SOMO LA 22
Kutumia Maandiko Vizuri
KUFUNDISHA wengine si kusoma tu maandiko ya Biblia. Mtume Paulo alimwandikia hivi mshiriki wake Timotheo: “Fanya yote uwezayo kabisa ili ujionyeshe mwenyewe kuwa mwenye kukubaliwa na Mungu, mtenda-kazi asiye na lolote la kuaibikia, ukilitumia sawasawa neno la ile kweli.”—2 Tim. 2:15.
Ili tufanye hivyo, ni lazima tufafanue maandiko kulingana na mafundisho ya Biblia. Hiyo inamaanisha tufikirie muktadha badala ya kuchagua tu maneno yanayotupendeza na kutoa maoni yetu wenyewe. Kupitia nabii Yeremia, Yehova aliwaonya watu wasiwasikilize manabii waliodai kusema maneno yake lakini kumbe walisema “maono ya mioyo yao wenyewe.” (Yer. 23:16) Mtume Paulo aliwaonya Wakristo wasichafue Neno la Mungu kwa falsafa za wanadamu alipoandika: “Tumeyakataa kabisa mambo ya kichinichini yaliyo ya kuaibikia, si kutembea kwa ujanja, wala tukilighushi neno la Mungu.” Siku hizo, wauzaji wa divai wenye pupa walikuwa wakitia divai maji ili iwe nyingi wapate pesa zaidi. Sisi hatughushi Neno la Mungu kwa kulichanganya na falsafa za wanadamu. Paulo alitangaza kwamba “sisi si wachuuzi wa neno la Mungu kama watu wengi walivyo, bali tunasema kwa weupe wa moyo, ndiyo, tukiwa waliotumwa kutoka kwa Mungu, mbele ya Mungu, kwa ushirika na Kristo.”—2 Kor. 2:17; 4:2.
Nyakati nyingine unaweza kunukuu andiko ili kukazia kanuni fulani. Biblia imejaa kanuni zenye mwongozo bora zinazotusaidia kushughulika na hali mbalimbali za maisha. (2 Tim. 3:16, 17) Lakini hakikisha kwamba unatumia kwa usahihi kanuni hizo na usitumie andiko vibaya, ukifanya andiko lionekane kana kwamba linasema jambo ambalo wewe unataka liseme. (Zab. 91:11, 12; Mt. 4:5, 6) Ni lazima utumie andiko kulingana na kusudi la Yehova, kupatana na Neno lote la Mungu.
‘Kulitumia sawasawa neno la ile kweli’ pia kunatia ndani kufahamu vile Biblia inavyosema. Biblia si “rungu” la kutwangia watu wengine. Walimu wa kidini waliompinga Yesu Kristo walinukuu Maandiko, lakini walipuuza mambo mazito ambayo Mungu alitaka yaonyeshwe kama vile haki, rehema, na uaminifu. (Mt. 22:23, 24; 23:23, 24) Yesu alionyesha utu wa Baba yake alipofundisha Neno la Mungu. Bidii ya Yesu kwa ajili ya ile kweli iliambatana na upendo mwingi aliowaonyesha watu aliofundisha. Tujaribu kuiga mfano wake.—Mt. 11:28.
Tunawezaje kuwa na hakika kwamba tunatumia maandiko vizuri? Kusoma Biblia kwa ukawaida kunasaidia. Pia tunahitaji kutambua kwamba Yehova ametuandalia “mtumwa mwaminifu na mwenye busara,” jamii ya Wakristo watiwa-mafuta ambayo Yehova anatumia kuandalia nyumba ya waamini chakula cha kiroho. (Mt. 24:45) Funzo la binafsi na kuhudhuria mikutano ya kutaniko kwa ukawaida na kuishiriki kutatusaidia kufaidika na mafunzo yanayoandaliwa kupitia jamii ya mtumwa mwaminifu na mwenye busara.
Ikiwa kitabu Kutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko kinapatikana katika lugha yenu, jifunze kukitumia vizuri na kitakusaidia sana kuelewa kwa urahisi jinsi ya kupata mwongozo unaohitaji ili kutumia vizuri mamia ya maandiko ambayo hutumiwa mara nyingi katika huduma ya shambani. Ikiwa unataka kutumia andiko ambalo hulifahamu, kwa unyenyekevu fanya utafiti ili ulitumie sawasawa neno la ile kweli.—Mit. 11:2.
Onyesha Vizuri Jinsi Andiko Linavyohusika. Unapowafundisha wengine, hakikisha wanaelewa vizuri uhusiano ulioko kati ya habari unayozungumzia na maandiko unayotumia. Ukiuliza swali kabla ya kusoma andiko, waonyeshe wasikilizaji jinsi andiko hilo linavyojibu swali lile. Ikiwa unatumia andiko kuunga mkono jambo fulani unalosema, hakikisha mwanafunzi anaona wazi jinsi andiko hilo linavyothibitisha jambo hilo.
Mara nyingi haitoshi tu kusoma andiko, hata kama unalisoma kwa mkazo. Kumbuka kwamba mtu wa kawaida hafahamu vizuri Biblia na ukisoma andiko mara moja tu labda hatakuelewa. Kazia sehemu ya andiko inayohusu jambo unalozungumzia.
