SOMO LA 42
Kuwaelimisha Wasikilizaji
HOTUBA inayoelimisha wasikilizaji si mazungumzo tu yanayopendeza. Jiulize: ‘Kwa nini wasikilizaji hawa wanahitaji kusikia habari hii? Niseme nini ili wasikilizaji wahisi wamefaidika kabisa na mazungumzo haya?’
Ukiwa na mgawo katika shule wa kuonyesha jinsi ya kumhubiria mtu, mwenyenyumba ndiye msikilizaji wako. Nyakati nyingine, wasikilizaji wako ni kutaniko unalohutubia.
Mambo Ambayo Wasikilizaji Wanajua. Jiulize, ‘Wasikilizaji wanajua nini kuhusu habari hii?’ Basi huo ndio msingi wa kuanzishia hotuba. Ikiwa unahutubia kutaniko ambalo lina Wakristo wengi wakomavu, usirudie-rudie mambo ya msingi ambayo wengi wanaelewa. Yatumie mambo hayo kama msingi wa hotuba. Lakini ikiwa wasikilizaji wengi ni wapya, yafikirie mahitaji yao na pia ya wale wakomavu.
Toa hotuba kwa mwendo unaolingana na mambo ambayo wasikilizaji tayari wanajua. Kama unazungumzia mambo madogo-madogo ambayo inaelekea wengi wanafahamu, pitia mambo hayo haraka. Lakini punguza mwendo unapozungumzia mambo ambayo huenda ni mapya kwa wasikilizaji wengi ili wayaelewe vizuri.
Mambo Ambayo Yataelimisha. Kuelimisha hakumaanishi kuzungumzia jambo jipya nyakati zote. Wasemaji wengine hufafanua kweli fulani zinazojulikana kwa njia rahisi hivi kwamba wakati huo ndipo wasikilizaji wengi huzielewa vizuri kwa mara ya kwanza.
Unapokuwa katika huduma ya shambani, haitoshi tu kutaja kisa fulani kilichoripotiwa kwenye habari ili kuthibitisha tunaishi katika siku za mwisho. Tumia Biblia kuonyesha maana ya kisa hicho. Kwa kweli jambo hilo litamwelimisha mwenye nyumba. Hali kadhalika, unapozungumzia jambo fulani la asili au mmea fulani au mnyama fulani, kusudi lako lisiwe tu kutaja mambo ya kisayansi yanayostaajabisha ambayo mwenye nyumba hajawahi kusikia. Badala yake, unapaswa kuunganisha jambo hilo na maneno ya Biblia yanayoonyesha kwamba kuna Muumba anayetupenda. Hiyo itamsaidia mwenye nyumba kuona mambo kwa njia mpya.
Si rahisi kuzungumzia jambo ambalo watu wamesikia mara nyingi. Lakini ili uwe mwalimu bora, unapaswa kujifunza kufanya hivyo. Unawezaje kufaulu?
Utafiti husaidia. Badala ya kuzungumzia mambo unayokumbuka kwa urahisi, tumia vifaa vya utafiti ambavyo vimetajwa katika ukurasa wa 33 hadi 38. Fikiria madokezo yanayotolewa na mambo unayojaribu kutimiza. Utafiti unaweza kuonyesha kwamba tukio fulani la kihistoria ambalo halijulikani sana linahusiana na hotuba yako. Au unaweza kupata habari fulani ya karibuni inayoonyesha mfano wa jambo unalopanga kuzungumzia.
Unapochunguza habari hiyo, chochea akili yako mwenyewe kwa kujiuliza maswali kama nini? kwa nini? lini? wapi? nani? na kwa njia gani? Kwa mfano: Kwa nini jambo hili ni kweli? Nawezaje kulithibitisha? Watu wanashindwa kuelewa kweli hii ya Biblia kwa sababu ya imani zipi wanazopenda? Kwa nini jambo hili ni muhimu? Jambo hili linapaswa kubadilije maisha ya mtu? Kuna mfano gani unaoonyesha faida ya kulifuata maishani? Kweli hii ya Biblia inafunua nini kuhusu utu wa Yehova? Ikitegemea habari unayozungumzia, unaweza kujiuliza: Jambo hili lilitukia lini? Tunaweza kutumiaje habari hii leo? Hata unaweza kufanya hotuba yako ichangamshe kwa kuuliza maswali haya na kuyajibu unapotoa hotuba.
Huenda hotuba unayotoa ina maandiko ambayo wasikilizaji wanayajua. Utatumiaje maandiko hayo kwa njia inayoelimisha? Yafafanue badala ya kuyasoma tu.
Maandiko kama hayo yanaweza kuelimisha ikiwa unayafafanua sehemu-sehemu, ukitenga sehemu zinazohusiana na hotuba yako na kuzifafanua. Ebu ona jinsi unavyoweza kufafanua andiko kama Mika 6:8 katika Biblia ya Union Version. “Haki” ni nini? Tunazungumzia kanuni ya nani ya haki? Unawezaje kuonyesha maana ya “kutenda haki”? Au maana ya “kupenda rehema”? Unyenyekevu ni nini? Unawezaje kutumia habari hii kumhusu mtu aliye mzee kwa umri? Bila shaka habari ambazo utatumia zinategemea mambo kama kichwa kikuu cha hotuba, kusudi la hotuba, wasikilizaji, na wakati uliowekewa.
