Onyesha Unawajali Wengine—Kwa Kuwatazama Wasikilizaji Inavyofaa
1 Tunapohubiri mahali pa umma na nyumba kwa nyumba, mara nyingi sisi huwatazama watu kabla ya kuzungumza nao. Katika kipindi hicho kifupi, uso wao unaweza kutusaidia kutambua hisia zao na jinsi wanavyohisi kwa sababu tumewatembelea. Vivyo hivyo wao pia wanaweza kutambua hisia zetu kwa kututazama. Mwanamke mmoja alisema hivi alipotembelewa na Shahidi mmoja: “Ninachokumbuka kuhusu uso wake wenye tabasamu ni utulivu aliokuwa nao. Upendezi wangu ulichochewa.” Hilo lilimfanya mwanamke huyo asikilize habari njema.
2 Kuwatazama wengine ni njia nzuri ya kuanzisha mazungumzo tunapohubiri barabarani au katika maeneo mengine ya umma. Ndugu mmoja hutazama macho ya watu wanaomkaribia. Wanapomtazama, yeye hutabasamu na kutoa magazeti. Kwa kutumia njia hiyo, yeye hufurahia mazungumzo mengi yenye kupendeza na kuwaachia watu vichapo vingi.
3 Tambua Hisia za Wengine: Kuwatazama watu kutatusaidia kutambua hisia zao. Kwa mfano, ikiwa mtu haelewi au hakubaliani na jambo ambalo tumesema, mara nyingi ataonyesha hilo usoni. Ikiwa ana shughuli au anaanza kukosa subira, tutatambua hilo kwa kumtazama uso. Hiyo itatusaidia kubadili au kufupisha ujumbe wetu. Kutambua hisia za wengine ni njia bora ya kuonyesha kwamba tunawajali kikweli.
4 Unyoofu na Usadikisho: Katika tamaduni nyingi, kumtazama mtu katika macho huonyesha kwamba una nia nzuri. Ona jinsi Yesu alivyoitikia wanafunzi walipomwuliza: “Ni nani kwa kweli anayeweza kuokolewa?” Biblia inaripoti hivi: “Akiwatazama usoni, Yesu akawaambia: ‘Kwa wanadamu jambo hilo haliwezekani, lakini kwa Mungu mambo yote yanawezekana.’” (Mt. 19:25, 26) Bila shaka, usadikisho ulioonekana katika macho ya Yesu uliongeza uzito wa maneno aliyosema. Kwa njia hiyohiyo, kuendelea kuwatazama watu kutatusaidia kuwasilisha ujumbe wa Ufalme kwa unyoofu na usadikisho.—2 Kor. 2:17; 1 The. 1:5.