Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Kusoma Maandiko kwa Mkazo Unaofaa
    Faidika na Elimu ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi
    • SOMO LA 21

      Kusoma Maandiko kwa Mkazo Unaofaa

      Unahitaji kufanya nini?

      Kazia maneno makuu ya habari unayozungumzia. Soma kwa hisia inayofaa.

      Kwa Nini Ni Muhimu?

      Uzito wa maandiko yanayosomwa hudhihirishwa kwa mkazo unaofaa.

      UNAPOZUNGUMZA na wengine kuhusu mambo ambayo Mungu amekusudia, iwe unamhubiria mtu au unahutubu jukwaani, unapaswa kutegemea Neno la Mungu. Mara nyingi mazungumzo hayo hutia ndani kusoma Biblia, na tunapaswa kuisoma vizuri.

      Mkazo Unaofaa Unatia Ndani Hisia. Tusome maandiko kwa hisia. Ebu ona mifano michache. Unaposoma kwa sauti Zaburi 37:11, sauti yako inapasa kuonyesha furaha ya kutazamia amani ambayo imeahidiwa katika andiko hilo. Unaposoma Ufunuo 21:4 kuhusu mwisho wa kuteseka na kifo, sauti yako ionyeshe shukrani za moyoni kwa sababu ya faraja hiyo nzuri ajabu ambayo imetabiriwa hapo. Soma Ufunuo 18:2, 4, 5 kwa sauti ya dharura kwa sababu linatuhimiza tutoke kwenye “Babiloni Mkubwa” mwenye dhambi tele. Hisia tunayoonyesha itoke moyoni lakini isipite kiasi. Kadiri nzuri ya hisia inategemea andiko unalosoma na jinsi unavyolitumia.

      Kazia Maneno Yanayofaa. Kama unazungumzia sehemu fulani tu ya andiko, kazia sehemu hiyo unaposoma. Kwa mfano, ikiwa unataka kuelezea maana ya “kutafuta kwanza ufalme” unaposoma Mathayo 6:33, usikazie “uadilifu wake” wala “vitu vingine vyote.”

      Tuseme umepanga kusoma Mathayo 28:19 katika hotuba utakayotoa katika Mkutano wa Utumishi. Utakazia maneno gani? Ikiwa unataka kutia watu moyo wawe na bidii kuanzisha mafunzo ya Biblia ya nyumbani, kazia ‘kufanya wanafunzi.’ Na kama unataka kuzungumzia daraka la Mkristo la kuwajulisha kweli za Biblia watu wa nchi za kigeni au kama unataka kuwatia moyo wahubiri wengine watumikie katika sehemu zenye uhitaji zaidi, unaweza kukazia “watu wa mataifa yote.”

      Mara nyingi tunasoma andiko kujibu swali au kuunga mkono jambo fulani ambalo wengine hubisha. Ikiwa unakazia kila wazo katika andiko hilo kwa kadiri ileile, wasikilizaji wanaweza kukosa kuelewa kusudi lako la kusoma andiko hilo. Wewe unaweza kufahamu wazi kusudi lako la kulisoma lakini huenda wao wasilifahamu.

      Kwa mfano, unaposoma Zaburi 83:18 katika Biblia ambayo ina jina la Mungu, mwenye nyumba anaweza kukosa kufahamu jambo linaloonekana kuwa wazi la kwamba Mungu ana jina ikiwa unakazia sana ile sehemu inayosema “Uliye juu.” Kazia jina “Yehova.” Lakini, unapotumia andiko hilo kuonyesha kwamba Yehova ni mwenye enzi kuu, kazia maneno “Uliye juu.” Vilevile unapotumia Yakobo 2:24 kuonyesha kwamba imani inapaswa kuonyeshwa kwa matendo, kukazia ‘kutangazwa kuwa mwadilifu’ badala ya kukazia “kazi” kunaweza kufanya wengine wasipate maana.

      Tunaweza kupata mfano mwingine mzuri katika Waroma 15:7-13. Hii ni sehemu ya barua ambayo mtume Paulo aliandikia kutaniko lenye mchanganyiko wa watu wa Mataifa na Wayahudi wa asili. Anasema hapo kwamba huduma ya Kristo haiwafaidi tu Wayahudi waliotahiriwa bali inawafaidi pia watu wa mataifa ili “mataifa yapate kumtukuza Mungu kwa ajili ya rehema yake.” Kisha ananukuu maandiko manne kuthibitisha jambo hilo. Unapaswa kusoma manukuu hayo kwa njia gani ili kukazia jambo ambalo Paulo alimaanisha? Ikiwa unatia alama maneno ya kukazia, unaweza kutia alama “mataifa” katika mstari wa 9, “nyinyi mataifa” katika mstari wa 10, “mataifa yote” na “vikundi vyote vya watu” katika mstari wa 11, na “mataifa” katika mstari wa 12. Ebu jaribu kusoma Waroma 15:7-13 kwa mkazo huo. Unapofanya hivyo, hoja ya Paulo itakuwa wazi na kueleweka kwa urahisi.

      Njia za Kutia Mkazo. Unaweza kutumia njia kadhaa kukazia maneno muhimu ambayo unataka yawe wazi. Njia unayotumia kutia mkazo ilingane na andiko unalosoma na muktadha wa hotuba yako. Hapa pana madokezo machache.

      Kutia mkazo kupitia sauti. Njia hii inahusisha kubadili sauti kwa njia yoyote inayofanya maneno yenye maana yawe wazi kuliko maneno mengine katika sentensi. Unaweza kutia mkazo kwa kuinua sauti au kuipunguza. Katika lugha nyingi, kuinua sauti kunaweza kuongeza mkazo. Lakini katika lugha nyinginezo, kuinua sauti kunaweza kubadili maana ya jambo unalosema. Ukipunguza mwendo wako na kuongea polepole unapofikia maneno makuu, maneno hayo hutokea kwa uzito zaidi. Katika lugha ambazo huwezi kukazia maneno fulani kwa kubadili sauti, unaweza kufuata desturi za kukazia maneno katika lugha hizo.

      Kutua kifupi. Unaweza kutua kifupi kabla ya kusoma sehemu kuu ya andiko au baada ya kuisoma, au kabla na baada ya kuisoma. Kutua kifupi kabla tu ya kusoma wazo kuu hufanya watu wawe na hamu ya kujua jambo linalofuata na kutua baada tu ya kulisoma hufanya jambo hilo lieleweke zaidi. Lakini ukitua-tua sana, hakuna jambo litakalokuwa wazi.

      Kurudia jambo kuu. Unaweza kukazia jambo fulani kwa kutua na kulisoma tena. Njia nzuri ya kutua inayotumiwa mara nyingi ni kumaliza kusoma andiko lote kisha urudie kusoma wazo kuu unalotaka kukazia.

      Ishara. Mara nyingi ishara za mwili na za uso zinaweza kuongezea hisia jambo unalosema.

      Hali ya sauti. Katika lugha fulani, nyakati nyingine maneno yanaweza kusomwa kwa sauti inayotokeza maana fulani na kuyatia mkazo. Pia unahitaji kutumia busara kuhusu jambo hili hasa unapotumia maneno ya dhihaka.

      Wengine Wanaposoma Maandiko. Mwenye nyumba anaposoma andiko, anaweza kukazia maneno yasiyostahili kukaziwa au labda asikazie neno lolote. Ufanye nini basi? Kwa ujumla ni vizuri ufafanue maana unapomwonyesha jinsi maandiko hayo yanavyotumika. Baada ya kufanya hivyo, unaweza kukazia hasa maneno yanayotokeza maana katika Biblia.

      KUJUA JINSI YA KUTUMIA MKAZO

      • Jiulize hivi kuhusu andiko lolote ambalo utasoma: ‘Maneno haya yanaonyesha hisia gani? Nionyeshe hisia hizo kwa njia gani?’

      • Chunguza maandiko unayopanga kutumia. Jiulize hivi kuhusu kila mojawapo ya maandiko hayo: ‘Andiko hili litatimiza kusudi gani? Nahitaji kukazia maneno gani kutimiza kusudi hilo?’

      MAZOEZI: (1) Chunguza andiko ambalo unataka kutumia katika utumishi wa shambani. Fanya mazoezi ya kulisoma kwa hisia inayofaa. Ukikumbuka jinsi unavyotaka kulitumia, lisome kwa sauti ukikazia neno au maneno yanayofaa. (2) Katika kichapo kinachotumiwa wakati huu kwenye funzo, chagua fungu moja ambalo lina manukuu ya maandiko. Chunguza jinsi ambavyo maandiko yametumiwa hapo. Tia alama maneno yanayotokeza maana. Soma fungu lote kwa sauti kwa njia inayokazia vizuri maandiko.

  • Kutumia Maandiko Vizuri
    Faidika na Elimu ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi
    • SOMO LA 22

      Kutumia Maandiko Vizuri

      Unahitaji kufanya nini?

      Hakikisha unatumia andiko kulingana na muktadha wake na kulingana na Biblia yote kwa ujumla. Pia tumia andiko kulingana na maelezo ambayo yamechapishwa na “mtumwa mwaminifu na mwenye busara.”

