heshima hii lazima itie ndani pia wanaume wazee wasio na maarifa na wasio na elimu. Yeye alitoa sababu ya kwamba “kuzeeka kwake kwenyewe lazima kuwe kuliwezekana kwa sababu ya ustahili fulani.”—The Jewish Encyclopedia.

      Leo Wakristo hawako chini ya wajibu wa kufuata Sheria ya Musa. (Warumi 7:6) Lakini jambo hili halimaanishi kwamba hawana tena wajibu wa kuwaonyesha watu wazee heshima ya pekee. Jambo hili linaonekana wazi kutokana na maagizo ambayo mtume Paulo alimpa mwangalizi Mkristo aliyeitwa Timotheo: “Usichambue vikali mwanamume mwenye umri mkubwa. Tofauti na hivyo, msihi kama baba . . . wanawake wenye umri mkubwa kama akina mama.” (1 Timotheo 5:1, 2, NW) Paulo alimwambia kijana Timotheo kwamba alikuwa na mamlaka ya ‘kuamuru.’ (1 Timotheo 1:3, NW) Hata hivyo, ikiwa mtu mwenye umri mkubwa kuliko yeye—hasa mmoja ambaye alikuwa anatumikia kama mwangalizi—alikosea katika hukumu au alisema neno lisilo sahihi, Timotheo hakupaswa ‘kumchambua vikali’ kama mdogo wake. Badala yake, kwa heshima alipaswa ‘amsihi kama baba.’ Timotheo alihitaji kuonyesha heshima inayofanana na hiyo kwa wanawake wenye umri mkubwa katika kundi. Ndiyo, kwa maana, angali ‘angemwondokea mtu mwenye mvi’!

      Hivyo Ukristo ni dini ambayo inawaheshimu watu wazee-wazee. Ingawaje, kinyume cha hivyo ni kwamba kadiri kubwa ya kuwatenda vibaya watu wenye umri mkubwa inatukia katika mataifa yanayojidai kuwa ya Kikristo. Hata hivyo, kuna waabudu ambao wangali wanashikilia viwango vya Biblia. Kwa mfano, Mashahidi wa Yehova wanafurahia kuwapo kwa maelfu ya watu wazee-wazee miongoni mwao. Wao hawawaoni kuwa mzigo au watu wa hasara tu. Kwa kuwa ingawa afya dhaifu inaweza kuwazuia watu hao wenye umri mkubwa wasiwe watendaji kama walivyokuwa wakati fulani, wengi wameacha nyuma kumbukumbu ndefu za utumishi mwaminifu wa Kikristo. Jambo hili linawatia moyo vijana Mashahidi ‘kuiiga imani yao.’—Waebrania 13:7.

      Hata hivyo, watu wazee-wazee hawatazamiwi wakae kitako tu katika kundi. Wao wanahimizwa waweke mifano bora katika kuwa “wenye kiasi, wenye kuchukua mambo kwa uzito, timamu katika akili, wenye afya katika imani . . . wenye kicho katika kujiendesha,” wakigawia wengine kwa uhuru hekima waliyo nayo na mambo waliyoona. (Tito 2:2, 3, W) Yoeli alitoa unabii kwamba miongoni mwa ‘wenye kutoa unabii,’ au kushiriki katika utangazaji wa ujumbe wa Biblia, kungekuwako na “wanaume wazee.” (Yoeli 2:28, NW) Bila shaka wewe binafsi umeona kwamba Mashahidi wengi wazee-wazee wangali wanafurahia kushiriki kwa bidii katika utendaji wa kuhubiri nyumba kwa nyumba.

      Kuwaonyesha Heshima kwa ‘Kuzidi Sana’

      Kwa njia nyingi Mashahidi wa Yehova wanajitahidi kuelekeza fikira za pekee kwa watu wenye umri mkubwa. Kwa mfano, kwenye mikusanyiko ya kidini ya kila mwaka, mara nyingi wanapanga ili wenye umri mkubwa wawekewe viti watakavyokalia. Wanaelekezewa fikira pia wakiwa mmoja mmoja. Katika Japani, Shahidi mmoja anaiacha nafasi ambayo angekalia katika gari la jamaa ili mwanamke wa miaka 87 aweze kupelekwa kwenye mikutano ya kundi. Yeye mwenyewe anafikaje kwenye mikutano? Kwa baiskeli. Katika Brazili kuna mwevanjeli wa wakati wote mwenye umri wa miaka 92. Watazamaji wanaripoti kwamba Mashahidi wa huko “wanamtendea kwa heshima, wanazungumza naye . . . mwanamume huyo ni sehemu yenye mafaa katika kundi.”

      Jambo hili halimaanishi kwamba hakuna nafasi ya kufanyia maendeleo katika kuwaheshimu watu wenye umri mkubwa. Paulo aliwaandikia Wakristo katika Thesalonike: “Katika habari ya upendano, . . . mnafanya neno hili kwa ndugu wote walio katika Makedonia yote. Lakini twawasihi, ndugu, mzidi sana.” (1 Wathesalonike 4:9, 10) Shauri linalofanana na hilo linahitajiwa leo kuhusu jinsi tunavyotendea watu wenye umri mkubwa. Kwa mfano, Mkristo mmoja mwenye umri wa miaka 85 alivunjika moyo wakati hakupokea kichapo kipya cha Kibiblia. Tatizo lilikuwa nini? Yeye ni karibu kiziwi na hakusikia tangazo likikumbusha kila mtu aagize kitabu hicho; wala hakuna mtu katika kundi aliyefikiria kumwagizia. Bila shaka, hali hiyo ilirekebishwa upesi. Hata hivyo, inaonyesha kuna uhitaji wa kujua sana mahitaji ya watu wenye umri mkubwa.

      Kuna njia nyingi ambazo katika hizo watu wa Mungu leo wanaweza kufanya hivyo kwa ‘kuzidi sana.’ Mikutano ya Kikristo inatoa nafasi ya ‘kuwahimiza’ wenye umri mkubwa “katika upendo na kazi nzuri.” (Waebrania 10:24, 25) Na ingawa vijana na watu wazee wanachangamana kwa uhuru katika Majumba ya Ufalme ya Mashahidi wa Yehova, labda hata jitihada zaidi zinaweza kufanywa katika jambo hilo. Kwa mfano, wazazi fulani sasa wanawatia moyo watoto wao kuwakaribia kwa heshima na kuzungumza na washiriki wenye umri mkubwa wa kundi.

      Heshima pia inaweza kuendelea kuonyeshwa kwa watu wazee-wazee kwa njia zisizopangwa rasmi. Kupatana na kanuni ambayo Yesu aliweka katika Luka 14:12-14, jitihada zaidi inaweza kufanywa kualika watu wenye umri mkubwa kwenye vikusanyiko vya starehe. Hata ikiwa hawawezi kuhudhuria, hakika watafurahia kwamba uliwakumbuka. Wakristo wanasihiwa zaidi ‘waufuate mwendo wa ukaribishaji.’ (Warumi 12:13, NW) Ukaribishaji huo hauhitaji uwe na mambo makubwa au madoido mengi. Anadokeza hivi Shahidi mmoja kutoka Ujeremani: “Waalike wenye umri mkubwa wanywe kikombe cha chai, na uache waeleze mambo waliyoyaona kibinafsi nyakati zilizopita.”

