SOMO LA 13
Kuwatazama Wasikilizaji
MACHO yetu huonyesha maoni yetu na hisia zetu. Yanaweza kuonyesha mshangao au hofu. Yanaweza kuonyesha huruma au upendo. Nyakati nyingine, yanaweza kuonyesha shaka au huzuni. Mtu mmoja mzee alisema hivi kuhusu wenzake waliokuwa wameteseka sana: “Macho yetu yanaonyesha masikitiko yetu.”
Watu wengine wanaweza kukata kauli juu yetu na juu ya mambo tunayosema ikitegemea mahali tunapotazama. Katika jamii nyingi, watu huelekea kumtumaini mtu anayewatazama macho kwa njia ya kirafiki. Kwa upande mwingine, ikiwa mtu anatazama miguu yake tu au vitu vingine badala ya kumtazama mtu anayeongea naye, watu wanaweza kuwa na shaka iwapo anasema kweli au wanaweza kutilia shaka uwezo wake. Na katika jamii nyingine, kumtazama sana mtu mwingine kwa macho kunaonwa kuwa ufidhuli, uchokozi, au ukaidi. Ndivyo ilivyo hasa unapoongea na mtu wa jinsia tofauti au mkuu fulani au mtu yeyote mwenye mamlaka. Na katika maeneo mengine, ni kukosa adabu ikiwa mtu mwenye umri mdogo atazama macho ya mtu mwenye umri mkubwa wanapoongea.
Lakini, mahali ambapo jambo hilo haliudhi, kumtazama mtu machoni unapotaja jambo muhimu kunaweza kukazia jambo hilo akilini mwake. Kufanya hivyo kunaweza kuonyesha kwamba unasadiki unayosema. Ona jinsi Yesu alivyojibu wanafunzi wake waliposhangaa na kusema: “Ni nani kwa kweli awezaye kuokolewa?” Biblia inasema: “Akiwatazama usoni, Yesu akawaambia: ‘Kwa wanadamu hilo haliwezekani, bali kwa Mungu mambo yote yawezekana.’” (Mt. 19:25, 26) Pia Maandiko yanaonyesha kwamba mtume Paulo alitazama kwa makini jinsi wasikilizaji walivyoitikia. Pindi moja, mtu fulani ambaye alikuwa mlemavu tangu kuzaliwa alikuwapo mahali Paulo alikuwa akizungumza. Andiko la Matendo 14:9, 10 linasema: “Mtu huyu alikuwa akisikiliza Paulo akisema, ambaye, alipomkazia macho na kuona alikuwa na imani ya kufanywa apone, alisema kwa sauti kubwa: ‘Simama wima kwa miguu yako.’”
Madokezo ya Kutumia Katika Huduma ya Shambani. Unapokuwa katika huduma ya shambani, uwe mwenye urafiki na mchangamfu unapowafikia watu. Ikiwa inafaa, tumia maswali yanayochochea akili ili kuanzisha mazungumzo kuhusu jambo ambalo linaweza kuwapendeza nyote. Unapofanya hivyo, jaribu kumtazama macho mtu huyo—au angalau mtazame usoni kwa heshima na fadhili. Tabasamu changamfu ya mtu mwenye shangwe ya moyoni huvutia sana. Tabasamu kama hiyo inaweza kumwonyesha wewe ni mtu wa aina gani na kumfanya astarehe zaidi mnapozungumza.
Ikiwa inafaa unaweza kujua jinsi ya kushughulika na mtu huyo kwa kumtazama machoni. Unaweza kutambua kama amekasirika au hapendezwi. Unaweza kutambua kama hakuelewi. Ni rahisi kutambua kama anachoka kukusikiliza. Pia itakuwa dhahiri ikiwa anapendezwa sana. Macho yake yanaweza kukuonyesha unahitaji kurekebisha mwendo wako wa kuongea, kujitahidi zaidi kumhusisha katika mazungumzo, kumaliza mazungumzo au, labda, kumwonyesha jinsi tunavyofanya funzo la Biblia.
Iwe unahubiri au unaongoza funzo la Biblia la nyumbani, jaribu kumtazama kwa heshima mtu unayezungumza naye. Lakini, usimkodolee macho kwani anaweza kuona haya. (2 Fal. 8:11) Lakini kwa njia ya kawaida na ya urafiki, mtazame mtu huyo usoni pindi kwa pindi. Katika nchi nyingi, kufanya hivyo huonyesha kwamba kwa kweli unapendezwa naye. Bila shaka macho yako yatakazia kile unachosoma katika Biblia au kichapo kinginecho kile. Lakini, unaweza kumtazama machoni kifupi unapotaka kukazia jambo. Utaweza kuona itikio lake ikiwa unamtazama pindi kwa pindi unaposoma.
Kama unashindwa kuwatazama watu machoni kwa sababu una haya, endelea kujitahidi. Ukifanya mazoezi, utaweza kuwatazama watu machoni kwa njia ya kawaida, na kuweza kuboresha uwezo wako wa kuwasiliana na wengine.
Unapotoa Hotuba. Biblia inatuambia kwamba kabla ya Yesu kuanza Mahubiri ya Mlimani, ‘aliinua macho yake kuwatazama wanafunzi wake.’ (Luka 6:20) Iga mfano wake. Kama utahutubia watu, watazame na utue kwa sekunde kadhaa kabla ya kuanza hotuba. Mahali pengi, kufanya hivyo kunahusisha kuwatazama baadhi ya wasikilizaji. Kutua kifupi kunaweza kukusaidia kuondoa wasiwasi. Pia kutawasaidia wasikilizaji wajipatanishe na hali yoyote au hisia yoyote ambayo uso wako unaonyesha. Vilevile kutua kifupi kutawawezesha wasikilizaji watulie na kuwa tayari kukusikiliza.
Unapotoa hotuba, watazame wasikilizaji. Usiwatazame tu watu wote kwa ujumla. Jaribu kutazama mtu mmoja-mmoja. Katika karibu kila jamii, msemaji hutarajiwa kuwatazama wasikilizaji kwa kadiri fulani.
Kuwatazama wasikilizaji si kupitisha tu macho kutoka upande mmoja hadi mwingine. Mtazame kwa staha mmoja wa wasikilizaji, na ikifaa, zungumza naye sentensi nzima. Kisha mtazame mtu mwingine, zungumza naye sentensi moja au mbili. Usimtazame mtu kwa muda mrefu hata aanze kuona haya, wala usikaze akili yako kwa watu wachache tu kati ya wasikilizaji wote. Endelea kuwatazama-tazama watu kwa njia hiyo, lakini unapoongea na mtu, ongea naye kabisa na utazame jinsi anavyoitikia kabla ya kuanza kuongea na mtu mwingine.
Maandishi yako yanapaswa kuwa kwenye kinara cha msemaji, au mkononi mwako, au katika Biblia yako ili uweze kuyatazama kwa kugeuza tu macho. Ikiwa ni lazima ugeuze kichwa chako chote kutazama maandishi yako, mawasiliano kati yako na wasikilizaji hayatakuwa mazuri. Unapaswa kufikiria mara ambazo unatazama maandishi yako na wakati wa kuyatazama. Ikiwa unatazama maandishi yako unapofikia kilele cha hotuba, utakosa kuona jinsi wasikilizaji wanavyoitikia na pia hutakazia mambo ifaavyo. Vilevile, kama unatazama maandishi yako daima, hakutakuwa na mawasiliano kati yako na wasikilizaji.
Ukimrushia mtu mpira, unatazama uone kama ameushika. Kila wazo katika hotuba yako ni kama mpira uliorushwa kwa wasikilizaji. Ukiona wakitikisa kichwa, wakitabasamu, wakikutazama kwa makini, basi wamelishika wazo lako. Ukidumisha mawasiliano mazuri na wasikilizaji kwa kuwatazama, unaweza kuwa na hakika wanakuelewa.
Ukipewa mgawo wa kusoma mbele ya kutaniko, je, unaweza kuwatazama wasikilizaji unaposoma? Kama wasikilizaji wanafuatana na wewe unaposoma Biblia, wengi wao hawatajua kama unawatazama au kama huwatazami. Lakini kuwatazama wasikilizaji kunaweza kufanya usome kwa bidii kwa sababu unaona vizuri itikio lao. Na msemaji akigongana macho na yeyote kati ya wasikilizaji ambaye haangalii Biblia na ambaye akili yake inatangatanga, msikilizaji hurejelea kile kinachosomwa. Bila shaka, unaweza kuwatazama tu kifupi, lakini usiwatazame kwa kiasi cha kufanya ujikwae unaposoma. Ili ufaulu, ni vizuri uishike Biblia mkononi mwako na kuinua kichwa chako, na usiinamishe kidevu chako.
Nyakati nyingine wazee hutoa hotuba za kusoma kwenye kusanyiko. Ili kufaulu, inatakikana msemaji awe na uzoefu, atayarishe vizuri, na kufanya mazoezi tele. Bila shaka hotuba za kusoma hufanya asiweze kuwatazama sana wasikilizaji. Lakini kama ametayarisha vizuri, anaweza kuwatazama wasikilizaji pindi kwa pindi bila kupotea anaposoma. Akifanya hivyo, ataweza kushika akili za wasikilizaji na kuwawezesha kufaidika kabisa na mafundisho hayo muhimu ya kiroho.