      KWA NINI NI MUHIMU?

      Kufundisha wengine Neno la Mungu ni jambo zito sana. Mungu anataka watu wapate “ujuzi sahihi wa kweli.” (1 Tim. 2:3, 4) Kwa hiyo tuna wajibu wa kufundisha Neno la Mungu kwa usahihi.

      KUFUNDISHA wengine si kusoma tu maandiko ya Biblia. Mtume Paulo alimwandikia hivi mshiriki wake Timotheo: “Fanya yote uwezayo kabisa ili ujionyeshe mwenyewe kuwa mwenye kukubaliwa na Mungu, mtenda-kazi asiye na lolote la kuaibikia, ukilitumia sawasawa neno la ile kweli.”—2 Tim. 2:15.

      Ili tufanye hivyo, ni lazima tufafanue maandiko kulingana na mafundisho ya Biblia. Hiyo inamaanisha tufikirie muktadha badala ya kuchagua tu maneno yanayotupendeza na kutoa maoni yetu wenyewe. Kupitia nabii Yeremia, Yehova aliwaonya watu wasiwasikilize manabii waliodai kusema maneno yake lakini kumbe walisema “maono ya mioyo yao wenyewe.” (Yer. 23:16) Mtume Paulo aliwaonya Wakristo wasichafue Neno la Mungu kwa falsafa za wanadamu alipoandika: “Tumeyakataa kabisa mambo ya kichinichini yaliyo ya kuaibikia, si kutembea kwa ujanja, wala tukilighushi neno la Mungu.” Siku hizo, wauzaji wa divai wenye pupa walikuwa wakitia divai maji ili iwe nyingi wapate pesa zaidi. Sisi hatughushi Neno la Mungu kwa kulichanganya na falsafa za wanadamu. Paulo alitangaza kwamba “sisi si wachuuzi wa neno la Mungu kama watu wengi walivyo, bali tunasema kwa weupe wa moyo, ndiyo, tukiwa waliotumwa kutoka kwa Mungu, mbele ya Mungu, kwa ushirika na Kristo.”—2 Kor. 2:17; 4:2.

      Nyakati nyingine unaweza kunukuu andiko ili kukazia kanuni fulani. Biblia imejaa kanuni zenye mwongozo bora zinazotusaidia kushughulika na hali mbalimbali za maisha. (2 Tim. 3:16, 17) Lakini hakikisha kwamba unatumia kwa usahihi kanuni hizo na usitumie andiko vibaya, ukifanya andiko lionekane kana kwamba linasema jambo ambalo wewe unataka liseme. (Zab. 91:11, 12; Mt. 4:5, 6) Ni lazima utumie andiko kulingana na kusudi la Yehova, kupatana na Neno lote la Mungu.

      ‘Kulitumia sawasawa neno la ile kweli’ pia kunatia ndani kufahamu vile Biblia inavyosema. Biblia si “rungu” la kutwangia watu wengine. Walimu wa kidini waliompinga Yesu Kristo walinukuu Maandiko, lakini walipuuza mambo mazito ambayo Mungu alitaka yaonyeshwe kama vile haki, rehema, na uaminifu. (Mt. 22:23, 24; 23:23, 24) Yesu alionyesha utu wa Baba yake alipofundisha Neno la Mungu. Bidii ya Yesu kwa ajili ya ile kweli iliambatana na upendo mwingi aliowaonyesha watu aliofundisha. Tujaribu kuiga mfano wake.—Mt. 11:28.

      Tunawezaje kuwa na hakika kwamba tunatumia maandiko vizuri? Kusoma Biblia kwa ukawaida kunasaidia. Pia tunahitaji kutambua kwamba Yehova ametuandalia “mtumwa mwaminifu na mwenye busara,” jamii ya Wakristo watiwa-mafuta ambayo Yehova anatumia kuandalia nyumba ya waamini chakula cha kiroho. (Mt. 24:45) Funzo la binafsi na kuhudhuria mikutano ya kutaniko kwa ukawaida na kuishiriki kutatusaidia kufaidika na mafunzo yanayoandaliwa kupitia jamii ya mtumwa mwaminifu na mwenye busara.

      Ikiwa kitabu Kutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko kinapatikana katika lugha yenu, jifunze kukitumia vizuri na kitakusaidia sana kuelewa kwa urahisi jinsi ya kupata mwongozo unaohitaji ili kutumia vizuri mamia ya maandiko ambayo hutumiwa mara nyingi katika huduma ya shambani. Ikiwa unataka kutumia andiko ambalo hulifahamu, kwa unyenyekevu fanya utafiti ili ulitumie sawasawa neno la ile kweli.—Mit. 11:2.

      Onyesha Vizuri Jinsi Andiko Linavyohusika. Unapowafundisha wengine, hakikisha wanaelewa vizuri uhusiano ulioko kati ya habari unayozungumzia na maandiko unayotumia. Ukiuliza swali kabla ya kusoma andiko, waonyeshe wasikilizaji jinsi andiko hilo linavyojibu swali lile. Ikiwa unatumia andiko kuunga mkono jambo fulani unalosema, hakikisha mwanafunzi anaona wazi jinsi andiko hilo linavyothibitisha jambo hilo.

      Mara nyingi haitoshi tu kusoma andiko, hata kama unalisoma kwa mkazo. Kumbuka kwamba mtu wa kawaida hafahamu vizuri Biblia na ukisoma andiko mara moja tu labda hatakuelewa. Kazia sehemu ya andiko inayohusu jambo unalozungumzia.

      Kwa kawaida unaweza kukazia jambo kwa kutenga maneno makuu, yaani maneno ambayo yanahusiana na jambo unalozungumzia. Njia rahisi zaidi ni kurudia kutaja maneno yenye mambo unayotaka kukazia. Ikiwa unazungumza na mtu fulani, unaweza kuuliza maswali ambayo yanaweza kumsaidia kutambua maneno makuu. Wasemaji wengine wanapohutubu, wao hupendelea kukazia maneno makuu kwa kutumia maneno mengine yenye maana sawa au kwa kurudia kutaja wazo kuu. Na ukiamua kufanya hivyo, hakikisha wasikilizaji wanaona jinsi jambo unalozungumzia linavyohusiana na andiko unalosoma.

      Ikiwa umetenga maneno makuu, basi umeweka msingi mzuri. Sasa jenga kwenye msingi huo. Kabla ya kusoma andiko, je, umeonyesha wazi sababu ya kulisoma? Ikiwa ndivyo, onyesha jinsi maneno ambayo umekazia yanavyohusiana na matarajio ya wasikilizaji kuhusu andiko hilo. Onyesha vizuri uhusiano ulioko. Hata kama utangulizi wa andiko hilo haukuwa dhahiri sana, onyesha sababu ya kulisoma.

      Mafarisayo walimwuliza Yesu swali ambalo walifikiri ni gumu, yaani: “Je, yaruhusika kisheria mtu kutaliki mke wake kwa kila namna ya sababu?” Yesu alitumia Mwanzo 2:24 kujibu. Ebu ona kwamba Yesu alitaja sehemu tu ya andiko hilo, kisha akaonyesha jinsi sehemu hiyo inavyohusika. Baada ya Yesu kutaja kwamba mwanamume na mke wake watakuwa “mwili mmoja,” alimalizia kusema: “Kwa hiyo, kile ambacho Mungu amefunga nira pamoja msiache mtu yeyote akitenganishe.”—Mt. 19:3-6.

      Unapaswa kufafanua andiko kwa kadiri gani ili liwe wazi? Hiyo inategemea wasikilizaji na umuhimu wa jambo unalozungumza. Kusudi lako liwe kufafanua andiko kwa njia rahisi na ya moja kwa moja.

      Tumia Maandiko Kutoa Sababu. Matendo 17:2, 3 linapozungumzia huduma ya mtume Paulo huko Thesalonike, linatuambia kwamba ‘alitoa sababu kutokana na Maandiko.’ Kila mtumishi wa Yehova anapaswa kujaribu kukuza uwezo huu. Kwa mfano, Paulo alisimulia mambo yaliyohusu maisha ya Yesu na huduma yake, akaonyesha kwamba mambo hayo yalitabiriwa katika Maandiko ya Kiebrania, kisha akamalizia kwa nguvu akisema: “Huyu ndiye Kristo, Yesu huyu ninayewatangazia nyinyi.”

      Paulo alinukuu Maandiko ya Kiebrania mara nyingi alipowaandikia Waebrania. Mara nyingi alitenga neno au maneno fulani kisha akaonyesha umuhimu wake ili kukazia jambo au kulifafanua vizuri. (Ebr. 12:26, 27) Katika masimulizi ya Waebrania sura ya 3, Paulo alinukuu Zaburi 95:7-11. Ona kwamba alifafanua sehemu tatu za maandiko hayo: (1) alitaja moyo (Ebr. 3:8-12), (2) umuhimu wa neno “Leo” (Ebr. 3:7, 13-15; 4:6-11), na (3) maana ya maneno haya: “Hawataingia katika pumziko langu.” (Ebr. 3:11, 18, 19; 4:1-11) Jaribu kuiga mfano huo unapoonyesha jinsi kila andiko linavyohusika na jambo unalozungumzia.