      Mtume Paulo alisema: “Katika kuonyeshana heshima iweni wa kwanza.” (Warumi 12:10, NW) Miongoni mwa Mashahidi wa Yehova, wazee wa kundi waliowekwa rasmi ndio hasa wanaokuwa wa kwanza katika kuonyesha heshima kwa Wakristo wazee-wazee. Mara nyingi wazee wanaweza kuwapa watu wenye umri mkubwa kazi zinazofaa ili wazifanye, kama vile kuwazoeza wapya wawe waeneza evanjeli au kusaidia na kazi ya kutengeneza vitu vilivyoharibika mahali pa mikutano ya Kikristo (panapoitwa Majumba ya Ufalme). Wanaume vijana wanaotumikia wakiwa wazee wa kundi wanawaonyesha heshima waangalizi wenye umri mkubwa kwa kuwakaribia kwa unyenyekevu wawape shauri, wakitumia utambuzi ili wachote maoni yao yaliyokomaa. (Linganisha Mithali 20:5.) Katika mikutano ya wazee wa namna hiyo, wanafuata mfano wa Kibiblia wa kijana Elihu na kwa heshima wanawaondokea wanaume wenye umri mkubwa, wenye maarifa zaidi, wakiwapa nafasi kamili ya kuyaeleza maoni yao kwanza.—Ayubu 32:4.

      Inakubalika kwamba, ni rahisi kutovumilia watu wazee-wazee kwa sababu hawawezi kwenda au kufikiri upesi kama vile vijana wanavyofanya. Dakt. Robert N. Butler anaeleza vizuri baadhi ya matatizo ambayo uzee unaleta: “Mmoja anapoteza nguvu zake za kimwili, uwezo wa kufanya mambo kwa mwendo wake wa zamani, na jambo hilo lenyewe laweza kuwa lenye kuogofya sana. Mmoja anaweza kupoteza hisia za maana kama vile kusikia au kuona.” Wakithamini jambo hilo, je! vijana hawapaswi kuonyesha hisia-mwenzi na huruma?—1 Petro 3:8.

      Ndiyo, Wakristo wa kweli leo wana wajibu wa kuwaonyesha watu wa umri mkubwa walio miongoni mwao upendo, hangaiko, na heshima ya kweli. Na miongoni mwa Mashahidi wa Yehova, jambo hilo linafanywa kwa njia iliyo mfano mwema. Ingawaje, ni jambo gani linalotukia wakati Wakristo wazee-wazee—au wazazi wa Wakristo—wanapokuwa wagonjwa au maskini? Ni daraka la nani kuwatunza? Makala zinazofuata zitachunguza-chunguza jinsi Biblia inavyojibu maulizo hayo.

  • ‘Kuendelea Kuangalia’ Masilahi za Watu Wazee-Wazee
    Mnara wa Mlinzi—1987 | Juni 1
    • ‘Kuendelea Kuangalia’ Masilahi za Watu Wazee-Wazee

      “Mkiendelea kuangalia, si masilahi ya kibinafsi juu ya mambo yenu wenyewe tu, bali pia masilahi ya kibinafsi juu ya mambo yale ya wengine.”​—WAFILIPI 2:4, NW.

      1, 2. (a) Baraza linaloongoza ya karne ya kwanza lilionyeshaje kuhangaishwa na mahitaji ya wazee-wazee? (b) Kuna ushuhuda gani kwamba kazi ya kuhubiri haikuachwa?

      MUDA mfupi baada ya Pentekoste 33 W.K. katika kundi la Kikristo “nung’uniko lilitokea kwa upande wa Wayahudi wasema-Kigiriki dhidi ya Wayahudi wasema-Kiebrania, kwa sababu wajane wao walikuwa wakipitwa bila kuangaliwa katika ugawaji wa kila siku [wa chakula kwa wahitaji].” Bila shaka hesabu fulani ya wajane hao walikuwa wazee-wazee na hawangeweza kujitunza wenyewe. Kwa kadiri yo yote, mitume wenyewe waliingilia jambo hili, wakiagiza: “Jitafutieni wanaume saba waliothibitishwa kuwa wanafaa kutoka miongoni mwenu, wenye kujaa roho na hekima, ili tupate kuwaweka rasmi juu ya hii shughuli inayohitajiwa kabisa.”​—Matendo 6:1-3, NW.

      2 Hivyo Wakristo wa kwanza waliliona jambo la kutunza wahitaji kama “shughuli inayohitajiwa kabisa.” Miaka mingi baadaye mwanafunzi Yakobo aliandika: “Dini iliyo safi, isiyo na taka mbele za Mungu Baba ni hii, Kwenda kuwatazama yatima na wajane katika dhiki yao, na kujilinda na dunia pasipo mawaa.” (Yakobo 1:27) Basi je! jambo hili lilimaanisha kwamba kazi ya kuhubiri iliyo ya maana kupita zote ilikuwa imeachiliwa? La, kwa sababu usimulizi katika Matendo unasema kwamba kazi ya kuwapa wajane msaada ilipokwisha kupangwa ifaavyo, “neno la Mungu likaenea; na hesabu ya wanafunzi ikazidi sana katika Yerusalemu.”​—Matendo 6:7.

      3. Ni kitia-moyo kipi kinachotolewa katika Wafilipi 2:4, na kwa sababu gani kinafaa sana leo?

      3 Leo tunakabili “nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo.” (2 Timotheo 3:1, 2 NW) Kuyatunza mahitaji ya maisha ya jamaa na kazi ya kimwili huenda kukatuachia nishati kidogo—au tamaa—ya kujishughulisha na mahitaji ya watu wazee-wazee. Kwa kufaa, basi, Wafilipi 2:4 inatuhimiza sisi ‘tusiangalie mambo yetu wenyewe, bali kila mtu aangalie mambo ya wengine.’ Jambo hilo linaweza kufanywaje katika njia iliyosawazika, yenye mafaa?

      Kuwaheshimu Wajane

      4. Kundi la karne ya kwanza ‘liliwaheshimuje’ wajane? (b) Je! maandalizi kama hayo yalihitajiwa kabisa sikuzote?

      4 Katika 1 Timotheo sura ya 5, Paulo anaonyesha jinsi Wakristo wa kwanza walivyowatunza wajane wazee-wazee katika kundi. Yeye alimhimiza Timotheo hivi: “Uwaheshimu wajane walio wajane kweli kweli.” 1 Timotheo 5(mstari 3) Wajane wazee-wazee walichaguliwa kama wenye uhitaji hasa wa kupokea heshima ikiwa kwa namna ya kupewa tegemezo la fedha kwa ukawaida. Wao walikuwa wamekatiliwa mbali kutoka njia zote zenye kuonekana za kujitegemeza na wangeweza tu ‘kumwekea Mungu tumaini lao, na kudumu katika maombi na sala mchana na usiku.’ (mstari 5) Sala zao za kutaka riziki zilijibiwaje? Kupitia kundi! Katika njia iliyopangwa kitengenezo, wajane waliostahili waliandaliwa riziki ya kiasi. Bila shaka, ikiwa mjane alikuwa na fedha au watu wa ukoo wenye kuweza kumpa tegemezo, maandalizi hayo hayakuhitajiwa kabisa.​—1 Timotheo 5mistari 4, 16.

      5. (a) Huenda ikawa wajane wengine ‘wameingilia kutafuta utoshelezaji wa hisia’ kwa njia gani? (b) Je! kundi lilikuwa na wajibu wa kuwategemeza hao?

      5 “Lakini yule [mjane] anayeingilia kutafuta utoshelezaji wa hisia,” akatahadharisha Paulo, “amekufa [kiroho] ingawa anaishi.” 1 Timotheo 5(mstari 6, NW) Paulo haelezi vile wengine walivyokuwa ‘wakijiendesha kwa kuamsha hisia,’ kama vile Biblia ya Kingdom Interlinear inavyofasiri maneno hayo kwa uhalisi. Huenda ikawa wengine walikuwa na pigano la kupambana na ‘nyege zao.’ 1 Timotheo 5(mstari 11, NW) Hata hivyo, kulingana na Liddell & Scott’s Greek-English Lexicon, ‘kujiendesha kwa kuamsha hisia’ kungaliweza kuwa kulitia ndani ‘kuishi kwa kujilegeza au katika starehe au anasa ya kupita kiasi.’ Labda, basi, wengine walitaka kundi liwatajirishe; ligharimie maisha ya kutapanya vitu, ya kujitia katika anasa nyingi na yasiyo na kiasi. Vyo vyote ilivyokuwa, Paulo anaonyesha kwamba wajane wa namna hiyo waliondolewa ustahili wa kupokea tegemezo la kundi.

