SOMO LA 20
Kutoa Utangulizi Mzuri wa Maandiko
MAANDIKO ndiyo msingi wa mafundisho yetu katika mikutano ya kutaniko. Pia, maandiko ya Biblia ndiyo msingi wa mahubiri yetu katika huduma ya shambani. Lakini, mafanikio yetu ya kutumia maandiko katika mazungumzo yanategemea kwa kiasi fulani utangulizi tunaotoa kabla ya kuyasoma.
Usirejelee tu andiko na kumwomba mtu afuatane nawe unapolisoma. Unapotaka kutaja andiko, jaribu kutimiza mambo haya mawili: (1) Chochea hamu ya kusoma andiko hilo, na (2) onyesha kusudi la kulisoma. Kuna njia mbalimbali za kutimiza mambo hayo mawili.
Uliza Swali. Njia hii ni bora ikiwa wasikilizaji bado hawajui vizuri jibu la swali unalouliza. Jaribu kuuliza swali kwa njia inayofanya watu wafikiri. Yesu alifanya hivyo. Mafarisayo walipomwendea hekaluni na kujaribu hadharani ujuzi wake wa Maandiko, Yesu aliwauliza: “Nyinyi mwafikiri nini juu ya Kristo? Yeye ni mwana wa nani?” Wakamjibu: “Wa Daudi.” Yesu akawauliza: “Basi, ni jinsi gani, kwamba Daudi kwa upulizio amwita yeye ‘Bwana’?” Kisha akanukuu Zaburi 110:1. Mafarisayo wakanyamazishwa. Lakini, umati ukamsikiliza Yesu kwa furaha.—Mt. 22:41-46.
Unaweza kutumia maswali kama haya kwenye utangulizi wako katika utumishi wa shambani: “Mimi nina jina na wewe una jina. Je, Mungu pia ana jina? Ebu tupate jibu katika Zaburi 83:18.” “Je, kweli itawezekana kuwe na serikali moja inayotawala wanadamu wote? Ebu ona jinsi Danieli 2:44 linavyojibu.” “Je, kweli Biblia inazungumzia hali za siku zetu? Ebu linganisha hali unazoona leo na hali zinazotajwa katika 2 Timotheo 3:1-5.” “Je, kweli kuna wakati ambapo kifo na kuteseka hakutakuwapo tena? Biblia inajibu swali hilo katika Ufunuo 21:4, 5.”
Kutumia maswali vizuri katika hotuba ili kutoa utangulizi mzuri wa maandiko kunaweza kuchochea wasikilizaji kuona maandiko kwa njia tofauti, hata kama ni maandiko wanayofahamu vizuri. Lakini, watafanya hivyo ikiwa tu maswali unayouliza kwa kweli yanawahusu. Hata kama wasikilizaji wanapendezwa na habari unayozungumza, akili zao zinaweza kutangatanga unaposoma maandiko ambayo wamesikia mara nyingi. Ili akili zao zisitangetange, fikiria sana jinsi ya kufanya hotuba yako ivutie.
Taja Tatizo Fulani. Unaweza kutaja tatizo fulani kisha uonyeshe andiko linalotaja suluhisho. Usiwafanye wasikilizaji watarajie suluhisho kubwa kuliko lile watakalopata katika andiko. Mara nyingi andiko huonyesha suluhisho la kadiri fulani tu. Lakini unaposoma andiko, unaweza kuuliza wasikilizaji wafikirie mwongozo unaopatikana katika andiko hilo unaosaidia kukabili tatizo mnalozungumzia.
Vilevile, unaweza kutaja kanuni fulani inayohusu mwenendo mzuri kisha utumie tukio fulani katika Biblia linaloonyesha hekima ya kufuata kanuni hiyo. Ikiwa andiko ambalo wasemaji wengine wanasoma lina mambo mawili hususa (au labda zaidi) ambayo yanahusiana na jambo wanalozungumzia, wao huwaomba wasikilizaji wawe makini kuyaona. Ikiwa inaonekana wasikilizaji fulani hawaelewi jambo unalozungumzia, unaweza kuchochea fikira zao kwa kutaja mambo yanayoweza kufanywa ili kulisuluhisha kisha utumie andiko kuonyesha suluhisho.
Rejelea Biblia. Ikiwa tayari umeamsha upendezi wa wasikilizaji katika habari unayozungumzia na tayari umetaja jambo moja au mambo mawili kuihusu, unaweza kusema hivi kabla ya kusoma andiko: “Ona jinsi Neno la Mungu linavyosema kuhusu jambo hili.” Ukifanya hivyo unaonyesha kwamba jambo unalotaka kusoma linategemea Neno la Mungu.
Yehova alitumia wanaume kama Luka, Paulo, Petro, na Yohana kuandika sehemu fulani za Biblia. Lakini wao ni waandishi tu; Yehova ndiye Mtungaji. Ikiwa unazungumza na watu ambao hawasomi Maandiko Matakatifu, huenda ikafaa zaidi kusema “Neno la Mungu” linasema kuliko kusema “Petro aliandika” au “Paulo alisema” kabla ya kusoma andiko. Ona kwamba nyakati nyingine Yehova alimwamuru Yeremia aseme maneno haya kabla ya kutangaza ujumbe wake: “Sikilizeni neno la BWANA.” (Yer. 7:2; 17:20; 19:3; 22:2) Iwe tunatumia jina la Yehova tunapotaka kusoma andiko au la, kabla ya kumalizia mazungumzo yetu, tujaribu kuonyesha kwamba yaliyomo katika Biblia ni neno lake.
Fikiria Muktadha. Unapaswa kuelewa muktadha unapofikiria utakavyotoa utangulizi wa andiko. Nyakati nyingine unaweza kutaja muktadha, lakini kwa njia nyinginezo ni muktadha unaoweza kuamua maneno utakayotumia. Kwa mfano, je, unaweza kutoa utangulizi wa maneno ya Yobu aliyemcha Mungu kwa njia ile ambayo ungetoa utangulizi wa maneno ya mmojawapo wa wafariji wake bandia? Luka aliandika kitabu cha Matendo, lakini pia ananukuu Yakobo, Petro, Paulo, Filipo, Stefano, na malaika, na vilevile ananukuu Gamalieli na Wayahudi wengine ambao hawakuwa Wakristo. Utasema ni nani aliyesema maneno unayonukuu? Kwa mfano, kumbuka kwamba Daudi hakutunga zaburi zote wala Solomoni hakuandika kitabu chote cha Mithali. Pia ni vizuri kujua mwandishi wa Biblia anazungumza na nani na kwa ujumla anazungumza habari gani.
Tumia Habari za Ziada. Hii ni njia bora ikiwa unaweza kuonyesha kwamba hali zinazohusu simulizi la Biblia unalosoma zinalingana na hali unazozungumzia. Nyakati nyingine unahitaji kutumia habari za ziada ili watu waelewe andiko fulani vizuri. Tuseme unataka kutumia andiko la Waebrania 9:12, 24 katika hotuba inayohusu fidia. Kabla ya kusoma andiko hilo unaweza kufafanua kifupi chumba cha ndani kabisa cha tabenakulo, ambacho maandiko yanaonyesha kinafananisha mahali ambapo Yesu aliingia alipoenda mbinguni. Lakini usitumie habari nyingi sana kiasi cha kufunika andiko ambalo unataka kusoma.
Ili utoe utangulizi wa maandiko kwa njia bora, chunguza jinsi wasemaji wenye ujuzi wanavyofanya. Tazama njia tofauti-tofauti wanazotumia. Ona matokeo ya njia hizo. Unapotayarisha hotuba zako, tambua maandiko makuu na ufikirie kwa makini jambo unalotaka kutimiza unaposoma kila andiko. Panga kwa uangalifu jinsi ambavyo utatoa utangulizi wa kila andiko ili liwe na matokeo bora zaidi. Baadaye, fanya vivyo hivyo na maandiko yote unayotumia. Unapoendelea kuboresha sehemu hii katika hotuba zako, utakuwa ukielekeza fikira zaidi kwenye Neno la Mungu.