      Ona jinsi Yesu alivyotoa sababu vizuri akitumia Maandiko katika Luka 10:25-37. Mtaalamu mmoja wa Sheria alimwuliza: “Mwalimu, ni kwa kufanya nini mimi nitarithi uhai udumuo milele?” Kwanza, Yesu akamwuliza mtu huyo maoni yake juu ya swali hilo, kisha Yesu akakazia kwamba ni muhimu kufanya kile ambacho Neno la Mungu linasema. Ilipokuwa wazi kwamba mtu huyo haelewi, Yesu alifafanua kabisa neno moja tu katika andiko hilo, “jirani.” Na badala ya kulifafanua tu neno hilo, Yesu alitumia mfano uliomwezesha mtu huyo afikie jibu linalofaa.

      Yesu alipokuwa akijibu maswali, hakunukuu tu maandiko na kutoa majibu rahisi na ya wazi. Alifafanua maandiko hayo na kuonyesha jinsi yanavyojibu swali aliloulizwa.

      Masadukayo walipopinga tumaini la ufufuo, Yesu alikazia sehemu fulani tu ya Kutoka 3:6. Lakini hakuachia hapo tu. Alisababu juu ya andiko hilo na kuonyesha wazi kwamba ufufuo ni sehemu ya kusudi la Mungu.—Mk. 12:24-27.

      Ili kuwa mwalimu bora ni muhimu kukuza uwezo wa kutumia Maandiko kutoa sababu vizuri na kwa matokeo mazuri.

      JINSI YA KUKUZA UWEZO HUO

      • Soma Biblia kwa ukawaida. Jifunze kwa makini Mnara wa Mlinzi, na utayarishe vizuri mikutano ya kutaniko.

      • Hakikisha unajua maana ya maneno unayotumia katika andiko lolote unalotaka kutumia. Soma andiko hilo kwa makini ili uelewe vizuri jambo linalosema.

      • Uwe na mazoea ya kutumia vichapo vyetu vya Kikristo kufanya utafiti.

      MAZOEZI: Fikiria 2 Petro 3:7. Je, linathibitisha dunia itaharibiwa kwa moto? (Unapofafanua maana ya neno “dunia,” pia fikiria maana ya “mbingu.” Ni maandiko gani yanayoonyesha kwamba “dunia” inaweza kuwa na maana ya mfano? Kulingana na mstari wa 7 ni nani, au ni nini kinachoharibiwa? Jambo hilo linalinganaje na tukio la wakati wa Noa linalotajwa katika mstari wa 5 na 6?)

  • Kuonyesha Wasikilizaji Jinsi ya Kutumia Habari
    Faidika na Elimu ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi
    • SOMO LA 23

      Kuonyesha Wasikilizaji Jinsi ya Kutumia Habari

      Unahitaji kufanya nini?

      Wasaidie wasikilizaji waone jinsi habari unayozungumzia inavyohusu maisha yao au jinsi wanavyoweza kuitumia vizuri.

      Kwa Nini Ni Muhimu?

      Kama watu hawaoni jinsi wanavyoweza kutumia habari unayosema, wanaweza kukuambia hawataki kusikiliza au wanaweza kuacha kukusikiliza na kuruhusu akili zao zitangetange.

      IWE unazungumza na mtu mmoja au watu wengi, si vizuri kudhani wasikilizaji watapenda habari yako eti kwa sababu unaipenda. Ingawa ujumbe wako ni muhimu, baada ya muda watu wanaweza kuacha kukusikiliza ikiwa huwaonyeshi faida yake.

      Ndivyo ilivyo pia na wasikilizaji katika Jumba la Ufalme. Wanaweza kusikiliza unapotumia mfano au unaposimulia tukio ambalo hawajasikia. Lakini wanaweza kuacha kukusikiliza unapozungumzia mambo ambayo tayari wanajua, hasa ukikosa kujenga hotuba yako juu ya mambo hayo. Unahitaji kuwasaidia waone kwa nini habari hiyo ina faida na pia inawafaidi kwa njia gani.

      Biblia inatuhimiza tufikiri kwa njia inayofaa. (Mit. 3:21) Yehova alimtumia Yohana Mbatizaji kuwaonyesha watu “hekima itumikayo ya walio waadilifu.” (Luka 1:17) Hekima hii inategemea kumcha Yehova. (Zab. 111:10) Wale wanaotambua hekima hii husaidiwa kukabiliana kwa mafanikio na maisha wakati huu, na kushika uhai halisi na wa milele wa wakati ujao.—1 Tim. 4:8; 6:19.

      Kuwaonyesha Wasikilizaji Jinsi ya Kutumia Habari. Ili hotuba yako ifaidi wasikilizaji, mbali na kuifikiria hotuba hiyo wafikirie wasikilizaji. Usiwafikirie tu kwa ujumla. Miongoni mwa wasikilizaji hao mna watu mmoja-mmoja na familia tofauti-tofauti. Huenda kuna watoto wadogo sana, vijana, watu wazima, na wengine ambao ni wazee. Huenda pia miongoni mwao mna wale wanaopendezwa na wale ambao walianza kumtumikia Yehova kabla ya wewe kuzaliwa. Huenda wengine wamekomaa kiroho, na huenda wengine bado wana mielekeo na hali fulani za kilimwengu. Jiulize: ‘Hotuba hii itawasaidiaje wasikilizaji? Nawezaje kuwasaidia kuelewa jambo ambalo nitazungumzia?’ Unaweza kuamua kukazia akili kikundi kimoja au vikundi viwili kati ya vikundi ambavyo tumetaja. Lakini usiwasahau wengine kabisa.

      Ufanyeje ukipewa hotuba inayozungumzia fundisho fulani la msingi la Biblia? Unaweza kufanya nini ili hotuba kama hiyo iwafaidi wasikilizaji ambao tayari wanafahamu fundisho hilo? Jaribu kuimarisha usadikisho wao kulihusu. Kwa njia gani? Kwa kutoa sababu za Maandiko zinazolithibitisha. Pia unaweza kuzidisha uthamini wao kuhusu fundisho hilo la Biblia. Unaweza kuzidisha uthamini wao kwa kuwaonyesha jinsi fundisho hilo linavyopatana na kweli nyinginezo za Biblia na jinsi linavyopatana na utu wa Yehova. Tumia mifano au ikiwezekana simulia matukio halisi maishani yanayoonyesha jinsi ambavyo watu wengine wamefaidika na kubadili maoni yao juu ya wakati ujao walipoelewa fundisho hilo.

      Usieleze kwa ufupi tu jinsi wanavyoweza kutumia habari hiyo mwishoni mwa hotuba yako. Tangu mwanzoni kabisa, kila msikilizaji anapaswa kuona kwamba “habari hii inanihusu.” Baada ya kuweka msingi huo, endelea kuwaonyesha jinsi wanavyoweza kutumia habari hiyo unapokuza kila moja ya mambo makuu ya hotuba na pia unapomalizia hotuba.

      Unapowaeleza akina ndugu jinsi wanavyoweza kutumia habari hiyo, fuata kanuni za Biblia. Hiyo inamaanisha nini? Inamaanisha kuwa mwenye upendo na hisia-mwenzi unapowaeleza jinsi wanavyoweza kutumia habari unayozungumzia. (1 Pet. 3:8; 1 Yoh. 4:8) Hata mtume Paulo alipokuwa akishughulikia matatizo mazito katika Thesalonike, alihakikisha ametaja maendeleo mazuri ya kiroho ya ndugu na dada zake Wakristo waliokuwa huko. Pia alionyesha ana hakika kwamba wanataka kufanya yaliyo sawa kuhusu jambo alilokuwa akizungumzia. (1 The. 4:1-12) Huo ni mfano mzuri sana ambao tunaweza kuuiga.

      Je, kusudi la hotuba yako ni kuchochea akina ndugu ili wahubiri na kufundisha wengine habari njema? Basi wasaidie wawe na shauku na kuthamini pendeleo hilo. Lakini wakati uo huo ukumbuke kwamba watu wana uwezo tofauti-tofauti, na hata Biblia inaonyesha hivyo. (Mt. 13:23) Usiwafanye akina ndugu wahisi hatia. Waebrania 10:24 linatuhimiza ‘tuchocheane kwenye upendo na kazi zilizo bora.’ Tukiwachochea kwenye upendo, watatenda kwa makusudio mazuri. Badala ya kuwaamuru-amuru, tambua kwamba Yehova anataka tuwachochee ‘watii kwa njia ya imani.’ (Rom. 16:26) Basi, tukikumbuka mambo haya tutajaribu kuimarisha imani yetu na imani ya wengine.