      6, 7, na maelezo yaliyo chini. (a) ‘Kuandikwa katika orodha’ kulikuwa nini? (b) Kwa sababu gani wale ambao walikuwa chini ya umri wa miaka 60 walikosa kupokea tegemezo hilo? (b) Paulo alizuiaje wajane vijana wasipokee “hukumu” kali?

      6 Ndipo Paulo akasema: “Mjane asiandikwe [kati ya wale wenye kupokea tegemezo la kifedha] isipokuwa umri wake amepata miaka sitini.” Katika siku za Paulo mwanamke aliyekuwa na umri zaidi ya 60 kwa wazi alionwa kuwa hawezi kujitegemeza mwenyewea na haikuelekea kwamba wangeolewa tena. “Kwa upande ule mwingine,” Paulo akaagiza, “uwakatalie wajane wenye umri mdogo [wasiandikwe katika orodha] kwa maana wakati nyege zao zimekuja kati yao na Kristo, wao wanataka kuolewa, wakiwa na hukumu kwa sababu wamepuuza wonyesho wao wa kwanza wa imani.”​—1 Timotheo 5Mistari 9, 11, 12, NW.

      7 Kama wajane wenye umri mdogo wangalikuwa wameruhusiwa kuandikwa katika “orodha,” labda wengine wangalitangaza haraka haraka nia ya kubaki wakiwa waseja. Wakati ulipopita, ingawa hivyo, labda wengine wangalipata tatizo la kuzuia “nyege” zao watake kuolewa tena, ‘wakiwa na hukumu kwa kupuuza wonyesho wao wa kwanza wa imani’ wa kubaki wakiwa waseja. (Linganisha Mhubiri 5:2-6.) Paulo alizuia matatizo kama hayo, kwa kutangaza zaidi kwamba, “napenda wajane, ambao si wazee, waolewe, wazae watoto.”​—1 Timotheo 5Mstari 14.

      8. (a) Miongozo ya Paulo ilililindaje kundi? (b) Je! wajane vijana na wanaume wazee-wazee wenye uhitaji walitunzwa pia?

      8 Mtume Paulo pia aliweka mpaka ili wenye kuandikwa orodhani wawe ni wale tu waliokuwa wametenda kwa muda mrefu kazi bora za Kikristo. 1 Timotheo 5(mstari 10) Hivyo kundi halikuwa ‘makao ya kutunza masilahi’ ya watu wavivu na wenye pupa. (2 Wathesalonike 3:10, 11) Lakini namna gani wanaume wazee-wazee au wajane wenye umri mdogo? Ikiwa wao wangetumbukia katika uhitaji, bila shaka kundi lingaliwatunza kama mtu mmoja mmoja.—Linganisha 1 Yohana 3:17, 18.

      9. (a) Kwa sababu gani mipango ya kutunza wazee-wazee leo inatofautiana na ile iliyofanywa katika karne ya kwanza? (b) Mazungumzo ya Paulo juu ya wajane katika 1 Timotheo sura ya 5 yanatusaidia tuthamini nini leo?

      9 Inaelekea mipango hiyo iliyatoshelea mahitaji ya makundi ya karne ya kwanza. Lakini kama vile The Expositor’s Bible Commentary kinavyoonelea: “Kwa vile leo kuna mapato ya bima, mpango wa kiserikali wa kusaidia wenye shida, na nafasi za kazi, hali hiyo ni tofauti sana.” Kwa sababu ya badiliko la hali za kijamii na kiuchumi, ni mara chache sana leo makundi yatakapohitajika kabisa kudumisha orodha zenye majina ya wafadhiliwa wazee-wazee. Hata hivyo, maneno ya Paulo kwa Timotheo yanatusaidia tuthamini kwamba: (1) Matatizo ya walio wazee-wazee yanahangaisha kundi lote—hasa wazee. (2) Utunzaji wa walio wazee-wazee unapasa upangwe vizuri kitengenezo. (3) Utunzaji wa namna hiyo unawekewa mpaka uwe wa wale tu ambao kweli wana uhitaji.

      Wazee ‘Kuendelea Kuangalia Masilahi Zao’

      10. Wazee leo wanaweza kuongozaje katika kuonyesha wanapendezwa kujua hali ya wenye umri mkubwa?

      10 Waangalizi leo wanaongozaje katika kuonyesha wanapendezwa kujua hali ya watu wenye umri mkubwa? Mara kwa mara wanaweza kupanga mahitaji ya wazee-wazee katika orodha ya mambo yanayokusudiwa kuzungumzwa kwenye mikutano yao. Msaada halisi unapohitajiwa, wao wanaweza kupanga ili utolewe. Huenda wao binafsi wasitoe utunzaji huo, kwa kuwa mara nyingi kuna wengi wenye nia—kutia na vijana—katika kundi ambao wanaweza kusaidia. Hata hivyo, wao wanaweza kusimamia utunzaji huo kwa ukaribu, labda kwa kumpa ndugu mmoja mgawo wa kusawazisha utunzaji ambao mtu fulani anapewa na watu mbalimbali.

      11. Wazee wanaweza kujifahamishaje na mahitaji ya wazee-wazee?

      11 Sulemani alishauri hivi: “Fanya bidii kuijua hali ya makundi yako.” (Mithali 27:23) Hivyo waangalizi wanaweza kuwatembelea wazee-wazee kibinafsi ili waamue njia iliyo bora zaidi ya ‘kugawana . . . kulingana na mahitaji yao.’ (Warumi 12:13, NW) Mwangalizi anayesafiri alieleza jambo hilo hivi: “Wazee-wazee fulani wanajitegemea sana, na si vizuri kuwauliza tu ni jambo gani linahitaji kufanywa. Jambo bora zaidi ni kutambua jambo linalohitaji kufanywa na kuanza moja kwa moja kuwafanyia kazi hiyo!” Katika Japani waangalizi fulani walipata kwamba dada mmoja mwenye umri wa miaka 80 alihitaji kuangaliwa sana. Wao wanaripoti: “Sasa tunahakikisha kwamba mtu fulani anakuwa naye mara mbili kwa siku, asubuhi na usiku, kwa kumtembelea au kumpigia simu.”—Linganisha Mathayo 25:36.

      12. (a) Wazee wanaweza kuhakikishaje kwamba wazee-wazee wananufaika kutokana na mikutano ya kundi? (b) Ni matumizi gani mazuri yanayoweza kufanywa kutokana na kanda za kunasa sauti ambazo zimetolewa na Sosaiti?

      12 Waangalizi pia wanaweza kushughulika kuona kwamba wazee-wazee wananufaika kutokana na mikutano ya kundi. (Waebrania 10:24, 25) Je! wengine wanahitaji njia ya kusafiri? Je! wengine wanakosa ‘kusikiliza na kufahamu’ mikutano kwa sababu ya kupungukiwa nguvu za kusikia? (Mathayo 15:11) Labda ingefaa kuwawekea chombo cha kusaidia kusikia. Vivyo hivyo, hesabu fulani ya makundi zina njia ya kupitisha mikutano katika simu ili wenye vizuizi vya kimwili waweze kusikiliza wakiwa nyumbani. Wengine wanairekodi mikutano yao katika kanda za kunasia sauti kwa ajili ya wale ambao ni wagonjwa sana hivi kwamba hawawezi kuhudhuria—katika visa vingine wakiwanunulia vyombo vyenyewe vya unasaji sauti. Na kuhusu kanda za kunasia sauti, mzee mmoja katika Ujeremani alionelea hivi: “Nimetembelea watu kadha wazee-wazee ambao waliketi tu mbele ya televisheni na kutazama vipindi ambavyo hata haviwezwi kuelezwa kuwa vyenye kujenga kiroho.” Badala yake mbona msiwatie moyo wasikilize kanda za kaseti zinazotolewa na Sosaiti, zilizo na midundo mitamu ya Ufalme na usomaji wa Biblia?

