SOMO LA 38
Utangulizi Unaoamsha Upendezi
UTANGULIZI ni sehemu muhimu ya hotuba yoyote. Ukiamsha vizuri upendezi wa wasikilizaji, watasikiliza kwa makini mambo yanayofuata. Ikiwa utangulizi wako hauamshi upendezi katika huduma ya shambani, unaweza kushindwa kuendeleza mazungumzo. Usipoamsha upendezi wa wasikilizaji unapotoa hotuba katika Jumba la Ufalme, hawataondoka kihalisi, lakini wengine wanaweza kuanza kufikiria mambo mengine.
Unapotayarisha utangulizi, kumbuka malengo yafuatayo: (1) kuvuta usikivu wa wasikilizaji, (2) kufanya habari unayozungumzia iwe dhahiri, na (3) kuonyesha wasikilizaji umuhimu wa habari hiyo. Nyakati nyingine unaweza kutumia njia zote tatu kwa wakati mmoja. Lakini nyakati nyingine, unaweza kutumia kila njia peke yake, ukizifuatanisha kwa njia yoyote ile.
Jinsi ya Kuvuta Usikivu wa Wasikilizaji. Hata kama watu wamekusanyika kusikiliza hotuba, hiyo haimaanishi wako tayari kusikiliza kwa makini. Kwa nini? Wana mambo mengi yanayowasumbua akilini. Labda wanahangaishwa na tatizo fulani la nyumbani au jambo jingine. Sasa, ni lazima wewe msemaji uendelee kuvuta usikivu wa wasikilizaji. Kuna njia nyingi za kuvuta usikivu wao.
Mojawapo ya hotuba mashuhuri zaidi zilizowahi kutolewa ni Mahubiri ya Mlimani. Hotuba hiyo ilianzaje? Kulingana na masimulizi ya Luka, Yesu alisema: “Wenye furaha ni nyinyi maskini, . . . wenye furaha ni nyinyi mlio na njaa sasa, . . . wenye furaha ni nyinyi mtoao machozi sasa, . . . wenye furaha ni nyinyi wakati wowote ule watu wawachukiapo nyinyi.” (Luka 6:20-22) Kwa nini maneno hayo yaliamsha upendezi? Kwa maneno machache, Yesu alitaja baadhi ya matatizo makubwa ya wale waliokuwa wakimsikiliza. Kisha, badala ya kuzungumzia matatizo hayo kwa urefu, alionyesha kwamba watu ambao wana matatizo kama hayo bado wanaweza kuwa na furaha, na alizungumza kwa njia iliyowafanya wasikilizaji wawe na hamu ya kuendelea kusikiliza.
Unaweza kutumia vizuri maswali ili kuamsha upendezi, lakini ni lazima maswali hayo yafae. Ikiwa maswali yako yanadokeza kwamba utazungumzia mambo ambayo wasikilizaji wanafahamu, upendezi wao utafifia upesi. Usiulize maswali ambayo yanawaaibisha wasikilizaji au ambayo yanawashusha chini. Badala yake, jaribu kuuliza maswali yanayofanya wafikiri. Tua kidogo baada ya kuuliza kila swali ili wasikilizaji wapate muda wa kujijibu wenyewe akilini. Unapohisi kwamba ni kama wanazungumza na wewe akilini, ujue wanakusikiliza kwa makini.
Njia nyingine nzuri ya kuvuta usikivu wa wasikilizaji ni kutumia mambo halisi yaliyoonwa. Lakini huenda usifaulu ukisimulia mambo ambayo yanamwaibisha mmoja wa wasikilizaji. Ikiwa watu watakumbuka simulizi lako lakini wasikumbuke somo lake, ujue umepiga hewa tu. Simulia jambo lililoonwa kwenye utangulizi ili kuweka msingi wa jambo muhimu utakalozungumzia katika sehemu kuu ya hotuba. Ingawa unaweza kutaja mambo mengine madogo-madogo ili jambo lililoonwa liwe wazi zaidi, jihadhari lisiwe refu mno.
Wasemaji wengine huanzisha hotuba kwa kutaja jambo fulani lililotajwa katika vyombo vya habari, au hunukuu gazeti fulani, au jambo lililotajwa na mtu fulani mashuhuri. Hayo pia yanaweza kuwa matangulizi bora ikiwa yanafaa kabisa habari na wasikilizaji.