      Kuwasaidia Wengine Kuona Faida ya Ujumbe Wetu. Unapohubiri, usisahau kuonyesha faida ya habari njema maishani mwao. Ili ufaulu, unahitaji kufahamu mambo yanayowahangaisha watu katika eneo lenu. Unawezaje kujua mambo hayo? Sikiliza habari kwenye redio au televisheni. Tazama ukurasa wa mbele wa gazeti la habari. Pia jaribu kuwafanya watu wazungumze, na uwasikilize wanapoongea. Unaweza kugundua wana matatizo makubwa kama vile kupoteza kazi, kulipa kodi ya nyumba, ugonjwa, kifo cha mshiriki wa familia, kupatwa na uhalifu, kutendwa isivyofaa na mtu mwenye mamlaka, kuvunjika kwa ndoa, kuwadhibiti watoto, na kadhalika. Je, Biblia inaweza kuwasaidia? Bila shaka, ndiyo.

      Inaelekea kwamba unapoanzisha mazungumzo utakuwa na jambo fulani akilini unalotaka kusema. Lakini ukiona kwamba mtu huyo ana jambo jingine linalomhangaisha sana, usisite kuzungumza naye jambo hilo ikiwezekana, au mwambie utamletea habari ambazo zinaweza kumsaidia. Ingawa tunaepuka ‘kujiingiza katika lile lisilotuhusu,’ tunafurahi kuwapa wengine mashauri ya Biblia ambayo wanaweza kutumia. (2 The. 3:11) Ni wazi kwamba jambo linalowavutia watu zaidi ni shauri la Biblia linalohusu maisha yao.

      Watu wasipoona jinsi ujumbe wetu unavyowahusu, wanaweza kukatiza mazungumzo haraka. Hata wakituruhusu tuendelee kuzungumza, tukikosa kuwaonyesha faida ya habari hiyo hawatafaidika. Lakini tukiwaonyesha faida ya ujumbe wetu, mazungumzo yetu yanaweza kubadili maisha yao.

      Unapofundisha watu Biblia, endelea kukazia jinsi wanavyoweza kutumia habari wanayojifunza. (Mit. 4:7) Wasaidie wanafunzi waelewe shauri, kanuni, na mifano inayopatikana katika Maandiko ambayo inawaonyesha jinsi ya kufuata njia za Yehova. Kazia faida ambazo watapata. (Isa. 48:17, 18) Kufanya hivyo kutawachochea wanafunzi wafanye mabadiliko yanayotakikana katika maisha yao. Wasaidie wampende Yehova na kuwa na tamaa ya kumpendeza, na pia wasaidie wachochewe na moyo wao wenyewe kutumia shauri la Neno la Mungu.

      JINSI YA KUFAULU

      • Mbali na kufikiria habari unapotayarisha hotuba, wafikirie pia wasikilizaji. Toa hotuba hiyo kwa njia ambayo itawafaidi kwelikweli.

      • Usieleze jinsi ambavyo wanaweza kutumia habari hiyo unapofikia mwisho tu wa hotuba. Bali eleza jinsi wanavyoweza kutumia habari hiyo kotekote katika hotuba.

      • Unapofanya matayarisho ya kuhubiri, fikiria mambo ambayo yanawahangaisha watu katika eneo lenu.

      • Unapohubiri, wasikilize watu kwa makini, na ubadilishe mahubiri yako kulingana na hali.

      MAZOEZI: Pitia matoleo ya Huduma Yetu ya Ufalme ambayo unaweza kupata, kisha chagua utangulizi mmoja au tangulizi mbili ambazo unaona zinafaa sana eneo lenu. Jaribu kuzitumia katika utumishi wa shambani.

  • Kutumia Maneno Yanayofaa
    Faidika na Elimu ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi
    • SOMO LA 24

      Kutumia Maneno Yanayofaa

      Unahitaji kufanya nini?

      Tumia maneno ya heshima na ya fadhili, yanayoeleweka kwa urahisi, yanayofanya usemi wako upendeze, na yenye mkazo na hisia zinazofaa. Fuata kanuni za sarufi katika mazungumzo yako.

      Kwa Nini Ni Muhimu?

      Maneno yanayofaa yanaonyesha unaheshimu ujumbe wako na pia jinsi unavyowaona wasikilizaji. Itikio la watu hutegemea maneno unayotumia.

      MANENO ni njia muhimu ya mawasiliano. Lakini ili maneno yetu yatimize kusudi fulani hususa, tunahitaji kuyachagua kwa makini. Neno ambalo linafaa wakati fulani huenda lisifae katika hali nyingine. Neno lenye kuchekesha likitumiwa vibaya linaweza kuwa ‘neno liumizalo.’ Mtu anaweza kutumia maneno kama hayo ikiwa anazungumza bila kufikiri, jambo linaloonyesha kwamba hajali. Kuna maneno ambayo yana maana mbili, mojawapo ikiwa maana mbaya au yenye kushusha heshima. (Mit. 12:18; 15:1) Kwa upande mwingine, “neno jema,” yaani neno la kutia moyo, humfurahisha yule anayelipokea. (Mit. 12:25) Si rahisi hata kwa mtu mwenye hekima kupata maneno yanayofaa. Biblia inatuambia kwamba Solomoni aliona anahitaji kutafuta “maneno yapendezayo” na “maneno ya kweli.”—Mhu. 12:10.

      Baadhi ya lugha zina desturi ya kutumia maneno fulani unapozungumza na mtu mwenye umri mkubwa au unapozungumza na mtu fulani mwenye mamlaka, na kutumia maneno tofauti unapoongea na marika wako au wale unaowazidi umri. Kupuuza desturi hizo huonwa kuwa kukosa adabu. Pia haifai kujibandikia heshima ambayo haikustahili kulingana na desturi. Biblia ina kanuni bora ya heshima kuliko hata kiwango cha heshima ambacho huenda kinaonyeshwa na sheria yenu au desturi zenu. Inawahimiza Wakristo ‘waheshimu watu wa namna zote.’ (1 Pet. 2:17) Wale ambao wanaheshimu wengine kutoka moyoni huzungumza na watu wa umri wote kwa njia ya heshima.

      Watu wengi ambao si Wakristo wa kweli husema maneno machafu yasiyo na adabu. Labda wanadhani kwamba wanakazia mambo wanapotumia maneno kama hayo. Au labda wanatumia maneno hayo kwa sababu wamepungukiwa sana na misamiati. Ikiwa mtu alizoea kutumia maneno kama hayo kabla ya kujifunza njia za Yehova, inaweza kuwa vigumu kuacha mazoea hayo. Lakini anaweza kufaulu. Roho ya Mungu inaweza kumsaidia mtu abadili usemi wake. Lakini mtu mwenyewe pia anapaswa kuwa tayari kujifunza maneno yanayofaa, yaani maneno yanayopendeza na kujenga, na kuyatumia kwa ukawaida.—Rom. 12:2; Efe. 4:29; Kol. 3:8.

      Lugha Inayoeleweka kwa Urahisi. Jambo kuu ni hili, usemi mzuri ni ule unaoeleweka kwa urahisi. (1 Kor. 14:9) Ikiwa wasikilizaji hawakuelewi kwa urahisi, ni kama unasema lugha ya kigeni.

      Kuna maneno ambayo huwa na maana ya kipekee miongoni mwa watu wa taaluma fulani-fulani. Labda wanatumia maneno hayo kila wakati. Lakini ukitumia maneno kama hayo katika hali tofauti, huenda watu wasikuelewe. Na hata unapotumia maneno ya kawaida, ukianza kufafanua mambo mengi yasiyo ya lazima, akili za wasikilizaji zitaanza kutangatanga.

      Msemaji mwenye kujali hutumia maneno ambayo hata wale wasio na elimu wanaelewa. Anamwiga Yehova kwa kuwajali “watu wa hali ya chini.” (Yobu 34:19, NW) Ikiwa ni lazima msemaji atumie neno ambalo wengi hawalifahamu, anapaswa kulitumia pamoja na maneno rahisi ili maana yake iwe wazi.

      Maneno rahisi ambayo yamefikiriwa vizuri huwasilisha mawazo vizuri sana. Ni rahisi kuelewa sentensi fupi-fupi na maneno rahisi. Unaweza kuchanganya sentensi kama hizo na sentensi ndefu-ndefu ili hotuba yako isisikike ni kama inakatika-katika. Lakini unapozungumzia mambo ambayo hasa unataka wasikilizaji wakumbuke, tumia maneno rahisi na sentensi fupi.

      Kutumia Semi Tofauti-Tofauti na Sahihi. Kuna maneno mazuri tele ya kutumia. Tumia semi tofauti-tofauti badala ya kutumia semi zilezile katika kila hali. Ukifanya hivyo, maneno yako yatapendeza na kujaa maana. Unawezaje kuongeza misamiati?

      Unaposoma, tia alama maneno ambayo huelewi vizuri kisha uyachunguze katika kamusi. Chagua maneno machache kati ya yale ambayo huelewi vizuri na ujitahidi kuyatumia unapopata nafasi. Yatamke vizuri na uyatumie kwa njia ambayo yanaeleweka kwa urahisi na wala si kwa kujielekezea tu fikira. Kuongeza misamiati kutakuwezesha kutumia semi tofauti-tofauti. Lakini jihadhari kwa sababu mtu anapotamka maneno vibaya au anapoyatumia vibaya, wengine watadhani kwamba hajui analosema.