      13. Wenye umri mkubwa wanaweza kusaidiwaje kuwa watendaji wakiwa watangazaji wa Ufalme?

      13 Washiriki fulani wa kundi wenye umri mkubwa wamekuwa wahubiri wasio wa kawaida au wasiotenda. Ingawa hivyo, kwa lazima uzee hauzuii mtu asiwe mtangazaji wa “habari njema ya ufalme.” (Mathayo 24:14) Huenda wengine wakaitikia mwaliko kidogo tu wa kufanya kazi pamoja nawe shambani. Labda wewe unaweza kuamsha upendo wao wa kuhubiri kwa kushiriki nao mambo yaliyoonwa katika utumishi wa shambani. Ikiwa kupanda ngazi ni tatizo, fanya mpango ili wafanye kazi katika nyumba zisizo na ngazi. Wahubiri wengine wanaweza kuwakaribisha wazee-wazee wajiunge nao katika mafunzo ya Biblia​—au wafanye funzo hilo katika nyumba ya mzee-mzee huyo.

      14 na sanduku. (a) Wazee wanaweza kufanyaje ikiwa ndugu mzee-mzee anatumbukia katika shida kubwa ya kifedha? (b) Makundi mengine yamejitoaje kutimiza mahitaji ya wahubiri wazee-wazee?

      14‘Fedha ni ulinzi.’ (Mhubiri 7:12) Hata hivyo, ndugu au dada wengi wazee wana shida kubwa sana ya kifedha na hawana watu wa ukoo ambao wana nia ya kusaidia. Ingawa hivyo, watu mmoja mmoja katika kundi mara nyingi wana furaha ya kusaidia wanapojulishwa uhitaji huo. (Yakobo 2:15-17) Wazee wanaweza pia kuchunguza waone kunapatikana utumishi gani wa serikali kusaidia wenye shida, mipango ya bima, malipo ya waliostaafu, na kadhalika. Hata hivyo, katika nchi nyingine, utumishi kama huo ni mgumu kupatikana, na huenda ikawa hakuna jambo jingine la kufanya isipokuwa kufuata kiolezo kilicho katika 1 Timotheo sura ya 5 na kupanga ili kundi zima litoe msaada. (Ona Tumefanywa Tengenezo Kutimiza Huduma Yetu, kurasa 122, 123.)

      Wahubiri katika Naijeria walimsaidia kwa ukawaida painia wa kawaida mwenye umri wa miaka 82 pamoja na mke wake kwa kuwapa zawadi za kimwili. Baada ya serikali, kuratibu kwamba jengo waliloishi ndani yalo lingebomolwea, kundi liliwaalika wahamie katika chumba kimoja kilichofungamana na Jumba la Ufalme mpaka mahali pengine pa kuishi paweze kupangwa.

      Katika Brazili kundi moja lilikodi mwuguzi wa kike ili awatunze mume na mke wazee-wazee. Wakati ule ule, dada mmoja alipewa mgawo wa kutunza nyumba iwe safi, kutayarisha chakula chao, na kutunza mahitaji yao mengine ya kimwili. Kila mwezi kundi linaweka akiba ya fedha kwa matumizi yao.

      15. (a) Je! kuna mipaka kuhusu msaada ambao kundi linaweza kutoa? (b) Shauri lililo katika Luka 11:34 linaweza kuwafaaje watu fulani wanaokuwa wenye kudai mno?

      15 Kama vile ilivyokuwa katika karne ya kwanza, maandalizi kama hayo ni kwa wale wanaostahili na wanaoyahitaji kweli kweli. Waangalizi hawana wajibu wa kushughulikia maombi yanayopita kiasi au kushughulikia madai yasiyo ya kiakili. Ni lazima pia wazee-wazee waendelee kuwa na ‘jicho rahisi.’​—Luka 11:34, NW.

      ‘Watu Mmoja Mmoja ‘Kuendelea Kuangalia Masilahi Zao’

      16, 17. (a) Kwa sababu gani ni jambo la maana kwa wengine kundini zaidi ya wazee kupendezwa na watu wazee-wazee? (b) Wahubiri wenye shughuli wanawezaje ‘kuukomboa wakati’ kwa ajili ya wazee-wazee?

      16 Wakati fulani uliopita dada mmoja mzee-mzee alilazwa hospitalini. Uchunguzi ulionyesha kwamba alikosa chakula kinachoufaa mwili. “Kama wengi kundini wangependezwa naye kibinafsi,” akaandika mzee mmoja, “labda jambo hilo halingetukia.” Ndiyo, si wazee peke yao wanaopaswa kuwatunza watu wazee-wazee. Paulo aliandika: “Kwa maana tu viungo, kila mmoja kiungo cha wenzake.”​—Waefeso 4:25.

      17 Bila shaka wengine wenu tayari mna mizigo ya madaraka ya kibinafsi. Lakini ‘endelea kuangalia, si masilahi ya kibinafsi juu ya mambo yako mwenyewe tu.’ (Wafilipi 2:4, NW) Kwa mpango mzuri, mara nyingi unaweza ‘kununua wakati.’ (Waefeso 5:16, NW) Kwa mfano, je! wewe unaweza kutembelea mmoja aliye mzee-mzee baada ya utumishi wa shambani? Mara nyingi siku za kati ya juma zinakuwa zenye upweke kwa wengine. Matineja, pia, wanaweza kuhusika katika kutembelea na kuwafanyia kazi wazee-wazee. Akasali dada mmoja aliyesaidiwa na kijana: “Asante Yehova kwa Ndugu kijana John. Yeye ni mtu mzuri sana.”

      18. (a) Kwa sababu gani nyakati nyingine maongezi pamoja na mzee-mzee yanaweza kuwa magumu? (b) Mtu anaweza kufanyaje ziara au maongezi pamoja na ndugu mwenye umri mkubwa yawe yenye kuwajenga wote wawili?

      18 Katika mikutano, wewe unawapa walio na umri mkubwa salamu ya juu-juu tu? Ni kweli kwamba huenda ikawa si jambo rahisi kuzungumza pamoja na mtu ambaye hasikii kwa wepesi au ana tatizo la kujieleza mwenyewe. Na kwa kuwa afya yenye kudhoofika polepole inatatiza sana pia, si wazee-wazee wote walio na maelekeo ya kuwa wachangamfu. Ijapokuwa hivyo, “afadhali mtu mwenye subira.” (Mhubiri 7:8, AW) Kwa kujitahidi kidogo, “mbadilishano wa kitia-moyo” halisi unaweza kutokea. (Warumi 1:12, NW) Jaribu kueleza jambo lililoonwa katika utumishi wa shambani. Shiriki nao jambo ulilosoma katika Mnara wa Mlinzi au Amkeni! Hata hivyo jambo bora zaidi ni kusikiliza. (Linganisha Ayubu 32:7.) Watu wenye umri mkubwa wana mambo mengi ya kushiriki ukiwaruhusu wafanye hivyo. Akakiri hivi mzee mmoja: “Kumtembelea ndugu yule mzee mwenye umri kulinifaidi sana.”

      19. (a) Hangaiko letu kwa wazee-wazee linanyooshwa kwa akina nani? (b) Ni nini baadhi ya njia tunazoweza kuthibitisha kwamba sisi tunasaidia jamaa ambazo zinawatunza wazazi wenye umri mkubwa?