Kwa kawaida unaweza kukazia jambo kwa kutenga maneno makuu, yaani maneno ambayo yanahusiana na jambo unalozungumzia. Njia rahisi zaidi ni kurudia kutaja maneno yenye mambo unayotaka kukazia. Ikiwa unazungumza na mtu fulani, unaweza kuuliza maswali ambayo yanaweza kumsaidia kutambua maneno makuu. Wasemaji wengine wanapohutubu, wao hupendelea kukazia maneno makuu kwa kutumia maneno mengine yenye maana sawa au kwa kurudia kutaja wazo kuu. Na ukiamua kufanya hivyo, hakikisha wasikilizaji wanaona jinsi jambo unalozungumzia linavyohusiana na andiko unalosoma.
Ikiwa umetenga maneno makuu, basi umeweka msingi mzuri. Sasa jenga kwenye msingi huo. Kabla ya kusoma andiko, je, umeonyesha wazi sababu ya kulisoma? Ikiwa ndivyo, onyesha jinsi maneno ambayo umekazia yanavyohusiana na matarajio ya wasikilizaji kuhusu andiko hilo. Onyesha vizuri uhusiano ulioko. Hata kama utangulizi wa andiko hilo haukuwa dhahiri sana, onyesha sababu ya kulisoma.
Mafarisayo walimwuliza Yesu swali ambalo walifikiri ni gumu, yaani: “Je, yaruhusika kisheria mtu kutaliki mke wake kwa kila namna ya sababu?” Yesu alitumia Mwanzo 2:24 kujibu. Ebu ona kwamba Yesu alitaja sehemu tu ya andiko hilo, kisha akaonyesha jinsi sehemu hiyo inavyohusika. Baada ya Yesu kutaja kwamba mwanamume na mke wake watakuwa “mwili mmoja,” alimalizia kusema: “Kwa hiyo, kile ambacho Mungu amefunga nira pamoja msiache mtu yeyote akitenganishe.”—Mt. 19:3-6.
Unapaswa kufafanua andiko kwa kadiri gani ili liwe wazi? Hiyo inategemea wasikilizaji na umuhimu wa jambo unalozungumza. Kusudi lako liwe kufafanua andiko kwa njia rahisi na ya moja kwa moja.
Tumia Maandiko Kutoa Sababu. Matendo 17:2, 3 linapozungumzia huduma ya mtume Paulo huko Thesalonike, linatuambia kwamba ‘alitoa sababu kutokana na Maandiko.’ Kila mtumishi wa Yehova anapaswa kujaribu kukuza uwezo huu. Kwa mfano, Paulo alisimulia mambo yaliyohusu maisha ya Yesu na huduma yake, akaonyesha kwamba mambo hayo yalitabiriwa katika Maandiko ya Kiebrania, kisha akamalizia kwa nguvu akisema: “Huyu ndiye Kristo, Yesu huyu ninayewatangazia nyinyi.”
Paulo alinukuu Maandiko ya Kiebrania mara nyingi alipowaandikia Waebrania. Mara nyingi alitenga neno au maneno fulani kisha akaonyesha umuhimu wake ili kukazia jambo au kulifafanua vizuri. (Ebr. 12:26, 27) Katika masimulizi ya Waebrania sura ya 3, Paulo alinukuu Zaburi 95:7-11. Ona kwamba alifafanua sehemu tatu za maandiko hayo: (1) alitaja moyo (Ebr. 3:8-12), (2) umuhimu wa neno “Leo” (Ebr. 3:7, 13-15; 4:6-11), na (3) maana ya maneno haya: “Hawataingia katika pumziko langu.” (Ebr. 3:11, 18, 19; 4:1-11) Jaribu kuiga mfano huo unapoonyesha jinsi kila andiko linavyohusika na jambo unalozungumzia.
Ona jinsi Yesu alivyotoa sababu vizuri akitumia Maandiko katika Luka 10:25-37. Mtaalamu mmoja wa Sheria alimwuliza: “Mwalimu, ni kwa kufanya nini mimi nitarithi uhai udumuo milele?” Kwanza, Yesu akamwuliza mtu huyo maoni yake juu ya swali hilo, kisha Yesu akakazia kwamba ni muhimu kufanya kile ambacho Neno la Mungu linasema. Ilipokuwa wazi kwamba mtu huyo haelewi, Yesu alifafanua kabisa neno moja tu katika andiko hilo, “jirani.” Na badala ya kulifafanua tu neno hilo, Yesu alitumia mfano uliomwezesha mtu huyo afikie jibu linalofaa.
Yesu alipokuwa akijibu maswali, hakunukuu tu maandiko na kutoa majibu rahisi na ya wazi. Alifafanua maandiko hayo na kuonyesha jinsi yanavyojibu swali aliloulizwa.
Masadukayo walipopinga tumaini la ufufuo, Yesu alikazia sehemu fulani tu ya Kutoka 3:6. Lakini hakuachia hapo tu. Alisababu juu ya andiko hilo na kuonyesha wazi kwamba ufufuo ni sehemu ya kusudi la Mungu.—Mk. 12:24-27.
Ili kuwa mwalimu bora ni muhimu kukuza uwezo wa kutumia Maandiko kutoa sababu vizuri na kwa matokeo mazuri.