      Kusudi la kuongeza misamiati ni kuweza kuwasiliana, wala si kujitukuza. Maneno yanayotatanisha na maneno marefu huelekeza fikira kwa msemaji. Tunapaswa kuwa na hamu ya kuwaeleza wengine habari muhimu na kufanya ipendeze wasikilizaji. Kumbuka ile mithali ya Biblia isemayo hivi: “Ulimi wa mwenye hekima hutamka maarifa vizuri.” (Mit. 15:2) Kutumia maneno mazuri, yanayofaa na kueleweka kwa urahisi, hufanya maneno yetu yafurahishe na kuchochea badala ya kuwa yenye kuchosha na yasiyopendeza.

      Unapoongeza misamiati, fikiria sana kutumia maneno yanayofaa. Maneno mawili yanaweza kuwa na maana moja lakini yatofautiane kidogo yakitumiwa katika hali tofauti. Ukitambua jambo hilo, unaweza kufanya usemi wako uwe wazi zaidi na kuepuka kuudhi wasikilizaji. Wasikilize kwa makini watu wanaoongea vizuri. Kuna kamusi ambazo huorodhesha kila neno na visawe vyake (maneno tofauti yanayokaribiana sana katika maana) na pia vitabu ambavyo vinaonyesha maneno ya kinyume. Kwa njia hiyo, mbali na kupata maneno tofauti-tofauti yanayofafanua wazo lilelile, pia unapata maana tofauti ndogo-ndogo ya wazo hilo. Jambo hilo linasaidia sana unapotafuta neno linalofaa hali fulani. Lakini, kabla ya kuanza kutumia neno jipya, hakikisha unafahamu maana yake, matamshi yake, na jinsi linavyotumiwa.

      Maneno yenye maana hususa hueleweka wazi kuliko maneno yanayotaja mambo kwa ujumla. Msemaji anaweza kusema: “Wakati huo, watu wengi wakawa wagonjwa.” Au anaweza kusema: “Miezi michache tu baada ya Vita ya Kwanza ya Ulimwengu, watu wapatao 21,000,000 walikufa kwa ugonjwa wa homa ya Hispania.” Ona tofauti kubwa inayotokea msemaji akionyesha wazi jambo ambalo anamaanisha kwa kutumia maneno kama “wakati huo,” “watu wengi” na “wakawa wagonjwa”! Ili uwe hususa unahitaji kujua mambo yanayohusiana na habari unayozungumzia na vilevile unahitaji kuchagua kwa makini maneno yanayofaa.

      Pia maneno yanayofaa yanaweza kukusaidia kutaja jambo kuu bila kutumia maneno mengi. Ukitumia maneno mengi, jambo kuu haliwi wazi. Maneno rahisi huwasaidia wasikilizaji kushika mambo muhimu na kuyakumbuka. Husaidia watu kuelewa ujuzi sahihi. Mafundisho ya Yesu Kristo yalikuwa ya pekee sana kwa sababu alitumia lugha rahisi. Mwige Yesu. (Ona mifano iliyoko katika Mathayo 5:3-12 na Marko 10:17-21.) Fanya mazoezi ya kuzungumza kwa maneno machache ambayo umechagua kwa makini.

      Maneno Yanayoonyesha Mkazo, Hisia, na Yanayovutia. Unapoongeza misamiati, mbali na kufikiria maneno mapya fikiria pia maneno yenye miundo fulani hususa. Kwa mfano, fikiria vitenzi vinavyotia mkazo; vivumishi vinavyopendeza; na maneno yanayoonyesha uchangamfu, fadhili, au bidii.

      Biblia imejaa mifano ya lugha iliyojaa maana. Kupitia nabii Amosi, Yehova alihimiza hivi: “Tafuteni mema, na wala si mabaya . . . Yachukieni mabaya; yapendeni mema.” (Amo. 5:14, 15, italiki ni zetu.) Nabii Samweli alimtangazia Mfalme Sauli hivi: “Leo, BWANA amekurarulia ufalme wa Israeli.” (1 Sam. 15:28, italiki ni zetu.) Yehova alitumia maneno yasiyoweza kusahaulika kwa urahisi alipokuwa akizungumza na Ezekieli: “Nyumba yote ya Israeli wana vipaji vigumu, na mioyo yenye ukaidi.” (Eze. 3:7, italiki ni zetu.) Yehova alikazia uzito wa makosa ya Israeli kwa kuuliza hivi: “Je! mwanadamu atamwibia Mungu? Lakini ninyi mnaniibia mimi.” (Mal. 3:8, italiki ni zetu.) Danieli alipokuwa akieleza juu ya jaribu la imani kule Babiloni, alikoleza usemi wake aliposema kwamba ‘Nebukadreza alijaa ghadhabu’ kwa sababu Shadraka, Meshaki, na Abednego walikataa kuabudu sanamu yake, akaamuru wafungwe na kutupwa ndani ya “tanuru iliyokuwa ikiwaka moto.” Danieli anatusaidia kufahamu ukali wa moto ule anaposema kwamba mfalme aliamuru watu wake “watie moto ile tanuru mara saba kuliko desturi yake ya kutiwa moto,” ikawa moto hivi kwamba watu wa mfalme wakafa walipoikaribia tanuru hiyo. (Dan. 3:19-22, italiki ni zetu.) Yesu alipozungumza na watu wa Yerusalemu siku chache kabla ya kifo chake, alisema hivi kwa hisia nyingi: “Ni mara nyingi kadiri gani nilitaka kuwakusanya watoto wako pamoja, kama vile kuku hukusanya vifaranga vyake pamoja chini ya mabawa yake! Lakini nyinyi watu hamkutaka hilo. Tazameni! Nyumba yenu mmeachiwa hali ya ukiwa.”—Mt. 23:37, 38.

      Maneno ambayo yamechaguliwa vizuri yanaweza kutokeza picha dhahiri akilini mwa wasikilizaji. Ukitumia maneno yanayogusa hisia, ni kana kwamba wasikilizaji wanaona na kugusa mambo unayosema, wanaonja na kunusa vyakula unavyotaja, na kusikia sauti unazofafanua na watu unaonukuu. Wasikilizaji watakusikiliza kwa makini kwa sababu unafanya mambo yawe halisi.

      Maneno yanayotokeza mambo kwa njia dhahiri yanaweza kufanya watu wacheke au walie. Yanaweza kumpa mtu tumaini, na kumfanya aliyeshuka moyo awe na hamu ya kuishi na kumchochea ampende Muumba. Watu ulimwenguni kote wamevutiwa sana na tumaini linalotokezwa na maandiko ya Biblia kama Zaburi 37:10, 11, 34; Yohana 3:16; na Ufunuo 21:4, 5.

      Unaposoma Biblia pamoja na vichapo vya “mtumwa mwaminifu na mwenye busara,” utaona unamna-namna wa maneno. (Mt. 24:45) Usiyasome tu na kuyasahau. Chagua yale yanayokufurahisha, uyaongeze kwenye msamiati wako.

      Usemi Unaopatana na Kanuni za Sarufi. Watu wengine wanatambua kwamba nyakati nyingine usemi wao haufuati kanuni za sarufi. Wanaweza kufanya nini?

      Kama ungali mwanafunzi shuleni, tumia nafasi hiyo kujifunza sarufi na kuchagua maneno yanayofaa. Kama huna hakika na kanuni fulani ya sarufi, mwulize mwalimu. Usijifunze sarufi ili ujue tu kutumia lugha. Una kichocheo ambacho huenda wanafunzi wengine hawana. Unataka kuwa mhudumu bora wa habari njema.

      Vipi ikiwa wewe ni mtu mzima na unazungumza lugha ya kigeni ambayo umejifunza baadaye maishani? Au labda hukuweza kujifunza vizuri lugha yako shuleni. Usivunjike moyo. Badala yake, tia bidii ili ufanye maendeleo kwa ajili ya habari njema. Sisi hujifunza mambo mengi kuhusu sarufi tunapowasikiliza wengine wakiongea. Basi sikiliza kwa makini wasemaji wenye uzoefu wanapotoa hotuba. Unaposoma Biblia na vichapo vinavyotegemea Biblia, tazama muundo wa sentensi, maneno yanayotumiwa katika fungu moja, na mazingira ambamo maneno hayo yametumiwa. Fuata mifano hiyo katika usemi wako.

      Watumbuizaji na waimbaji mashuhuri wanaweza kutumia maneno na usemi unaovunja kanuni za sarufi. Na watu huwaiga. Mara nyingi walanguzi wa dawa za kulevya na wengine wenye maisha ya uhalifu au yasiyo ya maadili hutumia lugha yao wenyewe, wakibadili kabisa maana ya maneno fulani katika usemi wao. Haifai Mkristo kuwaiga watu hao. Kuwaiga kunafanya tuwe kama wao na kuishi maisha kama yao.—Yn. 17:16.