      19 Je! hangaiko lako kwa wazee-wazee halipasi linyooshwe lihusu pia jamaa zinazowatunza? Mume na mke wanaotunza wazazi wanaoendelea kuzeeka waliripoti: “Badala ya kututia moyo sisi, wengine kundini wamekuwa wenye kulaumu-laumu. Dada mmoja alisema: ‘Mkiendelea kukosa mikutano, mtakuwa wagonjwa kiroho!’ Lakini yeye hakuwa na nia ya kufanya jambo lo lote kutusaidia sisi tufike kwenye mikutano.” Zenye kuvunja moyo pia ni ahadi zinazotolewa bila uhakika kamili (‘Ukihitaji msaada wakati wo wote, nijulishe.’), ambazo mara nyingi zinakuwa kama kusema, ‘Ukaote moto na kushiba.’ (Yakobo 2:16) Ingekuwa vizuri zaidi kuacha hangaiko lako lionekane kwa kitendo! Wanaripoti hivi wenzi wawili waliooana: “Akina rafiki wamekuwa wazuri sana na wenye kutegemeza! Wengine wanaweza kumtunza Mama kwa siku kadha mfululizo ili kwamba nasi tupate pumziko pindi kwa pindi. Wengine wanampeleka kwenye mafunzo ya Biblia. Na inatutia moyo sana wakati wengine wanapouliza juu ya hali yake.”

      20, 21. Wenye umri mkubwa wanaweza kufanya nini ili wasaidie wale ambao wanawapa utunzaji?

      20 Kwa kadiri kubwa watu wenye umri mkubwa kati yetu wanatunzwa vizuri. Hata hivyo, Mashahidi wazee-wazee wanaweza kufanya nini wao wenyewe ili kwamba kazi hii ifanywe “kwa furaha wala si kwa kuugua”? (Linganisha Waebrania 13:17.) Mshirikiane na mipango ambayo wazee wanafanya kwa utunzaji wenu. Onyesheni shukrani na uthamini kwa matendo yo yote ya wema yanayofanywa na mwepuke kuwa wenye kudai mno au wenye kulaumu-laumu mno. Na ijapokuwa maumivu na uchungu wa uzee ni halisi, jaribuni kuonyesha mwelekeo wa uchangamfu, wa kutazamia mazuri.​—Mithali 15:13.

      21 Wengi wenye umri mkubwa wamesikiwa wakisema hivi, ‘Akina ndugu ni wazuri sana. Sijui ningefanya nini bila wao.’ Hata hivyo, daraka kubwa la kuwatunza wazee-wazee ni la watoto wao. Hili linatia ndani nini, na mwito huo wa ushindani unaweza kukabiliwaje katika njia nzuri?

      [Maelezo ya Chini]

      a Walawi 27:1-7 linataja umri wa miaka 60 linapozungumza juu ya watu mmoja mmoja ‘waliotolewa kama mchango’ hekaluni (kwa kufanya nadhiri) wawe wafanya kazi. Bei ya kukombolewa ilitofautiana kulingana na umri. Kwenye umri wa miaka 60 bei hiyo ilianguka sana, inaonekana kwa sababu mtu mzee hivyo alionwa kuwa asiyeweza kufanya kazi kwa nguvu kama mtu mwenye umri mdogo. The Encyclopedia Judaica inaongezea hivi: “Kulingana na Talmudi, uzee . . . unaanzia miaka 60.”

      Je! Wewe Unakumbuka?

      ◻ Ni maandalizi gani yaliyofanywa katika karne ya kwanza kwa wajane wazee-wazee?

      ◻ Waangalizi wanaweza kupangaje utunzaji wa watu wenye umri mkubwa katika kundi?

      ◻ Watu mmoja mmoja katika kundi wanaweza kuonyeshaje upendezi katika ndugu na dada wazee-wazee?

      ◻ Watu wenye umri mkubwa wanaweza kufanya jambo gani ili wawasaidie wale wanaowatunza?

      [Sanduku katika ukurasa wa 11]

      Kuwasaidia Wazee-Wazee​—Yale Ambayo Wengine Wanafanya

      Kundi moja katika Brazili lilipata njia inayofaa ya kuyatunza mahitaji ya kimwili ya ndugu mmoja anayeishi karibu na Jumba la Ufalme lao: Kikundi cha funzo cha kitabu ambacho kimepewa mgawo wa kusafisha Jumba ndicho kinachosafisha nyumba yake pia.

      Kundi jingine huko lilipata njia rahisi ya kumfanya ndugu mmoja mwenye kizuizi cha kimwili aendelee kuwa mtendaji katika Shule ya Huduma ya Kitheokrasi. Zamu yake inapofika kutoa hotuba, ndugu anapewa mgawo wa kuchukua wahubiri wawili au watatu pamoja naye ili wamtembelee ndugu huyo. Mkutano mfupi unafunguliwa kwa sala, na ndugu huyo anatoa mgawo wake. Shauri linalofaa linatolewa. Ni kitia-moyo kilichoje ambacho ziara hii inatoa!

      Waangalizi wasafirio wameweka mfano mzuri wa kuongoza. Katika kundi moja, ndugu mmoja mzee-mzee aliyekuwa akikaa daima kwenye kiti-magurudumu cha wagonjwa alikuja kuwa mwenye kuudhika sana na kama matokeo hakutembelewa sana. Hata hivyo, mwangalizi asafiriye alipanga kumwonyesha ndugu huyo hotuba yake yenye slaidi faraghani. Ndugu huyo mwenye umri mkubwa alivutiwa sana na yale aliyoyaona mpaka akalia machozi. Anasema hivi mwangalizi huyo: “Nilihisi kuwa nimethawabishwa sana kwa kuona jinsi kumwelekezea fikira na upendo kidogo tu kulivyoweza kuleta matokeo mazuri kama hayo.”

      Wazee fulani katika Naijeria walifanya ziara ya uchungaji kwa ndugu mmoja mzee wakagundua kwamba alikuwa mgonjwa mahututi. Walimpeleka mara moja hospitalini. Ndugu huyo mwenye umri mkubwa alipatikana kuwa anahitaji utibabu wa muda mrefu lakini hangeweza kuulipia. Kundi lilipojulishwa uhitaji wake, wahubiri walichanga fedha za kutosha kulipia gharama zake. Wazee wawili walipokezana zamu za kumpeleka kwa gari hadi hospitalini na kumrudisha ijapokuwa jambo hilo lilihitaji waombe ruhusa kutoka kazini mwao. Ingawa hivyo, walipata furaha kuona ndugu huyo akipona ugonjwa wake na kufanya upainia msaidizi mpaka kifo chake miaka minne baadaye.

      Katika Ufilipino, dada mmoja mzee-mzee hakuwa na jamaa. Kundi lilimfanyia mpango ili atunzwe wakati wa miaka mitatu ya ugonjwa. Walimpa mahali padogo pa kuishi, wakamletea chakula kila siku nyakati za kula, na kutunza hali yake ya usafi.

      [Picha katika ukurasa wa 10]

      Wote wanaweza kushiriki katika kuheshimu watu wenye umri mkubwa walio kati yetu kundini

  • Kuzoea Bidii ya Kujitolea Mungu Kuhusiana na Wazazi Wazee-Wazee
    Mnara wa Mlinzi—1987 | Juni 1
    • Kuzoea Bidii ya Kujitolea Mungu Kuhusiana na Wazazi Wazee-Wazee

      “Lakini mjane akiwa ana watoto au wajukuu, na wajifunze kwanza kuyatenda yaliyo wajibu wao kwa jamaa zao wenyewe, na kuwalipa wazazi wao. Kwa kuwa hili lakubalika mbele za Mungu.” ​—1 TIMOTHEO 5:4.

      1, 2. (a) Ni nani ambao Biblia inawapa daraka la kuwatunza wazazi wanaozeeka? (b) Kwa sababu gani lingekuwa jambo zito kwa Mkristo kuuacha wajibu huo?

      ULIPOKUWA mtoto, walikulea na kukulinda. Ulipokuwa mtu mzima, ulitafuta shauri na tegemezo lao. Lakini sasa wamezeeka na wanahitaji mtu wa kuwategemeza. Anasema hivi mtume Paulo: “Lakini mjane akiwa ana watoto au wajukuu, na wajifunze kwanza kuyatenda yaliyo wajibu wao kwa jamaa zao wenyewe, na kuwalipa wazazi wao. Kwa kuwa hili lakubalika mbele za Mungu. Lakini mtu ye yote asiyewatunza walio wake, yaani, wale wa nyumbani mwake hasa, ameikana Imani, tena ni mbaya kuliko mtu asiyeamini.”​—1 Timotheo 5:4, 8.