Ni vizuri kufafanua mambo kwa njia rahisi. Watu wengine hushangaa kujifunza maana ya “ufalme” unaotajwa katika Mathayo 6:10. Ufafanuzi wa jambo hata unaweza kumsaidia Mkristo wa zamani kufahamu vizuri maana ya andiko fulani. Jambo hili ni wazi unaposoma 2 Petro 1:5-8 na kufafanua sifa zinazotajwa katika mistari hiyo: imani, wema wa adili, ujuzi, kujidhibiti, uvumilivu, ujitoaji-kimungu, shauku ya kidugu, na upendo. Ikiwa maneno yanayofanana yanatumiwa katika muktadha uleule, unaweza kuyafafanua ili kutofautisha maana ya neno moja na jingine. Ndivyo ilivyo kuhusu maneno kama hekima, maarifa, ufahamu, na busara ambayo yametumiwa katika Mithali 2:1-6.
Unaweza kuwaelimisha wasikilizaji ukisababu nao kuhusiana na andiko. Watu wengi hushangaa wanapotambua kwa mara ya kwanza kwamba katika tafsiri nyingine za Biblia Mwanzo 2:7 inasema Adamu ni nafsi hai na kwamba Ezekieli 18:4, Zaire Swahili Bible, inaonyesha nafsi hufa. Pindi moja, Yesu aliwashangaza Masadukayo aliporejelea Kutoka 3:6, ambalo Masadukayo walidai kuamini, kisha akaliunganisha na ufufuo wa wafu.—Luka 20:37, 38.
Nyakati nyingine inasaidia kuonyesha muktadha wa andiko, hali zilizokuwako wakati wa kuliandika, na kumtaja msemaji au msikilizaji anayetajwa katika andiko hilo. Mafarisayo walifahamu vizuri Zaburi 110. Lakini bado Yesu aliwafundisha jambo fulani muhimu katika mstari wa kwanza. Yesu aliwauliza: “‘Nyinyi mwafikiri nini juu ya Kristo? Yeye ni mwana wa nani?’ Wakamwambia: ‘Wa Daudi.’ Akawaambia: ‘Basi, ni jinsi gani, kwamba Daudi kwa upulizio amwita yeye “Bwana,” akisema, “Yehova alimwambia Bwana wangu: ‘Keti kwenye mkono wangu wa kuume mpaka niwekapo maadui wako chini ya miguu yako’”? Kwa hiyo, ikiwa Daudi humwita yeye “Bwana,” ni jinsi gani yeye ni mwana wake?’” (Mt. 22:41-45) Ukisababu kutokana na Maandiko kama Yesu, utawasaidia watu kusoma Neno la Mungu kwa makini zaidi.
Msemaji akitaja wakati kitabu fulani cha Biblia kilipoandikwa au wakati tukio fulani lilipotokea, anapaswa pia kufafanua hali zilizokuwako wakati huo. Kwa njia hiyo, wasikilizaji wataelewa kwa urahisi zaidi umuhimu wa kitabu hicho au tukio hilo.
Kulinganisha mambo kunaweza kufanya jambo unalosema lielimishe. Unaweza kulinganisha mambo ambayo watu wanapenda na maoni ya Biblia. Au unaweza kulinganisha masimulizi mawili ya Biblia yanayolingana. Je, kuna mambo yanayotofautiana katika masimulizi hayo? Kwa nini? Tunajifunza nini katika masimulizi hayo? Ukilinganisha mambo unaweza kuwasaidia wasikilizaji waione habari hiyo kwa njia mpya.
Ikiwa una mgawo wa kuzungumzia jambo fulani kuhusu huduma ya Kikristo, unaweza kuboresha hotuba kwa kutoa kwanza muhtasari. Zungumzia jambo linalohitaji kufanywa, kwa nini linahitaji kufanywa, na jinsi linavyohusiana na makusudi yetu tukiwa Mashahidi wa Yehova. Kisha eleza wapi, lini, na jinsi ya kulitimiza.
Namna gani kama hotuba yako inazungumzia baadhi ya “mambo yenye kina kirefu ya Mungu”? (1 Kor. 2:10) Ukianza kwa kutenganisha na kufafanua mambo makuu, wasikilizaji wataelewa kwa urahisi mambo madogo-madogo. Na ukimalizia kwa muhtasari mfupi, wasikilizaji wanaweza kuridhika kwamba kweli wamejifunza kitu.
Shauri la Maisha ya Kikristo. Wasikilizaji watafaidika hasa ukiwaonyesha jinsi hotuba hiyo inavyohusu maisha yao. Unapochunguza maandiko yaliyo katika hotuba yako, jiulize, ‘Kwa nini habari hii imehifadhiwa katika Maandiko hadi siku zetu?’ (Rom. 15:4; 1 Kor. 10:11) Fikiria hali za maisha za wasikilizaji. Fikiria hali hizo ukitumia shauri na kanuni za Maandiko. Katika hotuba yako, sababu kwa kutumia Maandiko ili kuonyesha jinsi kanuni hizo zinavyoweza kumsaidia mtu kutenda kwa hekima katika hali hizo. Usitaje mambo kwa ujumla. Zungumzia hali na matendo hususa.
Kwanza, tumia dokezo moja au madokezo mawili ambayo tumezungumzia katika hotuba unayotayarisha. Unapoendelea kupata uzoefu, tumia madokezo mengine. Baada ya muda, utaona kwamba wasikilizaji hutazamia kwa hamu hotuba zako, wakiwa na hakika kwamba watasikia jambo ambalo kweli litawafaidi.