      Uwe na zoea la kutumia usemi mzuri kila siku. Ukiacha usemi wako wa kawaida uwe wa kizembe, usitarajie kuzungumza vizuri katika pindi za pekee. Lakini kama kwa kawaida unatumia usemi mzuri, utazungumza kwa urahisi na kwa njia ya kawaida unapotoa hotuba jukwaani au unapohubiri kuhusu kweli.

      JINSI YA KUFAULU

      • Chagua jambo moja kati ya madokezo ambayo yameonyeshwa katika somo hili ambalo unataka kufanyia kazi. Lifanyie kazi kwa mwezi mmoja hivi au zaidi.

      • Kumbuka kusudi lako unaposoma. Likumbuke unaposikiliza wasemaji bora. Andika maneno ambayo ungependa kutumia katika usemi wako. Baada ya siku moja au mbili, tumia kila mojawapo ya maneno uliyoandika.

      MAZOEZI: Unapotayarisha Funzo la Mnara wa Mlinzi au Funzo la Kitabu la Kutaniko juma hili, chagua maneno machache ambayo huwezi kuyafafanua vizuri. Yatafute katika kamusi ikiwa inapatikana, au jadiliana maana yake na mtu ambaye anafahamu maneno vizuri.

      Misamiati ninayotaka kutumia

      Ili nisitumie maneno yaleyale na ili niwe sahihi Ili kuonyesha mkazo, hisia, au usemi unaopendeza

      ․․․․․․․․․․․․․․ ․․․․․․․․․․․․․․ ․․․․․․․․․․․․․․ ․․․․․․․․․․․․․․

      ․․․․․․․․․․․․․․ ․․․․․․․․․․․․․․ ․․․․․․․․․․․․․․ ․․․․․․․․․․․․․․

      ․․․․․․․․․․․․․․ ․․․․․․․․․․․․․․ ․․․․․․․․․․․․․․ ․․․․․․․․․․․․․․

      ․․․․․․․․․․․․․․ ․․․․․․․․․․․․․․ ․․․․․․․․․․․․․․ ․․․․․․․․․․․․․․

      ․․․․․․․․․․․․․․ ․․․․․․․․․․․․․․ ․․․․․․․․․․․․․․ ․․․․․․․․․․․․․․

      ․․․․․․․․․․․․․․ ․․․․․․․․․․․․․․ ․․․․․․․․․․․․․․ ․․․․․․․․․․․․․․

      ․․․․․․․․․․․․․․ ․․․․․․․․․․․․․․ ․․․․․․․․․․․․․․ ․․․․․․․․․․․․․․

      ․․․․․․․․․․․․․․ ․․․․․․․․․․․․․․ ․․․․․․․․․․․․․․ ․․․․․․․․․․․․․․

      ․․․․․․․․․․․․․․ ․․․․․․․․․․․․․․ ․․․․․․․․․․․․․․ ․․․․․․․․․․․․․․

  • Kutumia Muhtasari
    Faidika na Elimu ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi
    • SOMO LA 25

      Kutumia Muhtasari

      Unahitaji kufanya nini?

      Unahitaji kuzungumza ukitegemea muhtasari ambao umeandikwa au muhtasari ambao umeshika akilini, badala ya kusoma kila neno.

      Kwa Nini Ni Muhimu?

      Kutayarisha muhtasari kunakusaidia kupanga mambo unayotaka kusema. Kutumia muhtasari kunakuwezesha kutoa hotuba kwa njia ya mazungumzo na kuzungumza kutoka moyoni.

      WATU wengi huogopa kutumia muhtasari. Wao hufurahia zaidi ikiwa wameandika au kukariri kila jambo wanalotaka kusema.

      Lakini ukweli ni kwamba kila siku sisi huzungumza bila kutumia muhtasari. Sisi huzungumza na jamaa zetu na marafiki bila kutumia muhtasari. Sisi huzungumza bila muhtasari tunapokuwa katika huduma. Hatutumii muhtasari tunaposali kutoka moyoni, iwe tunasali binafsi au kwa niaba ya wengine.

      Unapotoa hotuba, je, kuna tofauti yoyote kati ya kusoma hotuba yako na kutumia muhtasari? Ingawa kusoma hotuba kunaweza kufanya utumie maneno yanayofaa na yaliyo sahihi, kufanya hivyo hakugusi mioyo. Mara nyingi ukisoma sentensi chache, utaanza kufuata mtindo fulani ambao ni tofauti na kawaida yako ya kuzungumza. Akili yako ikizama katika maandishi yako na kusahau wasikilizaji, huenda wengi wasisikilize kwa makini kama ambavyo wangesikiliza iwapo wangeona kwamba unawajali kweli na habari unayozungumzia inawahusu. Njia bora zaidi ya kutoa hotuba inayochochea kabisa ni kuitoa bila kutazama sana maandishi.

      Kusudi la Shule ya Huduma ya Kitheokrasi ni kutusaidia katika maisha ya kawaida. Tunapokutana na marafiki, je, sisi hutoa karatasi na kuwasomea mambo tunayotaka kuwaeleza eti kuhakikisha tunatumia maneno yanayofaa zaidi? Tunapokuwa katika utumishi wa shambani, hatubebi maandishi ya kusoma, eti kwa sababu tunaogopa tutasahau mambo fulani ambayo tungependa kuwaeleza watu. Unapotoa onyesho katika shule kuhusu kutoa ushahidi katika hali hizo, jizoeze kuzungumza kwa njia ya kawaida kwa kadiri iwezekanavyo. Ukitayarisha vizuri, utaona kwamba muhtasari ambao umeandika au umeshika akilini hutosha kukukumbusha mambo makuu ambayo unataka kuzungumzia. Lakini unawezaje kufaulu kutumia muhtasari?

      Panga Mambo Unayotaka Kuzungumzia. Ili uweze kutumia muhtasari, unahitaji kupanga mambo unayotaka kuzungumzia. Hiyo haimaanishi kuchagua maneno ambayo unapanga kutumia. Inamaanisha tu kufikiri kabla ya kuzungumza.

      Kwa kawaida, mtu ambaye huzungumza bila kufikiri hushtukia amesema mambo ambayo baadaye anajutia. Mwingine naye anaweza kuzungumza bila mpango, akitangatanga kutoka jambo moja hadi jingine. Unaweza kusuluhisha matatizo hayo vizuri kwa kutua na kupanga kwa ufupi mawazo yako akilini kabla ya kuzungumza. Kwanza kumbuka kusudi lako, kisha chagua mambo ambayo unahitaji kufanya ili kutimiza kusudi hilo, kisha uzungumze.

      Je, unajitayarisha kwa ajili ya utumishi wa shambani? Panga mkoba wako na ufikirie mambo utakayosema. Ukiamua kutumia mmojawapo wa utangulizi katika Huduma Yetu ya Ufalme, uusome mara kadhaa ili ukumbuke vizuri mambo makuu. Taja mambo hayo katika sentensi moja au mbili. Tumia maneno ya utangulizi huo kwa kupatana na hali zako na hali za eneo lenu. Inafaa kuwa na muhtasari fulani akilini. Muhtasari huo unaweza kuwa na nini? (1) Kwenye utangulizi, unaweza kutaja jambo ambalo linawahangaisha watu wengi katika eneo lenu. Mpe nafasi mwenye nyumba atoe maoni yake. (2) Fikiria jambo fulani hususa ambalo unaweza kuzungumza naye kuhusu habari hiyo, pamoja na andiko moja au maandiko mawili yanayoonyesha ahadi ya Mungu ya kusuluhisha tatizo hilo. Ukipata fursa, kazia kwamba Yehova atatatua tatizo hilo kupitia Ufalme wake, serikali yake ya mbinguni. (3) Mtie moyo mwenye nyumba achukue hatua juu ya jambo ambalo umezungumzia. Unaweza kumtolea kichapo au Funzo la Biblia na kufanya mipango hususa ya kuendeleza mazungumzo.

      Katika hali hizo utahitaji tu muhtasari ambao umeshika akilini. Ukitaka kuangalia muhtasari ulioandika kabla ya kufanya ziara ya kwanza, muhtasari huo uwe na utangulizi mfupi tu, andiko moja au mawili, na umalizio mfupi. Kutayarisha muhtasari kama huo na kuutumia hutusaidia tusitangetange katika mazungumzo. Pia kunatusaidia kumwachia mwenye nyumba ujumbe ulio wazi ambao anaweza kukumbuka kwa urahisi.

      Ikiwa swali fulani au kipingamizi fulani huzushwa katika eneo lenu, inaweza kufaa kufanya utafiti kulihusu. Kwa kawaida, unahitaji tu mambo makuu mawili au matatu pamoja na maandiko yanayoyaunga mkono. “Vichwa vya Biblia vya Mazungumzo” au vichwa vidogo vyenye maandishi mazito vinavyopatikana katika kitabu Kutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko vinaweza kuwa na muhtasari hususa unaohitaji. Unaweza kupata mnukuo mzuri katika kichapo kingine ambao unaweza kutumia pia. Tayarisha muhtasari mfupi, ambatanisha nakala ya mnukuo huo, kisha uziweke pamoja na vifaa unavyotumia katika utumishi wa shambani. Mwenye nyumba anapozusha swali lile au kipingamizi kile, mjulishe kwamba ungefurahi kumwambia sababu zinazokufanya uamini jambo hilo. (1 Pet. 3:15) Tumia muhtasari huo kumjibu.