      2 Maelfu ya Mashahidi wa Yehova leo wanawatunza wazazi wanaozeeka. Wanafanya hivyo si kwa sababu tu ni “fadhili” (The Living Bible) au “wajibu” (The Jerusalem Bible) bali kwa sababu ya “bidii ya kujitolea Mungu,” yaani, kicho kwa Mungu. Wanatambua kwamba kuwaacha wazazi pekee yao wanapohitaji msaada kungekuwa sawa na ‘kuikana imani [ya Kikristo].’​—Linganisha Tito 1:16.

      ‘Lichukue Furushi Lako Mwenyewe’ la Utunzaji

      3. Kwa sababu gani utunzaji wa wazazi wa mtu unaweza kuwa mwito wa ushindani kweli kweli?

      3 Kuwatunza wazazi wazee-wazee kumekuwa mwito wa ushindani kweli kweli, hasa katika nchi za Magharibi. Mara nyingi jamaa zinakuwa zimetawanyika. Gharama zimepanda kupita kiasi. Mara nyingi wake wenye kazi za nyumbani wana kazi za kuajiriwa. Hivyo kutunza mzazi anayezeeka kunaweza kuwa kazi kubwa sana, hasa wakati mwenye kutoa utunzaji si kijana tena yeye mwenyewe. “Sisi sasa tuna umri na miaka 50 na kitu, pamoja na watoto walio watu wazima na wajukuu ambao pia wanahitaji msaada,” anasema dada mmoja anayejikaza kutunza mzazi wake.

      4, 5. (a) Biblia inaonyesha kwamba mara nyingi furushi la utunzaji linaweza kugawanwa kati ya nani? (b) Wengine waliepukaje daraka la kuwatunza wazazi wao katika siku za Yesu?

      4 Paulo alionyesha kwamba daraka hilo lingeweza kugawanwa kati ya “watoto au wajukuu.” (1 Timotheo 5:4) Ingawa hivyo, nyakati nyingine watu wa ujamaa hawana nia ya ‘kulibeba furushi lao wenyewe’ la utunzaji. (Linganisha Wagalatia 6:5.) “Dada yangu mkubwa amenawa mikono kujiondoa kabisa katika hali hiyo,” analalamika mzee mmoja. Lakini je! mwendo kama huo unaweza kumpendeza Yehova? Kumbuka jambo ambalo Yesu aliwaambia Mafarisayo wakati mmoja: “Musa alisema, Waheshimu baba yako na mama yako . . . Bali ninyi husema, Mtu akimwambia babaye au mamaye, Ni Korbani, yaani, wakfu, kitu changu cho chote kikupasacho kufaidiwa nacho, huwa basi; wala hammruhusu baada ya hayo kumtendea neno babaye au mamaye; huku mkilitangua neno la Mungu kwa mapokeo yenu mliyopokeana.”​—Marko 7:10-13.

      5 Ikiwa Myahudi hakujali kuwasaidia wazazi wake maskini, alihitaji tu kuvitangaza vitu vyake kuwa ‘korbani’​—zawadi iliyowekwa kando kwa matumizi ya hekaluni. (Linganisha Walawi 27:1-24.) Hata hivyo, kwa wazi yeye hakulazimishwa mara hiyo kuitoa zawadi hiyo iliyosemekana ingetolewa. Hivyo angeweza kushikilia (na bila shaka kutumia) mali zake kwa wakati usiojulikana. Lakini ikiwa wazazi wake walihitaji msaada wa kifedha, yeye angeweza kujiponyoa kutoka wajibu wake kwa kusingizia anatangaza kwa heshima ya kimungu kwamba vyote alivyokuwa navyo vilikuwa “korbani.” Yesu alilaumu upunjaji huo!

      6. Ni jambo gani linaloweza kuwachochea wengine leo kuepuka wajibu walio nao kwa wazazi? Je! jambo hilo linampendeza Mungu?

      6 Hivyo Mkristo ambaye anatumia udhuru mtupu ili aepuke wajibu wake hampumbazi Mungu. (Yeremia 17:9, 10) Kweli, matatizo ya kifedha, afya inayodhoofika, au hali zinazofanana na hiyo zinaweza kuwekea mtu mipaka juu ya kadiri ya mambo anayoweza kufanyia wazazi wake. Huenda wengine wakathamini sana mali, wakati, na faragha zaidi ya hali ya wazazi wao. Ingawa hivyo, ungekuwa unafiki kama nini kulihubiri Neno la Mungu lakini ‘kulitangua’ kwa ukosefu wetu wa vitendo kuwaelekea wazazi!

      Ushirikiano wa Kijamaa

      7. Jamaa zinaweza kushirikianaje kutolea ulinzi mzazi anayezeeka?

      7 Wastadi wengine wanapendekeza kwamba shida kubwa inayohusu mzazi mzee ikitokea, mkutano wa jamaa uitwe. Huenda mshiriki mmoja wa jamaa akapaswa kuubeba mzigo wa daraka. Lakini kwa kushiriki katika “mazungumzo ya siri” kwa utulivu na katika njia isiyo ya kushambulia, mara nyingi jamaa zinaweza kutafuta njia za kushiriki furushi hilo la kazi. (Linganisha Mithali 15:22, NW.) Wengine wanaoishi mbali sana huenda wakaweza kutoa mchango wa fedha na kuzuru pindi kwa pindi. Wengine huenda wakaweza kufanya kazi ya nyumbani au kutoa peza za kusafiri. Kwani, kukubali tu kutembelea wazazi kwa ukawaida kunaweza kuwa mchango wenye thamani. Anasema dada mmoja mwenye umri wa miaka 80 na kitu kuhusu ziara za watoto wake, “Ni kama dawa ya kutia afya!”

      8. (a) Je! washiriki wa jamaa ambao wamo katika utumishi wa wakati wote wanaondolewa wajibu wa kushiriki utunzaji wa wazazi wao? (b) Wengine walio katika utumishi wa wakati wote wamefikia kwa kadiri gani katika kutimiza wajibu mbalimbali kuelekea wazazi?

      8 Ingawa hivyo, huenda jamaa zikakabiliana na tatizo gumu, wakati mshiriki yu katika utumishi wa wakati wote. Wahudumu wa wakati wote hawajiondoi katika wajibu kama huo, kwa kuwa wengi wamejitahidi kwa njia isiyo ya kawaida ili kuwapa wazazi wao utunzaji. Anasema hivi mwangalizi asafiriye: “Hatukuwazia jinsi ingeweza kuwa vigumu sana kuwatunza wazazi wetu kimwili na kimoyoni, hasa ikiwa mtu anajaribu kutimiza madai ya utumishi wa wakati wote wakati ule ule. Kwa kweli, sisi tumeifikia mipaka ya uvumilivu wetu na tumehisi uhitaji wa ‘uwezo unaopita ulio wa kawaida.’” (2 Wakorintho 4:7, NW) Yehova na aendelee kuwategemeza watu wa jinsi hiyo!

      9. Ni kitia-moyo gani wanachoweza kupewa wale ambao hawakuwa na jambo jingine la kufanya ila kuacha utumishi wa wakati wote ili watunze wazazi?