Ikiwa hotuba yako ni sehemu ya mfululizo wa hotuba au ni sehemu ya Mkutano wa Utumishi, basi kwa kawaida ni vizuri kutumia utangulizi mfupi usio na mambo mengi. Ikiwa unatoa hotuba ya watu wote, fuata kwa makini wakati uliowekwa kwenye sehemu ya utangulizi. Sehemu kuu ya hotuba ndiyo yenye habari inayofaidi zaidi wasikilizaji.
Kuna pindi ambazo unaweza kuwa na wasikilizaji wenye kutilia shaka au hata wakali. Unawezaje kuvuta usikivu wao? Stefano, Mkristo mmoja wa awali aliyetajwa kuwa ‘mwenye kujaa roho na hekima,’ alipelekwa kwa nguvu mbele ya Sanhedrini ya Kiyahudi. Akiwa mbele yao, alitetea Ukristo kwa ustadi sana. Alianzaje? Alianza kwa njia ya heshima na kwa kurejelea jambo ambalo yeye na Sanhedrini walikubaliana nalo. “Wanaume, akina ndugu na akina baba, sikieni. Mungu wa utukufu alimtokea baba yetu wa zamani Abrahamu.” (Mdo. 6:3; 7:2) Mtume Paulo alipokuwa kule Areopago, Athene, alitumia utangulizi uliofaa wasikilizaji waliokuwa na hali tofauti kabisa, akisema: “Wanaume wa Athene, naona kwamba katika mambo yote mwaonekana kuwa wenye mwelekeo zaidi wa kuhofu miungu kuliko wengine walivyo.” (Mdo. 17:22) Kwa sababu ya utangulizi mzuri, wasikilizaji walitaka kuwasikiliza zaidi.
Unapokuwa katika utumishi wa shambani, pia unahitaji kuvuta usikivu wa watu. Ikiwa hamkupanga kukutana, huenda ikawa mwenye nyumba ana shughuli nyingi. Katika sehemu fulani za ulimwengu, wageni wasiotarajiwa wanapaswa kutaja haraka kilichowaleta. Na katika sehemu nyinginezo, watu hufuata desturi ya kujuliana hali kabla ya kusema kilichowaleta.—Luka 10:5.
Kwa vyovyote vile, urafiki wa kweli unaweza kutokeza mazingira mazuri ya mazungumzo. Mara nyingi inafaa kuanza na jambo ambalo linamhusu mtu huyo. Unaweza kulitambuaje? Umemkuta akifanya nini? Labda analima, anatunza ua wa nyumba, anarekebisha gari, anapika, anafua, au anawashughulikia watoto. Je, kuna kitu anachotazama—gazeti fulani au tukio fulani barabarani? Je, kuna dalili nyumbani kwake kwamba anapenda kuvua samaki, michezo, muziki, kusafiri, kompyuta, au jambo jingine lolote? Mara nyingi, watu huhangaikia habari za redio au za televisheni. Swali fulani au jambo fupi kuhusu habari kama hizo linaweza kutokeza mazungumzo ya kirafiki.
Pindi ambapo Yesu alizungumza na yule mwanamke Msamaria kwenye kisima fulani karibu na Sikari ni mfano bora wa jinsi ya kuanzisha mazungumzo ili kuhubiri.—Yn. 4:5-26.
Unahitaji kutayarisha utangulizi kwa makini, hasa ikiwa eneo la kutaniko lenu linahubiriwa mara nyingi. Usipofanya hivyo, unaweza kushindwa kuhubiri.
Taja Hususa Habari Unayozungumzia. Katika kutaniko la Kikristo, kwa kawaida mwenyekiti au mtu mwingine anayekutangulia hutaja kichwa cha hotuba yako na kukukaribisha. Lakini ni vizuri kuwakumbusha wasikilizaji kichwa hicho unapotoa utangulizi. Unaweza kurudia kutaja kichwa chenyewe jinsi kilivyo au unaweza kukitaja kwa njia nyingine. Unapaswa kufafanua kichwa hicho kikuu unapoendelea kutoa hotuba. Kwa njia fulani kazia habari hiyo unapotoa utangulizi.
Yesu alipowatuma wanafunzi wake, alitaja wazi ujumbe ambao walipaswa kuhubiri. “Mwendapo, hubirini, mkisema, ‘Ufalme wa mbingu umekaribia.’” (Mt. 10:7) Yesu alisema hivi kuhusu siku zetu: “Habari njema hii ya ufalme itahubiriwa.” (Mt. 24:14) Tunahimizwa ‘tuhubiri neno,’ yaani, tushikamane na Biblia tunapohubiri. (2 Tim. 4:2) Na mara nyingi ni vizuri kutaja jambo linalohangaisha watu wakati huo kabla ya kufungua Biblia au kabla ya kuzungumza juu ya Ufalme. Unaweza kutaja uhalifu, ukosefu wa kazi, ukosefu wa haki, vita, jinsi ya kuwasaidia vijana, ugonjwa, au kifo. Lakini usizungumzie matatizo kwa urefu kwa sababu una ujumbe unaotia moyo. Jaribu kuelekeza mazungumzo kwenye Neno la Mungu na tumaini la Ufalme.
Onyesha Wasikilizaji Umuhimu wa Habari. Ikiwa unatoa hotuba kutanikoni, angalau una hakika kwamba kwa ujumla wasikilizaji wanapendezwa na jambo unalozungumzia. Lakini, je, watasikiliza kama ambavyo mtu husikiliza anapojifunza jambo linalomhusu? Je, watakuwa makini wakitambua kwamba mambo unayosema yanahusu maisha yao na unawachochea wachukue hatua fulani? Unaweza kufaulu ikiwa tu umefikiria kwa makini hali zao, mahangaiko yao, na maoni yao unapotayarisha hotuba. Ikiwa umefanya hivyo, basi tia katika utangulizi wako jambo linalowahusu.
Iwe unatoa hotuba jukwaani au unamhubiria mtu, mojawapo ya njia bora zaidi za kuamsha upendezi ni kuwahusisha wale wanaokusikiliza. Onyesha jinsi habari unayozungumzia inavyohusu matatizo yao, mahitaji yao, au maswali wanayofikiria. Ukionyesha wazi kwamba hutazungumza habari hiyo kwa ujumla bali utazungumzia mambo hususa, watakusikiliza kwa makini zaidi. Ni lazima utayarishe vizuri ili ufaulu.
Jinsi ya Kutoa Utangulizi. Mambo unayosema katika utangulizi ni muhimu sana, lakini jinsi unavyoyasema pia inaweza kuamsha upendezi. Basi unapofanya matayarisho, mbali na kufikiria mambo utakayosema, fikiria pia jinsi utakavyoyasema.
Ni muhimu kutumia maneno yanayofaa ili kutimiza kusudi lako, kwa hiyo inaweza kufaa kutayarisha kwa makini sentensi mbili au tatu za kwanza. Mara nyingi ni afadhali kutumia sentensi fupi-fupi zilizo rahisi. Ikiwa utatoa hotuba kutanikoni, unaweza kuandika sentensi za utangulizi, au unaweza kuzishika akilini ili utangulizi wako uweze kuvutia kabisa wasikilizaji. Kutoa utangulizi kwa utaratibu kunaweza kukusaidia kutoa hotuba yote kwa utulivu.
Wakati Unaofaa Kutayarisha Utangulizi. Kuna maoni tofauti-tofauti juu ya jambo hili. Wasemaji wengine wenye uzoefu wanaamini kwamba unapaswa kutayarisha utangulizi kwanza kabla ya hotuba. Wataalamu wengine ambao wamesomea ustadi wa kutoa hotuba wanasema kwamba unapaswa kutayarisha utangulizi baada ya kutayarisha sehemu kuu ya hotuba.
Jambo la hakika ni kwamba unahitaji kujua habari na mambo makuu unayopanga kuzungumzia kabla ya kutayarisha utangulizi unaofaa. Lakini vipi ikiwa unatayarisha muhtasari ambao umechapwa? Baada ya kusoma muhtasari huo, unaweza kuandika utangulizi unaofikiria. Pia kumbuka kwamba ili utangulizi wako ufae, ni lazima uwafikirie wasikilizaji na hotuba unayotoa.