      Ikiwa utatoa sala mbele ya familia, kikundi cha funzo, au kutaniko, ni vizuri kupanga mambo utakayosema. Kulingana na Luka 11:2-4, Yesu aliwapa wanafunzi wake muhtasari rahisi wa sala yenye maana. Na wakati wa kuweka hekalu wakfu huko Yerusalemu, Solomoni alitoa sala ndefu. Bila shaka alifikiria kimbele jambo la kusema. Kwanza alitaja Yehova na ahadi yake kwa Daudi; kisha akataja hekalu; kisha akataja hali hususa na makundi hususa ya watu. (1 Fal. 8:22-53) Mifano hiyo inaweza kutufaidi.

      Muhtasari Wako Uwe Rahisi. Je, muhtasari wako ni wa kutoa hotuba? Muhtasari huo uwe na habari gani?

      Kumbuka kwamba kusudi la muhtasari ni kukusaidia kukumbuka mawazo unayotaka kuwasilisha. Labda ungependa kuandika utangulizi wenye sentensi chache. Lakini baada ya hapo kazia akili mawazo unayotaka kuwasilisha na wala si maneno unayotaka kutumia. Tumia sentensi fupi-fupi unapoandika mawazo hayo. Mambo makuu machache ambayo unapanga kutumia yawe dhahiri katika muhtasari wako. Unaweza kuyafanya yawe dhahiri kwa kuyaandika kwa herufi kubwa, kuyapiga mstari, au kuyatia alama kwa rangi tofauti. Chini ya kila jambo kuu, orodhesha mambo ambayo unataka kutumia ili kulifafanua jambo kuu. Andika maandiko ambayo unapanga kusoma. Mara nyingi ni afadhali kusoma maandiko hayo katika Biblia. Andika mifano ambayo unataka kutumia. Pia unaweza kuwa na mnukuo mzuri uliopata katika vichapo vya kilimwengu ambao unafaa kutumiwa. Maandishi yako yawe na mambo hususa unayotaka kutaja. Ni rahisi zaidi kutumia muhtasari nadhifu.

      Wengine hutumia mihtasari ambayo ina mambo machache kabisa. Muhtasari unaweza kuwa na maneno machache makuu, maandiko ambayo msemaji atayanukuu kutoka akilini, na michoro au picha zinazomwezesha kukumbuka mambo anayotaka kusema. Kwa maandishi hayo tu, msemaji anaweza kutoa hotuba inayofuatana vizuri na kwa njia ya mazungumzo. Na hilo ndilo lengo la somo hili.

      Kuna mazungumzo yanayohusu “Kutayarisha Muhtasari” katika ukurasa wa 39 hadi 42 wa kitabu hiki. Kuna faida kubwa ya kusoma habari hiyo unaposhughulikia somo hili la “Kutumia Muhtasari.”

      Jinsi ya Kutumia Muhtasari. Wakati huu kusudi lako si kutayarisha muhtasari wa hotuba, bali ni kuutumia muhtasari vizuri.

      Hatua ya kwanza ya kutumia muhtasari ni matayarisho ya kuutoa. Chunguza kichwa kikuu, soma kila jambo kuu, na utambue uhusiano uliopo kati ya mambo hayo makuu na kichwa kikuu. Tazama muda ambao unaweza kutumia kwa kila jambo kuu. Kisha chunguza jambo kuu la kwanza. Pitia sababu zinazoonyeshwa, maandiko, na mifano ambayo unataka kutumia katika sehemu hiyo. Pitia sehemu hiyo mara kadhaa mpaka uielewe vizuri. Fanya hivyo na kila mojawapo ya mambo mengine makuu. Fikiria mambo ambayo unaweza kukosa kutaja hali ikikulazimu ili umalize kwa wakati. Kisha pitia hotuba yote. Kazia mambo makuu, na wala si maneno. Usikariri hotuba hiyo.

      Unapotoa hotuba, unapaswa kuwatazama wasikilizaji kwa njia nzuri. Mara nyingi baada ya kusoma andiko, unapaswa kusababu juu ya andiko hilo ukitumia Biblia bila kurudia maandishi yako. Vilevile ukitoa mfano, uutoe kama ambavyo ungewaeleza marafiki wako badala ya kusoma mfano huo katika maandishi yako. Unapozungumza, usitazame-tazame maandishi yako na kusoma kila sentensi. Zungumza kwa hisia, nawe utagusa mioyo ya wale wanaokusikiliza.

      Utakapokuwa stadi wa kutoa hotuba ukitumia muhtasari, utakuwa umepiga hatua kubwa ya kuwa msemaji mzuri unapohutubia watu.

      JINSI YA KUFAULU

      • Fikiria kabisa faida za kutumia muhtasari kuzungumza.

      • Katika mazungumzo ya kawaida, panga mambo unayotaka kusema kabla ya kuzungumza.

      • Ili upate ujasiri unaohitaji wa kutumia muhtasari, sali kwa Yehova, na uwe na mazoea ya kushiriki sana katika mikutano ya kutaniko.

      • Muhtasari wako usiwe na mambo mengi mno, na uwe rahisi kusoma unapoutazama.

      • Tayarisha hotuba kwa kupitia mawazo unayotaka kuwasilisha na wala si kukariri maneno.

      MAZOEZI: Kabla ya kwenda katika utumishi wa shambani juma hili, tayarisha muhtasari akilini mwako unaohusu jambo hususa ambalo unataka kusema. (Ona ukurasa wa 167, fungu la 3.) Chunguza ni mara ngapi unaweza kufaulu kuzungumza jinsi ulivyopanga unapokuwa katika utumishi au angalau mara ambazo ulifaulu kutaja jambo kuu la ujumbe wako.

  • Habari Inayofuatana Vizuri
    Faidika na Elimu ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi
    • SOMO LA 26

      Habari Inayofuatana Vizuri

      Unahitaji kufanya nini?

      Unahitaji kupanga habari unayozungumzia kwa njia inayoonyesha wazi jinsi mambo unayozungumzia yanavyohusiana, maamuzi unayofikia, au kusudi lako.

      Kwa Nini Ni Muhimu?

      Habari ikitolewa kwa njia inayofuatana vizuri, ni rahisi kwa wasikilizaji kuielewa, kuikubali, na kuikumbuka.

      KABLA ya kupanga habari kwa njia inayofuatana vizuri, unahitaji kuwa na lengo fulani. Je, lengo lako ni kufundisha wengine jambo fulani hususa—imani fulani, maoni fulani, sifa fulani, mwenendo fulani, au maisha ya aina fulani? Je, unakusudia kuunga mkono jambo fulani au kulikanusha? Je, unataka wasikilizaji wathamini jambo fulani au unataka kuwachochea wachukue hatua fulani? Iwe utazungumza na mtu mmoja au utahutubia watu wengi, ili ufaulu unahitaji kujua mambo ambayo tayari wanafahamu kuhusu habari hiyo na maoni yao kuihusu. Baada ya kufanya hivyo, panga habari kwa njia itakayokusaidia kutimiza kusudi lako.

      Matendo 9:22 linaripoti hivi kuhusu huduma ya Sauli (Paulo) kule Damasko: “Alikuwa akiwatatanisha Wayahudi waliokaa katika Damasko alipokuwa akithibitisha kwa mawazo yenye kufuatana vizuri kwamba huyu ndiye Kristo.” Uthibitisho huo wenye kufuatana vizuri ulihusu nini? Kama ilivyoonyeshwa na huduma ya Paulo ya baadaye kule Antiokia na Thesalonike, kwanza alitumia ule msingi wa kwamba Wayahudi walikubali Maandiko ya Kiebrania na walidai kuamini mambo ambayo Maandiko yanasema kumhusu Mesiya. Pili, Paulo alichagua Maandiko ambayo yalihusu maisha ya Mesiya na huduma yake. Aliyanukuu na kuyalinganisha na matukio yaliyomhusu Yesu. Kisha akafikia uamuzi wa wazi, kwamba Yesu ndiye Kristo, au Mesiya. (Mdo. 13:16-41; 17:2, 3) Hata wewe ukieleza wengine kweli ya Biblia kwa njia inayofuatana vizuri, hiyo kweli inaweza kuwavutia.

      Kupanga Hotuba. Unaweza kupanga habari kwa njia kadhaa zinazofuatana vizuri. Ikifaa, unaweza kutumia njia kadhaa kwa wakati mmoja. Ebu ona njia chache tu unazoweza kutumia.

      Kupanga habari kulingana na vichwa tofauti-tofauti: Huku ni kupanga habari katika sehemu mbalimbali, kila sehemu ikihusiana sana na lengo lako. Sehemu hizo zinaweza kuwa mambo muhimu yanayofanya habari yako ieleweke. Au zinaweza kuwa mambo hususa yanayothibitisha jambo au yanayolipinga. Mambo mengine yanayohusiana na habari hiyo yanaweza kutajwa au kuachwa bila kutajwa ikitegemea wasikilizaji wako au lengo lako.