      9 Ingawa hivyo, nyakati nyingine baada ya kuchunguza uwezekano mwingine wote, mshiriki wa jamaa hana jambo jingine isipokuwa kuuacha utumishi wa wakati wote. Inaeleweka kwamba mtu wa namna hiyo anaweza kuwa na hisia zilizovurugika juu ya kuacha mapendeleo yake ya utumishi. ‘Tunajua kwamba ni daraka letu la Kikristo kumtunza mama yangu mzee aliye mgonjwa,’ anasema mmoja aliyekuwa mmisionari. ‘Lakini nyakati nyingine ninahisi ajabu sana.’ Ingawa hivyo, kumbuka kwamba ‘kuzoea bidii ya kujitolea Mungu nyumbani kunakubalika machoni pa Mungu.’ (1 Timotheo 5:4, AW) Kumbuka, pia, kwamba “Mungu si dhalimu hata aisahau kazi yenu, na pendo lile mlilolidhihirisha kwa jina lake, kwa kuwa mmewahudumia watakatifu, na hata hivi sasa mngali mkiwahudumia.” (Waebrania 6:10) Wenzi wawili waliooana walioacha utumishi wa wakati wote baada ya kuufanya miaka mingi walisema: “Kwa maoni yetu, ni jambo la maana kwetu kuwatunza wazazi wetu sawasawa na lilivyokuwa jambo la maana kuwa katika utumishi wa wakati wote.”

      10. (a) Kwa sababu gani huenda wengine wakawa waliacha utumishi wa wakati wote upesi sana? (b) Jamaa zinapasa kuuonaje utumishi wa wakati wote?

      10 Ingawa hivyo, labda wengine wameacha utumishi wa wakati wote upesi sana—au bila uhitaji wa lazima—kwa sababu watu wao wa ukoo waliwaza: ‘Ninyi hamna kazi wala jamaa za kuwalemea. Mbona ninyi msiwatunze Baba na Mama?’ Hata hivyo, je! kazi ya kuhubiri siyo kazi ya haraka zaidi ya zote inayofanywa leo? (Mathayo 24:14; 28:19, 20) Hivyo wale walio katika utumishi wa wakati wote wanafanya kazi ya muhimu sana. (1 Timotheo 4:16) Pia, Yesu alionyesha kwamba, katika hali fulani-fulani, utumishi wa Mungu unaweza kuwa wa kwanza kuliko mambo ya kijamaa.

      11, 12. (a) Kwa sababu gani Yesu alishauri mtu mmoja ‘awaache wafu wawazike wafu wao’? (b) Ni mipango gani ambayo jamaa inaweza kufanya wakati mshiriki mmoja yu katika utumishi wa wakati wote?

      11 Kwa mfano, wakati mtu mmoja alipokataa mwaliko wa kuwa mfuasi wa Yesu, akisema, “Nipe ruhusa kwanza niende nikamzike baba yangu,” Yesu alijibu: “Waache wafu [kiroho] wawazike wafu wao; bali wewe enenda ukautangaze ufalme wa Mungu.” (Luka 9:59, 60) Kwa kuwa Wayahudi waliwazika wafu wao siku iyo hiyo, haielekei kwamba baba ya mtu huyo alikuwa amekufa hasa. Inaelekea kwamba mtu huyo alitaka tu kukaa na baba yake mzee mpaka kifo chake. Hata hivyo, kwa kuwa kulikuwa na watu wengine wa ukoo ambao wangetoa utunzaji huo, Yesu alimtia moyo mtu yule ‘kuutangaza ufalme wa Mungu’!

      12 Jamaa nyingine zimepata kwamba wakati washiriki wote wanaposhirikiana, mara nyingi inaweza kupangwa kwamba yule aliye katika utumishi wa wakati wote ashiriki katika kuwatunza wazazi bila kuacha utumishi wa wakati wote. Kwa mfano, wahudumu wengine wa wakati wote wanawasaidia wazazi wao wakati wa miisho-juma au wakati wa vipindi vya likizo. Jambo la kupendeza ni kwamba wazazi kadha wazee-wazee wamesisitiza kwamba watoto wao wabaki katika utumishi wa wakati wote, hata wakati kufanya hivyo kumehitaji wazazi hao wajidhabihu sana. Yehova anawabariki sana wale wanaoweka masilahi za Ufalme kwanza.​—Mathayo 6:33.

      “Hekima” na “Utambuzi” Wakati Wazazi Wanapohamia Kwenu

      13. Ni tatizo gani linaloweza kutokea ikiwa mzazi anaalikwa ahame aishi pamoja na watoto wake?

      13 Yesu alifanya mpango ili kwamba mama yake mjane aishi na watu wake wa ukoo wenye kuamini. (Yohana 19:25-27) Mashahidi wengi wamefanya vivyo hivyo kwa kuwaalika wazazi wao wahame na kuishi pamoja nao—kama matokeo wakapata nyakati nyingi zenye furaha na mibaraka. Hata hivyo, mitindo ya maisha isiyopatana, faragha iliyopungua, na mkazo wa kutoa utunzaji kila siku ni mambo yanayofanya mara nyingi kuhamishia mzazi katika nyumba yako kuwavuruge fikira wote wanaohusika. “Kumtunza Mama kumenifanya niwe zaidi na mikazo ya ndani,” anasema Ann, ambaye mama-mkwe wake ana ugonjwa wa Alzheimer. “Nyakati nyingine hata ninakosa subira na kumwambia Mama mambo yasiyo ya fadhili—na jambo hilo linanifanya nihisi nikiwa mwenye hatia sana.”

      14, 15. “Hekima” na “utambuzi” vinaweza kusaidiaje ‘kuijenga’ jamaa chini ya hali hizo?

      14 Sulemani alisema kwamba “kwa hekima nyumba na waliomo itajengwa, na kwa utambuzi itathibitika kuwa iliyosimamishwa imara.” (Mithali 24:3, NW) Kwa mfano, Ann, amejaribu kuwa mwenye kufahamu zaidi tatizo la mama-mkwe wake. “Ninafikiria akilini kwamba yeye ana ugonjwa na hatendi hivyo kwa makusudi.” Bado, “twajikwaa sisi sote pia katika mambo mengi. Mtu asiyejikwaa katika kunena, huyo ni mtu mkamilifu.” (Yakobo 3:2) Lakini hitilafu zinapotokea, onyesheni hekima kwa kutoruhusu uchungu ujazane ndani yenu au mpandwe na hasira. (Waefeso 4:31, 32) Zungumzeni mambo kama jamaa, na kutafuta njia za kufanya mapatano au marekebisho.

      15 Utambuzi pia unasaidia mmoja aweze kuwasiliana kwa njia yenye matokeo. (Linganisha Mithali 25:11.) Labda mzazi ana tatizo la kujirekebisha kulingana na kawaida ya nyumba mpya. Au kwa sababu ya uwezo uliodhoofika wa kufanya maamuzi, yeye anaelekea kuwa asiyeshirikiana. Chini ya hali fulani-fulani huenda kusiwe na jambo jingine la kufanya ila kuzungumza kwa imara sana. (Linganisha Mwanzo 43:6-11.) “Kama singemkataza mama yangu,” akasema dada mmoja, “yeye angetumia pesa zake zote.” Ingawa hivyo, mzee mmoja anapata kwamba nyakati nyingine anaweza kuambia mamaye jambo la kufanya kwa kutumia shauku ya upendo ambayo mamaye anayo kwake. “Nyakati nyingi ninapokosa kupata matokeo kwa kumtolea sababu za mambo, mimi nasema tu, ‘Mama, tafadhali fanya hivyo kwa sababu tu ni mimi nimekuambia,’ naye anasikiliza.”

      16. Kwa sababu gani ni lazima mume mwenye upendo amwonyeshe mkeye “utambuzi”? Anaweza kufanyaje hivyo?

      16 Kwa kuwa mara nyingi mke ndiye anayebeba sehemu kubwa ya mzigo wa utunzaji, mume mwenye utambuzi ataangalia kwamba mkeye hachoshwi sana—kimoyoni, kimwili, au kiroho. Inasema Mithali 24:10: “Ukizimia siku ya taabu, nguvu zako ni chache.” Mume anaweza kufanya nini airudishe shauku ya mkeye? “Mume wangu angekuja nyumbani,” anasema dada mmoja, “na kunizungushia mikono yake na kuniambia vile alivyonithamini sana. Singaliweza kufaulu bila yeye!” (Linganisha Waefeso 5:25, 28, 29.) Mume anaweza pia kujifunza Biblia na kusali kwa ukawaida pamoja na mwenzi wake. Ndiyo, hata chini ya hali hizi zenye ugumu, jamaa inaweza ‘kujengwa!’

      Utunzaji Kwenye Makao ya Watu Wazee

      17, 18. (a) Jamaa nyingine zimelazimika kuchukua hatua gani? (b) Katika visa kama hivyo, watoto ambao ni watu wazima wanaweza kusaidiaje wazazi wajirekebishe?

      17 Mstadi mmoja anayehusika na matatizo ya wazee anasema: “Inafikia mahali ambapo jamaa haina ustadi wala pesa za kuendelea kumweka [mzazi] nyumbani.” Kama anavyosema mume mmoja: “Ilifikia mahali ambapo afya ya mke wangu iliharibika sana kwa kujaribu kumtunza Mama kwa muda wa saa 24. Hatukuwa na jambo jingine la kufanya ili kumweka Mama katika makao ya kutunzia wazee. Lakini mioyo yetu ilihangaika sana kwa kufanya hivyo.”

      18 Huenda utunzaji wa makao ya wazee ukawa ndio utunzaji bora zaidi unaopatikana chini ya hali hizo. Lakini watu wazee wanaowekwa katika makao hayo mara nyingi wanafadhaika na kukasirika, wakihisi kwamba wamekataliwa. “Tulimweleza Mama kwa uangalifu kwa sababu gani tulipaswa kufanya hivyo,” anasema dada mmoja ambaye tutamwita Greta. “Yeye amejifunza kujirekebisha na sasa anayaona makao hayo kama nyumbani.” Ziara za ukawaida pia zinawastarehesha wazazi wazee kujirekebisha na zinawaonyesha “unyofu wa upendo wenu” kwao. (Linganisha 2 Wakorintho 8:8.) Mahali ambako mwendo ni tatizo, endeleeni kuwasiliana kwa njia ya simu, barua, na ziara za pindi kwa pindi. (Linganisha 2 Yohana 12.) Hata hivyo, kuishi miongoni mwa watu wa ulimwengu kunakuwa na vizuia-maendeleo vinavyoonekana wazi. ‘Yajue mahitaji yao ya kiroho.’ (Mathayo 5:3, NW) “Sisi tunamtolea Mama vichapo vya kusoma na kujaribu kuzungumza naye mambo ya kiroho kwa kadiri iwezekanavyo,” anasema Greta.

      19. (a) Ni uangalifu ambao lazima ufanywe katika kuchagua na kuangalia-angalia makao ya kutunzia watu wazee? (b) Mkristo ananufaikaje kwa kufanya yote anayoweza atunze mzazi?

      19 Jarida la The Wall Street Journal liliripoti juu ya uchunguzi wa makao 406 ya kutunzia watu wazee United States ambamo “kao moja kwa kila makao matano lilionekana linaweza kuwa lenye hatari kwa wakaaji na karibu nusu yayo tu ndiyo yaliyotimiza viwango vya hali ya chini.” Jambo lenye kuhuzunisha ni kwamba ripoti kama hizo kwa kawaida zinataabisha fikira. Kwa hiyo ikiwa utunzaji wa makao ya watu wazee unahitajiwa kabisa, uwe mwangalifu katika kuchagua moja. Wewe binafsi litembelee uone kama ni safi, linatunzwa vizuri, lina wafanya kazi wa kutosha na wanaostahili, hali yalo ni ya kinyumbani, na lina vyakula vya kutosha. Uwe ukiangalia-angalia kwa kiasi uwezacho utunzaji wanaopewa wazazi wako. Uwe mtetezi wao, ukiwasaidia waepuke hali zenye magumu ambazo zinaweza kutokea, labda kwa habari ya sikukuu za kilimwengu au tafrija. Kwa kufanya yote unayoweza ili kuwapa wazazi wako utunzaji ulio bora zaidi chini ya hali hizo, unaweza kujiondolea mwenyewe hisia za hatia ambazo zingaliweza kukusumbua.​—Linganisha 2 Wakorintho 1:12.

      Watoaji Wachangamfu, Wapokeaji Wachangamfu

      20. Kwa sababu gani ni jambo la maana kwamba watoto wawe ‘watoaji wachangamfu’?

      20 “Limekuwa jambo gumu,” asema mwanamke mmoja Mkristo kuhusu kuwatunza wazazi wake. Nimelazimika kupika, kuwasafishia, kushughulikia vipindi vyao vya kulia, kubadili shuka za kitanda waliposhindwa kujizuia wakaziendea haja.” “Lakini lo lote ambalo tumewafanyia,” mume wake anatoa kikumbusho, “tumelifanya kwa furaha—kwa uchangamfu. Tumejaribu sana tusiwafanye kamwe wazazi wetu wahisi kwamba tunachukizwa kuwatunza.” (2 Wakorintho 9:7, NW) Mara nyingi watu wenye umri mkubwa wanakataa msaada na hawataki kuwa “mzigo” kwa wengine. Hivyo ni jambo la maana sana kuangalia mwelekeo unaoonyesha.

      21. (a) Wazazi wanawezaje kuwa wapokeaji wachangamfu? (b) Ni kwa sababu gani ni jambo la hekima mzazi apangie wakati wake wa uzeeni kimbele?

      21 Wakati ule ule, mwelekeo ambao wazazi wanaonyesha pia ni wa maana. Anakumbuka hivi dada mmoja: “Jambo lo lote nililomfanyia Mama, halikutosha kamwe.” Kwa hiyo, wazazi, epukeni kupita kiasi na kuwa wenye kudai mno. Ingawaje, Biblia inasema “haiwapasi watoto kuweka akiba kwa wazazi, bali wazazi kwa watoto.” (2 Wakorintho 12:14) Wazazi wengine wanatumia vibaya mali zao na kuwa mzigo usio wa lazima kwa watoto wao. Hata hivyo, Mithali 13:22 inasema: “Mtu mwema huachia wana wa wanawe urithi.” Hivyo, kwa kadiri inavyowezekana wazazi wanaweza kupangia wakati wao wa uzeeni kimbele, wakiweka kando fedha na kufanya mapema mipango fulani ya kuwatunza.​—Mithali 21:5.

      22. Mtu anapaswa kuzionaje jitihada ambazo anatumia kuwatunza wazazi wake wanaozeeka?

      22 Paulo alilieleza jambo hili vizuri wakati aliposema kwamba kuwatunza wazazi wa mtu ni sawa na “kuwalipa.” (1 Timotheo 5:4) Kama anavyosema ndugu mmoja: “Mama alinitunza kwa miaka ishirini. Mimi nimefanya nini linalolingana na hilo?” Wakristo wote ambao wana wazazi wazee-wazee na wasukumwe na moyo ivyo hivyo ‘kuzoea bidii ya kujitolea Mungu nyumbani,’ wakijua kwamba watathawabishwa sana na Mungu ambaye anawaahidi hivi wale ambao wanawaheshimu wazazi wao: “Utakaa siku nyingi katika dunia.”—Waefeso 6:3.

      Mambo ya Kukumbuka

      ◻ Wengine katika siku za Yesu walitafutaje kuepuka daraka kuelekea wazazi?

      ◻ Ni nani ambao wanapaswa kuwatunza wazazi wazee-wazee, na kwa sababu gani?

      ◻ Ni matatizo gani ambayo jamaa zinaweza kupata wakati mzazi anapohama aishi pamoja nao, nayo yanaweza kushindwaje?

      ◻ Kwa sababu gani utunzaji kwenye makao ya watu wazee unaweza kuhitajiwa kabisa, na wazazi wanaweza kusaidiwaje ili wakabiliane na hali za kuishi huko?

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki