SOMO LA 19
Kuwasaidia Wasikilizaji Kutumia Biblia
KUSUDI letu ni kuelekeza fikira za kila mtu kwenye Neno la Mungu, Biblia. Kitabu hicho kitakatifu ndicho msingi wa ujumbe tunaohubiri, na tunataka watu watambue kwamba yale tunayosema yanatokana na Mungu wala hatusemi mambo yetu wenyewe. Watu wanahitaji kuitumaini Biblia.
Katika Huduma ya Shambani. Unapojitayarisha kwa ajili ya huduma ya shambani, sikuzote chagua andiko moja au zaidi ambalo utawaonyesha wale walio tayari kusikiliza. Hata kama unapanga kutoa kichapo fulani cha Biblia kwa muda mfupi tu, kwa kawaida ni vizuri kusoma andiko linalofaa la Biblia. Biblia ina uwezo mkubwa wa kuelekeza wenye mfano wa kondoo kuliko jambo jingine lolote ambalo tunaweza kusema. Ikiwa hali hazikuruhusu kusoma Biblia, unaweza kuinukuu. Katika karne ya kwanza, vitabu vya kukunjwa vya Maandiko havikupatikana sana. Hata hivyo, Yesu na mitume wake walinukuu sana Maandiko. Hata sisi tunapaswa kujitahidi kushika Maandiko na kuyatumia vizuri katika huduma yetu, nyakati nyingine tukiyanukuu tu.
Ikiwa hali zinakuruhusu kusoma Biblia, uishike vizuri ili mwenye nyumba aweze kufuatana nawe unaposoma. Ikiwa mwenye nyumba anafuatana nawe akisoma Biblia yake mwenyewe, yale anayosoma yanaweza kumfanya aitikie kwa njia nzuri zaidi.
Hata hivyo, ni lazima utambue kwamba baadhi ya watafsiri wa Biblia wamebadili Neno la Mungu. Huenda tafsiri zao hazipatani kwa kila hali na mambo yaliyokuwa katika lugha za awali za Biblia. Tafsiri kadhaa za kisasa zimeondoa jina la Mungu, hazisemi wazi kile ambacho maandishi ya lugha za awali yalisema kuhusu wafu, na zinaficha mafundisho ya Biblia kuhusu kusudi la Mungu kwa dunia. Ili kuonyesha mtu badiliko ambalo limefanywa, mnaweza kuchunguza maandiko hayo katika Biblia tofauti-tofauti au kuchunguza tafsiri za awali za Biblia za lugha iyo hiyo. Kitabu Kutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko kinalinganisha jinsi tafsiri kadhaa zinavyotafsiri maneno makuu ya maandiko ambayo hutumiwa mara nyingi. Mtu yeyote anayependa kweli atafurahi kujua mambo hayo.
Katika Mikutano ya Kutaniko. Wote wasaidiwe kutumia Biblia katika mikutano ya kutaniko. Kuna faida nyingi za kufanya hivyo. Kunawasaidia wasikilizaji wakazie fikira mambo yanayozungumzwa. Kunakazia maneno ya msemaji kwa sababu wasikilizaji wenyewe wanayasoma maneno hayo. Na kufanya hivyo kunawasadikisha wale wanaopendezwa kwamba kwa kweli Biblia ndiyo msingi wa imani yetu.
Wasikilizaji watafuatana nawe unaposoma Maandiko katika Biblia ikiwa tu utawasaidia kufanya hivyo. Mojawapo ya njia bora ya kuwatia moyo kutumia Biblia ni kuwaomba wafuatane nawe unaposoma andiko fulani.
Ni daraka la msemaji kuamua maandiko anayotaka kukazia anapowaomba wasikilizaji wafuatane naye. Inafaa kusoma maandiko yanayokusaidia kufafanua mambo makuu. Kisha kadiri wakati unavyoruhusu, ongezea maandiko mengine machache yanayotegemeza jambo unalozungumzia.
Kwa kawaida, haitoshi tu kutaja andiko fulani wala haitoshi kuwaomba wasikilizaji wafuatane nawe unapolisoma. Ukisoma andiko moja kisha usome jingine mbiombio hata kabla ya wasikilizaji kupata wakati wa kufungua lile la kwanza, upesi watachoka na wataacha kujaribu kufuatana nawe unaposoma Biblia. Uwe na utambuzi. Soma andiko wakati wengi wamelipata.
Fikiria kimbele. Taja vizuri andiko hilo mapema kabla ya kulisoma. Jambo hilo litapunguza wakati unaopotea unapongojea wasikilizaji wafungue Biblia zao. Ingawa hutaweza kuzungumzia mambo mengi sana ukiwapa wasikilizaji wakati wa kufungua Biblia, utawafaidi sana.