      Ebu ona mfano mmoja wa kupanga habari kulingana na vichwa tofauti-tofauti. Hotuba fupi inayohusu jina la Mungu inaweza kutia ndani (1) kwa nini ni muhimu kujua jina la Mungu, (2) Mungu anaitwaje, na (3) jinsi tunavyoweza kuliheshimu jina hilo.

      Tunaweza kujifunza mengi kuhusu kupanga habari kulingana na vichwa mbalimbali kwa kuchunguza vichapo ambavyo vimetayarishwa na “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” ambavyo vinatumiwa kuongoza mafunzo ya Biblia ya nyumbani. (Mt. 24:45) Mara nyingi vichapo hivyo hutia ndani vichwa ambavyo vinaweza kuwasaidia wanafunzi kufahamu kweli za Biblia kwa ujumla. Vichapo vikubwa hutumia vichwa vidogo kugawanya kila sura. Kila kichwa humtayarisha mwanafunzi kwa ajili ya mambo yanayofuata na kumsaidia kupata picha kamili ya habari inayozungumziwa.

      Kisababishi na matokeo: Kuzungumzia kisababishi na matokeo ya mambo ni njia nyingine ya kufuatanisha habari vizuri.

      Ikiwa unahutubia watu au unaongea na watu wanaohitaji kufikiria kwa makini matokeo ya jambo wanalofanya au wanalopanga kufanya, njia hii inaweza kufaa sana. Mithali sura ya 7 ina mfano bora wa njia hii. Inafafanua wazi jinsi kijana asiye na ujuzi ambaye ‘hana akili’ (kisababishi) anavyojihusisha na kahaba na kupata madhara mabaya sana (matokeo).—Mit. 7:7.

      Ili kukazia zaidi jambo unalozungumzia, unaweza kulinganisha matokeo mabaya yanayowapata wale wanaoshindwa kufuata njia za Yehova na matokeo mazuri wanayopata wale wanaomsikiliza Yehova. Musa alifanya hivyo alipochochewa na roho ya Yehova wakati alipozungumza na taifa la Israeli kabla ya kuingia katika Nchi ya Ahadi.—Kum., sura ya 28.

      Nyakati nyingine, ni vizuri kuanzisha mazungumzo kwa kutaja matokeo ya hali fulani kisha uzungumzie kisababishi. Mara nyingi hiyo inamaanisha kutaja tatizo kisha kuzungumzia suluhisho lake.

      Tatizo na suluhisho: Unapozungumzia tatizo linalohangaisha watu ukiwa katika huduma ya shambani na uonyeshe kwamba kuna suluhisho bora, watu wanaweza kuvutiwa kusikiliza. Huenda ukataja tatizo hilo au huenda yule unayezungumza naye akalitaja.

      Labda mnazungumzia kuzeeka na kufa, kuenea kwa uhalifu, au ukosefu mwingi wa haki. Huhitaji mazungumzo marefu kuthibitisha kwamba kwa kweli kuna tatizo hilo kwa sababu jambo hilo ni wazi. Anza kwa kutaja tu tatizo fulani, kisha zungumzia suluhisho ambalo Biblia inataja.

      Pia inawezekana kwamba mtu ana tatizo fulani, labda ni magumu ya kuwa mzazi asiye na mwenzi wa ndoa, kuvunjika moyo kwa sababu ya ugonjwa unaomsumbua, au magumu ya kutendwa vibaya na mtu mwingine. Ili ufaulu kabisa, ni lazima kwanza uwe msikilizaji mzuri. Biblia ina habari muhimu kuhusu matatizo hayo yote. Lakini tunahitaji kuitumia kwa busara. Ili umfaidi mtu, inafaa utaje mambo halisi. Hakikisha kwamba anaelewa wazi ikiwa unazungumzia suluhisho la kudumu, suluhisho la muda mfupi, au kama unazungumzia jinsi ya kukabiliana na tatizo ambalo haliwezi kusuluhishwa katika mfumo huu wa mambo. Yaani, hakikisha kwamba mambo unayomweleza kupitia Maandiko yanaunga mkono mkataa unaofikia. Usipofanya hivyo, huenda asielewe suluhisho unalotaja.

      Kwa kufuata utaratibu wa matukio: Habari nyingine hufaa kutolewa kwa kufuata utaratibu wa matukio. Kwa mfano, katika kitabu cha Kutoka, yale Mapigo Kumi yameorodheshwa kwa kufuata utaratibu wa jinsi yalivyotokea. Katika Waebrania sura ya 11, orodha ya mtume Paulo ya wanaume na wanawake wenye imani wanaostahili kuigwa inafuata utaratibu wa wakati.

      Kusimulia matukio yaliyopita kwa utaratibu wa jinsi yalivyotokea kunaweza kuwasaidia wasikilizaji waelewe jinsi hali fulani zilivyotokea. Hali hii inahusu historia ya siku hizi na vilevile matukio ya nyakati za Biblia. Kwa hiyo, unaweza kutumia kwa pamoja ile njia ya kufuata utaratibu wa jinsi mambo yalivyotokea na njia ya kuzungumzia kisababishi na matokeo yake. Kama umepanga kuzungumzia matukio ya wakati ujao kama yanavyoonyeshwa katika Biblia, wasikilizaji wanaweza kuelewa kwa urahisi na kukumbuka mambo ukitaja matukio hayo kwa kufuata utaratibu wa jinsi yatakavyotokea.

      Kuzungumzia matukio kwa kufuata utaratibu wa jinsi yalivyotokea hakumaanishi kwamba ni lazima nyakati zote uanze na tukio la kwanza. Nyakati nyingine, inaweza kuwa bora kusimulia kwanza sehemu yenye kutazamisha sana ya masimulizi hayo. Kwa mfano, unaposimulia jambo, unaweza kuchagua pindi ambapo uaminifu wa mtu kwa Mungu ulijaribiwa. Baada ya kuamsha upendezi kwa kusimulia sehemu hiyo kwanza, unaweza kusimulia mambo mengine yaliyoongoza kwenye hali hiyo kwa kufuata utaratibu wa jinsi yalivyotokea.

      Kutumia Habari Zinazohusika Pekee. Hata iwe umepanga habari yako kwa njia gani, tumia tu habari zinazohusika. Fikiria kichwa kikuu cha hotuba unapochagua habari ya kutumia. Pia wafikirie wasikilizaji. Jambo fulani linaweza kufaa sana wasikilizaji fulani ilhali linaweza kupita kiasi likitajwa kwa wasikilizaji wengine. Pia uwe na hakika ya kwamba habari zote unazotaka kutumia zitakusaidia kutimiza kusudi lako. Usipofanya hivyo, hotuba yako haitakuwa na matokeo hata ingawa inaweza kuwa yenye kupendeza.

      Unapofanya utafiti unaweza kupata habari nyingi zenye kupendeza zinazohusiana na habari yako. Utumie habari hizo kwa kadiri gani? Huwezi kufaulu ukiwalemea wasikilizaji kwa habari nyingi mno. Ni rahisi kukumbuka mambo machache yanayofafanuliwa vizuri kuliko mambo mengi yanayotajwa kwa mbio za kukata na shoka. Haimaanishi kwamba mambo madogo-madogo yenye kupendeza yasitajwe. Lakini mambo hayo yasikukengeushe kwenye lengo lako. Ona jinsi mambo madogo-madogo kama hayo yalivyoingizwa kwa busara katika Biblia kwenye Marko 7:3, 4 na Yohana 4:1-3, 7-9.

      Unapomaliza kuzungumzia jambo moja na kuanza jingine, jihadhari usikatishe mazungumzo kwa ghafula na kupoteza wasikilizaji. Ili mawazo yatokeze maana yakiwa pamoja, unaweza kuyaunganisha. Unaweza kutumia fungu fulani au sentensi nzima ambayo inaonyesha uhusiano ulioko kati ya mawazo hayo. Katika lugha nyingi, maneno rahisi yanaweza kutumiwa kuonyesha uhusiano ulioko kati ya wazo unaloanza kuzungumzia na wazo lililotangulia.

      Ukitumia habari zinazohusika pekee na kuzipanga kwa njia inayofuatana vizuri, zote zitakusaidia kutimiza kusudi lako.

      JIULIZE . . .

      • Lengo langu ni nini?

      • Je, kila jambo kuu linahusiana na lengo hilo?

      • Je, habari nilizochagua zinahusu mahitaji ya wasikilizaji?

      • Je, nimepanga habari kwa njia inayoongoza vizuri akili za wasikilizaji kutoka wazo moja hadi jingine bila kuacha mapengo kati ya mawazo hayo?

      MAZOEZI: Baada ya kusoma somo hili, lisome tena kwa mwendo wa kiasi, ukifikiria jambo kuu la kila fungu. Jaribu kuona jinsi kila fungu linavyochangia lengo la somo hili lote.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki